MAELEZO BINAFSI YA MHE. ZITTO ZUBERI KABWE DHIDI YA TUHUMA ZA RUSHWA HUSUSAN KUELEKEA KATIKA KUPITISHA BAJETI YA WIZARA YA NISHATI NA ...
MAELEZO BINAFSI YA
MHE. ZITTO ZUBERI KABWE DHIDI YA
TUHUMA ZA RUSHWA HUSUSAN KUELEKEA KATIKA KUPITISHA BAJETI YA WIZARA YA NISHATI
NA MADINI
Ndugu Waandishi,
Nalazimika kukutana
nanyi kutoa maelezo juu ya tuhuma zenye shinikizo la kisiasa zinazoelekezwa
kwangu binafsi kwamba hata mimi nimeshiriki katika vitendo vya
rushwa, kwa nafasi yangu kama Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Mashirika ya
Umma. Taarifa hizo, kama kawaida ya uzushi mwingine wowote zimesambazwa
kimkakati na kwa kasi kubwa kiasi cha kuukanganya umma.
Nafahamu nabeba
dhamana kubwa ya uongozi, taswira yangu ya uongozi daima imeakisi njozi na
matumaini ya wananchi wa Kigoma Kaskazini, wananchi wanyonge na vijana kote
nchini bila kujali itikadi zao za kisiasa, jinsia zao, makabila yao na rika
zao. Hivyo, nawajibika kupitia kwenu kuwatoa hofu juu ya hisia potofu
zinazopandikizwa kwao na wale wasiopenda kuona baadhi yetu tukiwaunganisha na
kuwasemea watanzania wasio na sauti, dhidi ya vitendo vya hujuma na vyenye
dhamira ovu kwa taifa.
Mkakati huo wa
kuniunganisha na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wanaotuhumiwa kwa kupokea Rushwa
unatekelezwa kwa njia zifuatazo:
1.
Kumekuwa na kauli za watendaji wa serikali ambao wamekuwa
wakizieneza na hususan kutoa taswira kwamba baadhi ya kauli zangu zinatokana na
ushawishi wa rushwa;
2.
Kuna taarifa ambazo zimeandikwa tena katika kurasa za
mbele za baadhi ya vyombo vya habari zikidai ’’Zitto kitanzini’’
ama ’’Zitto sawa na popo nundu’’ zikiashiria kwamba na mimi ni
mla rushwa; na
3.
Waandishi wa habari na jamii kwa ujumla wamefikia
kuaminishwa habari hizi kiasi cha wengine kuuliza kwa nini Mhe. Zitto Kabwehakutajwa katika
orodha iliyotolewa na Mnadhimu Mkuu wa Kambi ya Upinzani.
Ndugu Waandishi,
Naomba kutoa
ufafanuzi wa hicho kinachoelezwa kwamba nina ushiriki katika masuala ya rushwa
hususan kwenye masuala yanayohusu sekta ya Nishati na Madini:-
1.
Mara baada ya bodi ya Wakurugenzi ya Shirika la Usambazaji
wa Umeme Tanzania (TANESCO) chini ya Uenyekiti wake Meja Jenerali Mstaafu
Robert Mboma kutangaza kwamba imemsimamisha kazi Mkurugenzi Mkuu wa Shirika
hilo, Nd. William Mhando ili kupisha uchunguzi wa baadhi ya vitendo/mwenendo
wake, Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC) ambayo mimi ni Mwenyekiti
wake ilimuandikia Mhe. Spika kumuomba aridhie ili Kamati iweze kuwaita Bodi ya
TANESCO, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Mahesabu ya Serikali (CAG) na pia
Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA) kujiridhisha na tuhuma zote
zinazotajwa zinafanyiwa uchunguzi wa kina na hatua kuchukuliwa;
2.
Kamati ya POAC ninayoiongoza ilimuomba Mhe. Spika kuwaita
wahusika tajwa kwa kuwa zilikuwapo tetesi kuwa kusimamishwa kazi kwa Mkurugenzi
huyo siku chache kabla ya Bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini kulikuwa na
lengo la kufunika ’madudu’ makubwa zaidi kwa kulichagiza Bunge na tukio hilo
dogo, mkakati ambao naona umefanikiwa sana. Isitoshe, Kamati kutaka
kujiridhisha na hatua za Bodi ni sehemu ya msingi ya utekelezaji wa majukumu ya
Kamati yaliyowekwa kwa mujibu wa Kanuni za Kudumu za Bunge na pia Shirika la
TANESCO ni moja kati ya mashirika ambayo yanawajibika kwetu kwa hesabu zake na
pia ufanisi wake kwa ujumla. Tumefanya hivyo pia katika mashirika mengine, hili
la TANESCO sio tukio la kipekee;
3.
Kitendo hiki cha halali na kwa mujibu wa Kanuni kilichofanywa na
Kamati yangu kimetafsiriwa kwa makusudi na baadhi ya watu kwamba ni
ishara ya kuwa sisi au zaidi kwamba mimi nina maslahi binafsi na TANESCO na hususan
Mkurugenzi wake Injinia Mhando, ndio maana tumetaka maelezo ya Bodi. Ukweli
kwamba Kamati ya POAC tumewaita pia Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Mahesabu (CAG)
na Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA) kwa jambo hilo hilo umefichwa
kwa makusudi!
4.
Baada ya tukio hilo, nikiwa hapa Dodoma, mwandishi wa
habari wa gazeti moja alinifuata akiniambia kuwa wamekutana na Mhe. Waziri
Mhongo na Katibu Mkuu wake, Nd. Eliachim Maswi hapa hapa Bungeni na wamewaambia
kuwa mimi nimepewa rushwa. Hakutaja nimepewa rushwa na nani, kiasi gani na wala
kwa lengo gani!
5.
Nimejaribu kumtafuta kwa simu Mhe. Waziri Mhongo na Katibu Mkuu
wake ili wanipe ufafanuzi juu ya mimi na Kamati ya POAC kuhusishwa na tuhuma
hizi bila mafanikio, hali ambayo inaniondolea mashaka juu ya ushiriki wao
katika kueneza au kuthibitisha uvumi huo. Najaribu sana kujizuia kutokuwa na
mashaka na ushiriki wao huo ikizingatiwa uzito na taswira ya nafasi zao katika
jamii, lakini wameshindwa kunidhihirishia tofauti.
Sasa naomba kutoa
ufafanuzi rasmi kuhusu mlolongo wa matukio hayo tajwa ambayo yanatumiwa na
baadhi ya wanasiasa kuonesha kwamba eti nimehusika na vitendo vya rushwa.
1.
Binafsi sijawahi kuwa na mawasiliano ya aina yeyote na uongozi
wa TANESCO kushawishiwa juu ya hatua ambazo POAC ndio imezichukua za kutaka
kujiridhisha juu ya utaratibu uliotumika. Ieleweke wazi kabisa kuwa, hakuna
wakati wowote, popote ambapo mimi binafsi au Kamati yetu imekataa Mkurugenzi
Mkuu wa TANESCO kuchunguzwa kwa tuhuma zozote. Ambacho tumesisitiza wakati wote
ni ufuatwaji wa taratibu, kanuni na sheria, hili nitalisimamia iwe masika au
kiangazi;
2.
Ni kwa sababu hiyo, na kwa kujiamini kabisa nimeunga mkono suala
la tuhuma za rushwa zinazotajwa zichunguzwe na Kamati ya Haki, Maadili na
Madaraka ya Bunge kwa kina;
3.
Nimekwenda mbali zaidi kukiomba chama changu CHADEMA kifanye pia
uchunguzi na tathmini yake kwa kina kujiridhisha na tuhuma hizo;
4.
Natumia fursa hii pia kuomba vyombo vya Dola vichunguze tuhuma
hizo kwa nafasi yake ili kuweza kupata ukweli;
5.
Ninaahidi kushiriki kikamilifu iwapo nitatakiwa katika uchunguzi
wowote utakaofanywa na niko tayari kuwajibika iwapo nitakutwa na hatia yeyote.
Napenda niwatoe
hofu wananchi wa jimbo la Kigoma Kaskazini walionituma kuja kuwawakilisha hapa
Bungeni na Watanzania wote kwa ujumla kwamba:-
1.
Mimi Zitto Zuberi Kabwe sina bei, sijawahi kuwa nayo na
sitarajii kuwa nayo huko mbeleni. Daima nimesimamia kidete maadili ya uongozi
bora katika maisha yangu yote ya siasa, na nawaahidi sitarudi nyuma katika
mapambano dhidi ya rushwa katika nchi hii pamoja na mikakati ya aina hii ya
kunidhoofisha na kunivunja moyo;
2.
Nafarijika na salam mbali mbali zinazotolewa kunifariji na
kusisitiza kuwa nisilegeze kamba katika mapambano haya, nimepokea ujumbe mwingi
kwa simu, sms, tweeter na hata facebook na niko pamoja nanyi Watanzania
wenzangu kamwe sitarudi nyuma hadi kieleweke.Naamini katika nchi
yetu tunazo rasilimali za kutosha mahitaji/haja ya kila mmoja wetu lakini si
‘tamaa/ulafi’ wa baadhi ya watanzania wenzetu;
3.
Napenda kuweka rekodi sawa kwa Watanzania kwamba nimekuwa Mbunge
hiki ni kipindi cha pili, Mimi ni Mwenyekiti wa Kamati ya Hesabu za Mashirika
ya Umma (POAC) huu ni takriban mwaka wa saba sasa, Kamati yangu inasimamia
mashirika 259 ya Umma na si TANESCO peke yake. Mchango wa Kamati hii katika
Bunge na kwa ustawi wa Mashirika ya Umma ni bayana na haujawahi kutiliwa shaka.
Kamati yetu imeokoa upotevu mkubwa wa mali za umma na kuokoa fedha za umma
kutokana na umakini wake. Tumefanya hivyo CHC hivi karibuni, Kiwira na kwenye
mashirika mengine mengi. Kote huko uadilifu na uzalendo wa Kamati hii haujawahi
kuhojiwa. Inatuwia vigumu kuona kuwa tunahojiwa katika suala hili la TANESCO.
Hapa pana kitendawili.
4.
Zipo hoja pandikizi za kutaka Kamati ya POAC ivunjwe na haswa
zikinilenga mimi binafsi. Nafahamu kiu ya wasioitakia mema nchi yetu kuiona
POAC ikivunjwa au sura zikibadilishwa kwa kuwa Kamati hii imekuwa mwiba kwa
mikakati yao ya kifisadi. Kwa maoni yangu, Kamati ya POAC isihusishwe na tuhuma
hizi kwa vyovyote vile. Niko tayari nihukumiwe mimi kama mimi na sio kuhusisha
wajumbe wengine ambao hawatajwi mahala popote katika tuhuma hizi mbaya sana
katika historia ya Bunge letu. Nitakuwa tayari kunusuru Kamati ya POAC na
maslahi ya taifa letu kwa kujiuzulu Uenyekiti iwapo itathibitika pasipo shaka
kuwa nimehongwa. Kamati ya POAC ni muhimu zaidi kuliko mimi.
5.
Nafahamu pia kuwa kuna wanasiasa hasa wa Upinzani ambao
wanautaka sana Uenyekiti wa POAC na wanafanya kila njia kutaka kuidhoofisha.
Lakini hawajui kuwa anaepanga wajumbe wa Kamati ni Spika wa Bunge.
6.
Msishangae pia kuja baadae kubaini kwamba baadhi ya wanasiasa
wenye midomo mikubwa ya kutuhumu wenzao wao ndio vinara wa kupokea rushwa.
7.
Ni lazima tufike mahali kama viongozi kwamba utaratibu
unapokiukwa na yeyote yule, au uongo unapotolewa hadharani tuseme bila kuogopa.
Hili ndio jukumu letu kama wabunge na viongozi. Kusimamia ufuatiliaji wa
utaratibu ni jukumu letu kama Kamati ya POAC na ndio sababu ya msingi ya kuanzishwa
kwa mamlaka kama CAG na PPRA. Haiwezekani, tuwe na set ya kanuni kwa kundi
fulani na nyingine kwa makundi mengine, au kuhukumu ufuataji wa taratibu kwa
kuangalia sura ya mtu usoni
Mwisho
Kumejengeka tabia
hivi sasa ya kuwamaliza wanasiasa wenye kudai uwajibikaji na uzalendo.
Kumeanzishwa kiwanda kwenye medani ya siasa cha kuzalisha majungu na fitna
zenye lengo la kuwachonganisha wanasiasa wa aina hiyo na wananchi kwa kutumia
vyombo vya habari na nguvu ya fedha. Naamini mbinu hizi chafu, kama nyingine
nyingi zilizojaribiwa kwangu huko nyuma nazo zitashindwa.
Naamini katika
kweli na kweli daima huniweka huru. Naamini kuwa mwale mdogo wa mwanga wa
mshumaa hufukuza kiza. Kwa imani hiyo, sitasalimu amri mbele ya dhamira zao ovu
hata nitakapobaki peke yangu katika mapambano hayo ya kulinda na kutetea
rasilimali za taifa zinufaishe watanzania wote.
Daima nitaongozwa
na busara ya Hayati Shabaan Robert isemayo, ‘Msema kweli huchukiwa na marafiki
zake, nitakapofikwa na ajali hiyo, sitaona wivu juu ya wale wawezao kudumu na
marafiki zao siku zote, siwezi kuikana kweli kwa kuchelea upweke wa kitambo,
nikajitenga na furaha ya kweli itakayotokea pale uwongo utakapojitenga”.
Ahsanteni sana.
|
|
COMMENTS