. Mama moyo wangu! yaani mashaka na hofu barabarani,msituni .Dereva macho pima, abiria mapenzi, kinywaji,kuchimba dawa .Kondakta gari...
.Mama moyo wangu! yaani mashaka na hofu barabarani,msituni
.Dereva macho pima, abiria mapenzi, kinywaji,kuchimba dawa
.Kondakta gari halijai si ndoo ya maji,sogea kule,ukiwa mzee
balaa
NIMETUMIA takribani saa 37 kutoka Dar es salaam na kufika katika
makao makuu ya mkoa wa Katavi, mji unaonekana kubadilika kwa kasi wa
Mpanda.Na ninachoandika hapa si hadithi ya kubuni ni ukweli nikichukua muda
hadi muda.
Majira ni saa kumi na nusu alfajiri,naamshwa na watoto, nisije
nikachelewa kwani basi linaondoka saa moja kasoro robo na kwa utata wa usafiri
wa huku kwetu nikaapo, ni lazima ujihimu kidogo.Saa kumi na moja na dakika 15
naondoka nyumbani na dakika 25 baadaye nafika stendi ya kunipeleka Kimara,
hakuna basi , muda unaenda naamua kuchukua pikipiki.
Saa kumi na mbili na nusu ninafika Kimara, nasubiri basi
litakalonichukua hadi Mpanda kwa kupitia Mbeya na Sumbawanga, sikujua kwamba
nitalazimika kulala Mbeya; wenyewe waliniambia kwamba niwape 67,000 na
nitafikishwa Mpanda hawakunipa hadhari kwamba ni lazima nijitegemee kulala
Mbeya na tena nikifika Sumbawanga ni lazima niingie katika gari nyingine na
hivyo kuhamisha mizigo yangu.
Moja kasoro nikawapigia simu kwamba abiria wenu wa Kimara
nawasubiri,wakaniuliza gari la saa ngapi,nikawaambia la moja kasoro wakasema
linakuja wakanitajia gari namba 616 kwamba ndilo litakalonichukua kuelekea
Mpanda, mkoa mpya wa Katavi.
Wakati nashangaa kunataka kutokea nini pale kituoni , daladala
akabanana na basi ninalosafiria,akalambwa kioo nikasema ohoo ishakuwa nuksi
tena, manake hapa hamjatoka Dar, dereva kaonesha kutojua upana wa gari
lake.Nikalifuata pale nikaingia, wakamalizana tukaanza safari kuelekea Mpanda.
Mbezi tukachukua abiria mbele kidogo tukaanza mwendo. Basi
lilitakiwa kuwa lakshari, lakini haa, ndani utadhani halikaguliwi na Sumatra
manake viti hovyo, mikanda haipo na stuff carrier ilionekana kama inataka
kuachia japo ilitengenezwa kama yale ya kwenye ndege.
Mhh sikuwa pekee yangu aliyeshangaa, mtu aliyepanda Mbezi naye
alishangaa, wale waliokuwapo wakasema what kind of a car, ilikuwa kiinglish
lakini matamshi yake yalifanana na watu wanaotoka Zambia, Wanyanja wakijiuliza
ni aina gani ya gari wamo,kwani wanatazama mle ndani silo walilooneshwa jana
yake wakati wakikata tiketi linapiga madebe kwelikweli kwa ndani.
"Halafu konda hii bei ni ya lakshari kinywaji kipo? manake
basi lenyewe halielewekieleweki" alijibiwa kiinywaji kipo lakini he
Dar hadi Mbeya tulipewa kwa lazima Cocacola ya kwenye plastiki hawakuwa na
kinywaji kingine na wala maji hawakutoa.Walitupa kinywaji hiki kabla ya kuingia
Doma, mara tu baada ya kumaliza kuchimba dawa.
Mbali baada ya kuanza kupata mwendo tukaingia foleni ya Kibaha
na mbele ya Kibaha akapanda mama analalamika kwelikweli kaachwa na basi la
kampuni hiyo,kumbe asubuhi kampuni ile iliamua kukodisha basi bila taarifa kwa
watu wakajiendea tu.
Njiani jamaa anaovateki magari matatu manne na unajua barabara
ya Dar-Chalinze ilivyo, ikiwa na mibinuko ya ajabu, jamaa anazipangua
anaziweka, hapo roho inaanza kuwa mkononi, unashangaa umpigie Mpinga au nani
barabarani na namba walizosema wanaweka kwenye mabasi mle haipo, unakula
uchungu , mama moyo wangu! breki vuu, ghafla mnaingia kushoto. Mashaka barabara
ya lami.
Haya bora salama, Mungu anasaidia mnaacha miti ikirejea
nyuma na nyie mkisonga mbele mnaingia Morogoro, stendi ya Msamvu
unapumua,mnapakia abiria wengine, wanatoa chati kwa Sumatra na Polisi
wanaikagua wanaruhusu mnaingia barabarani tena mnaanza kuitafuta Mikumi, Mbele
kidogo kabla ya kufika Doma Kondakta anaelezea suala la kuchimba dawa.
Wazungu kama tisa hivi waliokuwa mle ndani hawakuelewa nini kinatokea.
" kuchimba dawa,” anashangaa .. "kuchimba ni to dig, dawa
medicine maana yake nini hasa" akajiuliza mtu aliyeonekana anajua
kiswahili zaidi ya wenzake walitaka maelezo.Watu (watumishi wa basi) hawakuzungumza
Kiinglish lakini walipoona, watu wanateremka waliteremka na wakabaini kwamba ni
suala la kujisaidia.
Unakumbuka maneno ya kuwepo na vyoo kwa ajili ya abiria
njiani , choo kile kinauwezo wa watu watatno, abiria sitini, wengine na wazungu
kadhaa waliingia msituni huku karibu na barabara kuna gulio la nyama.
Mnamaliza kuchimba dawa mnaingia , mnapita mbuga ya Mikumi na
spidi 110 wakati wenyewe wameweka matuta na kusema spidi inayofaa ni nusu yake,
unashangaa mkikutana na tembo itakuaje , ama tembo ama nyie.
Njiani sasa simulizi zinaanza zimeanzia katika suala la kuchimba
dawa. Masimulizi yanahama kushutumu serikali na matamko yake,wakaingia hapo
kuzungumzia urais na nia za akina fulani wakiwataja kwa majina kwamba wanawania
Urais huku wakiwa wagonjwa na wala hawawezi kabisa kuongoza taifa.
Siasa za kuanzia Morogoro hadi Comfort zilikuwa za wastani,
wakichamba elimu na kusifia namna watoto wanaojifunza Uganda walivyokuwa na
akili kuliko Tanzania kwa kuwa wanajua kupepeta Kiingereza.
"ahh kwa wale wa Uganda labda kiingereza lakini uchambuzi
na uelewa bure kabisa" niligeuka kutazama wanaozungumza nikagundua ni
vijana. Hawa walibishana kwelikweli manake walisema kwamba mfumo wa elimu
tanzania bado ni bomba mwingine akisema kwamba si kweli elimu ya Tanzania
imeoza watu wanajiumajiuma katika kujieleza.
Comfort, pale Kitonga tuliingia mapema,pamoja na ukweli kuwa eneo
limechakaa, hata akili za watu zimechakaa sana kwani wanauza bidhaa kama wapo
Mogadishu, aina moja bei ghali urafiki haupo, bure kabisa!
Mnamaliza mnaondoka, mtu na mkewe (vijana hao!) gari
limepiga mijihoni hawakusikia wala kuona na asali zikiwamiminika (si bure
wameona juzi hawa) tuko juu kelele mtindo mzima, bahati yao tulikuwa bado
kuingia barabara kuu na mzee moja akashtuka kiti kimoja hakina abiria.
"Mmeacha mtu na mkewe" anasema huku mtu mmoja
njiani mbele anapunga kwa nguvu kuashiria watu wanaokimbilia gari.Walipanda
hawana hata sura ya hasira wakaendelea na asali zao, hawa niliwapenda.
Kitonga ilipandishwa kama tambarare, siasa zikaelekea kwenye
shimo kubwa zaidi nani anafaa kuwa rais, wote wakawa wanajadiliana wagombea wa
CCM badala ya kuangalia na vyama vingine unasema kaazi kwelikweli.Ukimtazama
dereva, haongei na mtu anabadilisha gia,anakanyaga mafuta huku mguu upo kwenye
breki kama anaibia vile, staili ngumu zaidi. Kwa mwendo ule lazima awe macho
pima.
Saa tatu mnaingia Mbeya, unadhani mnaendelea:"wale abiria
wa Mpanda na Sumbawanga tukiingia mjini mfike ofisini kwa maelezo, mshuke na
mizigo yenu"
Kweli tulifika maelezo ni kuwa uripoti saa kumi na moja na nusu
na basi linaondoka saa 12 kamili kuelekea Mpanda nba wale wa Sumbawanga
wakaambiwa saa mbili asubuhi. Wapi pa kulala, mzee sio ndege uko tranziti, wewe
tafuta gesti zipo nyingi la maana kesho uawahi.
Naam linakushuka,usiku wewe mgeni, unampa mtu buku anakutoa
kidogo stendi anakufikisha gesti inaitwa sinahela. Unalala, umechoka hata hujui
itakuwaje saa kumi na moja hiyo unaomba msaada wa kuamshwa na mlinzi. Unagusa
maji ya baridi, unauliza maji vipi unaletewa maji ya moto unaoga na fasta
unalala.
Wala huhitaji kuamshwa, kwani usingizi wenyewe unao?Anafika
kukugongea anakukuta wewe unatoka kuoga angalau uchangamke. Unasubiri
kupambazuke unauliza je salama anakuambia salama. unaondoka na kufika stendi.
Unauliza ofisini basi la kwenda Mpanda wanakuambia mngoje
mhusika. Mhusika haji unatoka nje unaenda katika magari unauliza la Mpanda
wanakuonesha unasema duhh hii kali unaingia kukaa katika kiti cha pembeni
aliyekaa kala kiti kimoja na nusu halafu unajiangalia mwenyewe.
pembeni mwako wapo watu na asubuhi ile wanazungumzia siasa,
masuala ya sensa na jinsi wengine walivyogomea sensa.
Siasa za kuanzia Mbeya kuelekea Mpanda zilikuwa ni ukali wa
Chadema,na kutokuwa wavumilivu. He mwenzio kama jamaa yangu na khanga yake ya
CCM kafua kaianika wanakuja watu wenye nyumba wanaanza nani kaweka balaa hili
atowe mara moja, khanga ile si ilikuwa na maji wakamlaimisha aiondoe pale.
"Jamani chadema sijui vipi yaani washari shari".
Tukaondoka kondakta akisema wazi hataki mtu wa kusimamisha huku
dereva akilalamikia upangaji mbaya wa mizigonutamletea taabu kwenye mizani.
Tuliondoka njiani kote hakuna kupandisha wala kuongeza tukapita mizani,
tukaingia Tunduma tulipoachana na Polisi wa Tunduma na kutokomea zaidi katika
barabara ya vumbi inayojengwa, basi lilikuwa halijai labda ndoo ya maji.
Akaingia mtu mzima akaona haina maana akaweka begi lake chini,
akalikalia konda akasema weee!!! wala bibi hakujibu, mdada mmoja akasema mhh
wazee hawa wana lao, jamaa anasema wala hamjibu anayetaka kupita aende nyuma
yake na apite tu, anagemesha bega lake pembeni umruke. Inayojaa ndoo ya maji si
basi.
Njiani wanapanda wawili, mvulana na msichana inaonekana
wanajuana. wanakimwaga cha nyumbani lakini mvulana akamuona demu mmoja rangi ya
chungwa amesimama, akamwambia binti aliyeingia naye aanzishwe swaga za mapenzi,
jamaa alisahau kwamba kibantu tunasikilizana kwa asilimia 50 nikafuatilia
maagizo.
Mapenzi yalinoga sana katika gari hili la Mbeya kwenda Mpanda.
Jamaa alikuwa tayari kumshusha Laela binti wa watu na kumpandisha gari kesho
yake, mtoto akamsikiliza akamtolea nje.Akasema anajeuri ya fedha alikuwa
anafika laela kununua spea ya pikipiki yake, kisha simu hiyo inayothibitisha
kwamba ni dereva wa pikipiki jamaa anatafuta usafiri akamwambia yupon garini
anaenda laela kutwaa spea ya waya wa eksereta umekatika.
Anamaliza anaendelea kumpelekea rapu za mapenzi msichana yule
hadi anafika Laela akitaka kumpa fedha za kushika:Nikasema watu wanahatari
humjui mtu katoka wapi unataka kushuka naye.
Masikio yangu yalikuwa na utamu mkubwa, huku mapenzi, huku
uongozi ujao na katiba huku mama mmoja akisema kwamba haoni sababu ya kupiga
kura,wengine wakisema ni wajibu wake kuchagua viongozi.. wewe wanakusaidia nini
au tuseme wameshakusaidia nini.
Masikio yangu yalinogeshwa na siasa,mapenzi yanaendelea na kisha
inakuja suala la barabara. Vumbi linatimka watu wamefunga vioo kondakta
akagundua wageni wengi ndani ya basi. Jamani msifunge vioo tutakufa
wacheni vumbi liingie na kutoka. Basi limejaa ndindindi. lahela sick love boy
akashuka na mbele kidogo tukanasa katika maji madogo kwenye barabara
inayotengenezwa.
He tunashtukia tunaelekea katika majumba ya watu basi limeacha
njia, vile vimaji kidogo katika barabara viliharibu kabisa eneo tunalopita.
maji yale yalimwagwa katika barabara inayojengwa. Mhh ilituchukua dakika 15
kutoka hapo, watu wengine waliamua kutumia muda huo kuchimba dawa.
"Hawa wajanja wanataka kumaliza barabara hii muda mfupi
nkabla ya uchaguzi kujipa maileji" anasema mtu mmoja.Ahh tunajenga na
madafu yetu tunachelewa kodi hatulipi.. hapana bwana fedha hizi mbona ni za
MCC. " Nakuambia kumbe watu wanajua na uwezo wa kubishana upo, wanasema
kuhusu uchelewefu halafu wanauliza rais kwanini alimuondoa Magufuli.
Baada ya kukamata mwendo sasa ukafika muda rasmi wa kuchimba
dawa, watu waliposhushwa kulikuwa na mti wa matunda pori, wenyeji wanajua
wakaanza usijisaidie hapo( kwa lile neno halisi) kuna matunda , watu wakaenda
mbali kujisaidia wakirejea wanachukua matunda hata dereva naye alifanya hivyo
hivyo,ilituchukua muda kuondoka hapo.
Kutoka hapo ikawa pandisha shusha,ingia kushoto ingia kulia
mpaka tukafika Sumbawanga saa 9 na nusu, nimechakaa kwa vumbi na kutokuwa na
mahali pa kuegemea. Nabanwa na mwanamama aliyejaaliwa na katikati kuna mtu wa
kufa mtu wamesimama.mambo hayo nikatulia watu wakawa wanashuka. Mara mzee kama
unaendelea Mpanda ni basi hilo la pili hili hapa ndio mwisho wa safari.
Maskini mie nabadilisha basi mara ya tatu kwa tiketi moja ya
Dar-Mpanda. Nikachukua vitu vyangu nikaingia basi la pili, hapana mzee
kwanza ofisini ukabadilishe tiketi.Vitu vyangu? Hapa Sumbawanga atakayekuibia
lazima awe taahira.,
Unaweka begi kubwa unaondoka na beki lako dogo lenye vifaa vyako
vya kazi.
Unabadilisha tiketi. Unaingia msalani kumeandikwa bei 200 unatoa
hela unaambiwa bei 300 zi ile iliyoandikwa.
Basi linaondoka saa kumi hapa Polisi wanafanya kazi yao
wanasema zipo namba kama dereva anajaza au kukimbia tupigieni safarini salama.
kweli basi lile lilikuwa na namba za RPC wa Rukwa, Mbeya, katavi na
Dodoma. Mnaanza safari,mazungumzo hapa yanabadilika, watu wote wamechoka
wanatazama saa, simu zinaanza kuingia.
Kila anayejibu analalamika kuchelewa kwa gari, kumbe tulitakiwa
kuwa Sumbawanga saa saba ili saa moja tuwe Mpanda.
Jirani yangu akanisimulia jinsi ilivyo hatari kusafiri usiku na
kwamba basi lile lilishawahi kufanyiwa kitu mbaya na dereva yule yule. Watu
walikusanywa simu na fedha huku mkusanyaji akiwa ni dereva wa Fuso lililotekwa
kabla yake.
Paniki zinaanza kuingia, huwa
natembea na chuo kidogo cha sala, pamoja na kumuomba Raphael, malaika mkuu kuwa
nami safarini pamoja na abiria wengine na kumchunga dereva asifanye maamuzi ya
kipuuzi nilianza safari ya mateso ya Kristo, kuomba ulinzi kamili kwangu , basi
na abiria wengine kwa maana kulikuwa na wanawake wengi katika basi na watoto na
kila mmoja kwa namna fulani alionekana kugwaya.
Dereva alichapa mwendo na wakati kiza kinaingia tulikuwa njia
panda ya kwenda bandari ya Debwe, dakika 15 za ukweli za kuchimba dawa, hakuna
hata choo cha kulipia watu wakajitoma katika vichaka vichafu unachagua tu pa
kuweka uchafu wako pia.
Dakika 15 ziliisha na kisha tukaanza mwendo tukaingia katika
Mbuga kila mtu alikuwa kimya mbele kidogo kwenye kiteremko kibaya gari
likasimama, akashuka Kondakta, mara dereva akasema Hassan mbele yako kuna simba,
watu wote wakataharuki, mama mmoja akafungua simu akaanza kusoma duwaa,kiza
kilikuwa kimetanda. Hapa ni Lyamba la Mfipa.
Yule mtu akaingia tukaanza taratibu kushuka,mama mmoja jirani
yangu akasema pale si pazuri hata kidogo wakiweka mtego hatuwezi kupona, lakini
jambazi anayekaa msitu wa simba naye lazima awe kanuia kufa. Lakini ni katika
hifadhi watu wanatekwa. Paniki, nikasema damu azizi ya Kristo iliyomwagika
msalabani tuondolee kiwewe. hata ile ya Getsmane sikuikumbuka. Kila mmtu
alionekana kivyake sana.
Saa mbili usiku bado tupo katikati ya msitu, unaowaka moto na
baadaye tukaupita tukakutana na magari kadhaa na saa tatu kasoro tukaona umeme,
dalili ya kumalizika kwa msitu,lakini kumbe watekaji nyara ndio maeneo yao,
kijiji cha kwanza tu kutoka mbugani.
"Naomba nishuke ..."sikusikia alisema kama kwa kilugha
lakini aliyeshuka usiku ule eneo lile lisilokuwa na umeme alikuwa na watoto
sita akiwemo mchanga mgongoni, watu wakasema jamani usiku na watoto,ulikuwa
usiku lakini kile kilikuwa kijiji, mbele watu walikuwa wakitembea.
Tulipiga mwendo, mbele zaidi kiboko akawa ametulia katikati ya
barabara.Jamaa akafunga breki akazima taa akawasha. akazima tena. Alipowasha
kiboko yule akajiondoa pale barabarani tukapita.
Saa nne tunaingia Mpanda hoi bin taaban, kasheshe za kutafuta
mahali pa kulala.Muungwana mmoja alifika akanipokea akanifikisha nyumba ya
wageni,tukala saa tano na sita kamili nilijitupa kitandani sikujua kinaendelea
nini.
mwisho
COMMENTS