TAMKO LA TEF KUHUSU UONGOZI WA WIZARA YA HABARI, VIJANA, UTAMADUNI NA MICHEZO KUTOSHIRIKI MKUTANO WA WAHARIRI NA MCT MKOANI MOROGORO ...
TAMKO LA TEF KUHUSU UONGOZI WA WIZARA YA HABARI, VIJANA, UTAMADUNI NA MICHEZO KUTOSHIRIKI MKUTANO WA WAHARIRI NA MCT MKOANI MOROGORO
Mwenyekiti wa Jukwaa Absalom Kibanda |
UTANGULIZI
Juni 3 –
5, 2012, wahariri watendaji na waandamizi wa vyombo vya habari nchini
walikutana mjini Morogoro katika Mkutano Mkuu wa Kwanza wa Mwaka wa Mashauriano
kati yao na Baraza la Habari Tanzania (MCT).
Mkutano
huu ulioshirikisha wahariri kutoka katika vyombo vya serikali, binafsi na vile
vinavyomilikiwa na vyama au taasisi za kidini pamoja na mambo mengine ulijadili
hali na mwenendo wa vyombo vya habari hapa nchini kwa sasa na kwa siku zijazo.
Katika
mkutano huo zilijadiliwa mada mbalimbali ambazo kwa ujumla wake zililenga
kuwezesha kazi ya uandishi wa habari kufanyika kwa kuzingatia maadili, wajibu
na weledi wa kitaaluma.
Pia mada
hizo zililenga kuimarisha, weledi wa kitaaluma, uwajibikaji utendaji wa kazi,
na uhuru wa vyombo vya habari na zaidi kujenga mfumo wa usimamizi wa maadili
ndani ya vyombo vya habari.
Mbali ya
hayo, wahariri na wadau wengine wa habari waliohudhuria mkutano huo walijadili
kuhusu Mchakato wa Sheria ya Haki ya Kupata Habari na Huduma za Vyombo vya
Habari nchini ambao umekuwa ukisuasua kwa takriban miaka 10 sasa.
Ifahamike
kwamba, mkutano huu ulikuwa na uzito wa pekee hasa kwa kuzingatia ukweli
kwamba, wahariri ndio wasimamizi na watoa uamuzi wa mwisho katika vyumba vya
habari kuhusu masuala yote yanayohusu habari, makala na taarifa zinazotolewa
katika vyombo wanavyofanyia kazi.
USHIRIKI WA SERIKALI
Kwa
masikitiko makubwa, Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella
Mukangara na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Seth Kamuhanda hawakushiriki hata kwa
kufungua mkutano huu kama walivyoombwa na Baraza la Habari Tanzania na wao
wenyewe kuthibitisha kwa nyakati tofauti.
Kwa
mshangao wa wahariri na wadau wengine waliohudhuria mkutano huo, viongozi hao
wawili mbali ya kutumiwa rasimu ya hotuba ambayo ilipaswa kusomwa kwanza na
waziri ambaye ndiye alipaswa kuwa mgeni rasmi, kabla ya yeye mwenyewe (waziri)
kutoa taarifa MCT kwamba, angewasilishwa na Katibu Mkuu wa Wizara hawakutokea
katika mkutano huo wala kutuma mwakilishi mwingine yoyote, huku wakitoa udhuru
kwamba walikuwa na kazi nyingine.
Hatua ya
viongozi hao kushindwa kufika katika mkutano huo muhimu kwa maendeleo ya tasnia
ya habari nchini ikiwa ni pamoja na kushindwa kwao kutuma mwakilishi mwingine
kutoka wizarani, si tu iliwashtua wahariri, bali iliwasononesha na
kuwashangaza.
Taarifa
ambazo tulizipata zinaonyesha kuwapo kwa msuguano usio na afya kwa tasnia ya
habari, kwa wizara na kwa serikali nzima kati ya Waziri na Katibu Mkuu. Kitendo
cha wao kushindwa kutuma mwakilishi kutoka kwa viongozi na watendaji wengi
waliojaa katika wizara hiyo ni ushahidi wa namna hali ilivyo mbaya na tete
kimahusiano na kikazi katika wizara hiyo.
MTIZAMO WA WAHARIRI
Kitendo
cha wiki hii kinatupa mashaka iwapo tunastahili kuendelea kuwa na uongozi wa
Waziri na Katibu Mkuu wa sasa katika wizara hii. Tunasema hivyo kwani tuna
shaka sana kama siku zijazo watatoa ushirikiano wa kutosha, hasa katika
mchakato wa kupata sheria nzuri za Huduma za Vyombo vya Habari na ya Haki ya
Kupata Habari.
Tukio
hili kwetu wahariri limetupunguzia imani kwa viongozi hawa iwapo wataweza
kutuvusha katika mabadiliko ya kitaaluma na yale ya kimfumo katika kukusanya na
kutoa habari nchini.
Kwa maana
hiyo tumeazimia kwamba kwanza; Tunatoa taarifa rasmi ili umma wa Watazania
uweze kufahamu hali hii, lakini pili tutawasilisha rasmi malalamiko yetu kwa
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete aweze
kuingilia kati hali hii kwa nia ya kuiokoa tasnia ya habari, ambayo ni muhimu
kwa ustawi na afya ya taifa hili.
Tunapenda
kuwahakikishia Watanzania na Serikali kwa ujumla kuwa vyombo vya habari
vimejizatiti na kujipanga kuwatumikia Watanzania kwa kuzingatia maadili na
weledi wa hali ya juu pia kwa kuzingatia matakwa na maslahi ya umma.
Tunachoomba
ni zana za kufanyia kazi hii. Zana hizi si nyingine bali ni Sheria ya Huduma za
Vyombo vya Habari na Sheria ya Haki ya Kupata Habari, ambazo mchakato wake
umedumu kwa zaidi ya miaka 10 sasa bila sheria hizi kupatikana.
Tunasema
mikingamo inayokwamisha sheria hii imalizwe ili tuweze kupata sheria nzuri na
kufanya kazi kwa uhuru na uhakika zaidi.
Hili la
Waziri na Katibu Mkuu wizarani linaongeza wasiwasi wa kupatikana kwa sheria
hizi.
Mungu
ibariki Tanzania.
Neville Meena,
Katibu – Jukwaa la Wahariri (TEF)
Dar es Salaam,
Juni 07, 2012.
COMMENTS