UNAPENDWA NA KUOGOPWA NA WATU WENGI DUNIANI UKO HATARINI KUPOTEZA ASILI YAKE KABISA Masumbiwi au kwa majina mwengine ndondi au ...
UNAPENDWA NA KUOGOPWA
NA WATU WENGI DUNIANI
UKO HATARINI KUPOTEZA
ASILI YAKE KABISA
Masumbiwi au kwa majina mwengine ndondi au ngumi na kwa majina ya
mitaani ndogwa, mawe n.k. ni mchezo unapoendwa sana na watu wengi. Aidha mchezo
huu ni kati ya michezo inayoogopwa sana duniani. Mchezo wa ngumi uko hatarini
kupoteza maana yake ya asili yaani kucheza kama burudani, kuwakilisha nchi na
kujenga ushupavu wa mchezaji. Mamilioni ya watu wanaojazana kuutazama
wasingependa kabisa kujiingiza kuucheza mchezo wa ngumi.
Japokuwa katika maisha ya kawaida watu wengi hupigana kwa sababu
mbalimbali kama vile kuwa na hasira, kujilinda au kuwaonea tu wengine kwa
sababu mbalimbali lakini kwa kawaida ni watu wachache sana walio tayari
kujiingiza katika kuucheza mchezo huu.
Kama tulivyokwisha ona kwenye makala zilizotangulia, ngumi ni mchezo
ambao ulianza wakati wanadamu walipoanza tu kukunja ngumi na kurushina kama
mchezo. Mchezo wa ngumi upo wa aina mbalimbali.
Japokuwa kumbukumbu nyingi zinaonyesha kwamba chimbuko haswa la mchezo
huu linakubalika kuwa ni nchi za kusini mwa Ulaya hususan Uyunani (leo Ugiriki)
na Urumi (Italia ya leo) lakini kuna mataifa au dola nyingine nyingi zilizokuwa
na aina yao ya michezo iliyofanana na ngumi. Wanazuoni wa maswala ya
michezo wanaifananisha michezo yote ya kupigana iwe ni kwa kutumia mikono na
miguu au kutumia silaha za aina mbalimbali na mchezo wa ngumi.
Aidha mchezo wa ngumi ni kati ya michezo inayojenga ushupavu wa
wachezaji na kuwafanya washujaa wa jamii. Wachezaji wa ngumi mara nyingi ni
watu wanaoonekana kama mashujaa kutokana na ujasiri wanaoonyesha katika mchezo
wenyewe.
Wakati wa utawala wa Marcus Aurelius, mtawala shupavu wa iliyokuwa dola
ya Roma (Italia ya leo) na aliyepata mafanikio makubwa ya kuipanua dola ya
Warumi (Italia) toka ukanda wa bahari ya Mediterania hadi jangwa la barafu la
Siberia huko Urusi, mashujaa wengi wa michezo walichuana kwenye mashindano
yaliyofanyika Coliseum (uwanja mkubwa uliokuwa umejengwa katika jiji la
Roma).
Mashujaa hawa ni pamoja na wapiganaji ngumi na wengine walioshiriki
kwenye michezo yenye hatari na kujijengea umaarufu mkubwa kwenye jamii ya
Warumi. Dola ya Warumi ilikuwa na nguvu sana katika bara la Ulaya na ilienea
hadi kaskazini mwa bara la Afrika. Hivyo utamaduni wao hususan michezo
iliyochezwa baada ya ushindi wa vita ulienea kwenye himaya yao yote.
Kwa mfano katika dola ya Manchuria (China ya leo) iliyotawala kutoka
Uchina na nchi nyingi za mashariki ya kusini mwa Asia ngumi zilijulikana kama
Kung-Fu ambazo japokuwa kuchezwa kwa ngumi hizi huchanganywa na mateke.
Maaskari wengi walitakiwa wawe wamejifunza kupigana Kung Fu na waujue
mchezo wenyewe kwa kiwango kikubwa. Kwao Kung Fu ilikuwa ni aina nyingine ya
silaha na walizitumia ipasavyo kwenye kukabiliana na maadui kwenye vita.
Baada ya ushindi wa vita walikusanyika katika viwanja vikubwa na kucheza michezo
hii kama isahara ya kusheherekea ushindi wao.
Dola ya Kijapani iliyotawala nchi nyingi za Asia ikiwa ni mpinzani
mkubwa wa dola ya Manchuria katika karne ya 12 nayo ilikuwa na mchezo wa ngumi
uliojulikana kama Karate. Mashujaa wengi wa Kijapani walitakiwa wawe na ujasiri
wa hali ya juu wa kupigana Karate.
Kwao Karate ilikuwa sio mchezo tu bali ni ufundi wa kumshinda adui
kwenye vita. Ushindani mkubwa kati ya Wachina na Wajapani uliifanya michezo ya
Karate na Kung Fu kupata umaarufu mkubwa sana. Kila upande uliuona mchezo wake
kama bora kuliko mwingine.
Katika miaka ya karibuni watawa wengi katika ukanda huu wanaojulikana
kama Monks (monki) waiijifunza Karate na Kung Fu kwa kiwango cha juu ili
kujilinda na Maharamia waliokuwa wanawavamia na kuiba mali zao.
Mtawala Genghis Khan wa dola ya Mongolia (Mongol Empire) ambayo
ilitawala kuanzia Mongolia yenyewe hadi Persia (Irani), Babilon (Iraki) na
baadhi ya nchi za Balkan (Ulaya ya Kati) aliwachagua wapiganaji wake kwa ustadi
na uangalifu mkubwa. Kwa kutumia wapiganaji waliosheheni kila aina ya ushupavu
aliweza kushinda majeshi mengi na kuwa kati ya watawala walioogopewa sana
wakati wa enzi yake.
Dola
ya Otoman ya Kituruki iliyotawala katika karne ya 19 ilitumia mchezo
ulioulikana sana na wengi kama Mieleka ukichanganya na utumiaji wa farasi. Mara
nyingi wachezaji wa mchezo huu walifariki kutokana na ugumu wa mchezo wenyewe
na watanzamaji walisisimka sana kuona damu ikimwagika. Kwao huu ulikuwa ndio
ushujaa tosha.
Nazo dola za Mafarao wa Misri zilikuwa na aina yao ya michezo iliochezwa
haswa na watumwa kwa minajili ya kuwafurahisha Mafarao na familia zao hata
katika kujitetea au kushambulia maaduni! Kwa dhati kabisa mchezo wa ngumi
ulivyojulikana na Wanafalsafa wa zamani katika ukanda wa Mediterania katika
dola nilizotaja hapo juu ulikuwa ni mojawapo ya vipimo vya ujasiri wa mtu.
Sio
vibaya watanzania wakaelewa kuwa ngumi ni mchezo wa zamani sana kuchezwa hata
kabla nchi yetu haijatawaliwa na wakoloni katika karne ya 19. Michezo hii
iliyochezwa katika viwanja vikubwa vyenye mikusanyiko mikubwa ya watu
(Coliseum) huko Roma na (Arena) huko Athina, iliyokuwa katika hekalu kubwa la
ufalme wa Wayunani (Ugiriki) la Akropolis.
Viwanja hivi vilikuwa ndio mwanzo wa ulingo wa kisasa kwani japokuwa
ulingo wa kisasa ni wa mraba lakini mwanzo wake ni Arena ya mduara.
Mwandishi wa makala
haya Onesmo Ngowi ni: Rais wa Kamisheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania (TPBC), Shirkisho la
Ngumi za Kulipwa Afrika Mashariki na Kati (ECAPBF), Shirikisho la Ngumi la
Kimataifa bara la Afrika (IBF/AFRICA) na Mkurugenzi wa Baraza la Ngumi la
Jumuiya ya Madola (CBC). E-mail: ibfafrica@yahoo.cm
COMMENTS