CHECK AGAINST DELIVERY HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JAKAYA MRISHO KIKWETE, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWA WANANCHI, TAREH...
CHECK
AGAINST DELIVERY
HOTUBA
YA MHESHIMIWA DKT. JAKAYA MRISHO KIKWETE, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA
TANZANIA KWA WANANCHI, TAREHE 31 JULAI, 2014
Utangulizi
Ndugu wananchi;
Naomba nianze kwa
kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema, kwa kutujalia uzima na kutuwezesha
kwa mara nyingine tena kuzungumza na taifa juu ya masuala muhimu yanayohusu
nchi yetu. Mwezi wa Saba tunaoumaliza leo ulikuwa na matukio mengi baadhi
yakiwa makubwa na kushtusha na mengine yalikuwa matukio ya kawaida.
Mashambulio ya Mabomu
Ndugu Wananchi;
Tarehe 3 Julai, 2014 na
tarehe 07 Julai, 2014 kulitokea mashambulizi ya mabomu nyumbani kwa Sheikh Sudi
Ally Sudi na katika mgahawa wa Vama kwa mfuatano huo. Kabla ya hapo, kulikuwa na matukio mengine
matatu: Kanisa la Olasiti tarehe 5 Mei,
2012, Mkutano wa Kampeni wa CHADEMA tarehe 15 Juni, 2013 na Baa ya Arusha Night
Park tarehe 13 Aprili, 2014. Hali
kadhalika, tarehe 13 Juni, 2014 kulitokea shambulizi la mabomu katika eneo la
Darajani, Zanzibar.
Kila lilipotokea
shambulizi uchunguzi ulifanyika na watuhumiwa kukamatwa. Lakini, watuhumiwa waliokamatwa safari hii
wanaelekea kutoa sura nzuri zaidi ya mtandao wa watu wanaofanya vitendo hivi
vya kikatili pale Arusha na kwingineko nchini.
Watu 38 wameishafikishwa
Mahakamani, wengine 8 watafikishwa
Mahakamani kesho na uchunguzi na msako unaendelea kote nchini kuwapata
watuhumiwa wengine.
Napenda kutumia nafasi hii
kutoa pongezi za dhati kwa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama kwa kazi kubwa na
nzuri iliyotufikisha hapa tulipo sasa. Tunawaomba
waongeze bidii, maarifa na ushirikiano mpaka wote waliohusika wakamatwe na
kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.
Aidha, natoa pongezi na
shukrani maalum kwa wananchi wema waliotoa taarifa zilizowezesha kukamatwa kwa
watuhumiwa. Napenda kutumia nafasi hii
kuwasihi wananchi wenye taarifa kuhusu wanaotafutwa au ye yote anayejihusisha
na vitendo hivi viovu watoe taarifa kwenye vyombo vya usalama ili hatua
zipasazo zichukuliwe.
Kutupwa Viungo vya Binadamu
Ndugu Wananchi;
Tarehe 22 Julai, 2014,
katika Bonde la Mto Mpiji lililopo eneo la Bunju Wilaya ya Kinondoni, Dar es
Salaam, viligunduliwa viungo vya binadamu na baadhi ya vitendea kazi vya
madaktari vikiwemo aprons na gloves. Viungo
hivyo vilivyokutwa vimekakamaa na kuhifadhiwa katika mifuko myeusi 85, vilikuwa vimetupwa jana yake tarehe
21 Julai, 2014. Tukio hilo lilileta
taharuki na hofu kubwa katika Jiji la Dar es Salaam na nchini kwa ujumla.
Uchunguzi uliofanywa
uligundua kuwa viungo hivyo vilikuwa vinatumika kufundishia wanafunzi wa
udaktari katika Chuo Kikuu cha Tiba kilichoko Mbezi Beach maarufu kwa jina la
IMTU. Ni utaratibu wa kawaida kwa vyuo
vikuu vya udaktari nchini na kote duniani kutumia miili ya wanadamu waliofariki
kufundishia. Hata hivyo, pale viungo
hivyo vinapokuwa havihitajiki tena kwa shughuli hiyo, zipo taratibu zake za kuvisitiri
ambazo hazikufuatwa. Bahati nzuri
mamlaka husika zimeona kasoro hiyo na hatua zimeanza kuchukulikuwa. Tuziachie mamlaka hizo kuchukua hatua
zipasazo kwa mujibu wa madaraka yao na kwa mujibu wa Sheria na Kanuni
zinazotawala shughuli za namna hiyo. Ni
matumaini yangu kuwa yaliyofanywa na IMTU hayatafanywa tena na Chuo hicho wala
chuo kingine cho chote hapa nchini.
Ziara
Yangu Mikoani
Ndugu Wananchi;
Katika
mwezi huu wa Julai, nimefanya ziara katika ya mikoa ya Tanga na Ruvuma. Nimefurahishwa sana na hatua kubwa ya
maendeleo waliyopiga wananchi wa mikoa hiyo.
Pamoja na mchango wa Serikali, ari na mwamko mkubwa wa kujiletea maendeleo
walionao viongozi na wananchi wa mikoa hiyo vimechangia sana katika kuongeza
kasi ya maendeleo na mafanikio yanayoendelea kupatikana. Katika ziara hizo, nilizindua miradi iliyokamilika na kuweka mawe ya msingi ya
ujenzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo ile ya barabara, umeme,maji,
afya, elimu, majengo ya Serikali, nyumba na kadhalika.
Nimepata faraja kubwa
kupata taarifa kuwa ahadi zangu nyingi na zile zilizomo kwenye Ilani ya Chama
cha Mapinduzi zimekamilika na zingine ziko katika hatua mbalimbali za
utekelezaji. Ndoto ya miaka mingi, kabla
na baada ya Uhuru, ya wananchi wa Mikoa ya Kusini ya kutaka Mikoa yao ifunguke
na kuunganishwa na mikoa mingine kwa barabara za lami sasa kuna uhakika wa kukamilika. Barabara ya kutoka Mbinga, Songea hadi
Namtumbo iliyojengwa kwa msaada wa Serikali ya Marekani imekamilika na
tuliizindua. Tuliweka mawe ya msingi ya
kujenga barabara ya lami kutoka Namtumbo, Tunduru, Mangaka hadi Mtambaswala
kwenye Daraja la Umoja linalounganisha Tanzania na Msumbiji kwa msaada wa Benki
ya Maendeleo ya Afrika na Serikali ya Japan.
Barabara ya kutoka Mangaka hadi Masasi iliyojengwa kwa msaada wa
Serikali ya Japan imekamilika na tuliizindua.
Katika barabara ya kutoka Mtwara hadi Mbamba Bay kimebaki kipande cha kilometa 66 kutoka Mbinga kwenda Mbamba
Bay ambacho hakikuwa na mpango wo wote wa kuwekewa lami kwa sasa. Bahati nzuri, Mwakilishi Mkazi wa Benki ya
Maendeleo ya Afrika (ADB), Bibi Tonia
Kandiero alitangaza pale Namtumbo kuwa Benki yake itafadhili ujenzi wa barabara
hiyo. Mambo sasa yamekamilika.
Kule
Masasi mkoani Mtwara na Nachingwea mkoani Lindi tulizindua kukamilika kwa mradi
mkubwa wa maji wa Mbwinji unaomaliza tatizo kubwa la maji kwa miji hiyo kwa
miaka mingi ijayo.
Nyumba
za Bei Nafuu
Ndugu Wananchi;
Nikiwa
wilayani Mkinga na katika Manispaa ya Songea nilizindua nyumba za gharama nafuu
zilizojengwa na Shirila la Nyumba la Taifa (NHC). Nyumba hizo za vyumba viwili na vitatu
zinauzwa kwa bei ya shilingi milioni 31
hadi 42. Wenzetu wa NHC walinieleza utayari
wa kujenga nyumba zaidi endapo watapatiwa maeneo na Halmashauri za Wilaya na
Miji. Walinilalamikia kuwa hawapati
ushirikiano wa kutosha kutoka mamlaka husika.
Nilipokuwa Mkinga na Songea niliagiza Halmashauri hizo na nyinginezo
nchini kutenga maeneo kwa ajili ya NHC na Mifuko ya Hifadhi za Jamii yote ili
waweze kujenga nyumba za bei nafuu kwa ajili ya wafanyakazi na wananchi kwa
ujumla.
Hii ni fursa ya aina yake kwa wananchi wa
kipato cha chini na cha kati kuweza kujipatia nyumba kwa urahisi. Halmashauri zisiwe kikwazo wakati ardhi
imejaa tele na kila wakati wanapima viwanja vipya. Jambo lingine zuri waliloniambia viongozi wa
NHC ni kwamba zipo Benki ambazo wanashirikiana nazo kutoa mikopo kwa watu
wanaonunua nyumba zao. Ni matarajio
yangu kwamba uongozi wa Halmashauri zote nchini utaitikia maelekezo
yangu na kwamba utatenga maeneo kwa ajili ya mashirika yetu hayo.
Matibabu
kwa Wazee
Ndugu Wananchi;
Nilipokuwa wilaya ya
Kilindi nilifurahishwa sana na utaratibu wa kuwapatia wazee huduma ya
matibabu. Kama mjuavyo Sera ya Afya
inataka wazee na watoto wa chini ya miaka mitano watibiwe bure katika hospitali
za Serikali. Bahati mbaya vitambulisho
wanavyopata wazee vimekuwa havithaminiwi ya kutosha. Kwa sababu hiyo, nafuu wanayostahili kupata
imekuwa haipatikani kwa urahisi na wengine huikosa kabisa.
Katika Wilaya ya Kilindi, Halmashauri ya
wilaya imeamua kuwakatia wazee hao Bima ya Afya inayotolewa na Mfuko wa Afya ya
Jamii (CHF) na hivyo kuondoa kabisa migogoro inayohusiana na vitambulisho vya
wazee vilivyokuwepo kabla. Kwa
kuzingatia malalamiko ya mara kwa mara ninayoyapata kutoka kwa wazee kuhusu
matibabu, nashauri Halmashauri zote nchini ziige mfano wa Wilaya ya Kilindi.
Kama Kilindi wameweza kwa nini wengine washindwe.
Ndugu Wananchi;
Katika
mikoa hii miwili nilipokea taarifa za kutia moyo kuhusu juhudi za wananchi na
Serikali katika kupanua fursa za elimu.
Vijana wengi wenye umri wa kujiunga na shule za msingi wanafanya hivyo
na wale wote wanaofaulu mtihani wa darasa la saba wanapata fursa ya kwenda
sekondari. Hatuna tena tatizo la
fursa. Pamoja na mafanikio hayo mazuri,
taarifa za wanafunzi wengi kushindwa kumaliza elimu ya msingi na sekondari,
zimenishtua na kunisikitisha sana.
Katika Mkoa wa Tanga kwa mfano,
kati ya wanafunzi 50,921 walioanza darasa la kwanza mwaka 2007 , ni
wanafunzi 41,017 tu ndiyo waliofanya
mtihani mwaka 2013. Hivyo basi, wanafunzi
9,904 ambao ni sawa na asilimia 19.4 hawakumaliza elimu ya msingi. Kwa upande wa sekondari, katika mkoa wa
Ruvuma, kwa mfano, kati ya wanafunzi 18,892
walioanza kidato cha kwanza mwaka 2010 ni wanafunzi
9,968 sawa na asilimia 52.76
ndiyo waliofanya mtihani wa kidato cha nne. Hivyo basi, wanafunzi 8,924 sawa na asilimia 47.2
hawakumaliza elimu ya sekondari. Taarifa
za namna hii nilizipata pia katika ziara zangu ya Mikoa ya Kagera, Geita na
Simiyu. Nina kila sababu ya kuamini kuwa
hali ni hiyo hiyo kwa Mikoa mingine mingi nchini. Kwa kweli kiwango hiki cha wanafunzi
wanaoshindwa kumaliza elimu ya msingi na sekondari ni kikubwa mno. Kinanisikitisha sana, hakikubaliki na
hakiwezi kuachwa kiendelee.
Ndugu Wananchi;
Kwa
maoni yangu wazazi, walimu na viongozi wanao wajibu maalumu wa kuhakikisha kuwa
wanafunzi wote wanahudhuria masomo shuleni tangu wanapoanza mpaka wanapomaliza
masomo yao. Huu ni wajibu wa lazima na siyo hiari. Ni wajibu wa kisheria. Kwa hiyo, nimeagiza kwamba, wazazi, walimu,
Maafisa Elimu wa Wilaya wa Msingi na Sekondari na Kamati husika katika Halmashauri
zote nchini ziwajibike ipasavyo kuhakikisha kuwa utoro mashuleni
unakomeshwa. Ajenda ya mahudhurio
shuleni iwe ni ya kudumu katika vikao vyote vya Halmashauri.
Kuanzia sasa Walimu Wakuu na
Wakuu wa Shule ni lazima watoe taarifa za mahudhurio ya wanafunzi kwa Maafisa Elimu
wa Wilaya kila miezi mitatu. Maafisa
Elimu wa Wilaya nao watalazimika kutoa taarifa kwenye vikao vya Halmashauri mwezi
mmoja baada ya kupokea taarifa hizo. Halmashauri
hazina budi kuchukua hatua stahiki za kijamii na kisheria kuhakikisha kuwa watoro
wanarudi shuleni. Wazazi wa watoto hao
au mtu ye yote atakayebainika kuhusika na utoro huo abanwe ipasavyo.
Sheria ya Elimu ya 1978
ipo, itumieni kwa ukamilifu kulitatua tatizo hili. Haipendezi kusubiri mpaka miaka saba kwa
wanafunzi wa shule ya msingi au miaka minne kwa wanafunzi wa sekondari ipite
ndipo taarifa za utoro kwa wanafunzi zitolewe au zijulikane. Lazima ufuatiliaji wa mahudhurio uwe wa mara
kwa mara ili hatua za kuzuia ziweze kuchukuliwa mapema. Ninawataka viongozi wa TAMISEMI, Mikoa na
Wilaya kuchukua hatua stahiki kudhibiti tatizo hili la utoro na watoto wengi
kutokumaliza masomo. Litarudisha nyuma
maendeleo ya taifa.
Umeme
Vijijini
Ndugu Wananchi;
Nilipokuwa
mkoani Ruvuma nimezindua ujenzi wa miradi mingi ya umeme vijijini. Kwa mujibu wa miradi hiyo vijiji 309 vitapatiwa umeme kati ya vijiji 509 vya Mkoa huo vinavyohitaji
umeme. Napenda kutumia nafasi hii kutoa
pongezi za dhati kwa Waziri wa Nishati na Madini, Prof. Sospiter Muhongo na
viongozi wenzake, viongozi na wafanyakazi wa Wakala wa Umeme Vijijini (REA) pamoja
na TANESCO kwa kazi kubwa na nzuri waifanyayo ya kufikisha umeme vijijini. Kwa kweli ni mara ya kwanza katika historia
ya nchi yetu suala la umeme vijijini kupewa msukumo mkubwa kiasi hiki, kwani
kinachofanyika Ruvuma kipo nchi nzima.
Nawaomba wananchi wanaofikishiwa umeme wautumie. Hata gharama za kuunganisha umeme
zimepunguzwa makusudi, ili watu wengi waweze kumudu kuingiza umeme majumbani na
kwenye shughuli za kichumi na huduma.
Mchakato
wa Katiba Mpya
Ndugu Wananchi;
Kama
tujuavyo, Bunge Maalum la Katiba lililoahirishwa tarehe 25 Aprili, 2014 kupisha
Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Baraza la Wawakilishi kushughulikia
bajeti za Serikali husika, litakutana tena tarehe 5 Agosti, 2014 kuendelea na
kazi yake ya kutunga Katiba Mpya. Kwa
vile Bunge Maalumu la Katiba halikuweza kumaliza kazi yake ndani ya siku 70
zilizotengwa kwa mujibu wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, nimeliongezea Bunge
hilo siku 60 kwa ajili ya kukamilisha kazi yake. Nimefanya hivyo kwa mujibu wa mamlaka
niliyopewa na Sheria hiyo hiyo.
Hatua
Iliyofikiwa Kabla ya Kuahirishwa kwa Bunge
Ndugu Wananchi;
Itakumbukwa pia kuwa, tarehe
16 Aprili, 2014, baadhi ya Wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba hasa kutoka vyama
vya CHADEMA, CUF na NCCR-Mageuzi walisusia
mjadala uliokuwa unaendelea Bungeni na kutoka nje. Wakati wanatoka Bungeni, kazi kubwa ilikuwa
imefanyika. Tayari Kamati zote 12 za
Bunge hilo zilikuwa zimekamilisha kujadili Sura
ya Kwanza na ya Sita za Rasimu ya Tume.
Sura hizo zinazungumzia utambulisho wa nchi na muundo wa muungano. Kamati zote zilipiga kura ya kupitisha
uamuzi wao kuhusu sura hizo mbili. Kamati kadhaa ziliweza kupata theluthi mbili ya kura kwa Wajumbe wa
pande zote mbili za Muungano, jambo lililoonyesha dalili njema kwamba Katiba
mpya inaweza kupatikana.
Baada ya hapo, taarifa ya kila
Kamati iliwasilishwa kwenye Bunge zima. Kwa
mujibu wa Kanuni za Bunge Maalumu la Katiba, maoni ya wachache nayo
yaliwasilishwa. Kazi iliyokuwa inafuatia,
kwa mujibu wa Kanuni za Bunge ni kwa Kamati ya Uandishi kukamilisha taarifa yake na kuiwasilisha kwenye Bunge zima kwa
ajili ya kujadiliwa. Baada ya Wajumbe
kujadili taarifa hiyo itafuatia kupiga kura ili kuamua kuhusu Sura hizo mbili. Kama yalivyo masharti ya Sheria ya Mabadiliko
ya Katiba, uamuzi utafanywa kwa theluthi
mbili ya kura za kila upande wa Muungano wetu.
Sababu za Baadhi ya Wajumbe Kususia
Bunge Maalumu la Katiba
Ndugu Wananchi;
Sote tumewasikia Wajumbe
wa Bunge Maalumu la Katiba waliosusia vikao vya Bunge hilo wakielezea sababu
zilizowafanya watoke Bungeni. Walitoa
matamko kwenye vyombo vya habari na pia katika mikutano ya hadhara
waliyoiitisha na kuhutubia sehemu mbalimbali nchini. Sababu walizotoa zimekuwa zikiongezeka na
kubadilika kadri siku zinavyosonga mbele na upepo wa kisiasa unavyokwenda.
Hivi sasa wanazungumzia mambo mawili. Kwanza, kwamba Bunge Maalumu halina mamlaka
ya kuifanyia mabadiliko yo yote Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa na Tume ya Mabadiliko
ya Katiba. Kwa maoni yao, kazi ya Bunge
Maalumu la Katiba ni kujadili na kupitisha tu Rasimu ya Katiba ya Tume na siyo
kubadili cho chote. Pili, wametoa sharti
la wao kurudi Bungeni ni kuhakikishiwa kwamba, kitakachojadiliwa Bungeni ni
Rasimu ya Tume. Bila ya sharti hilo kukubaliwa, wamesisitiza
kutorudi Bungeni.
Mamlaka ya Bunge Maalum la Katiba
Ndugu Wananchi;
Mimi nimehusika katika
kubuni wazo la kuwa na mchakato wa kuandika Katiba Mpya, na katika maandalizi
ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, ya kuongoza na kuendesha mchakato huo. Kwa kweli sikumbuki wakati wo wote katika
vikao vya Baraza la Mawaziri kujadili Rasimu ya Muswada wa Sheria ya Mabadiliko
ya Katiba tulipozungumzia Rasimu ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba kuwa haiwezi
kufanyiwa marekebisho na Bunge Maalumu la Katiba.
Mimi siyo Mwanasheria na
hivyo nakiri kwamba naweza kuwa na upungufu katika kuelewa maana ya baadhi ya
maneno ya kisheria. Hata hivyo, sikumbuki
kuwepo kwa kifungu cho chote katika Sheria kinachosema kuwa Bunge Maalumu la
Katiba halina mamlaka hayo. Tangu
tulipoyasikia maneno hayo yakisemwa nimeuliza nithibitishiwe ukweli wa madai
hayo bado sijaambiwa vinginevyo. Kama ukweli huo upo naomba anisaidie. Badala yake naambiwa kuwa maneno yaliyotumika
katika Sheria haiakisi dhana inayotolewa kuwa kazi ya Bunge Maalum la Katiba ni
kubariki Rasimu na siyo kufanya vinginevyo.
Nimeambiwa kuwa sheria inasemaTume
itaanda Rasimu ya Katiba na Bunge Maalum la Katiba litatunga Katiba
iliyopendekezwa.
Ndugu Wananchi;
Tarehe 30 Desemba, 2010,
nilipozungumzia dhamira yangu ya kuanzisha mchakato wa kuandika Katiba Mpya
nilieleza wazi nia ya kuwepo kwa uwakilishi mpana wa Watanzania katika mchakato
huo. Ndiyo maana katika Sheria tukaweka
ngazi nne katika mchakato wa kutunga
Katiba. Ngazi ya kwanza ikiwa ya
wananchi kutoa maoni yao juu ya kila wanachotaka kijumuishwe katika Katiba ya
nchi yao. Ngazi ya pili, ni ya wananchi
kupitia wawakilishi wao katika Mabaraza ya Katiba ya Wilaya na Mabaraza ya
Kitaasisi kutoa maoni yao kuhusu Rasimu ya kwanza ya Katiba iliyotayarishwa na
Tume.
Ngazi ya tatu inajumuisha
wawakilishi wa wananchi waliopo kwenye Mabaraza ya Kutunga Sheria ya Sehemu
zetu mbili za Muungano, yaani Bunge la Jamhuri ya Muungano na Baraza la Wawakilishi,
wakichanganyika na Wawakilishi wa makundi mbalimbali ya jamii ya Watanzania
kutoka pande zote mbili za Muungano.
Hawa ndio wanaounda Bunge Maalumu la Katiba, lenye jukumu la kutunga
Katiba inayopendekezwa.
Mamlaka ya kutunga Katiba
kwa mila na desturi za Mabaraza ya Kutunga Sheria ni uwezo wa kurekebisha,
kubadili, kufuta na hata kuongeza kilichopendekezwa. Ingekuwa kilichokusudiwa ni kubariki tu
lisingetumiwa neno la kutunga Katiba.
Hali kadhalika, lisingewepo sharti la kupiga kura na msisitizo wa kupata
theluthi mbili kwa kila upande wa Muungano.
Aidha, kama ingekuwa jukumu la Bunge Maalumu ni kubariki tu Rasimu lisingepewa
siku 70 za kazi na Rais kupewa
mamlaka ya kuongeza siku zaidi kadri aonavyo yeye inafaa.
Ngazi ya nne na ya mwisho,
tuliweka kura ya maoni ya wananchi kukubali au kukataa Katiba inayopendekezwa
na Bunge Maalumu la Katiba. Kama
ingekuwa Rasimu ya Tume haiwezi kubadilishwa hata nukta kwa nini basi tuweke
kura ya maoni ya kuwahusisha wananchi wote?
Ndugu Wananchi;
Tulizibuni ngazi hizi nne kwa dhana kwamba kile ambacho
hakikuonekana au hakikuwekwa sawa katika ngazi moja kitaonekana na kurekebishwa
katika ngazi inayofuata katika ngazi zile tatu za mwanzo. Na, iwapo Katiba iliyotungwa haitawaridhisha
wananchi wanayo haki ya kuikataa. Kwa kufanya hivyo, wananchi ndiyo waliopewa
turufu ya mwisho.
Ndugu wananchi;
Kwa
kweli, napata shida kuelewa mkanganyiko unatoka wapi na hasa wale wanaoongoza
kuhoji mamlaka ya Bunge Maalumu kuwa ni wale wale waliotunga Sheria ya
Mabadiliko ya Katiba tena hatua kwa hatua. Nashangazwa zaidi ninapoona wale
wale waliotunga Kanuni za Bunge Maalumu ndiyo wanaoongoza kuhoji uhalali wa
kile walichokitunga.
Kanuni za Bunge Maalumu la
Katiba, Ibara ya 33 (8) inasema: Nanukuu:
“Wakati wa mjadala, Mjumbe yoyote anaweza kutoa mapendekezo ya
marekebisho, maboresho au mabadiliko yaliyomo katika Sura za Rasimu ya Katiba
zinazojadiliwa kwa utaratibu ufuatao: (a)
Ikiwa ni marekebisho, maboresho au mabadiliko yanayobadilisha jambo la
msingi, au yanayobadilisha maudhui ya Ibara, mapendekezo ya marekebisho
yatapelekwa kwa maandishi kwa Katibu siku moja kabla ya mjadala wa Ibara
husika. (b) Ikiwa ni marekebisho madogo,
ambayo hayabadili msingi au maana, mapendekezo ya marekebisho yatawasilishwa na
mjumbe wakati wa mjadala baada ya kupata ruhusa ya Mwenyekiti”. Mwisho wa kunukuu.
Kanuni hii ilipotungwa, Wajumbe
wote wa Bunge Maalumu pamoja na wale ambao baadae walisusia vikao vya Bunge walikuwepo
Bungeni na walishiriki kuipitisha. Tena
basi, baadhi yao walikuwa Wajumbe wa Kamati ya Kanuni iliyopendekeza Kanuni
hizo. Unapowaona watu wale wale sasa
wanakuwa vinara wa kuhoji mamlaka ya Bunge Maalumu la Katiba, unajiuliza
maswali mengi kuhusu watu hao bila ya kupata majibu yaliyo sahihi na
kutosheleza akili na ufahamu wetu.
Ndugu Wananchi;
Unaposoma Sheria ya
Mabadiliko ya Katiba na Kanuni za Bunge Maalumu, hii ni dhahiri kwamba wote
walikuwa na uelewa wa pamoja kuhusu mamlaka ya Bunge Maalumu ya kujadili Rasimu iliyoandaliwa na Tume na
kutunga Katiba inayopendekezwa kwa wananchi kwa ajili ya kupigiwa kura.
Kinachojadiliwa Bungeni ni Rasimu ya Tume
Ndugu Wananchi;
Yapo madai yanayotolewa na
kuenezwa na Wajumbe waliosusia Bunge Maalumu la Katiba kwamba kinachojadiliwa
Bungeni siyo Rasimu ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba, ndiyo maana basi wanaweka
sharti la kujadiliwa Rasimu ya Tume ya Jaji Warioba ndipo warudi Bungeni. Madai haya nayo yananipa taabu
kuyaelewa. Ndugu zetu hawa walishiriki
siku zote 19 za Kamati 12 zilipokutana kujadili Sura ya Kwanza na ya Sita za Rasimu
ya Tume. Halikadhalika. walikuwepo na
kushiriki kwa ukamilifu wakati taarifa za Kamati, tangu ya Kwanza mpaka ya 12, zilipowasilishwa
kwenye Bunge zima. Aidha, na wao walishiriki
kutoa maoni ya wachache kwa dakika 20
na kutoa ufafanuzi kwa muda wa dakika 30 kwa kila Kamati. Haya maneno ya sasa kwamba kinachojadiliwa
Bungeni siyo Rasimu ya Tume ya Jaji Warioba bali nyingine kabisa ambayo wanadai
eti ni ya CCM yanatoka wapi.
Mimi nadhani kuwa huenda
katika Kamati kumefanyika marekebisho kwenye Rasimu ambayo
hayakuwapendeza. Kama hivyo ndivyo, wawe
wakweli kuhusu jambo hilo kuliko kusema mambo yasiyowakilisha ukweli halisi wa
Rasimu inayojadiliwa. Matokeo yake ni
kuwafanya wafuasi wao na wapenzi wao na hata watu wengine waamini kuwa
kinachojadiliwa siyo Rasimu ya Tume ya Jaji Warioba bali nyingine tena ni ya
CCM. Jambo hilo si kweli na wenyewe
wanajua kwamba si kweli ila sijui kwa nini wameamua kupotosha ukweli.
Ndugu Wananchi;
Kinachonishangaza, zaidi ni
kwamba, kama hawakuridhishwa na yaliyofanyika, kwa nini wasingetumia mifumo
waliyojitengenezea wenyewe kwenye Kanuni kumaliza tofauti zao? Kanuni zinaelekeza kuwa mambo wasiyoridhika
nayo yajadiliwe kwenye Kamati ya Mashauriano na Maridhiano. Ukiacha mifumo ya maridhiano ndani ya Bunge
ukaenda nje kwa wananchi au vyombo vya habari na mitandao si jawabu la tatizo.
Ndugu Wananchi;
Ndiyo maana nashawishika
kuunga mkono wale wote wanaowasihi Wajumbe wa CHADEMA, CUF na NCCR-Mageuzi na
wengine warejee Bungeni. Watumie mifumo
maalum ya Bunge iliyowekwa na Kanuni kutafuta maridhiano. Hali kadhalika, wasichoke kuwa na mawasiliano
na vyama vingine vya siasa na hasa CCM kutafuta maelewano. Mimi niko tayari kusaidia pale watakapoona
inafaa kufanya hivyo kama ambavyo nimekuwa nikifanya ziku za nyuma.
Nililolisema mwanzoni
kabisa mwa mchakato na nalirudia tena
leo kwamba, ili tuweze kufanikiwa kupata Katiba Mpya ambayo sote tunaitaka,
maelewano baina ya wadau wakuu wa kisiasa ni jambo lisilokuwa na badala
yake. Vinginevyo kupata theluthi mbili
kwa pande zote mbili za Muungano haitawezekana.
Ndiyo maana nampongeza sana Msajili wa Vyama vya Siasa, Mheshimiwa Jaji
Francis Mutungi, kwa uamuzi wa kuvikutanisha vyama vinne vikuu vya siasa
kujadili namna ya kuondoa mtihani uliopo sasa katika mchakato wa Katiba.
Ombi langu kwa viongozi wa
vyama hivyo ni kuitumia vyema fursa ya majadiliano kuukwamua mchakato kwa
maslahi ya nchi yetu na watu wake. Hali
kadhalika nampongeza sana Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Mheshimiwa
Samwel Sitta, kwa kuitisha kikao cha
Kamati ya Mashauriano na Maridhiano. Bahati
mbaya ni kwamba Wajumbe wa vyama vilivyosusia Bunge Maalumu hawakushiriki. Ni matumaini yangu kuwa Mheshimiwa Sitta
hatokata tamaa kuendeleza juhudi za mashauriano na kwamba katika vikao vijavyo
na wenzetu hawa watashiriki.
Ndugu Wananchi;
Hivi
karibuni kumekuwepo pia madai yanayoelekeza lawama kwangu. Kwanza nalaumiwa eti kuwa mambo yalikuwa
yanaenda vizuri mpaka pale nilipotoa hotuba ya ufunguzi wa Bunge Maalumu ndipo
yalipoharibika. Pili nalaumiwa kwamba
nawezaje kuikana Rasimu ya Katiba ambayo na mimi ni mmoja wa watu waliotia
sahihi katika Rasimu hiyo.
Niruhusuni
nianze na hili la pili. Nadhani ndugu
zetu wanaotoa madai haya yameitafsiri isivyo sahihi yangu katika Gazeti la Serikali
lililotangaza rasmi Rasimu ya Katiba na Taarifa ya Tume ya Mabadiliko ya
Katiba. Kwa mujibu wa Sheria ya
Mabadiliko ya Katiba baada ya Tume kumaliza kazi yake ya kuandika Rasimu ya
Katiba, Rais wa Jamhuri ya Muungano amepewa kazi tatu kufanya. Kwanza, kupokea Rasimu hiyo na Taarifa ya
Tume kutoka kwa Mwenyekiti jambo ambalo lilifanywa tarehe 30 Desemba,
2013. Pili, amepewa kazi ya kuitangaza
rasmi Rasimu ya Katiba na Taarifa ya Tume kwa watu wote kuiona na kuisoma ndani
ya siku 30. Alipewa sharti la kuitangaza
katika Gazeti la Serikali na vyombo vingine vya habari. Hili nalo lilifanywa hivyo tarehe 22 Januari,
2014.
Ndugu Wananchi;
Katika
kutangaza katika Gazeti la Serikali sharti linamtaka anayetangaza ajitambulishe
kuwa yeye ni nani na atie sahihi yake.
Kwa kufanya hivyo, hakumfanyi yeye kuwa naye ni mhusika na maudhui ya
kila kinachopendekezwa na Tume. Sahihi
zilizomo ndani ya Rasimu na Taarifa ya Tume ni za Wajumbe wa Tume, kamwe sahihi
ya Rais haimo hivyo hawezi kulaumiwa kuwa anaikana sahihi yake. Yeye ametimiza wajibu wake wa kutangaza, akaiweka
hadharini kwa umma wa Watanzania kuiona na kusoma Rasimu ya Katiba na Taarifa
ya Tume vilivyotayarishwa na kutiwa sahihi na Wajumbe wa Tume ya Mabadiliko
ya Katiba. Kazi ya tatu ni kuitisha
Bunge Maalumu ambayo nayo imekamilika tangu tarehe 18 Februari, 2014.
Ndugu Wananchi,
Jambo
lingine linalofanana na hilo ni yale madai kwamba nilikuwa napata taarifa ya
maendeleo ya mchakato ndani ya Tume mara kwa mara, iweje leo nitoe maoni tofauti
kama niliyoyatoa katika hotuba yangu kwenye Bunge Maalumu. Ni kweli kabisa Mwenyekiti wa Tume ya
Mabadiliko ya Katiba, Mheshimiwa Jaji Joseph Warioba, Makamu wake, Mheshimiwa
Jaji Agustino Ramadhani na Mheshimiwa Dkt. Salim Ahmed Salim wamekutana na mimi
kwa nyakati mbalimbali kuzungumzia mwenendo wa mchakato. Lakini, hayakuwa mazungumzo ya kina kuhusu
nini kiwe vipi katika maudhui na mapendekezo ya Tume. Ukweli ni kwamba Rasimu zote mbili nilizipata
mara ya kwanza nilipokabidhiwa rasmi, tena kwa uwazi. Napenda watu wasijenge dhana kuwa nilipewa
Rasimu na kuisoma kabla ya kukamilika na hivyo nilitoa maoni yangu. Tume hii ilikuwa huru na niliiacha iwe
hivyo. Sikuiingilia kwa namna yo yote
ile kupenyeza mambo ninayotaka yawemo.
Kuthibitisha dhamira yangu ya kutaka Tume iwe huru katika kufanya kazi
zao hata pale waliponitaka nitoe maoni niliwaomba tusifanye hivyo ili
nisiwakwaze katika kufanya kazi zao, wakapata taabu ya kuwianisha wanayofikiria
na mawazo yangu.
Ndugu Wananchi;
Kuhusu madai
kwamba mambo yalikuwa yanakwenda vizuri na kwamba hotuba yangu iliyavuruga,
napenda kusema wazi kuwa lawama hizo hazina ukweli wo wote. Ni madai yasiyokuwa na msingi. Kwani mimi hasa siku ile nilifanya lipi la
ajabu. Ukweli ni kwamba nilisema yale
yale ambayo Tume yenyewe imeyasema katika Rasimu ya Katiba na Taarifa za
Tume. Niliyoyasema kuhusu malalamiko ya
watu wa pande zetu za Muungano na uzuri na changamoto za miundo ya Serikali
mbili na Serikali tatu ni yale yale yaliyomo kwenye taarifa za Tume. Nimetumia takwimu zile zile za Tume. Pengine kilichoonekana kuwa kibaya ni jinsi
nilivyozifasiri taarifa hizo na mapendekezo ya Tume.
Jambo
lingine ambalo nimelifanya ni kutoa maoni yangu kuhusu baadhi ya vipengele vya
Rasimu hususan uandishi na dhana mbalimbali zilizokuwamo. Silioni kosa langu kwa kufanya hivyo, kwani
Rasimu imetolewa hadharani kwa watu kuijadili.
Na mimi kama raia ninayo haki ya kufanya hivyo kama wafanyavyo wengine. Kwa nini nilaumiwe kwa kutumia haki yangu hiyo.
Lakini, pia
mimi ndiye Rais wa nchi yetu, ninayo dhamana ya uongozi na ulezi wa taifa
letu. Itakuwaje kwa jambo kubwa la hatma
ya nchi yetu nilinyamazie kimya.
Watanzania wangeshangaa na wangekuwa na haki ya kuhoji Rais wao ana
maoni gani. Bahati nzuri nilitoa maoni
yangu mahali penyewe hasa, na kwa uwazi, kwenye Bunge Maalumu la Katiba. Hata hivyo, ni muhimu kusisitiza kuwa namna
nilvyotoa maoni yangu sikuwa natoa maagizo wala kushurutisha, ndiyo maana kila
wakati niliwakumbusha Wajumbe kuwa mamlaka ya uamuzi ni yao. Yangu yalikuwa
maoni tu wanahiyari ya kuyakubali au kuyakataa.
Niliwataka Wajumbe wasome na
kuielewa vyema Rasimu. Nilisema wasome
sura kwa sura, mstari kwa mstari na neno kwa neno. Niliwaomba wajiridhishe kuhusu uandishi na
dhana mbalimbali. Nilitoa mifano ya
mambo yahusuyo uandishi ambayo ni vyema wayatazame. Pia nilitoa mifano ya dhana ambazo niliwasihi
wajiridhishe juu ya kufaa kwake kuwepo.
Kuhusu muundo wa Serikali tatu, nilieleza
wazi kuwa sina tatizo nao kama ndiyo matakwa ya Watanzania. Lakini, nilieleza hofu yangu kuhusu
mapendekezo ya Tume na kuwataka Wajumbe wafanye kazi ya ziada kuondosha udhaifu
iwapo wataukubali muundo unaopendekezwa.
Nilieleza nia yangu ya kutaka tuwe na Serikali ya Muungano yenye ukuu
unaoonekana, yenye nguvu ya kuweza kusimama yenyewe, inayoweza kuwa tegemeo kwa
nchi Washirika, Serikali isiyokuwa tegemezi wala egemezi kwa nchi washirika na ambayo
inavyo vyanzo vya uhakika vya mapato.
Hivi kwa kutoa ushauri huo kwa Wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba
inageuka kuwa nongwa. Kwa kweli sielewi
lawama ni ya nini?.
Naamini sistahili
lawama bali pongezi kwa kuwa muwazi na kutoa ushauri wa msingi ambao utasaidia
nchi kupata Katiba nzuri inayojali maslahi ya watu wa nchi yetu na ya nchi zetu
mbili zilizoungana miaka 50 iliyopita.
Hitimisho
Ndugu Wananchi;
Mwisho, ni
maoni yangu ya dhati kuwa mgogoro uliopo sasa katika mchakato wa Katiba hauna
sababu ya kuendelea kuwepo. Naamini hayo
yote ambayo Wajumbe wa CHADEMA, CUF na NCCR-Mageuzi wanayalalamikia yanaweza
kushughulikiwa kwa ukamilifu katika mifumo ya Bunge Maalumu la Katiba
iliyotengenezwa na Wajumbe wote na wao wakiwemo. Nawasihi waitumie. Hali kadhalika, kwa kupitia mazungumzo wanayofanya
na wenzao wa Chama cha Mapinduzi wanaweza kutengeneza nguvu ya pamoja kutatua
changamoto za sasa na zitakazojitokeza baadaye.
Kilicho muhimu ni kwa pande zote kuwa na dhamira ya dhati ya kutoka hapa
tulipo sasa. Kama utashi wa kisiasa upo
kwa kila mmoja wetu, hilo ni jambo linalowezekana kabisa. Narudia kuahidi
utayari wangu wa kusaidia kadri inavyowezekana tusonge mbele.
Mungu Ibariki Afrika!
Mungu Ibariki Tanzania!
Asanteni sana kwa kunisikiliza.
COMMENTS