"POLE sana kwa Kanumba, Hongera kwa Simba" huo ulikuwa ujumbe wa SMS katika simu yangu, ujumbe kutoka kwa mkuu wangu wa kazi, Jos...

"POLE sana kwa Kanumba, Hongera kwa Simba" huo ulikuwa ujumbe wa SMS katika simu yangu, ujumbe kutoka kwa mkuu wangu wa kazi, Joseph Kulangwa ambaye ndiye Mhariri wa Gazeti la HabariLeo, moja ya magazeti yanayomilikiwa na Kampuni ya Magazeti ya Serikali ya TSN. Sikuelewa Pole ya Kanumba, niliweza kuelewa Hongera ya Simba.
Kabla sijaamua kumpigia simu kujua kulikoni, kwani sikuwa najua kilichotokea, ujumbe mwingine kutoka kwa rafiki yangu mmoja kutoka Dodoma uliingia "Steven Kanumba amekufa".
Sasa usingizi ukanitoka, Duhh. Kutoka hapo nikawa na mfululizo wa salamu na nilipofungua kompyuta asubuhi nikakutana na maneno haya: Beda, Kama ujuavyo Kanumba alikuwa mdau na shabiki mkubwa wa ZIFF. Sisi hata huku tumehuzunika sana kwa kifo chake. Langu ni shairi tu kwa rafiki yangu aliyenitangulia Steven Kanumba. Martin
*ULALE PEMA PEPONI STEVEN KANUMBA* Ulikuwa mtu mbele ya watu, ukajivika tabasamu cheko na bashasha, ulikuwa wa mwanzo na jemadari, kuona mbele na safari kuongoza, Ulikuwa wa mwisho kununa, uliposimangwa kwa kero na ujuvi, Wewe ulishika panga, ukaingia mwituni na njia kutupasulia!
Eh jiti kuu la mwituni, ndege wema na wabaya watamiapo, Eh mzizi ulotambaa, ukagusa nyika na bahari kwa pamoja, Eh mbuyu wa thamani, dawa poa na sumu kali zote zipo, Eh wimbo wa pozeo, jua la kuchea na mwezi wa kuchwea.
Nikwambe nini jabali, ulobeba tasnia, Nikusifuje kwa hili, mbinguni wakasikia, Leo dunia hulali, Pepo yakutazamia, Ugone mpheho Steven, Umbudo nakukumbuka.
Naam Kumbe ni kweli Steven Kanumba amekufa, na shairi katungiwa na Profesa Martin Mhando, Mwalimu wa mambo ya filamu aliyeko Chuo Kikuu cha Murdoch nchini Australia. Profesa Mhando ni mtu niliyetokea kumfahamu sana si kwa sababu ya U profesa bali alivyosimamia Tamasha la Filamu la Zanzibar kwa miaka kadhaa akituunganisha wapenzi na wadau wa masuala ya filamu na aliondokea kumpenda sana Kanumba kwa kuonesha njia kwenye tasnia ya filamu.
Je, mimi namjua Kanumba, kijana wa Kisukuma kutoka Shinyanga? Inawezekana kabisa simjui lakini nimefanya naye kazi kadhaa kama mwandishi na mara ya mwisho nilizungumza naye katika Red Carpet ya Ziff pale New Maisha Club na akaniambia kazi zikipungua tukutane tuzungumze.
Pamoja na hayo napenda kukiri kwamba nilivoti kwake katika masuala kadhaa niliyoletewa mezani kwangu kama mhakiki wa filamu na mara kadha nimepigia vyema sinema zake na nne kati yake zilipata nafasi mbalimbali ikiwamo ya The Devils Kingdom na This Is It.
Nilifanya naye mahojiano mara kadhaa, lakini nayakumbuka majibu yake matatu manne hivi yanayoweza kukupa kiwi:“Hakuna dhambi mpya” alisema haya wakati anajibu swali la kwa nini sinema za Bongo zinafanana na sinema za Nigeria, huu ulikuwa mwaka 2010.
“Kwani wewe unanionaje?” Ni swali alilouliza Kanumba kwa mwanafunzi mmoja wa Zanzibar kutoka Shule ya Sekondari ya Forodhani alipoenda kutoa salamu kama mgeni wa ZIFF. Swali hilo lilitokana na maelezo ya wajihi wake Kanumba wakati akiigiza katika sinema zake na kama Kanumba anajisikiaje na anaonekana vipi kwa wananchi wengine kwa kuigiza katika sinema kama mchawi.
"Hapana, Msimbe ni lazima kuangalia kwamba kazi hii inakuwa bora kwa jinsi inavyostahili. Unapoigiza na watu wa kimataifa kama hawa," alisema nilipomuuliza mbona anachukua muda mrefu kutoa filamu yake ya Devil’s Kingdom.
Pia hakuwa na dhiki kueleza changamoto, furaha na mafanikio yake na haya unaweza kuyaona katika mahojiano na Mwandishi wa HabariLeo Jumapili Angela Semaya (nilikuwapo):Alisema hivi:"Mimi Steven Kanumba nikiwa kama producer (projuza)na director (muongozaji) niliyevumbua kipaji cha Jennifer, nikiwa Mkurugenzi wa KANUMBA THE GREAT FILMS (kampuni inayoshughulika na masuala yote ya sanaa ya Jeniffer) nachukua nafasi hii kumpongeza Jennifer kwa hatua aliyofikia akiwa bado na umri mdogo hakika najivunia hili." alisema Kanumba.
Pamoja na kwamba mbunifu, mtundu, mcheshi alikuwa anapenda kuzungumza ukweli na asiyependa bifu kwa waigizaji wenye umri mdogo aliona umuhimu wa kuwalinda. Aliwalinda sana watoto anaoigiza nao kwa kuwa alisema wasipolindwa watalemewa na umaarufu na kushindwa kutekeleza wajibu wao. Mara kadhaa gazeti la HabariLeo liliwahi kumuomba kuwafanyia mahojiano watoto hao na ilipendeza alivyotupa ruksa tulimjua kwamba ni mwangalifu na ni mweledi katika fani yake.
Maneno ya Angela Semaya ( katika face book):Yaani mbali na kuwa msanii mzuri lakini nitamkumbuka Kanumba kwa kunipa kibali cha kufanya mahojiano na watoto wawili maarufu alioigiza nao, Jenniffer wa This Is It na Sophia wa Big Daddy kwa ajili ya makala ya nyota, yanadhihirisha ukweli ninaouzungumza kumhusu Kanumba katika ulinzi na weledi kama muongozaji na mlezi. Kanumba alishawahi kumwambia: “Wewe ni mama nakuamini nakuruhusu kufanya mahojiano na watoto hawa. Alisema sitaki watoto wa watu wahojiwe na kuandikwa vibaya,” Kimsingi unaona alipenda watoto. Katika kazi yangu ya uandishi sijawahi kukutana na mtu ambaye yuko radhi kwa mahojiano, anayekubali kushindwa na anayejenga hoja miongoni mwa wasanii kama Kanumba. Kanumba ni miongoni mwa wasanii ambao wameitambulisha sana Tanzania nje kwa sasa katika tasnia ya filamu, ametumia sana ujuu wa Nigeria katika filamu barani Afrika kutengeneza jina lake na pia kufanya nao kazi. Kutokana na yeye pasi shaka ndio akina Monalisa nao wanaangalia soko la Magharibi kwa kuingilia milango ya Ghana kwa lengo lile lile kupanda chati katika tasnia hii. Kwa kazi alikuwa mahiri mno hata kama projekti ambayo si yake. Unaweza kuiona katika kazi ya Pilipili ya Black Sunday (hii filamu nilishawahi kusema mwandishi wake amekopi "Butterfly on a Wheel" ya Liongate), Komedi hii inavyokuwa ya aksheni na kuwaacha washiriki wake wakiwa katika patashika kubwa ya kuonesha uasili wake katika mchezo ambao ama hakika kama ni stori ya Tanzania thamani yake ni kubwa.
Katika filamu hii ambayo washiriki wake ni Steven Kanumba, Yvonne Cheryl 'Monalisa', na Yusuf Mlela mambo yanayofanyika yamefanana sana na sinema ya mwaka 2007 ya Marekani iliyotolewa na Lionsgate ya "Butterfly on a Wheel".
This Is It ni moja ya filamu bomba ya kwake mwenyewe kuanzia wazo hadi kuitengeneza. Filamu hii imempeleka kwenye Tamasha la Filamu la Afrika (Fespaco) pamoja na kwamba ni ya Kiswahili . Filamu hiyo pia ilinikutanisha tena na Kanumba katika mahojiano yaliyofanywa na Angela Semaya wa HabariLeo Jumapili.
Mahojiano hayo ndio yaliyozaa nyota wetu binti mdogo wa miaka 11 Khanifa Daudi (Jennifer) ambaye pamoja na mambo mengine Jennifer alielezea anavyomjua Kanumba na jinsi alivyofanikisha uigizaji wake.
This Is It ni sinema ya ulozi ambayo imeondokea kupendwa sana pia nchini Kongo na Rwanda kiasi ya kwamba wakati wanaenda kuitambulisha wananchi wa Kongo na Rwanda walimshangilia sana Jennifer.
Nilikutana naye tena Kanumba katika RED CARPET katika ukumbi wa New Maisha Club siku ya Jumapili tarehe 22 Januari 2012. Hapa nilimuuliza kaka vipi akasema mambo yako taiti ana programu ndefu lakini yenye tija, tukimaliza miezi mitatu hii tuonane kuna project za kufa mtu (akimaanisha atakonga nyoyo za wapenzi wake). Ndoa Yangu akiwa na Wolper ilitarajiwa mwezi huu.
Pamoja na kusema ukweli ninavyomfahamu mimi, kwa kumuona katika kikundi cha Kaole, nimeanza kumfuatia katika habari zake kikamilifu mwaka 2007 baada ya kuona kwamba kuna kitu kipo kwa msanii huyu ambaye ni mbunifu na matata katika kazi zake.
Kanumba, ambaye amekufa akiwa na umri wa miaka 28, naweza kuthubutu kusema kwamba ni miongoni mwa waigizaji bora hapa nchini ambao walikuwa wanasafisha njia kwa staili ambayo ni nadra kuonekana katika historia za ukuaji wa sinema duniani.
Kwa miaka kumi aliyokuwapo katika anga za sanaa katika televisheni na video (filamu) kasi ya kijana huyu ilionesha kwamba tupo (kama taifa) karibu sana na matumizi ya kamera ya mm35 na grafiki zilizotulia, baada ya kupotea kwenye miaka ya 1970 tulipomaliza Fimbo ya Mnyonge. Akiwa amezaliwa kama Steven Charles Kanumba kutoka kwa bwana na bibi Charles Meshark Kanumba Januari 8, 1984, alikua katika familia ya Kikristo na dada wawili.
Akiwa anatokea Shinyanga na Msukuma kwa kabila ( si ajabu lafudhi yake inakuwa nzito) amepitia Shule ya Msingi Bugoyi kisha akaingia Mwadui Seminari iliyopo Shinyanga na kukamilisha masomo yake ya O-Level Shule ya Dar es Salaam Christian Seminary. Masomo ya kidato cha tano na sita alichukulia Jitegemee .
Alijiunga na Kaole Sanaa Group ya Dar es Salaam kama muigizaji na kuanza kutokea katika vipindi vya kuigiza vya televisheni za TBC na ITV ikiwemo ‘Jahazi’, ‘Dira’, ‘Zizimo’, ‘Tufani’, ‘Sayari’, ‘Taswira’, ‘Gharika’ na ‘Baragumu’. Mwaka 2009, Kanumba alialikwa katika Big Brother Africa House na akaleta zogo kubwa nchini kwamba hajui Kiingereza. Lakini kama msanii yeyote yule alikuwa na namna ya kulizungumzia hilo na tuliobaki tulicheka.
Sijaona kazi zote za Kanumba lakini nusu yake zilionesha wazi kwamba alikuwa na safari fupi ya uhakika kuingia katika mambo ya Hollywood kule kwenye kitita chenye uhakika.
Buriani Steven Kanumba umefumba wakati unachanua.
Imeandikwa na Beda Msimbe
ilitoka kwa mara ya Kwanza Habarileo Jumapili 8/4/2012
COMMENTS