HOTUBA YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA DKT. JAKAYA MRISHO KIKWETE, AKIFUNGUA WARSHA YA WAZI (OPEN DAY) KUH...
HOTUBA
YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA
TANZANIA,
MHESHIMIWA DKT. JAKAYA MRISHO KIKWETE, AKIFUNGUA WARSHA YA WAZI (OPEN DAY)
KUHUSU MFUMO MPYA WA UFUATILIAJI NA TATHMINI YA UTEKELEZAJI WA MIRADI YA
KITAIFA YA KIPAUMBELE, VIWANJA VYA MAKUMBUSHO YA TAIFA, DAR ES SALAAM, MEI 24,
2013
Mhe. Dkt. Mohammed Gharib Bilal, Makamu wa Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mhe. Dkt. Ali Mohammed Shein, Rais wa Serikali ya
Mapinduzi Zanzibar;
Mhe. Mizengo Kayanza Peter Pinda (Mb), Waziri Mkuu
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mhe. Seif Shariff Hamad, Makamu wa Kwanza wa Rais
wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar;
Waheshimiwa Mawaziri na Manaibu Waziri;
Balozi Ombeni Sefue, Katibu Mkuu Kiongozi;
Makatibu Wakuu;
Dkt. Philip Mpango, Katibu Mtendaji wa Tume ya
Mipango;
Washirika na Wadau wa Maendeleo;
Viongozi wa Taasisi za Serikali na Mashirika ya
Umma;
Viongozi wa Kidini na Sekta Binafsi;
Wataalamu Elekezi kutoka PEMANDU na Mckinsey;
Washiriki wa Maabara;
Ndugu Wananchi;
Mabibi na Mabwana:
Napenda kuchukua fursa hii
kuwakaribisha wote katika Warsha ya Wazi kuhusu mfumo mpya unaoanzishwa na
Serikali wa ufuatiliaji na tathmini ya utekelezaji wa miradi ya kitaifa ya
kipaumbele. Warsha hii inatoa nafasi ya
pekee kwa wananchi kushiriki na kutoa mawazo yao jinsi ya kuboresha mfumo huo
unaopendekezwa. Ni Warsha ya
kuelimishana, kubadilishana mawazo na kufahamishana mipango na mambo ambayo
Serikali inatarajia kuyafanya katika siku za karibuni.
Namshukuru Balozi Ombeni
Sefue, Katibu Mkuu Kiongozi, Dkt. Philip Mpango, Katibu Mtendaji wa Tume ya
Mipango, viongozi na watumishi wote wa Tume ya Mipango kwa kuandaa Warsha hii
mahsusi. Kwa namna ya pekee nawashukuru
pia wataalamu wa PEMANDU na McKinsey kwa kushirikiana vizuri na wataalam wetu katika
kila hatua ya safari hii ambayo Serikali yetu imeianza.
Ndugu Wananchi;
Kupanga na kutekeleza mipango
ya maendeleo sio jambo geni hapa nchini.
Ni jambo ambalo tumelifanya tangu tupate Uhuru na tunaendelea nalo. Serikali ya Awamu ya Kwanza chini ya Baba wa
Taifa Hayati Mwalimu Julius Nyerere, ilianza na Mpango wa Kwanza wa Maendeleo
mwaka 1961 – 1964. Mpango huo uliainisha
maadui watatu wa maendeleo ambao ni umaskini, ujinga na maradhi. Mikakati mbalimbali na mipango madhubuti ya
maendeleo ilibuniwa ili kupambana na maadui hao. Baada ya hapo ukaja Mpango wa Maendeleo wa
Miaka 15 wa mwaka 1964 – 1980, uliokuwa umegawanywa katika vipindi vitatu vya utekelezaji
vya miaka mitano mitano.
Baadhi yenu mtakumbuka kuwa
utekelezaji wa vipindi viwili vya mwanzo ulikuwa wa kuridhisha. Hata hivyo, utekelezaji wa kipindi cha mwisho
cha Mpango ule, yaani kati ya mwaka 1975 – 1980, ulikuwa duni mno. Utekelezaji wake ulivurugwa sana na
changamoto za wakati ule kama vile kupanda sana bei ya mafuta, kuvunjika kwa
Jumuiya ya Afrika Mashariki (1977) na Vita ya Kagera. Mambo haya yalisababisha fedha zetu nyingi kutumika
kuagiza mafuta, kujenga taasisi zetu wenyewe na kutetea mipaka ya nchi
yetu. Rasilimali kidogo tuliyonayo
ikaenda huko badala ya kugharamia miradi ya maendeleo.
Ndugu Wananchi;
Pamoja na changamoto zilizojitokeza, Serikali iliamua
kuanzisha mpango mwingine wa maendeleo wa muda mrefu wa mwaka 1981 – 2000. Kwa bahati mbaya mpango huo nao
haukutekelezwa kufuatia kuendelea kudorora kwa uchumi. Kati ya mwaka 1981 na miaka ya 90 mwanzoni, Serikali
ilianza kufanya mabadiliko makubwa ya kiuchumi.
Tukawa na National Economic Survival Programme (NESP) mwaka 1981 – 82 na
Structural Adjustment Programme (SAP) mwaka 1982 – 1985. Mipango hiyo haikutekelezwa vizuri kutokana
na sababu mbalimbali ikiwemo ya ukosefu wa rasilimali za kutosha. Kati ya mwaka 1986 – 89, Serikali kwa
kushirikiana na Mfuko wa Fedha wa Kimataifa (IMF) ikaanza kutekeleza programu
ya kwanza ya kufufua uchumi (ERP – I).
Ya pili ikafuatia kati ya mwaka 1989 – 1992.
Mwaka 1994 Serikali ikaanza kuandaa mpango wa maendeleo
wa muda mrefu utaowezesha kuzikabili changamoto mpya kufuatia mageuzi ya
kiuchumi na kijamii yaliyokuwa yanaendelea nchini na duniani kwa ujumla. Kazi hiyo ilikamilika mwaka 1999 na kuzinduliwa
kwa Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2025. Malengo
ya Dira hiyo ni kuleta maendeleo ya haraka nchini na kuifanya Tanzania kuwa
nchi ya uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.
Maana yake ni kwamba wananchi wawe na chakula cha kutosha, huduma ya
elimu na afya iliyo bora iwafikie watu wengi zaidi, vifo vya watoto na akina
mama vipungue, wastani wa kuishi uongezeke, maji safi na salama yapatikane kwa
wote, uhalifu upungue na umaskini uliokithiri usiwepo kabisa na pato la wastani
la Watanzania liwe zaidi ya dola za
Kimarekani 3,000. Vile vile pawe na
maendeleo ya viwanda, matumizi ya teknolojia na sayansi yaongezeke, miundombinu
ipanuke na uchumi ukue kwa asilimia 8 au
zaidi.
Ndugu Wananchi;
Juhudi kubwa zilizofanywa na
Serikali za awamu zote ikiwemo na hii ninayoiongoza mimi zimeleta mafanikio ya
kutia moyo. Kwa mfano, uchumi wa nchi
umekua kwa wastani wa asilimia 7 kwa
miaka kumi iliyopita, mfumuko wa bei upo chini ya asilimia 10, mapato ya ndani yameongezeka, mauzo ya nje
yameongezeka na hifadhi ya fedha za kigeni imeongezeka pia. Hata hivyo, idadi ya Watanzania walio maskini
bado ni kubwa hususan umaskini wa kipato.
Vile vile bado hatujafanikiwa kufikia malengo katika maeneo mengi
tuliyojiwekea. Hata tathmini ya
utekelezaji wa Dira ya Maendeleo 2025 tuliyofanya mwaka 2000 imethibitisha
hivyo. Hatuendi kwa kasi inayotakiwa na
utekelezaji wake siyo wa kuridhisha. Matokeo
yake tupo nyuma ya hatua tuliyotakiwa kuwa.
Kwa mfano, kwa upande wa safari ya kuelekea pato la wastani la watu kuwa
dola 3,000 mwaka 2025, tulitakuwa
tuwe tumefikia dola 995 mwaka
2010. Lakini ilikuwa tumefikia dola 545 tu. Kwa ukuaji wa uchumi, tulitakiwa tuwe asilimia 8, lakini tulikuwa asilimia 7.
Zipo changamoto nyingi za
ndani na nje, zilizofanya tusifikie malengo hayo: Kubwa ni misukosuko ya uchumi wa dunia, uhaba
wa rasilimali fedha na ufuatiliaji mdogo katika utekelezaji wa miradi
iliyoainishwa kuleta maendeleo. Aidha, mipango na mikakati ya maendeleo ilikuwa
na vipaumbele vingi kwa wakati mmoja wakati rasilimali za utekelezaji wake ni
kidogo. Hali hii haikutuwezesha
kujielekeza ipasavyo kwenye maeneo yenye kuleta matokeo makubwa na kwa haraka.
Ndugu Wananchi;
Baada ya kutafakari yote haya,
tukafikiria namna ya kuweza kufikia malengo yetu ya Dira ndani ya muda uliobakia.
Hivyo, tukaamua kuja na Mpango ya Maendeleo wa Muda Mrefu wa Miaka 15 ambao
utatekelezwa katika awamu tatu za miaka mitano mitano. Katika Mpango wa Kwanza Maendeleo
wa Miaka Mitano (2011/12-2015/16), maeneo yaliyopewa kipaumbele ni Miundombinu,
Kilimo, Viwanda, Huduma za jamii na Uendelezaji Rasilimali Watu na Utalii,
Biashara na Huduma za Fedha. Changamoto
kubwa ikabaki kuimarisha mfumo wetu wa kusimamia utekelezaji wa mipango ya
maendeleo ili kuleta matokeo ya haraka.
Kuendelea kufanya vilevile tulivyokuwa tukifanya kusingeweza kuleta mabadiliko tuliyokuwa
tunayataka katika utekelezaji wa mipango yetu.
Ilibidi tubadilike, ikiwezekana tukimbie pale ambapo wengine
wanatembea.
Ndugu Wananchi;
Tukiwa katika hali hiyo ya kutafakari cha kufanya, mwezi Mei,
2011 ikawa bahati mimi kuhudhuria Mkutano wa Kimataifa wa “Langkawi International Dialogue” uliofanyika mjini
Kuala Lumpur, Malaysia. Katika mkutano
huo, Serikali ya Malaysia iliwasilisha mada jinsi inavyoendesha na kusimamia
utendaji wake ikiwemo utekelezaji wa miradi ya maendeleo na huduma kwa jamii. Mimi na viongozi wenzangu tuliohudhuria
mkutano huo tulivutiwa sana na mfumo wa utendaji wa Malaysia na tukadhamiria
kujifunza zaidi kutoka kwao. Tukaomba
watusaidie. Bahati nzuri Serikali ya
Malaysia ikakubali ombi letu na kuandaa warsha maalum mwezi Novemba, 2011. Ujumbe wa Tanzania kwenye warsha hiyo ya aina
yake uliongozwa na Dkt. Philip Mpango. Waliporudi,
tukaamua kuwa na sisi tuanze kutumia utaratibu wa Malaysia wa “Matokeo Makubwa
Sasa” ama kwa Kiingereza “Big Results Now”.
Ndugu Wananchi;
Utekelezaji wa mfumo wa “Big
Results Now” hapa nchini ulianza kwa kuainisha maeneo sita yenye uwezo wa
kutupatia matokeo makubwa kwa haraka. Maeneo hayo ni nishati, elimu, maji,
miundombinu, kilimo na utafutaji fedha.
Kazi ya kuchagua maeneo sita ya kwanza nayo haikuwa rahisi. Tulibishana sana katika kuchagua vipaumbele
vichache lakini vyenye kuleta matokeo makubwa.
Hatimaye tukafanikiwa. Vipaumbele
hivi vinabeba msingi wa kufungulia fursa za ukuaji uchumi wa Tanzania kwa
ujumla na kuchochea ustawi wa maisha bora kwa wananchi.
Hatua ya pili ikawa ni kufanya
uchambuzi wa kina kupitia awamu ya kwanza ya maabara (lab) kama alivyoeleza Katibu Mkuu Kiongozi. Kazi hiyo ilitekelezwa
kwa wiki sita mfululizo na wataalam wetu zaidi ya 300 kutoka nyanja na sekta mbalimbali na kukamilika tarehe 05
Aprili, 2013. Nawapongeza sana kwa kazi hiyo kubwa na moyo wao wa kujitolea. Tumeandaa
ratiba ya utekelezaji kwa kila mradi na programu ikionyesha kazi zilizopangwa
kufanywa, mtekelezaji-husika na muda na kukamilisha kazi.
Katika mfumo huu, Mawaziri na
Watendaji katika Wizara na Idara watapimwa kwa vigezo vilivyo wazi na ninyi
wananchi mtapata fursa ya kuvijua vigezo hivi pamoja na matokeo ya
upimaji. Hapatakuwa na siri. Hii
itarahisisha usimamizi wa utendaji kwa maana Waziri au Katibu Mkuu atajifunga
yeye mwenyewe kimaandishi na ataweka saini yake kwenye vigezo ambavyo atapimwa
navyo na wananchi mtashuhudia matokeo ya upimaji huo.
Ndugu Wananchi;
Ili kuweza kuratibu vyema
shughuli za ufuatiliaji wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika mfumo huu
mpya, nimeunda chombo maalum kitakachokuwa chini ya Ofisi yangu ambacho
kitajulikana kama President’s Delivery
Bureau (PDB). Kazi zake za msingi zitakuwa ni pamoja na: kupanga na
kuendesha shughuli za uchambuzi wa kina wa kimaabara (labs); kuandaa mikataba ya kupima utendaji kazi wa Mawaziri kwenye
miradi na programu za maendeleo katika wizara zao; kwa kushirikiana na Tume ya
Mipango kuishauri Serikali kuhusu maeneo machache ya kipaumbele yenye kuleta
matokeo ya haraka (National Key Results Areas); kusaidia sekta binafsi kuwekeza
kwenye maeneo hayo; na kufanya tathmini huru ya utendaji kwa viongozi wote
hususan Mawaziri katika utekelezaji wa maeneo muhimu ya kitaifa.
Ndugu Wananchi;
Tumefanya kazi kubwa sana ya
kuandaa na kuainisha maeneo ya kimkakati na kuyaandalia programu za kina kwa
ajili ya utekelezaji. Lakini tumeona ni vyema kuwashirikisha wadau na wananchi
katika jambo hili kubwa. Ndio maana tupo
hapa kuhakikisha kuwa wananchi kwa ujumla wenu mnapata fursa ya kuchangia
katika miradi na programu hizo kwa maendeleo ya taifa letu na watu wake.
Ndugu Zangu;
Sitapenda kuongea sana hivyo
basi nataka niwape nafasi wananchi na wadau wengine mliofika hapa kupita katika
eneo la kila maabara na kupata maelezo ya kina kutoka kwa wataalam. Muwe huru kuuliza maswali, kujenga hoja,
kutoa maoni na kukosoa na kuboresha katika kila maabara. Baada ya kupata maoni
yenu ndipo tutaboresha na kwenda kuyafanyia kazi maoni na ushauri wenu.
Ndugu Wananchi;
Baada ya
kusema hayo, napenda kutamka kuwa Warsha ya Wazi imefunguliwa rasmi. Ninawatakia majadiliano mazuri na uchangiaji
mzuri.
Asanteni kwa kunisikiliza

COMMENTS