JUUYA MUUNGANO:
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Nimeshitushwa
na gazeti moja la kila siku (Tanzania
Daima la tarehe7 Agosti 2012) lilonipandikizia maneno katika kichwa chake cha
habari kwamba ‘Shivji, Lwaitama wataka Muungano uvunjwe’. Siwezi nikamsemea Dr.
Lwaitama lakini kwa upande wangu sijasema wala kumaanisha kwamba ‘Muungano
uvunjwe’.
Nikitoa
mchango wangu baada ya mada mbili kuwasilishwa na Prof. Abdul Sheriff na Dr. Azaveli Lwaitama, nilisisitiza mambo haya
matatu ya msingi.
Mosi, kwamba
wasomi, wakiwemo wanahabari, wana jukumu zito la kutokupinda ukweli wa kihistoria kwa lengo la kuhalalisha
mtazamo na msimamo wao kuhusu Muungano.
Nikatoa mfano wa jinsi Merehemu Sheikh Karume anavyodekezwa katika msimamo wake juu ya Muungano. Wasemaji
hapa bara wanamsifu kwa kuwa muasisi
mwaminifu na mshabiki mkubwa wa Muungano tangu mwanzo. Huko Zanzibar, wasemaji hawachoki kumnukuu Mzee
Karume kuwa tangu mwanzo yeye hakutaka
Muungano isipokuwa alikuwa anafikiria Shirikisho.
Wanaendelea
kusema kwamba aliposaini Mkataba wa Muungano, Mzee Karume alifikiri kwamba
anasaini Shirikisho la Serikali tatu, lakini kutokana na kiwango cha elimu yake hakuelewa vizuri mantiki na maana
ya alichokuwa anasaini.
Nikaendelea
kueleza kwamba maelezo haya yote mawili hayaungwi mkono na ushahidi wa
kihistoria. Ukweli ni kwamba, Mzee Karume aliingia katika Muungano kutokana na
hesabu zake mwenyewe za kisiasa. Muungano kwake ulikuwa njia ya kuondoa
upinzani, au upinzani tarajiwa, wa utawala wake. Yaani ilikuwa ni tendo la mwanasiasa
yeyote yule kudumisha utawala wake (political survival).
Na kwa
watawala wote wa Zanzibar waliomfuata, wakiwemo wa upinzani, ndivyo ilivyokuwa.
Wamekuwa wakitumia mwavuli wa muungano wakati utawala wao uko hatarini na
kushawishi wananchi wao dhidi ya muungano wakitafuta umaarufu wa kisiasa.
Nikitoa
mfano nikasema kwamba kuna taarifa kwamba chama kimoja huko Zanzibar
kinapandikiza pendekezo la ‘muungano wa mkataba, sio wa katiba’ bila ya kueleza
waziwazi maana yake. Ukweli ni kwamba huwezi ukawa na muungano wa mkataba bila
kwanza kuuvunja muungano. Kwa hivyo, wanachoshawishi moja kwa moja ni kuuvunja
muungano. Basi waseme hivyo badala ya kujificha nyuma ya pazia la ‘muungano wa
mkataba’.
Jambo la
pili nililorudia ni kwamba tuliangalie suala zima la muungano kwa mtazamo na
maslahi na matakwa ya Umma wa Zanzibar na Umma wa Tanzania bara, hususan matabaka
ya hali ya chini. Katika hali yao kimaisha – kiuchumi na kisiasa – hakuna
tofauti kati ya wananchi wa Zanzibar na wananchi wa Tanzania bara. Uduni wa
hali yao ni uleule; ukosefu wa ajira ni uleule; kutokuwa na mfumo wa dhati wa
demokrasia unaojali walalahoi ni kulekule.
Kwa hivyo,
umuhimu kwao ni mshikamano wao kuboresha mifumo ya uchumi na siasa. Wasiburuzwe
na wanasiasa na vyama vyao kwa maslahi yao binafsi ya muda mfupi ya kudumisha, au kuingia kwenye,
utawala.
Jambo la
mwisho nililogusia ni kwamba kiini cha suala la muungano si idadi ya serikali
(mbili au tatu) bali ni mgawanyo wa madaraka (distribution of power) kati ya dola la Zanzibar na dola la Muungano. Na
katika hili kila muungano duniani ni wa kipekee kutokana na hali halisi yao ya
kihistoria na uwiano wa kisiasa. Sisi pia tukiwashirikisha wananchi kikamilifu
na tukaelewa vizuri matakwa yao tunaweza kubuni muundo wetu wa muungao ambao ni
wa kipekee bila kujali idadi ya serikali.
Nimeona
niweke wazi mtazamo wangu kwa sababu ya baadhi ya vyombo vya habari kuwa na
hulka ya kupotosha mambo kutokana na ushabiki wao bila kujali madhara yanayoweza kutokea.
Mwishoni
ningependa kusema kwa dhati kwamba uvunjaji wa muungano hauwezi kuwa kwa
manufaa ya walio wengi. Ukweli ni kwamba unaweza ukasambaratisha nchi na jamii zetu pande zote mbili za
muungano. Tukianza kubaguana kati ya Watanganyika na Wazanzibari, tutaendelea
kubaguana kwa msingi wa Uislamu na Ukristo,
na Usukuma na Uchaga, Uarabu na Uafrika, weusi na weupe bila kikomo.
Kama alivyosema
Mwalimu, ukishaonja nyama ya mtu basi utaendelea kumtafuna.
Issa Shivji
Profesa wa
Kigoda cha Mwalimu Nyerere,
Chuo Kikuu
cha Dar es Salaam.
Agosti 8,
2012








0 comments:
Post a Comment