Mwenda alikuwa na kazi kubwa ya kutambua kwamba baba yake ana ugonjwa gani na hali hiyo haikumpendeza hata kidogo. Kitu cha kwanza ambacho a...
Mwenda alikuwa na kazi kubwa ya kutambua kwamba baba yake ana ugonjwa gani na hali hiyo haikumpendeza hata kidogo. Kitu cha kwanza ambacho alifikiria usiku huo ni kuhakikisha kwamba anapata majibu ya maswali yote madogo madogo ambayo yangelimsaidia kutambua hali halisi ya baba yake. Maswali hayo angeliyajua kupitia mazungumzo na mama yake na pia kupitia vipimo vidogo ambavyo angelipendelea kujua kabla ya kupeleka vipimo Morogoro.
Hakuwa na shaka kuwa baba yake alikuwa na tatizo la ugonjwa wa kifua kikuu ambacho kimeachwa kumtafuna kwa muda mrefu. Lakini matatizo mengi katika watu ambao wamepita umri kidogo huambatana sana na shida ambayo inaweza kuwa nayo katika mzunguko wa hewa hasa katika nyumba za msonge ambazo uwapo wa madirisha huwa ni wa aina yake na wakati mwingine hakuna kabisa.
Ilikuwa shida tupu, lakini ni wazi kuwa hakuwa na muda wa kujadiliana kuhusu suala hilo ni mazoea tu yamewaweka watu katika nyumba hizo ambazo mzunguko wa hewa kwa mgonjwa huwa taabu. Kutokana na baridi watu wengi wamekuwa wakiishi katika hali ya kujifungia zaidi.
Haikuwa rahisi kuondokana na dhana ya zamani kwamba madirisha yanaruhusu wanga kupita na kwamba kuwa na madirisha makubwa ni kuwakaribisha wachawi kukuroga.Zilikuwa imani za kijinga lakini zenye mwelekeo ambao si wa kawaida hata kidogo.
Utamaduni ambao umejijenga kuhusiana na maisha ya kawaida ya wanadamu wa maeneo haya ya mlimani, hofu ya maisha ya kurogana na pia hali ya kutokuaminiana imefanya mazingira ya maisha kuwa na aina fulani ya mfuatano na hata ujenzi kufanana. Baada ya kukamilisha kila kitu pamoja na mawazo, kula chakula na kuoga Mwenda alirejea katika chumba chake na kisha akaenda kumwangalia mama yake jinsi anavyohangaika kumsaidia baba yake kula chakula.
"Baba Mwenda kidogo tu angalau uonyeshe kwamba unakula kwa mtoto" alisema mama Mwenda. Kweli baba alijitahidi lakini mwishoni hakuweza aliashiria kunawishwa na kuachwa kupumzika.
"Nitakula baadaye" alisema kwa sauti ya chini kabisa ambayo ilisikiwa na Mama Mwenda pekee.
Mwenda alimtazama baba yake alivyokuwa akihangaika akabaki anajiuliza kama maisha mwishoni ni hivyo hivyo kwa kila mtu. Kuwa mzima na kijana kuhangaika na mwishoni kuwa mzee na kujikuta huna nguvu hata ya kuhimili magonjwa. Katika maisha yake hakuwahi hata mara moja kumuona baba yake katika hali hiyo ya kudhoofu. Alikuwa baba ambaye siku zote anajituma.
"Mama ilikuwa siku zote hali hiyo au.."
"Siku hizi afadhali mzee Mkalindi anamsaidia kwa dawa zake. Baba yako karogwa halafu mtesi wake ndiye yule yule. Mzee Malinyingi sijui tumemkosea nini"
"Mama nawe unaamini hayo?"
"Nisiamini hayo unadhani sisi wewe kwenda Ulaya tuna heri hapa? Hata ndugu za baba yako wanatuonea"
"Sipendi kuamini."
"Amini mwanangu manake haya ni mambo ambayo hayaeleweki, ulimwengu wa kiza."
"Ingawa nimefika namuona baba mgonjwa mpaka nitakapoondoka baba yangu atakuwa shwari we ngoja uangalie.Hamkupeleka bure Mwenda, mmempeleka awasaidie na sasa ndio wakati wangu" alisema huku akitoka nje kwani mama yake alimfanyia ishara kuwa anataka kumsafisha baba yake.
Akiwa nje akawa anafikri sana. Fikira zake zilikuwa katika dunia nyingine dunia ya watu kutofahamu vyanzo vya magonjwa na kuishiwa kudanganywa na waganga wa kienyeji.Dunia ya kuoanisha ilikuwa ngumu kwani yapo mambo yanafanyika ambayo hayakuwa na msimamo hata kidogo wala kuwa na uhusiano na mgonjwa.Mama alikuwa na nafasi yake ya woga na japokama alikuwa anaamini kwamba Mungu yu pamoja nao amekuwa na mashaka na jinsi ndugu wa mume wake walivyomtenga yeye na mume wake wakimwacha ahangaike.
Haikuwa inaswihi kwa namna yoyote ile lakini ni wazi haikuwa sawasawa pia.
Mungu hata hivyo amewakumbuka kwani wakati anamuomba amsaidie binti yake arejee kuona sura ya mwisho ya baba yake amerejea kweli kweli na amerejea huku akiwa hajui kama ni kwa muda au kwa kuendelea.
Alimuosha mume wake pale akampa dawa zake za kuchemsha na baada ya kuona jasho linamtoka akamfunika na blanketi akapunguza taa na kumfuata mwanawe ukumbini, alijua muda wa kuwa macho bado.
Alifika na kuketi akiwa amechoka sana.
"Nakuona mama huna hata hamu ya kuzungumza."
"Nina hamu kubwa mwanangu lakini sina furaha hata chembe."
"Unataka furaha gani mama zaidi ya mwanao kurejea" alimuuliza kwa mzaha alikuwa anajua nini maana yake.
"kweli mwanangu umerejea lazima niwe na furaha lakini umekua wewe kuna zaidi ya hili la wewe kurejea. Nimeishi na baba yako tangu ubikira wangu mpaka nazeeka, sijui mume mwingine mimi na huyu sasa ni zaidi ya mume ni rafiki kipenzi mwaminifu na ambaye kumkosa siwezi hata kidogo."alisema na kushusha pumzi.
Ni kweli baba Mwenda alikuwa rafiki mwema na mwaminifu na hata wakati alipokuwa akihangaika kupata mtoto huku watoto wake akizika mmoja baada ya mwingine mara tu baada ya kujifungua , baba Mwenda alibaki kuwa mume anayejali. Hakusikiliza kauli za ndugu zake wala maneno ya kuzusha na kuudhi kutoka kwa mawifi zake yeye alibaki akiwakodolea macho wala hawajibu. Walipomkera akasema hovyo wakataka kumtenga.
"Mwanamke gani anazaa panya wanaokufia mshimoni" walisikika wazi wakisema na hiyo ilimuuma sana lakini aliendelea hivyo, wakahangaika kwa waganga ndipo alipompata Mwenda ambaye alitulia na kuendele akupumua hakuamini miezi iliyofanya miaka mpaka anaondoka kwenda shule na anaondoka kwenda ulaya na sasa anarejea ilikuwa tamu mno kwake yeye ambaye alionekana kama mwanamke mwenye laana kubwa.
Alijua kwanini alikuwa akihesabika na laana alikuwa ni mwanamke ambaye hakuwa chaguo la kijiji kile ,alikuwa chaguo la baba Mwenda ambaye alikutana naye katika ngoma kijiji cha nne ambacho walifika kupeleka pombe.Kwa ufupi yeye pale alikuwa anaonekana kama mtoka mbali aliyekuja kupora mali. hakuwa na haja na mali zao yeye alikuwa mwanake ambaye anajua dasturi za kiluguru na hakuwa na sababu za kuhangaika na mali ambazo si zake.
"Mama nakuona una mawazo mengi sana?"
"Umesema mambo ambayo yamefanya moyo wangu ulipuke ukumbuke mambo mengi sana, mengi si mazuri na hivyo baba yako akiondoka namie nitaondoka nitakuacha katika mji wa watu ambao si wema hata kidogo" alisema na baadaye kuendelea kumkumbusha mtoto wake jinsi walivyomlea kwa shida lakini walivyotukanwa sana mpaka yeye anaondoka anaenda shule anamaliza na kwenda zake Ulaya.
"Mhh nambie mwanangu sasa wewe ni daktari?"
"Sana mama . Mimi daktari ninaelimu sawa na madaktari wengine japokama nimejifunza Urusi" alisema kwa tabasamu kubwa huku akimkumbatia mama yake.Ilikuwa ni kumbatio zuri ambalo lilikuwa na kila aina ya upendo.
"sasa mwanangu ni kama unavyoona nilikuwa nasali kila siku kwa mizimu yetu ikurudishe salama ili angalau umuone baba yako manake nimekuwa nikiishi katika dunia ya woga muda wote huu."
"Kweli mama nimemuona baba na hali yake hairidhishi hata kidogo. Pamoja na kuona kama nimechelewa lakini nataka kujaribu kurejesha afya ya baba"
"Sidhani kama unaweza mwanangu. Sumu imesambaa kila mahali ndivyo mganga alivyosema"
"Mama waganga nao ni watu kama sisi si miungu. Mimi naamini baba kama ameweza kufika muda huu ni lazima atapona. Nitahakikisha atapona. Naona ameanza kukohoa nenda kamsaidie lakini ninataka kukuambia mama hakuna kurogwa wala nini hii hali ya kawaida na hospitali watatuambia nini. Kesho asubuhi nataka kutwaa vipimo vyote vya baba nivipeleke hospitalini Morogoro nitarejea na majibu."
"Haya sasa utachukuaje vipimo hivyo?"
"Mungu akituamsha asubuhi sana basi nataka makohozi yake, na nitamtoa damu kidogo kuondoka nayo vifaa ninavyo"
"Damu mwanangu umekuwa chinjachinja?"
"Wala mama nataka kujua kitu kilichopo ndani ya damu ya baba niweze kumsaidia baba yangu."
"Mama huyo baba yako ni mume wangu mimi lazima umsaidie.Una moyo wa kujituma kama baba yako akupe na moyo wa kusamehe pia kama hali haitakuwa sawasawa" alisema mama yake.Mama aliondoka pale na mtoto alisema wazi kwamba atashinda gemu ile japo inaonekana kuwa ngumu kidogo.
Asubuhi ilipofika ilikuwa taabu kubwa kwani haikuwa rahisi kwa Mwenda kuondoka baba yake alikuwa amebanwa sana. Lakini kwa ishara alimruhu kuondoka naye akaondoka haraka zaidi.
Alifika madukani kabla ya kucha na kupata lifti ya landrover iliyokuwa inampeleka hospitali ya mkoa wa Morogoro mgonjwa mmoja.
Alifika Morogoro moja kwa moja na kama ameandikiwa bahati alikutana na mtu ambaye alimwacha Urusi miaka mitatu iliyopita Dk Madelaine ambaye alimkumbuka moja kwa moja.
"Hee Mwenda umeingia lini" walisemezana kwa Kirusi baada ya kufahamiana.
"Ndugu yangu nimerejea jana nimepandisha mlimani nimekuta baba yangu hoi nimechukua sampuli nije hapa nione ana nini."
"Hilo tu dogo mimi nipo hukohuko maabara".Waliondoka na kuelekea maabara ambako walihangaika pamoja na baada ya saa nne waliweza kubainisha kwamba baba yake ana kifua kikuu, ana tatizo la ini , ana malaria na pia alikuwa na tatizo la figo.
"hili la malaria na kifua kikuu hakuna shida hebu chukua za kumwanzishia dozi kama wiki mbili hivi akipanda vyema mlete tuone hilo ini na figo lina matatizo gani" alisema Medeline ambaye baadaye aliondoka na kumsindikiza rafiki yake mpaka soko kuu la Morogoro ambako alipanda lori kurejea nyumbani kwao Mgeta.
Itaendelea Jumatatu ijayo
COMMENTS