.Kampuni za vigogo wa CCM zatajwa kuifilisi .Ni Tan Power ya Yona na TPI ya Madabida .Ni baada ya kuchukua mikopo bila riba .Wizara ya Madin...
.Kampuni za vigogo wa CCM zatajwa kuifilisi .Ni Tan Power ya Yona na TPI ya Madabida .Ni baada ya kuchukua mikopo bila riba .Wizara ya Madini yashindwa kukusanya mrahaba MFUKO wa Pensheni kwa Wafanyakazi wa Serikali Kuu (PSPF) uko hatarini kufilisika baada ya ukaguzi uliofanywa na Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kubaini kuwa uwezo wake wa kifedha unaendelea kushuka. Katika ripoti ya CAG aliyoiwasilisha bungeni inaonyesha kuwa ukadiriaji thamani wa mfuko huo ulibaini hasara halisi ya Sh trilioni 6.5 “Hivyo mfuko uko kwenye hatari ya kutoweza kujiendesha kama juhudi hazitachukuliwa na Serikali.” Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali, Ludovick Utouh alisema pamoja na mfuko kuwa katika hali mbaya kifedha, amebaini kuwa mfuko ulitoa mikopo kwa mashirika yaumma na taasisi nyingine ambayo yamedhaminiwa na Serikali yenye jumla ya Sh bilioni 67.2 bila riba. Madeni hayo ambayo hayajalipwa na hayana riba ni Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HESLB) ambayo deni lake ni Sh bilioni 54.6, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) ambayo deni lake ni Sh bilioni 6.7 na Kiwanda cha madawa Tanzania (TPI) wamekopa Sh milioni 435.1 kwenye mfuko huo. Kiwanda hicho kinamilikiwa na makada wa CCM ambao ni Ramadhani Madabida na mkewe Zarina Madabida ambaye ni mbunge wa viti maalum (CCM). Taasisi nyingine binafsi ambazo zimekopa kwenye mfuko huo chini ya udhamini wa Serikali na zimeshindwsa kulipa madeni yake ni kampuni ya Tan Power Resources ambayo imekopa Sh bilioni 5.4 bila riba. Kampuni hiyo ambayo inamilikiwa na viongozi wa zamani wa Serikali Daniel Yona na Rais Mstaafu Benjamini Mkapa ndio waliokuwa na mgodi wa Makaa ya Mawe Kiwira na baadaye wakashindwa kuuendesha na kuurejesha serikalini. Serikali Kuu WIZARA ya nishati na Madini imelaumiwa na mkaguzi na mdhibiti mkuu wa hesabu za Serikali (CAG) kwa kushindwa kukusanya Sh bilioni 19.7 ambazo ni mirahaba ya madini. Malipo hayo ni kutokana na mabadiliko ya sheria ya madini iliyorekebishwa kiwango cha mrahaba kutoka asilimia 3 kwenda asilimia 4. Pia wizara hiyo ilitajwa kupoteza Sh bilioni 1.6 ambazo ni maduhuli ambayo hayakukusanywa kutoka vyanzo mbalimbali kama vitalu vya madini na leseni za umeme. Kwa upande wa wizara ya miundombinu inashutumiwa kutumia Sh bilioni 252.9 ambazo zilitengwa kwenye bajeti ya wizara hiyo kwa ajili ya ujenzi wa barabara katika mwaka wa fedha 2011/2012 zilitumika kulipa madeni ya wizara ya mwaka 2010/11 jambo ambalo liliathiri utekelezaji wa miradi ya barabara. CAG alisema dhamana za jumla ya Sh bilioni 578.4 zilikuwa zimeisha muda wake na hivyo kuifanya serikali kama mdhamini kuwajibika kulipa deni hilo. Mashirika ya Umma Kwa upande wa mashirika ya umma ambako ukaguzi ulifanyika kwa mashirika 126 kati ya 176, mapungufu yaliyojitokeza ni tatizo la ujangili ambalo linaelezwa kuwa vitendo vya uwindaji haramu vimeongezeka na taarifa za mbuga saba jumla ya tembo 110 waliuawa katika kipindi cha mwaka 2011/12. “Hii ina athari kubwa kwa taifa na serikali isipochukua hatua baada ya miaka michache ijayo hakutakuwa na mnyama anayeitwa tembo katika hifadhi zetu,” alisema Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali Ludovick Utouh. Utouh pia alishangazwa na mamlaka ya bandari kuzuia kontena mbili za vitabu vya shule vilivyotolewa kama msaada kutokana tu na bodi ya huduma ya maktaba (TLSB) kushindwa kulipa ushuru wa Sh milioni 147 tangu mwaka 2009. Alisema kwa sasa deni halisi la kugombo vitambu hivyo ambavyo vilitolewa kama msaada na Shirika la Kimataifa la kufadhili Watoto halijulikani kwani inasadikiwa kuwa gharama hizo zitakuwa zimeongezeka. “Vitabu hivi vinaenda kusaidai watoto wetu na hata wafadhili wakisikia msaada walioutoa umekwama bandarini watashindwa kushiriki wakati mwingine.” CAG pia alibainisha malipo yasiyo ya faida ya Sh bilioni 2.2 yaliyolipwa kwa mkandarasi baada ya kusitishwa kwa mkataba na mamlaka ya bandari (TPA) kama faini kwa mkandarasi kampuni ya Oceana Advanced Industries Ltd kutokana na kushindwa kumkabidhi mkandarasi eneo husika la kazi. Kwa upande wa Shirika la Utangazaji (TBC), Utouh alisema mwaka 2010 TBC ililipa Sh milioni 618.3 kwa Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Mawasiliano ya Tanzania (TCRA) kwa niba ya Star Times (SMT)kwa ajili ya leseni ya biashara. Alisema lakini ukaguzi ulibaini kwamba kampuni hiyo ina mkataba wa utendaji uliosainiwa na kituo cha uwekezaji cha Tanzania (TIC) ambapo SMT imepewa msamaha wa kulipa leseni ya biashara kwa kipindi cha miaka 10. CAG kwa mtazamo wake alisema kiasi hicho cha fedha kilicholipwa na TBC kingeweza kuwa ni sehemu ya hisa za shirika kwa SMT kama kusingekuwa na msamaha wa leseni ya biashara. “Malipo haya yaliyolipwa kimakosa na TBC hayajerejeshwa na TCRA.” Pia alisema baadhi ya wizara zinaingilia bodi za maishirika na akatoa mfano kuwa wizara ya maliasili na utalii ilihamisha Sh milioni 771.2 kwenda bodi ya utalii kw ashughuli ambazo sio za bodi ya utalii. Alisema fedha hizo zilichukuliwa kwa maelekezo na maagizo kutoka wizarani. Pia CAG amemtaja mkurugenzi mkuu wa Tanesco alitumia vibaya madaraka yake kwa kuipa zabuni kampuni ya McDonald Live Line Technologh Ltd ya kutengeneza njia za umeme hai, mikataba iliyosainiwa kwa nyakati tofauti mwaka 2008 hadi 2011. Alisema ilikuwa ni kinyume na kanuni za maadii za Tanesco na kanuni za maadili za viongozi kwa mkurugenzi wa Tanesco kuipa mikataba ya kazi kampuni hiyo ambayo yeye ni mdau. Kiasi cha Sh bilioni 1.12 zililipwa kwa kampuni hiyo, malipo hayo ni pamoja na kodi ya ongezeko la thamani ambazo ni Sh milioni 168.9 ambazo hazikuwasilishwa TRA. ends
COMMENTS