Kocha Kim Poulsen anayeinoa timu ya vijana wenye umri chini ya miaka 20 cha Tanzania (Ngorongoro Heroes) ameahidi kikosi chake kufanya v...
Kocha Kim Poulsen anayeinoa timu ya vijana wenye umri chini ya miaka 20 cha Tanzania
(Ngorongoro Heroes) ameahidi kikosi chake kufanya vizuri kwenye mechi dhidi ya
Sudan.
Akizungumza jana (Aprili 20 mwaka huu) kwenye mkutano na Waandishi wa Habari,
Poulsen amesema timu yake imejiandaa vizuri kwa mechi hiyo na kiu yao ni kushinda.
Kwa upande wake Kocha wa Sudan, Azhari Osman El Tahir amesema ingawa haifahamu
vizuri timu ya Tanzania, lakini wamejiandaa kushinda kwani kwa muda mrefu walikuwa
hawajashiriki mashindano ya vijana ya kimataifa.
Mechi hiyo ya michuano ya Afrika kwa vijana wenye umri huo itachezwa kesho (Aprili
21 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 10 kamili jioni kwa
viingilio vya sh. 3,000, sh. 5,000, sh. 10,000 na sh. 15,000.
Sudan iliwasili nchini jana (Aprili 19 mwaka huu) ikiwa na kikosi cha wachezaji 20,
viongozi kumi na mwandishi wa habari mmoja kwa ajili ya mechi hiyo ya kwanza kabla
ya timu hizo kurudiana jijini Khartoum kati ya Mei 4, 5 na 6 mwaka huu.
Mechi hiyo itachezeshwa na mwamuzi Brian Miiro atakayesaidiwa na Mark Ssonko, Lee
Patabali na Denis Batte wote kutoka Uganda. Ejigu Ashenafi wa Ethiopia ndiye
atakayekuwa Kamishna wa mechi hiyo namba 15.
Fainali za Afrika kwa michuano hiyo zitafanyika Machi mwakani nchini Algeria wakati
za Dunia zitafanyika nchini Uturuki kuanzia Juni hadi Julai mwakani. Katika fainali
za Dunia, Afrika itawakilishwa na timu nne za kwanza kwenye fainali za Algeria.
MALINZI MGENI RASMI MKUTANO MKUU TFF
Mwenyekiti wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Dioniz Malinzi anatarajia kuwa mgeni
rasmi kwenye ufunguzi Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania
(TFF) utakaofanyika kwa siku mbili (Aprili 21 na 22 mwaka huu) kwenye ukumbi wa NSSF
Waterfront jijini Dar es Salaam.
Wajumbe wa mkutano huo watawasili jijini kesho (Aprili 20 mwaka huu) na watafikia
kwenye hoteli ya Royal Valentino. Wajumbe wanatoka katika vyama vya mpira wa miguu
vya mikoa, vyama shiriki na klabu za Ligi Kuu ya Vodacom.
Mkutano huo utakaoanza saa 3 asubuhi utakuwa na ajenda kumi na moja. Baadhi ya
ajenda hizo ni hotuba ya Rais wa TFF, taarifa ya utendaji ya mwaka 2011, bajeti ya
mwaka 2012 na taarifa ya ukaguzi wa hesabu (audited accounts).
MECHI ZA VPL WIKIENDI HII, MAREKEBISHO
Ligi Kuu ya Vodacom inaingia raundi ya 24 wikiendi hii kwa mechi mbili
zitakazochezwa Aprili 22 jijini Dar es Salaam. Villa Squad itaumana na African Lyon
kwenye Uwanja wa Chamazi wakati Yanga itakuwa mwenyeji wa Polisi Dodoma katika
Uwanja wa Taifa.
Azam na Mtibwa Sugar zilizokuwa zicheze Aprili 21 mwaka huu sasa zitacheza Aprili 23
mwaka huu kwenye Uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam wakati siku hiyo hiyo jioni
kutakuwa na mechi kati ya Simba na Moro United. Mechi zote zitaanza saa 10.30 jioni.
Aprili 25 mwaka huu Oljoro JKT itaikaribisha Yanga kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya
Sheikh Kaluta Amri Abeid jijini Arusha wakati JKT Ruvu itakuwa mwenyeji wa Ruvu
Shooting kwenye Uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam.
Raundi ya 25 itakamilika kwa mechi nne; Aprili 28 mwaka huu Coastal Union itakuwa
mwenyeji wa Kagera Sugar kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga huku Mtibwa Sugar
ikiwa mgeni wa African Lyon kwenye Uwanja wa Chamazi. Azam na Toto African zitacheza
Chamazi, Aprili 30 mwaka huu wakati Mei 1 mwaka huu Villa Squad itaumana na Oljoro
JKT kwenye Uwanja wa Chamazi.
Ligi hiyo itafunga msimu wa 2011/2012, Mei 5 mwaka huu ambapo timu zote 14 zitakuwa
uwanjani. Simba vs Yanga (Uwanja wa Taifa), Oljoro JKT vs Polisi Dodoma (Sheikh
Kaluta Amri Abeid, Arusha), Ruvu Shooting vs Villa Squad (Mabatini, Mlandizi),
Coastal Union vs Toto African (Mkwakwani, Tanga), African Lyon vs JKT Ruvu (Manungu,
Morogoro), Azam vs Kagera Sugar (Chamazi, Dar es Salaam) na Moro United vs Mtibwa
Sugar (Jamhuri, Morogoro).
WASWAZI KUCHEZESHA SIMBA, AL AHLY SHANDY
Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limeteua waamuzi kutoka Swaziland
kuchezesha mechi ya kwanza ya 16 bora ya Kombe la Shirikisho kati ya Simba na Al
Ahly Shandy ya Sudan itakayochezwa Aprili 29 mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es
Salaam.
Waamuzi hao wa mechi hiyo namba 71 ni Nhleko Simanga Pritchard atakayepuliza filimbi
wakati wasaidizi wake ni Mbingo Petros Mzikayifani na Sibandze Thulani. Mwamuzi wa
mezani atakuwa Fakudze Mbongiseni Elliot.
CAF pia imemteua Kayijuga Gaspard wa Rwanda kuwa Kamishna wa mechi hiyo.
COMMENTS