Taarifa kwa Vyombo Vya Habari, 30 Octoba 2014 Sikika imesikitishwa na tamko lililotolewa na Waziri wa Afya na Ustawi wa Ja...
Sikika imesikitishwa na tamko lililotolewa na Waziri wa Afya na
Ustawi wa Jamii, kuhusiana na kushindwa kwa vituo vya huduma za afya kununua
dawa MSD kutokana na kuongezeka kwa deni. Ni wazi kuwa waziri hajalipa tatizo
hili uzito unaotakiwa na kutambua kuwa baadhi ya wagonjwa wanaweza kupoteza
maisha kutokana na tatizo hili.
Sikika inatambua kuwa, mapato yatokanayo na uchangiaji katika
huduma za afya ni moja tu ya vyanzo vinavyotumika katika kuongeza upatikanaji
wa dawa na vifaa tiba nchini. Na pia inatambua kuwa chanzo hiki pekee hakiwezi
kuziba pengo kubwa la ufinyu wa bajeti ya dawa na vifaa tiba muhimu ambao
hauendani na mahitaji halisi. Kwa mfano, makadirio ya mahitaji ya dawa nchini
kwa mwaka wa fedha 2014/15 ni shilingi bilioni 500 lakini bajeti iliyopangwa na
kupitishwa ni shilingi bilioni 70.5 ambayo inakidhi mahitaji kwa asilimia 14
tu!
Sikika inapenda kuikumbusha Wizara ya Afya na Ustawi wa jamii
kuwa, takribani asilimia 75 ya wagonjwa wanaopata huduma katika hospitali
za Manispaa wapo katika kundi la msamaha wa huduma za afya. Kundi hili
linahusisha wajawazito, watoto chini ya miaka mitano, wazee, watu wenye magonjwa
sugu, watu wasiojiweza pamoja na watu wenye ulemavu. Hii inamaanisha kuwa
Serikali inategemea asilimia 25 tu ya wagonjwa wanaoweza kuchangia huduma
kama chanzo kikuu cha fedha za dawa zitokanazo na uchangiaji.
Serikali inatakiwa kuwajibika katika hili na sio kuwatupia mzigo wananchi
wachache.
Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii atambue kuwa, kuzitaka hospitali
kulipa deni la MSD kwa kutumia fedha za uchangiaji badala ya kutumia fedha hizo
kununua dawa kutokana na ufinyu wa bajeti, ni chanzo cha kuzifanya hospitali
hizo kuendelea kukopa zaidi na hivyo kuendelea kukuza tatizo badala ya
kutafuta suluhu. Tunamkumbusha kwamba hili ni tatizo linalotokana mfululizo wa
upangaji wa bajeti finyu kwa makusudi. Baadhi ya hospitali hizi zimekuwa
zikitumia fedha za uchangiaji kununua dawa lakini bado zina madeni. Kwa hiyo,
agizo la Waziri halitakuwa na tija katika kutatua tatizo hili kwa sasa.
Hii sio mara ya kwanza kwa Wizara ya Afya kuzitaka hospitali
kupeleka MSD asilimia 50 ya mapato yao uchangiaji. Agizo hili limekuwa
likijirudia tangu mwaka 2012 bila ya kuwa na usimamizi katika utekelezaji na
ufuatiliaji. Kwa mfano, mwezi Julai 2014, Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii
aliziagiza hospitali zote kupeleka MSD asilimia 50 ya mapato yao. Kwa kuwa
agizo hili limekuwa likishindwa kutatua tatizo la upatikanaji wa dawa,
tulitarajia mbinu mbadala kutoka serikalini.
Sikika ingependa pia kujua ni jinsi gani hospitali ya Taifa, za
rufaa na maalumu ambazo zinachangia asilimia kubwa ya deni (67%) katika kundi
la madeni ya vituo vya huduma za afya zitalipa deni hilo, kwani agizo la waziri
lililenga hospitali za wilaya na mikoa pekee. Vile vile,
tungependa kujua Wizara imeweka mipango gani katika kulipa deni lake ambalo ni
zaidi ya asilimia 70 ya deni lote ambalo MSD wanadai. Deni hilo la Wizara
linatokana na gharama za kugomboa, kuhifadhi na kusambaza bidhaa za miradi
misonge (vertical programs).
Mbali na hilo, tamko la Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kwa Umma
la tarehe 27 Oktoba 2014 linaeleza kuwa, Serikali imekuwa ikilipa Deni la MSD
kwa awamu. Hata hivyo, Waziri hakuweka wazi kwamba pamoja na kulipa kwa awamu,
deni limekuwa likiongezeka kwa sababu serikali inalipa kiwango kidogo na kukopa
kiwango kikubwa. Kwa mfano, mwaka 2013 deni lilikuwa kiasi cha Tsh. bilioni
76.4 lakini kufikia Septemba 2014 deni limekuwa na kufikia kiasi cha Tsh.
bilioni 102 ingawa serikali ilifanya malipo ya Tsh. bilioni 10 .
Sikika ingependa kupata ufafanuzi kutoka kwa Waziri wa Afya na
Naibu Waziri wa Wizara ya Fedha, Mh. Mwigulu Nchemba ambaye hivi karibuni
alinukuliwa na baadhi ya magazeti akisema kuwa kiasi cha fedha zilizotolewa kwa
ajili ya dawa katika mwaka 2013/14 ilikuwa Tsh. bilioni 47 lakini ni Tsh.
bilioni 7 tu ndizo zilitumika katika kununua dawa. Sikika, pamoja na watanzania
wote, ingependa kujua ni wapi fedha hizi zimepelekwa na ni kwa
sababu zipi hususan katika kipindi hiki cha uhaba wa dawa na vifaa
tiba katika vituo vya huduma za afya.
Sikika pia ingependa kutoa ufafanuzi kwa umma kwamba misaada
iliyositishwa na wafadhili ni kwenye bajeti ya kuu tu (General Budget
support) na si kwenye mfuko wa pamoja wa sekta ya afya (Health Basket
Fund). Kwa kipindi cha Julai-Septemba 2014, zaidi ya Tsh bilioni 20
zilitolewa na wafadhili kwa ajili ya kusaidia halmashauri zote nchini ambapo kwa
kawaida, theluthi moja ya fedha hizo inapaswa kutumika kwa ajili ya manununzi
ya dawa na vifaa tiba muhimu.
Sikika inatambua juhudi za serikali kujumuisha sekta ya afya
katika mpango wa matokeo makubwa sasa (BRN), ambao kwa kiasi unaweza kuchangia
kupunguza uhaba sugu wa dawa na vifaa tiba katika vituo vya huduma
za afya vya umma. Hata hivyo, mpango huo utaanza kutekelezwa rasmi mwaka wa
fedha 2015/16, hivyo hauwezi kutatua tatizo la sasa la dawa. Waziri atambue
kwamba wagonjwa wanateseka na pengine baadhi kufariki kwa sababu ya ukosefu huu
wa dawa na vifaa tiba.
Mwisho, Sikika inaitaka Wizara ya afya na Ustawi wa Jamii kuchukua
hatua za haraka katika kutatua tatizo hili sugu la ukosefu wa dawa na vifaa
tiba katika vituo vya huduma za afya vya umma. Uhaba wa dawa unawanyima
wananchi kupata haki ya huduma bora za afya ambazo huweza kusababisha vifo.
Serikali inapaswa kulipa deni la MSD na kuwezesha upatikanaji wa dawa na vifaa
tiba kwa dharura na haraka. Sio haki kwa serikali yoyote kuacha wananchi wake
wakiteseka ama kupoteza maisha kutokanana sababu zinazoweza kuzuilika.
Mr. Irenei Kiria,
Executive Director of Sikika,
P. O. Box 12183 Dar es Salaam,
Tel: +255 222 666355/57, Fax: 2668015, Email: info@sikika.or.tz, Twitter: @sikika1, Facebook: Sikika Tanzania, Website: www.sikika.or.tz
COMMENTS