*Ukadiriaji wanafunzi wakifeli wazikwa rasmi *Mfumo upangaji madaraja nao wabadilishwa *Utaanza na mtihani wa ‘moko’ kida...
*Ukadiriaji
wanafunzi wakifeli wazikwa rasmi
*Mfumo
upangaji madaraja nao wabadilishwa
*Utaanza
na mtihani wa ‘moko’ kidato cha nne
USAHIHISHAJI
mpya wa mitihani ya Taifa kwa kidato cha nne na sita, unaoendana na utaratibu
mpya wa upangaji wa ufaulu na madaraja, unatarajiwa kuanza kutumika katika
mtihani wa majaribio wa kidato cha nne mwaka huu nchini kote, na kufuatiwa na
mitihani yote ya kidato cha nne na sita.
Akitangaza
mabadiliko hayo muhimu jana Dar es Salaam, Katibu Mtendaji wa Baraza la
Mitihani (Necta), Dk Charles Msonde, alisema tayari maelekezo kuhusu mabadiliko
hayo, yameshatolewa kwa wakuu wa shule za sekondari nchini.
Baadhi
ya faida ya mabadiliko hayo kwa mujibu wa Dk Msonde, ni pamoja na kuondoa
ukadiriaji wa alama za ufaulu, uliokuwa ukitumiwa awali, kuweka uwazi katika
usahihishaji na kumwezesha mwanafunzi kukokotoa ufaulu wake hata kabla ya
matokeo na hata mwalimu kukotoa ufaulu wa wanafunzi wake kabla hata ya matokeo.
Kwa
mujibu wa Dk Msonde, mwalimu na mwanafunzi wataweza kukokotoa alama za ufaulu,
kwa kuwa majibu yanayotumika kusahisha mitihani kila mwaka na namna wanafunzi
walivyojibu, yatarejeshwa shuleni, ili mwalimu afahamu hali ya wanafunzi na
ufundishaji.
Pili
kwa mujibu wa Dk Msonde mabadiliko ya sasa, yatamwezesha mwalimu kufahamu shida
ya wanafunzi wake kulingana na taarifa ya ufaulu wa waliopita na kufahamu wapi
patumike mbinu gani kuinua ufaulu.
*Ukadiriaji
Kwa
mujibu wa Dk Msonde, mabadiliko hayo yanaanza katika mfumo wa viwango vya
ufaulu, kutoka katika Mfumo wa Viwango vya Ufaulu Vinavyobadilika, kwenda
katika Mfumo wa Viwango vya Ufaulu Visivyobadilika.
Mfumo
wa Viwango vya Ufaulu Vinavyobadilika, Dk Msonde alisema ulianza kutumia tangu
mwaka 1973, wakati Necta ilipoanzishwa mpaka 2011.
Akifafanua
kuhusu mfumo huo ulioachwa mwaka 2011 na kuzikwa rasmi kuanzia mwaka huu, Dk
Msonde alisema wanafunzi wakifeli sana, Necta ililazimika kukadiria viwango vya
ufaulu kuwa vya chini kabla ya kutoa matokeo.
Alisema
walikuwa wakiangalia wastani wa ufaulu na kulinganisha na mwaka uliopita, kama
ni wa chini waliangalia waliofaulu sana na waliofeli sana, kisha
waliangalia tofauti ya alama ya ufaulu kati ya waliofaulu na baada ya hapo
walikuwa wakibadilisha viwango vya ufaulu kuwa vya chini kabla ya kutoa
matokeo.
Alitoa
mfano, kama mwaka uliopita wastani viwango vya ufaulu wa somo kama Historia
ulikuwa 60 na mwaka huo wastani huo ukashuka kuwa 40, ilikuwa ishara ya kwanza
kuwa somo husika mwaka huo wamefeli sana.
Kutokana
na hali hiyo, alisema kama alama A ilianzia 80 mpaka 100, Necta iliweza
kushusha ianzie 70 mpaka 100, ili hata waliopaswa kuwa na alama B, wapande
kidogo na hivyo hivyo katika alama zinazofuata.
“Hivyo
katika mfumo huu, viwango vya ufaulu hupangwa kwa kutegemea watahiniwa
walivyofaulu somo husika, hivyo viwango hivyo vya ufaulu hutofautiana baina ya
somo na somo na kati ya mwaka mmoja na mwingine,” alisema Dk Msonde.
Matokeo
yake, Dk Msonde alisema viwango vya ufaulu vilikuwa siri na Baraza halikuwahi
kueleza popote kuhusu usiri huo na wadau walikuwa na habari za kupotosha kuwa A
ilikuwa inaanzia 81 na D ikianzia 21, wakati katika hali halisi kuna wakati
viwango hivyo vilishuka.
*Kuzika
ukadiriaji
Kuanzia
mwaka huu Mfumo wa Viwango vya Ufaulu Visivyobadilika, unaanza kutumika na
viwango hivyo ni vipya baada ya kupangwa kwa kuangalia mwenendo wa ufaulu wa
miaka 12, kuanzia 1999 hadi 2011.
Dk
Msonde alisema katika miaka hiyo 12 ya kuangalia, A ya juu ilikuwa mwaka
1999 na 2011, ambapo ilianzia 70 mpaka 90. Alisema hakuna mwaka A
ilishuka chini ya 70. Alama D katika miaka hiyo 12, ilianzia 30 mpaka 45.
Baada
ya kupata alama hizo, Dk Msonde alisema walitafuta wastani wa A katika miaka
hiyo 12 ambao ulikuwa ni 76.2 na wengi waliopata A ya chini katika muda huo
ilikuwa 75.
Katika
kutafuta wastani wa D katika miaka hiyo 12, ulikuwa 33.3 na D iliyotumika sana
katika miaka hiyo ilikuwa 30 ndipo wakaamua kuweka viwango vipya vya ufaulu.
*Viwango
vipya
Baada
ya wastani huo, Dk Msonde alisema walianza kupanga viwango vipya vya ufaulu
ambavyo vitatumika katika usahihishaji wa mtihani wa taifa wa kidato cha nne na
mtihani wa taifa wa kidato cha sita, ambao hautakuwa na tofauti katika ya
mitihani hiyo.
Kabla
ya viwango hivyo, kidato cha sita kilikuwa na alama saba za ufaulu, yaani A, B,
C, D, E, S na F wakati kidato cha nne kilikuwa na alama sita za ufaulu, yaani
A, B, C, D na F.
Katika
viwango vipya kutakuwa na alama saba za ufaulu kwa mitihani yote ya kidato cha
nne na kidato cha sita, ambayo ni A ambayo itaanzia (75-100), tafsiria yake ni
Bora sana.
Kutakuwa
na B+ (60-74, vizuri sana); B (50-59, vizuri); C (40-49, wastani); D (30-39,
inaridhisha); E (20-29; hairidhishi) na F (0-19, amefeli).
*
Madaraja zamani
Mbali
na mabadiliko katika viwango vya ufaulu, mabadiliko mengine yaliyofanyika ni
katika ukokotoaji wa madaraja ya ufaulu, kutoka Mfumo wa Ukokotoaji wa Jumla wa
Pointi (TPGS), ambao umekuwa ukitumiwa tangu 1973 mpaka 2014 kwenda Mfumo
wa Wastani wa Ukokotoaji wa Pointi (GPA) utakaotumika katika matokeo ya kidato
cha nne ya mwakani.
Katika
mfumo wa TPGS, alama A ilikuwa na pointi 1; alama B+, pointi 2; B, pointi 3; C
pointi 4; D pointi 5; E pointi 6 na F pointi 7.
Kwa
kuwa upangaji wa madaraja, uliangalia masomo saba ambayo mwanafunzi alifaulu
zaidi, mwanafunzi aliyefaulu sana katika mfumo huo, kwa maana ya kupata alama A
masomo yote saba, alipata Daraja la Kwanza lenye pointi saba, kwa maana
na kila somo pointi moja.
*Madaraja
mapya
Katika
mfumo wa GPA, Dk Msonde alisema alama A inakuwa na pointi 5; B+, pointi 4, B
pointi 3; C pointi 2; D pointi 1; E pointi 0.5 na F pointi 0. Katika hilo,
mtahiniwa ataanza kuhesabika amefaulu somo endapo atapata alama D, ambayo ni
sawa na pointi 1.
Akielezea
namna alama hizo zitakavyotumika kupanga madaraja, Dk Msonde alisema mfumo
utakuwa kujumlisha alama za ufaulu za mwanzo katika masomo saba na kugawanya
kwa saba, hivyo mwanafunzi atakayefaulu sana na kupata alama A katika masomo
saba, atapata jumla ya alama 35, ambayo ikigawanywa kwa masomo hayo saba,
atapata pointi 5, ambayo ndiyo utaulu wa juu utakaoitwa ‘Distinction’.
Hivyo
madaraja mapya kwa kidato cha nne yatakuwa daraja la kwanza ‘Distinction’
pointi (3.6-5.0); pili ‘Merit’ (2.6-3.5); tatu ‘credit’ (1.6-2.5);
nne pass (0.3-1.5) na aliyefeli ‘fail’ (0.0-0.2).
Kwa
kidato cha sita, atakayefaulu sana kupata A katika masomo matatu ya ‘combination’,
atakuwa amepata jumla ya pointi 15 na ukigawanya kwa tatu, yaani masomo
matatu ya ‘combination’, naye atapata 5.
Hivyo
madaraja mapya kwa kidato cha sita yatakuwa daraja la kwanza ‘Distinction’
pointi (3.7-5.0); pili ‘Merit’ (3.0-3.6); tatu ‘Credit’ (1.7-2.9); nne ‘pass’
(0.7-1.6) na aliyefeli ‘fail’ (0.0-0.6).
source:Habarileo
COMMENTS