WIKI iliyopita tuliona majibu ya mama Kibua kwa mwane kuhusu udugu wake na Silvesta na kulitokea nini baada ya yeye kuachana na mzazi...
WIKI iliyopita tuliona majibu ya mama Kibua kwa mwane kuhusu
udugu wake na Silvesta na kulitokea nini baada ya yeye kuachana na mzazi
mwenzake. Je kunaendelea nini katika maisha ya Kibua. Beda Msimbe anasimulia
zaidi.
“Sikia baba wewe ndiwe unayenianzishia matanga katika maisha
yangu ningali hai” alisema Kibua kwa hasira baada ya baba yake kusema kwamba
hawezi kuwa na mtoto kahaba, bazazi kama yeye.
Maneno ya baba yake yalimchoma kama mkuki moyoni hasa baada ya
m zee huyo akiwa na mkewe, kumzodoa
Kibua ambaye alifika hapo baada ya mama yake kumweleza ukweli kuwa
juhudi za kumpeleka baba yake pale nyumbani zimeshindikana na hataki hata
kusikia kwamba ana mtoto kwa jinsi anavyotia kinyaa.
Baada ya mama yake kusema hayo Kibua hakutaka hata kumjibu,
alichofanya aliingia ndani akavaa nguo za ushauri akajitanda mtandio na
kuelekea kwa baba yake ambaye hajawahi kumuona wala kumsikia kwa miaka yote.
Alipofika pale alimkuta Silvesta ambaye alikuwa akifunga mbuzi kisha kumwamkua alimkaribisha
nyumbani pale na kwenda kuwaita wazazi wake ambaow alikuwa katika nyumba ya
jiko.
Alipomuona,mama yake Silvesta aliiona sura ya mtoto wake pale
akashindwa kuelewa.
“karibu ndani”
Kauli ya karibu ilimuingiza Kibua ndani ambaye aliwasalimia
wazazi wake wale kwa adabu kubwa.
“Mimi naitwa Kibua, nimefika hapa kuzungumza na baba ambaye
hanitambui tangu kuzaliwa kwangu hadi leo”
“Taratibu mwali, umesema unaitwa Kibua”
“Ona mai (ndio mama) “ alisema kwa kikwao akiachana na kiswahili
tena kwa adabu kubwa.
“Mtoto wa nani?” aliuliza tena.
Hakumjibu na badala yake akamtazama baba yake na kunyanyua
mdomo.
“Baba unaweza kujibu?”
Hapo ndipo maneno ya hovyo yalipoanza kumtoka Baba Slivesta,
maneno ambayo yalimkera sana binti huyo ambaye alishakuwa kama mwehu kutokana na kusimangwa.
“Sikia baba umesema maneno mengi sana. Naweza kuwa mtovu wa
adabu kukukaripia kwa kushindwa kunirejesha kitandani wewe na mwenzako, kukataa
kabisa kumuona mama yangu pamoja na kumtafadhalisha kwamba utaendelea kumpenda.
Umenikana kiasi ya mama kutokusema kitu bali baba yangu amekufa”
“Ndio baba yako amekufa”
“We mzee we usilete majanga hapa duniani.Usinifanyie matanga
katika maisha, mimi bado nipo hai , usibane maisha yangu kwa starehe zako.”
“Starehe zangu, hebu ondoka hapa” alisema kwa ghadhabu na kutaka
kuinuka akashikwa na mkewe pale.
“Mama wala usimshike.Mwache aje anipige kama kuna tusi
nimemfanyia kuliko yeye. Sikuja hapa kumdai kitu chochote. Nimekuja hapa
aniambie mimi ni mwanae au si mwanae na kama mimi si mwanae nijue nitampata
wapi baba yangu, kwani lazima nitambike na lazima watu waje kula mahali.”
Baba akawa anatetemeka.
Akaketi chini na kumwangalia. Hakujibu.
“Sikia baba kama mimi si mwanao, mruhusu Silvesta aje atoe
mahali. Alisema mwenyewe amependa bodi hili”
Akasema kwa maringo.
“Unasemaje?” alimaka.
“Silvesta juzi ulisema
nini pale mgahawani?”
“Lakini sista si
tulimaliza pale pale?”
“Hatujamaliza, baba anasema mimi si mwanae.Lete posa
nitaikubali” alinyanyuka na kuanza kuondoka.
“Sista haiwezekani.Nimepewa taarifa zote. Baba anaweza kusema
hakujui. Mimi nimefurahi kwamba nina dada nilidhani nipo peke yangu.”
Akamtazama, akatabasamu.
“Msikilize baba yako, mimi nakuachia huru kuamua kuja kunioa
kama ulivyotaka au kwa vyovyote vile. Karibu kwetu.Lakini ukija ujuwe umemsikia
baba yako”
Akajitupia khanga yake na kwa maringo akaondoka katika eneo lile taratibu akijua
kuwa ameshinda vita, kwa kuangalia sura ya baba yake na mama yake na hasa ya
kaka yake.
Jinsi alivyokuwa amejawa na hasira alienda moja kwa moja
nyumbani akabadilisha nguo na kuamua kwenda kimbinyiko alikuwa na kazi ya
kufanya kabla hajafanya kitu chochote, kulipiza kisasi.
Alipofika nyumbani, mama yake alikuwa na kila sababu ya
kuzungumza lakini yeye alimwambia kwamba hawatazungumza kwa kuwa anakitu cha
muhimu sana anataka kukifanya, aliondoka.
“Mama naenda zangu kwenye mambo yangu naomba tu usiniulize”
akaondoka bila kusubiri jibu.
Wakati anafika Dawilo, kaka yake Silvesta alikuwa anaingia
katika makazi yake lughongo akiwa na kondoo alikuwa kondoo wa tambiko.
Silvesta alifika pale na kuangalia zizi lililipokuwepo akamfunga
kondoo yule bila kumsalimia mtu akaondoka zake taratibu, alijua wanajua nini
kinatakiwa itakuwa kazi yao kuwaita wajomba.
Wakati anaondoka pale Kibua, mzozo mkubwa ulizuka kati ya Silvesta
na baba yake, mzozo ambao uliamualiwa na mama yake.
“Mama nimesikia mlivyomtukana dada, lakini amefanana sana na
baba pengine kuliko mimi, baba hawezi kunikatalia dada yangu. Mbaya zaidi
nusura nifanye faulo kama tusingeambiwa na mtu anayetufahamu sote.Nilikuwa
naleta aibu kubwa katika ukoo baba hata kama mlikuwa na hitilafu zenu na mama
mkubwa”
Maneno yaliyomtoka Silvesta yalikuwa makali na mama yake
alimshauri kutogombana na baba yake kwani wakati huo haukuwa sawa.Alitulia,
lakini kilichomtuliza sana, ni kule kuambiwa akamate kondoo na kwenda kumfunga
nyumbani kwa akina Kibua.
Itaendelea
COMMENTS