Jana tarehe 6 Septemba 2012 Mahakama Kuu Kanda ya Dar es salaam imetupa ombi la Shirika la Umeme (TANESCO) lililokuwa linaomba mahakama ...
Jana tarehe 6 Septemba 2012
Mahakama Kuu Kanda ya Dar es salaam imetupa ombi la Shirika la Umeme (TANESCO)
lililokuwa linaomba mahakama itoe amri ya kuzuia utekelezwaji wa ukazaji wa
hukumu ya mahakama hiyo iliyoruhusu tuzo ya dola 65,812,630.03 za Marekani
iliyotolewa na Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi wa Migogoro ya Kibiashara
(ICC) mwaka 2010 kwa kampuni ya Dowans Holding SA (Costa Rica), sasa Dowans
Tanzania Ltd isisajiliwe nchini.
Kufuatia huku hiyo nimetakiwa
kutoa maoni yangu maoni kwa nafasi yangu ya
Waziri Kivuli wa Nishati na Madini na pia mbunge wa jimbo la Ubungo ilipokuwepo Richmond, mitambo ya Dowans na
sasa Symbions ambapo pia yapo makao makuu ya TANESCO.
Hivyo, serikali isitumie
kizingizio cha maamuzi ya jana
kuharakisha mpango wa kuilipa kulipa Dowans kwa fedha za walipa kodi watanzania
au kubebesha mzigo huo kwa wateja wa TANESCO na iwapo Serikali inayoongozwa na
Rais Jakaya Kikwete imezidiwa na Dowans kwa sababu ya kujiingiza katika
mikataba mibovu inapaswa kuwabebesha deni hilo wazembe, mafisadi na waliokuwa
wakihujumiana ndani ya Serikali waliosababisha hali hiyo.
Badala yake Serikali kupitia
Waziri wa Nishati na Madini Prof. Sospeter Muhongo anapaswa kueleza ni hatua
gani ilichukua kutoka TANESCO ilipowasilisha mahakama ya rufani taarifa ya
kusudio la kupinga hukumu iliyotolewa na Jaji Emilian Mushi Septemba 28 mwaka
2011 iliyoruhusu tuzo hiyo isajiliwe.
Aidha, Mwanasheria Mkuu wa
Serikali aeleze ni kiasi cha fedha kilichotumika kwenye kuendesha kesi za
Dowans, na IPTL mpaka sasa na hatua zilizochukuliwa dhidi ya mawakili wa
TANESCO na makampuni binafsi yanayotuhumiwa kusababisha mzigo mkubwa wa gharama
za kesi ambazo serikali inashindwa kwa nyakati mbalimbali.
Ni muhimu umma ukafahamu kuwa kwa
mwaka wa fedha 2011/2012 pekee jumla ya shilingi bilioni 10 zimetumika kwa
ajili ya gharama za kuendesha kesi hizo kwa kuilipa
kampuni ya Rex Attorneys na
Makampuni mengine ambayo kwa nyakati mbalimbali yamekuwa yakiiwakilisha
serikali na TANESCO na kushindwa katika mahakama za kitaifa na kimataifa.
Hukumu ya jana inapaswa kuibua
tena mjadala uliodumu kwa miaka minne kuanzia mwaka 2008 tangu yalipopitishwa maazimio 23 ya Bunge juu
ya Mkataba baina ya TANESCO na Kampuni ya Richmond Development Company LLC
ikiwemo kuhusu mkataba na Dowans.
Uamuzi huu wa mahakama unaibua
mjadala mwingine kuhusu uwezo na dhamira ya wanasheria wa Serikali na TANESCO
katika kesi hizi kwa kuzingatia mtiririko mzima wa masuala na matukio katika
majadiliano ya mkataba wa Richmond na hatimaye Dowans kati ya mwaka 2006 mpaka
2012.
Katika mazingira haya namtaka
Waziri wa Nishati na Madini Prof Muhongo kueleza kwa umma mabilioni mangapi
yamelipwa na TANESCO mpaka hivi sasa kwa kampuni hiyo na nyingine na sababu za
kuendelea kuilipa kampuni hiyo pamoja na kuwepo kwa uzembe wa wazi wenye
kulisababishia hasara taifa.
Umma uzingatie kwamba gharama
kama hizi za Dowans na mikataba mingine mibovu ndizo zinazoongeza mzigo wa
gharama za uendeshaji za TANESCO na kuchangia katika ongezeko la bei ya umeme
na ongezeko la gharama za maisha kwa ujumla.
Maelezo haya ni muhimu yakatolewa
na Serikali kwa kina badala ya kuendelea kutoa kauli za ujumla bila kuchukua
hatua za kusafisha safu yake ya kisheria ambayo imeingiza TANESCO katika
mikataba mibovu na madeni makubwa.
Ikumbukwe pia kwamba iwapo hoja
binafsi niliyoiwasilisha ofisi ya bunge mwaka 2011 kutaka utekelezaji wa
maazimio yote yaliyobaki kuhusu mkataba kati ya TANESCO na Richmond Development
Company LLC ingejadiliwa bungeni, hatua zaidi zingechukuliwa kwa mafisadi na
wahujumu uchumi waliohusika na Richmond, Dowans na masuala mengine ya kisheria
yanayosababisha mzigo mkubwa kwa TANESCO na wananchi.
Kutokana na rekodi za maamuzi
mbalimbali ya kimahakama kuanzia mwaka 2010 mpaka 2012 sasa inajulikana wazi
kuwa Mkataba wa TANESCO na Richmond ulirithishwa kinyemela Oktoba 14, 2006
kwenda kwa Dowans huo kama inavyoononekana katika nyaraka za mahakama ambapo
Dowans na Richmond zinadaiana huko Marekani; na kwa kuwa hilo lilifanyika bila
kuitaarifu TANESCO kinyume na kifungu cha 15.12 cha Mkataba huo.
Kutokana na hukumu ya Dowans
ushahidi umepatikana na kuwa mashahidi mbalimbali walioitwa mbele ya Kamati
Teule ya Bunge na wakiwa chini ya kiapo walitoa taarifa za uongo kuwa mkataba
kati ya Richmond na TANESCO ulihamishwa kwenda Dowans Disemba 23, 2006 na hivyo
wahusika hao mbalimbali – wakiwemo wamiliki wa Richmond; walidanganya au
kuficha ukweli mbele ya Kamati Teule na hivyo kuonesha dharau dhidi ya Bunge.
Hata Hivyo, masuala hayo hayawezi
kujadiliwa bungeni mpaka kwanza mjadala husika uweze kufunguliwa; hivyo hoja
binafsi niliyowasilisha ililenga kutaka uamuzi kubadilishwa na mjadala
kufunguliwa ili kuongeza msukumo wa utekelezaji wa maazimio ya bunge na hivyo
kuchangia katika mapitio ya mikataba yenye kuongeza mzigo wa gharama kwa watanzania; kuweka mfumo wa kulihusisha bunge katika
maandalizi ya mikataba mikubwa yenye maslahi ya taifa na kuwezesha uwajibikaji
na hatua kamili kuchukuliwa kwa waliohusika na ufisadi na uzembe
uliolisababishia hasara taifa.
Kufichwa kwa taarifa hizo muhimu
ndiko kulichangia kukubaliwa kwa kampuni ya Dowans kuchukua Mkataba wa
Richmond; wakati tayari ilikuwa imerithishwa kinyume cha mkataba wenyewe hivyo
kuliingiza taifa katika deni kubwa ambalo serikali ilionyesha dhamira ya kutaka
kulilipa kinyemela na linataka kugeuzwa kuwa
mzigo mkubwa migongoni mwa walipa kodi wa Tanzania katika utekelezaji wa
maamuzi ya mahakama.
Hoja yangu pamoja na mambo
mengine ingependekeza bunge kuazimia
kuweka muda usiopungua miezi mitatu kwa serikali kutekeleza Maazimio yote ya
Bunge yaliyokuwa yamesalia katika sakata hili la Richmond ili mara moja na
daima sakata hili la Richmond na Dowans limalizwe na kufungwa baada ya
kutekeleza maazimio yote.
Haiwezekani taifa likawa kila
wakati kwenye mjadala wa Richmond na Dowans; hali ambayo imefanya kwamba hata
katika utekelezaji wa mpango wa dharura wa umeme unaouhusisha pia kampuni ya
Symbion iliyonunua mitambo ya Dowans mianya imeachwa ambayo inaweza
ikasababisha kesi zingine kama za IPTL, Richmond, Dowans iwapo hatua za haraka
hazitachukuliwa kuepusha hali hiyo.
John
Mnyika (Mb)
Waziri
Kivuli wa Nishati na Madini
07/09/2012
COMMENTS