WASIFU WA HAYATI BOB NYANGA MAKANI Hayati Bob Nyanga Makani alizaliwa mwaka 1936 katika Hospitali ya Kolandoto, Shinyanga. Alikuwa...
WASIFU
WA HAYATI BOB NYANGA MAKANI
Hayati Bob Nyanga Makani
alizaliwa mwaka 1936 katika Hospitali ya Kolandoto, Shinyanga. Alikuwa ni mmoja wa watoto wengi katika familia
ya Mzee Makani.
Alipokuwa na umri
wa miaka sita, alianza masomo yake kwenye shule ya Msingi Ibadakuli, Shinyanga.
Kama ilivyokuwa kawaida ya Serikali ya Mkoloni Muingereza hapa Tanzania wakati
huo, watoto wa Machifu walipelekwa kusoma Shule ya Sekondari Tabora, ndivyo
ilivyokuwa kwa Hayati Bob pia.
Kutokana na uhodari
wake katika masomo, Mheshimiwa Bob Makani
alifaulu na kupelekwa Chuo Kikuu Cha Makerere, wakati huo kikiwa ni Chuo
Kikuu cha pekee Afrika Mashariki, ambako alifuzu na kupata Shahada ya Kwanza
katika Uchumi (BA Economics).
Hakuridhika na shahada
hiyo. Mwaka wa 1961 alikwenda Chuo Kikuu cha Liverpool, nchini Uingereza na
1965 akatunukiwa Shahada ya Sheria (LLB). Kwa mujibu wa Sheria za Uingereza,
anayehitimu Shahada ya Sheria ni lazima vilevile apasi mitihani ya Sheria
kwenye Middle Temple, London, Uingereza na Mheshimiwa Bob Makani alifanikisha
hiyo mwaka huo huo na kurejea nyumbani Tanzania.
Aliporudi Tanzania
aliajiriwa na Serikali kama Mwanasheria wa Serikali kwa muda mfupi kabla
hajapandishwa cheo na kuwa Exchange Control Manager wa Benki Kuu.
Hapo ndipo
alipokutana na kuwa karibu na Mhe. Edwin Mtei aliyekuwa Gavana wa Benki Kuu
wakati huo. Ndiyo maana haikuwa ajabu lilipoanza
vuguvugu la siasa za mabadiliko nchini mwaka 1966, Mhe. Makani na Mhe. Edwin
Mtei walikuwa pamoja.
Mwaka wa 1992 mfumo
wa vyama vingi vya siasa ulipokubaliwa rasmi nchini, Mhe. Bob Makani na Mhe.
Edwin Mtei walikuwa mstari wa mbele kwenye uundwaji wa chama cha siasa. Mwaka huo Mhe. Bob Makani alistaafu kazi
yake ya Unaibu Gavana wa Benki Kuu ili aweze kuelekeza shughuli zake zote
kwenye uanzishaji wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).
Mheshimiwa Bob Makani
ni mwasisi wa CHADEMA na ana kadi ya Chama Namba tatu baada tu ya Mhe. Edwin
Mtei, No. I na Marehemu Brown Ngilulupi Kadi No. 2.
Tangu mwanzo
kabisa, CHADEMA kilifaidi mengi kwa utumishi uliotukuka toka kwake Bob
Makani. Kwanza kabisa, CHADEMA kilifaidika
na utaalam wake wa Sheria ambao pamoja na busara zake zilikisaidia chama kutengeneza
Katiba na taratibu za Uongozi/Administrative Structure) ambayo hadi sasa ni
msingi wa aina ya uongozi tuliojenga ndani ya CHADEMA.
Jambo la pili ni
kuwa Mhe. Bob Makani kwanza kwa asili na pili kwa maumbile yake, alikuwa mtu wa
watu. Ijapo ameshika vyeo vikubwa ndani
ya Serikali, Bob alikuwa na kipaji cha kuwaelewa wananchi na kuungana nao katika
kutafuta ubora wa maisha kwa ujumla.
Urefu aliomjalia Mwenyezi Mungu, ulihakikisha anaonekana! Hali kadhalika, kwa ucheshi wake. Alisikika na kueleweka.
Ni kwa kutambua
uwezo na vipaji vyote hivi, ndiyo maana hapo hapo kwenye kikao cha Mkutano Mkuu
wa kwanza wa CHADEMA Desemba 1991, ndipo Mhe. Bob Makani akachaguliwa kuwa
Katibu Mkuu wa kwanza wa CHADEMA.
Hali kadhalika, kutokana
na usemi uliopo kuwa KAZI NGUMU MPE MSUKUMA, Chama nacho hakikuchelewa kumpa
Bob Makani kazi ngumu ya kueneza Chama kipya Tanzania nzima.
Mhe. Bob Makani
alipewa kazi maalum ya kukipeleka chama mikoa ya Morogoro, Kigoma, Tabora,
Singida, Mwanza na Rukwa. Hapa ikumbukwe
kuwa wakati huo, kuanzisha chama kipya ilionekana kama ni uasi au uhaini na
kwenye mikutano mingi ya hadhara kwenye mikoa hiyo, alipokelewa kwa matusi na
mara nyingine matusi na mawe.
Kwenye mazingira
haya magumu na ikizingatiwa kuwa chama hakikuwa na ruzuku, alitumia rasilimali
zake bila uchoyo ili kukijenga kile alichokiamini kuwa ni chombo cha ukombozi
wa wananchi kwa ajili ya maendeleo ya watu.
Sisi tuliopo CHADEMA
leo, tunajua na kuamini kuwa tokana na ujasiri wa uongozi wa Mhe. Bob Makani
kama Katibu Mkuu wa kwanza wa chama, ndipo Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere aliweza
kutamka wazi kuwa CHADEMA ndicho chama pekee cha upinzani alichoona kina sera
na mwelekeo sahihi. Akakitumia kama mfano wa kukiasa chama chake, CCM kuiga
utengenezaji wa sera zinazoweza kutekelezwa.
Mwaka wa 1998, Mhe.
Bob Makani akachaguliwa kuwa Mwenyekiti Taifa wa CHADEMA, wadhifa alioshika hadi
2003 alipomaliza muda wake na wakati huo akaendelea na kazi zake kama
mwanasheria wa kujitegemea lakini akibaki kuwa kiongozi na mshauri wa chama
hadi kifo kilipomfikia.
Katika uhai wake
Mhe. Bob Makani tokana na uadilifu na utaalam wake aliteuliwa kukshika nafasi
nyingi za uongozi zikiwemo:-
1.
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya
Shirika la Ndege Tanzania.
2.
Mkurugenzi wa Bodi ya Williamson
Diamonds
3.
Mkurugenzi Bodi ya Tanzania
Breweries
4.
Mkurugenzi Bodi ya Benki ya Taifa ya
Biashara
5.
Rais wa Chama cha Wanasheria
Tanganyika Law Society
Marehemu alianza
kusumbuliwa na uogonjwa wa moyo tangu 2009.
Mwaka uliofuata 2010 alipelekwa India kwa matibabu na alipata nafuu kwa muda. Mwaka huu, Bob Makani alipelekwa Nairobi kwa
Operation ndogo lakini baada ya hapo hakuweza kuendelea na kazi.
Mnamo saa za jioni
tarehe 9 Juni alizidiwa na kukimbizwa Hospitali ya Aghakhan ambapo alifariki
saa saba usiku. Marehemu ameacha wajane,
watoto saba na wajukuu wanane.
Mwenyezi Mungu
ailaze mahali pema peponi roho ya Marehemu Bob Nyanga Makani.
AMINA.
COMMENTS