
HOTUBA YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA MHESHIMIWA JAKAYA MRISHO KIKWETE, KWENYE MAHAFALI YA 10 YA CHUO KIKUU CHA MTAKATIFU AGOSTINO TANZANIA (SAUT) MWANZA,
TAREHE 22 NOVEMBA, 2008
Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Askofu Mkuu
wa JimboKuu la Dar es Salaam;
Mhashamu Askofu Jude Ruwaichi, Mwenyekiti wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania;
Mhashamu Askofu Mkuu Joseph Chennoth, Mwakilishi wa Vatican;
Mhashamu Askofu Anthony Mayala, Askofu Mkuu wa Mwanza;
Wahashamu Maaskofu wote mlioko hapa;
Mheshimiwa Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Tanzania;
Waheshimiwa Mawaziri;
Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa;
Waheshimiwa Wabunge;
Waheshimiwa Wakuu wa Wilaya;
Bwana Sandy Weill wa TOUCH FOUNDATION;
Dkt. Antonio Gotto, Mwakilishi wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Weill Cornell cha New York, Marekani;
Bwana Angus O’Shea, Mkurugenzi Mtendaji wa TOUCH FOUNDATION;
Profesa Joseph Shija;
Wageni Waalikwa;
Mabibi na Mabwana:
Naomba nianze kwa kukushukuru wewe Muhashamu Kardinali, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania na Mkuu wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agostino Tanzania kwa heshima hii kubwa mliyonipa ya kujumuika nanyi katika siku hii muhimu na ya kihistroria. Kama tulivyoelezwa na Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo, leo tunaua ndege wawili kwa jiwe moja. Mbali na mahafali ya 10 ya Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agostino na mahafali ya kwanza ya Chuo Kikuu cha Tiba cha Weill Bugando, leo pia tunaadhimisha miaka 50 ya uhai wa Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC).
Kwa hakika leo ni siku ya aina yake. Mimi na mke wangu, Salma tumefarijika sana kuwa miongoni mwa watu waliopata bahati ya kuishuhudia siku hii. Sote hatuna budi kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema, kwa kutujaalia uhai na afya njema na kutuwezesha kuwepo na kushiriki katika sherehe hii adhimu.
Shukrani kwa Waliosaidia
Muadhama Kardinali, Wahashamu Maaskofu, Wageni Waalikwa;
Napenda pia kuitumia nafasi hii kuungana na wasemaji walionitangulia kuwakaribisha wageni wetu waliotoka nje ya Tanzania. Tunawakaribisha kwa mikono miwili nchini mwetu na hasa hapa jijini Mwanza. Kuwepo kwao miongoni mwetu siku ya leo ni jambo la faraja kubwa. Tunatambua wanayo majukumu mengi lakini uamuzi wao wa kuwa nasi hapa Bugando ni kielelezo tosha cha mapenzi yao kwetu Watanzania.
Namshukuru kwa namna ya kipekee Bw. Sandy Weill kwa msaada mkubwa alioutoa na anaoendelea kuutoa katika ujenzi wa Chuo Kikuu cha Tiba cha Bugando. Chuo hiki kipo katika hali hii hivi sasa kutokana na mchango wake mkubwa. Na, kwa msaada wake na ushirikiano wake, nina imani kuwa Chuo chetu kitakuwa bora zaidi siku za usoni. Naomba kwa niaba yenu nyote nimshukuru sana kwa msaada wake na moyo wake wa huruma na upendo kwa nchi yetu na watu wake.
Namshukuru pia Dkt. Antonio Gotto, Mwakilishi wa Chuo Kikuu cha Weill Cornell cha New York, Marekani. Chuo hicho kimekuwa na ushirikiano wa karibu na Chuo Kikuu cha Bugando na kupitia ushirikiano huo, Chuo chetu kimeweza kupata misaada ya fedha, wakufunzi na vifaa mbalimbali vya mafunzo. Ni ushirikiano huo ndiyo uliwezesha kumvuta Bw. Sandy Weill kutusaidia kama anavyofanya sasa.
Nitakuwa mwizi wa fadhila kama sitamtaja Bw. Angus O’Shea, Mkurugenzi Mtendaji wa Touch Foundation ya Marekani ambao wamekuwa mstari wa mbele kusaidia masuala ya uendeshaji na kutafuta wafadhali wa ujenzi wa Chuo hiki.
Let me take this opportunity to extend a warm welcome to all our guests from abroad. We welcome you to Tanzania and to Mwanza in particular. We feel greatly honoured to have you here with us today. I hope that all of you will have an enjoyable and memorable stay in our country. To Mr. Sandy Weill, I express my sincere thanks to you, I can’t find suitable word to express our immense appreciation for the generous support you extended to Weill Bugando University. The University is what it is today because of your support. On the same vein I thank Dr. Antonio Gotto, the Dean of the Weill Cornell Medical College of the University of Cornell from New York for coming and the cooperation and support of Weill Cornell Medical college to Bugando. To Mr. Oshea and to Touch Foundation we thank you for the invaluable contribution you have made towards the management and raising requisite resources. We are deeply touched
Pongezi
Muadhama Kardinali na Wahashamu Maaskofu;
Nakupongeza sana wewe binafsi na Maaskofu wote wa Kanisa Katoliki nchini kwa kutimiza miaka hamsini tangu kuanzishwa kwa Baraza la Maaskofu wa Kanisa Katoliki Tanzania. Ilikuwa ni miaka 50 ya mafanikio mengi ya kujivunia na kutolewa mfano. Sisi sote ni mashuhuda wa mafanikio yaliyopatikana kwani yanajieleza yenyewe na yanaonekana katika nyanja mbalimbali za maisha ya Watanzania. Mafanikio haya ni matokeo ya uongozi wenu mahiri na uliotukuka, kufanya kazi kwa bidii na maarifa, moyo wa uvumilivu na upendo kwa waumini wenu na wananchi wote wa nchi yetu. Mambo ni mengi na orodha ni ndefu sana nachelea kuyataja yote kwani tutakesha na hatutayamaliza.
Kwa niaba ya Serikali na kwa niaba yangu binafsi, natoa pongezi na shukrani nyingi kwa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania na kwa Kanisa Katoliki kwa jumla kwa mchango wake mkubwa na adhimu iliyoutoa na inayoendelea kutoa kwa maendeleo ya nchi yetu na watu wake. Tanawatakia mafanikio maradufu katika miaka hamsini ijayo.
Napenda kuwahakikishia kuwa Serikali inatambua na kuthamini sana mchango wenu. Naahidi kuwa Serikali itaendelea kushirikiana nanyi katika juhudi zenu za kuwahudumia na kuwatumikia Watanzania katika harakati zao za kujiletea maendeleo na maisha yaliyo bora zaidi.
Mheshimiwa Kardinali na Wahashamu Maaskofu;
Nawapongeza na kuwashukuru sana kwa uamuzi wenu wa kuanzisha Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agostino na Vyuo Vikuu Vishiriki vitatu kikiwemo hiki cha cha Tiba hapa Bugando. Mahafali haya ya leo ni kielelezo dhahiri cha usahihi wa uamuzi wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania. Aidha, ni ushahidi wa ninyi kuwa watu makini mnaotekeleza kwa vitendo maamuzi yenu. Uamuzi wenu huo umesaidia sana katika kuimarisha jitihada zetu kitaifa za kupata wataalamu zaidi wa kusukuma mbele gurudumu la maendeleo ya nchi yetu. Leo tunashuhudia mahafali ya kumi ya SAUT na mahafali ya kwanza ya Vyuo Vikuu Vishiriki yakilipatia taifa wataalamu wapatao 900 wa fani mbalimbali. Nimepungukiwa maneno bora zaidi ya kuelezea furaha yangu na shukrani zangu kwenu. Naomba mridhike nikisema Asanteni sana, tena sana.
Pia napenda kuitumia nafasi hii kutoa pongezi zangu za dhati kwa uongozi wa Chuo cha Mtakatifu Agostino na ule wa Vyuo Vikuu Vishiriki vyote vitatu pamoja na wahadhiri na wafanyakazi wote kwa kazi nzuri waifanyayo na mafanikio yanayoendelea kupatikana. Ni ukweli ulio wazi kuwa bila ya juhudi zao, mafanikio yote haya yasingepatikana na wala tusingekuwa na mahafali haya hapa leo. Kwenu nyote nasema asanteni sana kwa kazi nzuri. Nawaomba muendelee na moyo huo. Nawahakikishieni ushirikiano na msaada wangu na wa wenzangu Serikalini kwenu. Mimi na wenzangu tunatambua fika kwamba mafanikio yenu ndiyo mafanikio yetu. Hivyo, tunao wajibu wa kusaidiana.
Muadhama Kardinali, Wahashamu Maaskofu na Wageni Waalikwa;
Mwisho katika pongezi, ingawaje siyo mwisho kwa umuhimu, napenda kuwapongeza wahitimu wote ambao wanatunukiwa vyeti na shahada zao siku ya leo. Huu ni mwanzo wa safari yenu ndefu ya kujenga maisha yenu na ya familia zenu, wakati huo huo mkiwahudumia Watanzania wenzenu na wanadamu kwa jumla. Kama alivyosema Mkuu wa Chuo sote tunawatarajia kufanya kazi kwa bidii na maarifa mkitumia elimu yenu huku mkizingatia maadili na miiko ya kazi na taaluma zenu. Kwa maneno mengine tunawategemea mtoe utumishi uliotukuka kwa Watanzania na wanaadamu wenzenu wote wakati mtakaopata fursa ya kuwahudumia. Naungana nae na wote tuliokuja kushuhudia mahafali yenu, kuwatakia kila la heri. Inshalla, Mwenyezi Mungu atawaongoza ila msimsahau kumuomba na kumtanguliza kwa kila hatua muipigayo.
Naomba mtambue sasa kuwa mambo ya uanafunzi sasa yameshafika mwisho na yale ya mwalimu dunia ndiyo yanaanza. Tena ni vyema mkajua kuwa mambo ya mwalimu dunia wakati mwingine huwa magumu. Lakini ni mambo yanayowezekana. Wapo wenzenu wengi wengine wameweza, kwa nini wewe usiweze? Kinachohitajika ni wepesi wa utambuzi wa mambo, ubunifu, moyo wa kujituma, uvumilivu nidhamu uwapo kazini na nje ya kazi.
Natambua kuwa baadhi yenu mtaajiriwa Serikalini na kwingineko. Kwa hakika walimu na madaktari tutawaajiri wote labda mtu akatae mwenyewe kuwa mtumishi wa Serikali. Najua wengine wataajiriwa na wadau wengine ikiwemo sekta binafsi. Lakini wapo wengine ambao hawataajiriwa na Serikali au kupata ajira kwingineko, naomba msikate tamaa. Tafuteni fursa ya kujiajiri wenyewe. Mimi niko tayari kuwasaidia kadri iwezekanavyo pale mtakapohitaji msaada wangu wa uwezeshaji kwa mipango yenu.
Elimu ya Juu
Muadhama Kardinali, Wahashamu Maaskofu na
Wageni Waalikwa;
Naomba nirudie tena kutoa shukrani zangu kwa Kanisa Katoliki kwa mchango mkubwa inaoendelea kuutoa katika kuendeleza elimu nchini. Natambua kwamba kasi yenu ya uwekezaji katika elimu ilipungua baada ya uhuru, pale Serikali ilipotaifisha shule mlizokuwa mnamiliki na kuendesha nchini. Sera ile na hatua zile zilikuwa ni za muhimu kuchukua kwa wakati ule. Zimesaidia katika kujenga msingi wa utangamano, umoja na utaifa tulionao sasa katika nchi yetu.
Wahenga wanasema kila zama na mambo yake. Baadae katika nusu ya mwisho ya miaka ya 1980 na miaka ya 1990 kumekuwepo na mageuzi makubwa ya sera za kiuchumi na kisiasa nchini. Sera ile kuhusu shule zinazomilikuwa na madhehebu ya dini ikaguswa nayo. Kwa sababu hiyo, baadhi ya shule zilizokuwa zinamilikiwa na madhehebu ya dini zilirejeshwa. Nasema baadhi ya shule kwa sababu ulegezaji uliofanywa katika sera haukulenga kurejesha shule zote. Ilionekana haingekuwa jambo la busara kwa serikali kufanya hivyo.
Lakini, jambo kubwa na la msingi lililoletwa na mageuzi hayo ni kule kuruhusu madhehebu ya dini na mashirika ya kidini na watu binafsi kuanzisha vyuo vya elimu ya juu nchini. Chuo kikuu cha Mtakatifu Agostino ambacho leo tunasherehekea mahafali yake ya 10, ndiyo matunda ya sera hiyo mpya ya Serikali.
Hakika sera hiyo imekuwa na manufaa kwa nchi yetu na watu wake. Hivi sasa, pamoja na SAUT, tunavyo vyuo vikuu na vyuo vikuu vishiriki binafsi 20 vyenye wanafunzi 18,286. Idadi hii tunapoichanganya na ile ya vyuo vikuu vya umma 11 vyenye wanafunzi 64,666, ndiyo inayotufikisha kwa uwiano wa asilimia 2 wa vijana wa umri wa kupata elimu ya chuo kikuu kuwa vyuoni. Kiasi hicho bado ni chini ukilinganisha na majirani zetu wa Kenya na Uganda au hata na wenzetu wengi wa nchi za Kusini mwa Afrika katika SADC.
Muadhama Kardinali, Wahashamu Maaskofu na
Wageni Waalikwa;
Hatuna budi sisi katika Serikali, mashirika ya dini na wadau wengine wa elimu tuendelee kushirikiana katika kukuza na kuendeleza elimu ya juu nchini. Mahitaji bado ni makubwa kwani vijana wengi wenye sifa ya kujiunga na vyuo vikuu bado wanakosa fursa hiyo. Kwa mfano, kwa mafunzo ya udaktari mwaka wa jana asilimia 76 ya vijana wenye sifa hawakuchukuliwa katika vyuo vyetu vikuu. Wakati huo huo nchi ina upungufu mkubwa wa madakatari. Hapa nchini daktari mmoja anahudumia watu 28,000. Hali ni hivyo hivyo kwa fani nyingine muhimu. Mimi naamini tukiendelea kushirikiana kama tufanyavyo tutalikabili ipasavyo tatizo hili.
Muadhama Kardinali, Wahashamu Maaskofu;
Nawaahidi mambo mawili kutoka Serikalini. Kwanza kwamba sera ya kuruhusu wadau wengine zaidi ya Serikali kujenga, kumiliki na kuendesha vyuo vya elimu ya juu nchini, na vyuo vikuu, yaani pamoja tutaidumisha na kuiendeleza. Katu hatutageuka nyuma na kuwakatalia wengine washiriki au kutaifisha vyuo vyao na taasisi zao.
Na, pili tutaendelea kushirikiana na kusaidiana katika uendeshaji wa vyuo vyetu hivi kadri inavyowezekana. Kwa ajili hiyo, Serikali itaendelea kutoa mikopo kwa wanafunzi wanaosoma vyuo vikuu vya serikali na visivyokuwa vya Serikali kwa mujibu wa taratibu zilizowekwa au zitakazowekwa na Serikali.
Mikopo ya Wanafunzi
Natambua kuwa suala la mikopo ya wanafunzi limekuwa chanzo cha misuguano kati ya wanafunzi na serikali. Misuguano hiyo imekuwa inachukua sura mbalimbali kwa nyakati mbalimbali. Kuna wakati misuguano ilihusu utaratibu wa utoaji na ulipaji wa mikopo kwenye Bodi ya Mikopo. Kuna wakati kulikuwa na misuguano kuhusu uchangiaji kwa uwiano wa asilimia 60 kwa 40. Baada ya kulalamikiwa kuwa utaratibu huo haukujali na kutofautisha watoto wa mwenye uwezo na wasiokuwa na uwezo, Serikali ikautazama upya. Ukaanzishwa utaratibu mpya wa kutoa mikopo kulingana na uwezo wa mwanafunzi au wazazi au walezi wake kuchangia ukaanzishwa. Yaani “means testing” ambao unatumika katika nchi kadhaa katika ukanda wetu. Kwa ajili hiyo, wapo wanafunzi wanaopata mkopo kwa asilimia 100 kwa kukosa uwezo na wapo wanaojigharamia wenyewe kwa asilimia 100 kwa sababu wanao uwezo. Pia wapo wanaopata mikopo pungufu kwa viwango mbalimbali kutegemea na uwezo wao.
Kwa mujibu wa takwimu, hadi sasa kati ya jumla ya wanafunzi 41,396 walioingizwa kwenye utaratibu wa mikopo, wanafunzi 5,835 au asilimia 14 wanapata mkopo asilimia 100, wanafunzi 23,936 au asilimia 57.8 wanapata mkopo asilimia 80, wanafunzi 10,278 au asilimia 24.8 wapata mkopo wa asilimia 60, wanafunzi 1,288 au asilimia 3.1 wanapata mkopo asilimia 40, na ni wanafunzi 59 tu wanapata mkopo asilimia 20.
Tulipofanya marekebisho hayo, tulidhani tumetoa jibu. Bahati mbaya haikuwa hivyo. Tena, sasa kukaja madai mapya kwamba utaratibu huu wa kutoa mikopo kwa mujibu wa uwezo wa kila mtu kulipia usiwepo kabisa, bali kila mmoja apewe mkopo kwa asilimia 100. Jazba zikapanda au kupandishwa na kwingineko migomo ikachochewa na hata ghasia, hivyo kusababisha baadhi ya vyuo kufungwa.
Muadhama Kardinali, Wahashamu Maaskofu;
Ndugu zangu, Watanzania wenzangu;
Sera ya wananchi kuchangia sehemu ya gharama kwa huduma za maji, elimu na afya zitolewazo na Serikali iliyoanza kwenye miaka ya 1990, ilibuniwa kwa sababu za msingi kabisa na kwa nia njema. Ni sera ambayo ilibuniwa na kutekelezwa kwa sababu ya manufaa yake. Haikubuniwa kwa roho mbaya au kwa nia ya kutesa au kukomoa wananchi. Hivyo sivyo hata kidogo na, hiyo kamwe haiwezi kuwa dhamira ya Serikali.
Hali kadhalika, katika uchangiaji kwa huduma zote, suala la uwezo wa mtu kulipia lilizingatiwa. Wakati wote wale wasiokuwa na uwezo walihurumiwa na wale wenye uwezo waliachwa kulipia kwa uwezo wao. Ni ukweli usiopingika kuwa wapo miongoni mwetu wenye uwezo wa kulipa.
Kama tujuavyo au tukumbukavyo, kabla ya mabadiliko hayo ya kisera huduma hizo zilikuwa zinatolewa bila ya wananchi kuchangia. Lakini, kwa sababu ya mahitaji ya huduma hizo na shughuli nyingine za Serikali kuendelea kukua kwa sababu ya idadi ya watu kuongezeka na nyakati kubadilika, uwezo wa Serikali wa kubeba mzigo wa kugharamia huduma hizo kwa kiasi na ubora ule ule ukazidi kupungua.
Mwaka hadi mwaka hali ya upatikanaji wa huduma hizo ukaanza kushuka na kuwa wa kiwango cha chini kwa maana ya kutokidhi mahitaji ya watu na ubora wake kuwa chini. Kwa kutambua ukweli huo, na kwa nia ya kutaka kuona wananchi walio wengi wanapata huduma hizo na zinapatikana kwa ubora wa kuridhisha, ndipo sera ya uchangiaji na ushirikishaji wa wadau wengine ikabuniwa na kuanza kutekelezwa.
Serikali ilikuwa mkweli kwa wananchi inaowaongoza kuhusu hali halisi ilivyokuwa na uwezo wake wa kuwahudumia. Nia ilikuwa njema, lakini uwezo ulikuwa mdogo na ulizidi kupungua kadri watu walivyoongezeka.
Ni ukweli ulio wazi kuwa sera hiyo mpya ya uchangiaji imekuwa na manufaa kwa taifa letu na watu wake. Watu wengi zaidi wakawa wanapata huduma za maji, elimu na afya kuliko ilivyokuwa zamani. Aidha, hata ubora wa huduma hizo sasa ni wa juu zaidi kuliko ilivyokuwa zamani. Hata hivyo, bado wako watu wengi nchini ambao hawapati huduma hizo na ubora bado si wa kiwango cha juu vya kutosha ingawaje umepanda kiasi. Maana yake ni kwamba bado tunayo kazi kubwa ya kufanya mbele yetu ili watu wengi zaidi wapate huduma za maji, elimu na afya na kukuza zaidi ubora wa huduma hizo.
Ndugu Zangu, Watanzania Wenzangu;
Kwa hali yetu ya sasa ya uchumi, wingi wa watu na uwezo wa kifedha wa Serikali, hatuwezi kurudi kule tulikokuwa wa huduma hizo kutolewa asilimia 100 kwa gharama za Serikali. Tukifanya hivyo matokeo yake yatakuwa ni yale yale yaliyowafanya viongozi wetu walionitangulia wa Awamu ya Pili na Tatu wafanye mageuzi tunayoendelea kuyatekeleza sasa. Tutawahudumia watu wachache zaidi na hata ubora wa huduma utaathirika.
Muadhama Kardinali na Wahashamu Maaskofu;
Kwa upande wa vyuo vya elimu ya juu, tukirudia mfumo wa zamani, tutachukua wanafunzi kidogo zaidi wa kujiunga na vyuo hivyo. Hatari nyingine ninayoiona hapa, pia ni ule uwezekano wa Serikali kuanza kuwa mbinafsi kwa kutoa kipaumbele kwa wanafunzi wa vyuo vyake tu tofauti na ilivyo sasa inagharamia hata wanafunzi wa vyuo binafsi kama SAUT na vinginevyo. Isitoshe, hata kama Serikali ingeamua kugharamia wanafunzi watakaosoma katika vyuo vyake pekee, naamini bado hatutamudu kuwahudumia wanafunzi wote ipasavyo. Hata huko itabidi wahudumiwe baadhi tu. Kwa sababu hizo na nyinginezo, naamini mfumo wa sasa wa kila mwenye uwezo kuchangia kwa uwezo wake unawawezesha vijana wetu wengi zaidi kupata fursa ya kusoma katika Vyuo Vikuu. Kinyume chake wachache watapata fursa hiyo. Wenye uwezo wanapochangia nguvu na Serikali inawawezesha wasiokuwa na uwezo kusaidiwa.
Napenda kuwahakikishia vijana na Watanzania wenzangu wote kuwa ningependa sana kila Mtanzania apate elimu bure, maji bure, na matibabu bure. Lakini, natambua kuwa uwezo wa Serikali yetu kufanya hivyo kwa sasa ni mdogo. Ni kutokana na ukweli huo ndiyo maana ikaamuliwa tufanye kinachowezekana. Kufanya hivyo ni kwa manufaa yetu sote. Ni kwa maslahi ya taifa letu. Kufanya vinginevyo ni hasara kwetu sote.
Kuhusu manung’uniko yahusuyo taratibu za utoaji wa mikopo katika Bodi ya Mikopo napenda kusema kuwa tumeyasikia na tunayafanyia kazi. Tunafikiria mambo kadhaa ya kufanya. Miongoni mwake tunafikiria kuangalia uwezekano wa kuvifanya vyuo kuwa wakala wa Bodi ya Mikopo. Maana yangu ni kwamba tunatazama kama shughuli ya utoaji wa mikopo ya mwanafunzi iwe pale chuoni anaposoma. Yapo pia mawazo mengine ambayo yanaendelea kutazamwa kwa nia ya kurahisisha utaratibu wa upatikanaji wa mikopo na kuondoa usumbufu uliopo sasa.
Muadhama Kardinali, Wahashamu Maaskofiu;
Ndugu Wananchi,
Napenda kuitumia fursa hii, tena kwa moyo mzito sana, kuelezea masikitiko yangu kuhusu tabia wanayoinyesha baadhi ya wanafunzi wa baadhi ya vyuo vikuu. Kwanza ni matumizi ya migomo. Ndugu zangu mimi sina tatizo na wanafunzi kudai haki zao pale inapostahili. Mimi mwenyewe niliwahi kuwa kiongozi wa Serikali ya Wanafunzi pale Mlimani na nilifanya kazi hiyo. Tatizo langu ni pale wanafunzi wanapoonyesha ubabe, wanapofanya fujo, wanapoharibu mali na wanapopiga wenzao wasiotaka kushiriki migomo. Hii siyo sawa. Unaweza kudai haki bila kugoma na pale inapokuwa hapana budi kugoma, kufanya vurugu siyo lazima. Kingine kinachonisikitisha pia ni lugha inayotumika na kuelekezwa kwa walimu wao, viongozi wao wa Chuo, viongozi wa serikali na hata watu wengine wa umri kuzidi wa kwao.
Ukiisikiliza ile lugha wanayotumia baadhi ya wanafunzi, unajiuliza maswali mengi kuhusu jamii yetu: tulipo na mbele tuendako kuhusu malezi na maadili ya mtoto wa Kitanzania tunayoyajua sisi sote. Narudia kusema kuwa mimi naamini kabisa kwamba wanafunzi wanaweza kudai kile wanachoona wanakistahili bila kufanya fujo, bila matusi, bila ubabe, bila kudharau, kutukana na kukejeli walimu na viongozi wao, na bila kupiga wenzao walioamua kufanya kile kilichowapeleka Chuoni kwa kutoshiriki kwenye migomo na kuingia madarasani. Hili la malezi, nawasihi wazazi wenzangu tuendelee kulipa uzito unaostahili kwani ndiyo taswira yetu na jamii yetu itakayoonekana mbele yetu na wenzetu.
Lakini kwa upande wa Serikali, tutaendelea kuchukua hatua madhubuti kabisa kuhakikisha kwamba sheria za nchi zinafuatwa na zinaheshimiwa. Na pale fujo au uchochezi wa kuvunja amani utakapotokea basi sheria itafuata mkondo wake. Si busara kuwafumbia macho wachache wanaochochea migomo na kusababisha vurugu.
Muadhama Kardinali, Wahashamu Maaskofu;
Madaktari na Wauguzi wa Hospitali ya Bugando;
Kwa upande wa Hospitali ya Bugando napenda kuwahakikishia kuwa Serikali itaendelea kuimarisha ushirikiano uliopo na Kanisa Katoliki kama ulivyoainishwa kwenye makubaliano yetu ya mwaka 1971. Katika makubaliano hayo Serikali iliomba Hospitali ya Bugando kutoa huduma za afya za rufaa kwa Kanda ya Ziwa. Tulikubaliana kuwa ili kufanikisha hayo Serikali inalo jukumu la kutoa fedha zinazohitajika kuendesha hospitali. Fedha hizo ni kwa ajili ya mishahara ya watumishi, dawa, vifaa-tiba na matumizi mengine ya maendeleo ya hospitali.
Nafurahi kusema kuwa Serikali imekuwa inatimiza wajibu wake huo. Katika kipindi cha kuanzia mwaka wa fedha 2004/2005, Serikali imetoa shilingi 17,772,915,763 kwa ajili ya uendeshaji wa hospitali ya Bugando. Napenda kuwahakikishia kuwa tutaendelea kutimiza wajibu wetu huo ili kuiwezesha hospitali yetu hii kutoa huduma bora zaidi za matibabu kwa wakazi wa Ukanda huu wa Ziwa.
Hitimisho
Muadhama Kardinali, Wahashamu Maaskofu na Wageni Waalikwa;
Naomba nimalize hotuba yangu kama nilivyoanza. Nawashukuru tena kwa kunialika na kuniwezesha kushiriki katika tukio hili la kihistoria. Nawashukuru pia kwa kazi nzuri mnayoifanya ya kufundisha wataalamu katika nchi yetu. Leo hapa tumeshuhudia wahitimu wa fani mbalimbali zikiwemo za Udaktari, Ualimu, Uhasibu, Uanasheria, Uchumi na Mawasiliano ya Umma. Kada zote hizi ni chachu muhimu katika kusukuma mbele gurudumu la maendeleo ya nchi yetu.
Aidha, tunawashukuru tena wafadhili mbalimbali ambao wamekuwa wakichangia katika jitihada zetu za kuimarisha na kupanua elimu ya juu. Mchango wao bado unahitajika kwani safari yetu bado ni ndefu. Hivyo tunawaomba wasichoke bali waendelee kutusaidia.
Kwa upande wa Vyuo vyetu Vikuu, napenda kurudia wito wangu kwenu kuhusu umuhimu wa kutoa wahitimu waliobobea katika fani walizosomea. Vyuo vyetu viwe ni tanuru la kuoka na kuivisha wataalamu watakaokuwa na uwezo wa kuwahudumia vizuri wananchi na kuleta mabadiliko katika jamii yetu. Aidha, wataalamu tunaowafundisha pia wawe na uwezo wa kukubalika nchini na popote duniani.
Na mwisho kabisa napenda kuwahakikishia tena nia ya Serikali ya kuendelea kufanya kazi pamoja na Kanisa Katoliki na madhehebu mengine ya dini pamoja na wadau wengine katika kuimarisha na kupanua elimu ya juu na elimu kwa jumla hapa nchini. Serikali itaendelea kutimiza wajibu wake wa msingi wa kuweka mazingira mazuri yatakayowawezesha watu binafsi na madhehebu ya dini kushiriki kwa ukamilifu katika kuendeleza elimu ya Chuo Kikuu hapa nchini.
Hivyo msichoke kutukumbusha wajibu wetu kama ambavyo na sisi hatutachoka kuomba ushirikiano na msaada wenu pale inapostahili. Ni ukweli kwamba sote tuna lengo moja la kuwahudumia Watanzania ili wawe na maisha yaliyo bora zaidi. Nina hakika kuwa tukiendelea kushirikiana na kufanya kazi kwa pamoja kama ambavyo tunafanya hivi sasa tutatimiza malengo yetu.
Mungu ibariki Tanzania.
Nawatakia maadhimisho mema.
Nawashukuruni sana kwa kunisilikiza.
Pichani: Rais Jakaya Kikwete akimpongeza Sista Alicia Masenga aliyehitimu Shahada ya udaktari wa Magonjwa ya binadamu Wakati wa Mahafali iliyofanyika katika Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agustino mkoani Mwanza leo . Wapili kushoto ni Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania Askofu Thadeus Ruwaichi na watatu kushoto ni makamu Mkuu wa Chuo Padre Joseph Kitima. Picha hii ni mali ya Freddy Maro.