Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Jaji Joseph Warioba akiongea na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo (Jumatatu, A...
Tume ya Mabadiliko ya Katiba imesema imejipanga kuandaa rasimu ya katiba itakayoweka mbele maslahi ya taifa na kuwaomba wananchi waijadili na kutoa maoni yao katika mabaraza ya katiba yatakayokutana kuanzia mwezi Juni mwaka huu (2013).
Mwenyekiti wa Tume hiyo Jaji Jospeh Warioba amesema leo (Jumatatu,
Aprili 29, 2013) jijini Dar es Salaam kuwa katika kuandaa rasimu hiyo, Tume
yake haitapokea shinikizo kutoka taasisi, asasi, makundi au vyama vya siasa.
“Tume haitengenezi katiba ya vikundi au vyama, tunaandaa katiba ya
nchi,” amesema Jaji Warioba katika mkutano wake na waandishi wa habari katika
ofisi za Tume na kufafanua kuwa Tume inazingatia uzito wa hoja
zilizotolewa na wananchi na sio idadi ya watu waliotoa maoni.
Jaji Warioba amewataka wananchi kutokubali kutumiwa na makundi,
asasi, taasisi na vyama wakati wa kujadili na kutoa maoni katika mabaraza ya
katiba ya wilaya.
Mabaraza ya Wananchi wenye ulemavu
Akizungumza kuhusu ushiriki wa walemavu katika mabaraza ya katiba,
Jaji Warioba amesema Tume yake inatarajia kuunda mabaraza ya Katiba ya watu
wenye ulemavu ili kuwapa fursa walemavu kutoka Tanzania Bara na Zanzibar kutoa
maoni yao kuhusu rasimu ya Katiba itakayotolewa na Tume.
Hatua hii inafuatia ombi la Shirikisho la Vyama vya Watu wenye
ulemavu Tanzania (SHIVYAWATA) na Umoja wa Watu wenye ulemavu Zanzibar (UWAZA)
waliloliwasilisha kwa Tume.
Jaji Warioba amesema Baraza moja litaundwa Tanzania Bara na
jingine Zanzibar na kwamba yatashirikisha wananchi kutoka ngazi ya chini ya
wilaya hadi Taifa.
“Tunaelewa kuwa watu wenye ulemavu ni karibu asilimia 10 ya
watanzania wote na mchakato huu hauwezi kuwatenga katika ngazi yoyote,” amesema
Jaji Warioba na kuongeza kuwa taarifa ambazo Tume yake inazo zinaonyesha baadhi
ya watu wenye ulemavu wamependekezwa na mitaa, vijiji, vitongoji na shehia kuwa
Wajumbe wa Mabaraza ya Katiba ya Wilaya.
Chaguzi za Wajumbe Mabaraza ya Katiba ya Wilaya.
Mwenyekiti
wa kamati ya uwasilishaji wa mapendekezo ya muundo wa mabaraza ya Katiba kwa
jamii ya watu wenye ulemavu, Bw. David Nyendo (kushoto) akiwasilisha maoni yake
ya kamati hiyo kwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba katika mkutano baina yao
uliofanyika ofisi za Tume Jijini Dar es Salaam tarehe 13 Feb mwaka huu
(2013). Kulia ni Mjumbe wa Tume, Dkt. Salim Ahmed Salim. (Picha na Tume ya
Katiba)
Aidha, Jaji Warioba amezungumzia mafanikio na changamoto
zilizojitokeza katika chaguzi zilizofanyika nchini kote hivi karibuni za
kuchagua Wajumbe wa Mabaraza ya Katiba kuanzia ngazi ya mitaa, vijiji,
vitongoji na shehia.
Kwa mujibu wa Jaji Warioba, tathmini ya Tume inaonyesha kuwa kwa
kiwango kikubwa viongozi na watendaji katika ngazi za vijiji, mitaa, shehia na
kata walizingatia mwongozo uliotolewa na Tume na kuwa maeneo mengi wananchi
walichaguana kwa amani na utulivu.
“Kwa mfano jumla ya shehia 323 sawa na asilimia 96.4 kati ya
shehia 335 kwa upande wa Zanzibar zimekamilisha vizuri mchakato huu, hali
kadhalika jumla ya Kata 3,331 sawa na asilimia 99.8 kati ya Kata 3,339 kwa
Tanzania Bara nazo zimekamilisha mchakato wa kuwapata wajumbe wa Mabaraza ya
Katiba ya Wilaya kwa kuzingatia utaratibu uliotolewa kwa mujibu wa Mwongozo,”
amesema Jaji Warioba.
Kuhusu hatua inayofuata baada ya chaguzi hizo, Jaji Warioba
alisema Tume inaendela kupokea majina kutoka kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa
na ya wananchi wote waliopendekezwa kutoka katika Kata na Shehia na kazi hiyo
inatarajia kukamilika ifikapo tarehe 30 Aprili mwaka huu (2013).
Changamoto
Akizungumzia kuhusu changamoto zilizojitokeza katika chaguzi hizo,
Jaji Warioba amesema kuwa pamoja na mafanikio yaliyopatikana pia kulijitokeza
changamoto kadhaa ambazo zilisabishwa na misimamo ya kisiasa na kidini
“Katika baadhi ya maeneo mikutano ya uchaguzi ngazi za vijiji,
mitaa na shehia ilishindwa kufanyika kutokana na mivutano ya kisiasa na kidini
zilizosababishwa na baadhi ya wananchi kufangamanisha chaguzi za Wajumbe wa
Mabaraza ya Katiba ya Wilaya na masuala ya kisiasa na kidini,” amesema Jaji
Warioba.
Jaji Warioba ametaja changamoto nyingine kuwa ni pamoja na baadhi
ya wananchi kujiingiza katika vitendo vya rushwa katika chaguzi hizo ili
wapendekezwe kuwa wajumbe wa mabaraza hayo ya katiba.
“Tumepokea pia malalamiko ya vitendo vya rushwa,” alisema
Mwenyekiti huyo na kusema vitendo hivyo ni kinyume cha sheria na kuongeza kuwa
taasisi zenye mamlaka ya kupambana na vitendo hivyo zinapaswa kushughulikia
malalamiko hayo.
Aina na Majukumu ya Mabaraza ya Katiba
Katika mkutano huo uliofanyika katika katika Ofisi za Tume
zilizopo mtaa wa Ohio jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti huyo pia alizungumza
kuhusu aina na majukumu ya Mabaraza ya Katiba.
Kwa mujibu wa Jaji Warioba, Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, Sura
ya 83 imetoa fursa ya kuundwa kwa mabaraza ya aina mbili ambayo ni Mabaraza
yatakayoundwa, kusimamiwa na kuendeshwa na Tume katika muda na tarehe
itakayopangwa na Tume.
Aina ya pili, kwa mujibu wa Mwenyekiti huyo, ni Mabaraza ya Katiba
ya Asasi, Taasisi na Makundi mbalimbali yenye malengo yanayofanana. Mabaraza
haya yatajiunda, yatajisimamia na kujiendesha yenyewe na kisha kuwasilisha
maoni yao kuhusu rasimu ya Katiba ndani ya muda utakaopangwa na Tume.
“Kazi kubwa ya Mabaraza ya Katiba ya aina zote mbili ni kuipitia,
kuijadili na kuitolea maoni rasimu ya Katiba itakayokuwa imeandaliwa na Tume
kutokana na maoni yaliyokusanywa kutoka kwa wananchi,” alisema Jaji Warioba na
kuziomba taasisi, makundi, asasi na vyama mbalimbali kutumia fursa hiyo ya
kisheria kuunda mabaraza na kutoa maoni yao kuhusu rasimu ya Katiba
itakayotolewa.
Source:Tume ya katiba
COMMENTS