TAARIFA KWA UMMA Leo tarehe 03 Agosti 2012 kwa mujibu wa Kanuni ya 68 (7) ya Kanuni za Kudumu za Bunge na kwa kuzingatia kuwa marekebish...
TAARIFA
KWA UMMA
Leo tarehe 03 Agosti 2012 kwa mujibu
wa Kanuni ya 68 (7) ya Kanuni za Kudumu za Bunge na kwa kuzingatia kuwa
marekebisho yamefanyika kwenye ratiba ya bunge ambapo Mkutano wa Bunge sasa
umepangwa kuahirishwa tarehe 16 Agosti 2012 na hoja za wabunge zimeondolewa
kwenye ratiba.
Nimeomba muongozo ama Serikali
itoe kauli bungeni ya kutengua tangazo lililotolewa na Mamlaka ya Usimamizi na
Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii (SSRA) ili kuwezesha mafao ya kujitoa
kuendelea kutolewa au uongozi wa Bunge uruhusu niwasilishe muswada binafsi wa
sheria kwa hati ya dharura tarehe 16 Agosti 2012 kwa ajili ya kufanya
marekebisho kwenye sheria husika ili kuruhusu mafao ya kujitoa kuendelea
kutolewa.
Pamoja na hatua hiyo ya kuomba
muongozo nimechukua hatua ya ziada ya kumwandikia Katibu wa Bunge kumweleza
kusudio la kuwasilisha Muswada Binafsi wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya
Sheria za Hifadhi ya Jamii (The Social Security Laws (Ammendments) Act wa mwaka
2012 kwa hati ya dharura kwa mujibu wa Kanuni ya 81 ya Kanuni za Kudumu za
Bunge (Toleo la Mwaka 2007).
Lengo la Muswada huo ni kufanya
marekebisho yenye kuwezesha kurejeshwa kwa fao la kujitoa (withdrawal benefits)
ili kuruhusu kuendelea kutolewa kwa mafao kwa mwanachama wa mfuko ya hifadhi ya
jamii anapoacha kazi na kuhitaji kupewa mafao yake kabla ya kufikisha umri wa
kustaafu kwa hiari (miaka 55) au kwa lazima (miaka 60) au pale anapopata
ulemavu wa kudumu.
Nimeomba kupatiwa ushauri na
usaidizi wa kisheria kwa mujibu wa Kanuni ya 21 (1) (d), (e) na (2) ili kuweza
kuandaa Muswada Binafsi wa Sheria kwa mujibu wa Kanuni ya 81 (1), Taarifa ya
Muswada huo kwa mujibu wa Kanuni ya 81 (2), hati ya kuwasilisha muswada kwa
dharura na hoja ya kutengua masharti kuhusu muda wa utangazaji wa Miswada ya
Sheria kwa mujibu wa Kanuni ya 81 (5) ya Kanuni za Kudumu za Bunge (Toleo la
Mwaka 2007).
Kwa mujibu wa Kanuni ya 81 (5)
masharti kuhusu muda wa utangazaji wa Miswada ya Sheria yanaweza kuwekwa kando
na kutenguliwa kwa hoja kutolewa na kuamuliwa kama kutawasilishwa Bungeni hati
iliyowekwa saini na theluthi mbili ya Wajumbe wote wa Kamati kama ni Muswada wa
Kamati na kwa Muswada wa Mbunge hati iliyowekwa saini na Wabunge wasiopungua
kumi inayoeleza kuwa muswada binafsi uliotajwa katika hati hiyo ni wa dharura.
Naomba kutoa taarifa kwamba
kuanzia jumatatu tarehe 6 Agosti 2012 nitaanza kukusanya saini za wabunge
wanaounga mkono kuwasilishwa kwa muswada tajwa kwa hati ya dharura kufanya haraka marekebisho yenye kuwezesha kurejeshwa
kwa fao la kujitoa (withdrawal benefits) ili kuruhusu kuendelea kutolewa kwa
mafao kwa mwanachama wa mfuko ya hifadhi ya jamii.
Nimeomba pia kwa Katibu wa Bunge
kwa mujibu kifungu cha 10 cha Sheria ya ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge Cap
296 R.E 2002 kupatiwa nakala ya taarifa na nyaraka zifuatazo kwa ajili ya
kujiandaa kuwasilisha muswada husika: Social Security Ammendment Act no.5 ya
mwaka 2012, Sheria za Hifadhi ya Jamii zinazohusika, Taarifa na mapendekezo
yaliyowasilishwa na kupelekea kufutwa kwa mafao ya kujitoa (withdrawal
benefits) na maelezo kuhusu hatua ambayo kifungu husika kiliingizwa na hatimaye
kupitishwa na Bunge tarehe 13 Aprili 2012.
Pamoja na kuomba taarifa na
nyaraka kupitia kwa Katibu wa Bunge natoa mwito kwa wadau wa mifuko ya hifadhi
ya jamii kutunipatia maoni na mapendekezo kwa ya kuzingatiwa kwenye Muswada
Binafsi wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Sheria za Hifadhi ya Jamii (The
Social Security Laws (Ammendments) Act wa mwaka 2012 katika kipindi cha wiki
moja.
Ikumbukwe kwamba kifungu cha
kufuta mafao ya kujitoa kilichozua mgogoro hakikuwepo wakati muswada uliposomwa
kwa mara ya kwanza bungeni tarehe 1 Februari 2012 bali kiliwasilishwa kupitia
jedwali la marekebisho ya Wizara lililowasilishwa tarehe 13 Aprili 2012 bila
malengo na madhumuni yake kuelezwa kwa ukamilifu.
Kupitishwa kwa kifungu hicho
kumethibitisha maneno niliyoyatoa bungeni kuwa tumefika hapa tulipo kutokana na
‘uzembe wa bunge na wabunge’ na kwa hili pamoja na mchango nilioutoa bungeni
kwa maandishi siku hiyo juu ya haja ya kuwa mfumo mpana zaidi wa pensheni na
hifadhi ya jamii (universal pension and social security) pamoja na kuwa
sikuunga mkono kifungu husika kilichoingizwa kinyemela naomba radhi kwa
wananchi wa Ubungo na wafanyakazi kwa kutokuwasilisha jedwali la marekebisho
kupinga kifungu hicho kuingizwa.
Izingatiwe kuwa ili kurekebisha
hali hiyo tarehe 27 Julai 2012 kwa nafasi yangu ya Waziri Kivuli wa Nishati na
Madini kwa niaba ya Kambi Rasmi ya Upinzani niliitaka Serikali itoe maelezo
maelezo kuhusu taarifa zilizotolewa bungeni tarehe 13 Aprili 2012 kuwa
wafanyakazi ikiwemo wa migodini kupitia vyama vyao walihusishwa kutoa maoni
yaliyopelekea kufutwa kwa fao la kujitoa (withdrawal benefits); suala ambalo
Chama Cha Wafanyakazi wa Migodini (TAMICO) kililikanusha.
Hata hivyo, Waziri wa Nishati na
Madini wakati wa majumuisho ya Hotuba yake tarehe 28 Julai 2012 hakutoa majibu
yoyote bungeni kuhusu suala hilo hali ambayo imesababisha migongano kuendelea
katika migodi mbalimbali kuhusu madai hayo hali ambayo kwa taarifa nilizozipata
tarehe 1 na 2 Agosti 2012 inaweza kusababisha migomo migodini. Kufutwa kwa fao
la kujitoa kumelalamikiwa pia na wafanyakazi na wadau wa hifadhi ya jamii
katika Jimbo la Ubungo na katika taifa kwa ujumla.
Hata hivyo, suala hili na tukio
husika litumike kama rejea ya bunge na wabunge kuikatalia Serikali kuwasilisha
marekebisho yenye athari kubwa kipindi cha mwisho na hivyo wabunge kukosa fursa
ya kupata maoni ya wananchi na pia Serikali itakiwe kuomba radhi kufuatia
kulipotosha bunge kuwa wadau wa hifadhi ya jamii hususan wafanyakazi na vyama
vyao walishirikishwa na kuridhia wakati ambapo wamejitokeza na kukanusha madai
hayo yaliyotolewa na Wizara bungeni.
Kwa upande mwingine kufutwa kwa
mafao ya kujitoa msingi wake haupo kwenye marekebisho ya sheria yaliyofanyika
tarehe 13 Aprili 2012 pekee bali ni udhaifu katika mfumo mzima wa kisera na
kisheria wa hifadhi ya jamii nchini hali ambayo inahitaji wadau kutaka
mabadiliko makubwa.
Hivyo, naungana na wote wenye
kutaka Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii (SSRA)
kutengua taarifa kwa umma iliyotolewa ya kueleza kuwa “kufuatia kuanza kutumika
kwa Sheria hiyo (ya 13 Aprili 2012) maombi mapya ya kujitoa yamesitishwa kwa
kipindi cha miezi sita hadi pale miongozo itakapotolewa ili kuwezesha Mamlaka
na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kutoa elimu kwa Wadau”.
Aidha, pamoja na Mamlaka kueleza
kwamba sitisho la fao la kujitoa si kwa
sababu za Kiserikali au Mifuko kufilisika ni vizuri mamlaka ikaeleza kwa uwazi
na ukweli sababu zingine za kufanyika kwa marekebisho hayo zaidi ya ile ya
kutimiza malengo ya Hifadhi ya Jamii ambayo ni kuhakikisha kuwa Mwanachama
anapostaafu anapata mafao bora yatakayomwezesha kumudu hali ya maisha ya
uzeeni. Tahadhari za Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) katika taarifa za
Hesabu za mwaka 2010/2011 na miaka mingine zinaashiria masuala ya ziada ambayo
yanaweza kuwa yameisukuma Serikali kuja na mbinu zingine za kuhakikisha
uendelevu wa mifuko ikiwemo kupitia marekebisho ya sheria za hifadhi ya jamii.
Ili bunge liweze kutimiza wajibu
wa kuishauri na kuisimamia serikali kufanya marekebisho yanayostahili ya sheria
husika kwa haraka ni muhimu ratiba ya bunge ikabadilishwa.
Tafsiri ya marekebisho ya ratiba yaliyofanyika ni kuwa hoja binafsi
niliyoiwasilisha kwa katibu wa Bunge kutaka bunge lijadili na kupitisha
maazimio ya hatua za haraka za kuboresha upatikanaji wa majisafi na
ushughulikiaji wa majitaka haitapata nafasi ya kujadiliwa bungeni. Aidha ratiba
hiyo mpya hoja binafsi iliyoelezwa kuwa itawasilishwa na Mbunge wa Kisarawe
Seleman Jafo kuhusu kufutwa kwa mafao ya kujitoa kufuatia marekebisho ya sheria
za Hifadhi za Jamii nayo haitawasilishwa kwenye mkutano huu wa Bunge
unaoendelea kama ratiba haitafanyiwa marekebisho.
Hata hivyo, izingatiwe kuwa
chanzo cha kufutwa kwa mafao ya kujitoa ni marekebisho ya sheria za hifadhi ya
jamii hivyo ufumbuzi wa kurejesha fao la kujitoa unapaswa kuwa ni marekebisho
ya sheria hatua ambayo njia ya haraka ya kuifikia ni kuwasilishwa kwa muswada
wa sheria ama na serikali au kamati au mbunge badala ya hoja binafsi.
Hoja binafsi inaweza kuwezesha
bunge kujadili na kupitisha maazimio ya kuitaka Serikali kuwasilisha
marekebisho ya sheria au kuishauri na kuisimamia serikali na mamlaka zake
katika utekelezaji wa sheria lakini sheria itaendelea kuwa palepale mpaka
marekebisho yatakapofanywa kwa kuwasilishwa muswada wa sheria hatua ambayo
nimeamua kuanzisha mchakato wa kuwezesha ichukuliwe.
Wenu katika kuwawakilisha
wananchi,
John Mnyika (Mb)
03/08/2012
Bungeni-Dodoma
COMMENTS