TAMKO 27 Januari 2015 MAADHIMISHO YA MAUAJI YA JANUARI 26 NA 27, 2001 YA CUF YATOKANAYO NA MAANDAMANO YA KUDAI HAKI Siku ya l...
TAMKO
27 Januari 2015
MAADHIMISHO YA MAUAJI YA JANUARI
26 NA 27, 2001 YA CUF YATOKANAYO NA MAANDAMANO YA KUDAI HAKI
Siku ya
leo siyo siku ya furaha hata kidogo na wala si siku ya kujifaharisha, ni siku
ya kihistoria kwa chama chetu, ni siku ya kukumbukwa sana, miaka kumi na nne
iliyopita tarehe kama ya leo tarehe 27 Januari, 2001 na tarehe kama ya jana
tarehe 26 Januari 2001, Wanachama wenzetu waliojitoa muhanga, leo hii hawapo
wamekwenda mbele ya haki katika siku kama hii, mama zetu na dada zetu wanaikumbuka
kwa huzuni kubwa siku kama hii ya leo, kwani si vyema kuwakumbusha lakini
inatubidi tuyakumbuke yaliyowakuta siku kama hii ya leo, mama zetu na dada zetu
walibakwa na kunajisiwa na askari wa kidhalimu wa Serikali ya Chama cha
Mapinduzi, na wengine wakaachwa mayatima kwa waume zao kuuwawa na askari hao
hao wa kidhalimu, na kutuachia mayatima na wengine hadi leo wanaishi na
ulemavu.
Kwa mara
ya kwanza nchi yetu ilizalisha wakimbizi kwa ndugu zetu na wanachama wenzetu
ilibidi wakimbilie Mombasa nchini Kenya katika kunusuru maisha yao, wapo
wengine waliyakimbia makazi yao na
kuishi maporini na wengine walifia baharini wakati wakijaribu kujinusuru.
Tukizikumbuka
nasaha nzuri alizozitoa Mwenyekiti wetu Prof. Ibrahim Haruna Lipumba mwezi
Oktoba 2001 pale Bwawani Hotel Zanzibar wakati wa kutiliana saini mkataba wa
Muafaka alisema kwamba “Ni vyema tukaendelea kuyakumbuka yaliyotokea ili ibaki
kuwa kovu itakayotufanya tusiweze kuyarudia tena yale yaliyosababisha maafa
kama yale kutokea”.
Tukiikumbuka
siku kama ya leo inatubidi pia kuzikumbuka siku mbili kabla ya leo, yaani
Januri 25, 2001 wakati Mwenyekiti Prof. Ibrahim Haruna Lipumba alipopigwa na
wenzake na kuvunjwa mkono na askari wa Serikali ya Chama cha Mapinduzi na
kumkamata pamoja na Viongozi wengine waandamizi na wanachama wenzetu na
kuwafungulia kesi ya uchochezi.
Mwenyekiti
alikuwa akitekeleza misingi ya Demokrasia kwa mujibu wa katiba ya nchi ya
kukusanyika na kutoa mawazo yako hadharani, jambo ambalo aliyekuwa Rais wa
awamu ya tatu Wiliam Benjamin Mkapa alishatoa amri kwenyae hotuba yake ya
kuuaga mwaka 2000 na kuingia mwaka mpya wa 2001 kwa kukataza mikutano ya
hadhara pamoja na maandamano akidai kwamba uchaguzi umemalizika na washindi
wameshajulikana hivyo ni vyema tukaungana katika kuijenga nchi kupitia ilani ya
Chama cha Mapinduzi.
Mwenyekiti
Prof. Ibrahim Lipumba katika hotuba yake pale Mbagala Zakiem kabla ya kukamatwa
kwake, pamoja na kusisitiza nchi kuendeshwa kwa kufuata misingi ya utawala
bora, demokrasia na utawala wa sheria, lakini pia aliahidi kuwa kwa vile nchi
yetu imepoteza sifa na dira ya kuitwa nchi yenye misingi hiyo, suluhisho pekee
ni kufanya maandamano nchi nzima na yeye ndie atakae yaongoza maandamano hayo
ambayo aliyatangaza kufanyika siku ya tatu yake yaani tarehe 27, Januari 2001.
Katika
maandamano hayo tulikuwa na madai manne;
- Kutomtambua Rais wa Zanzibar Amani Abeid Karume na kutaka uchaguzi urudiwe
- Kudai Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi
3.
Daftari la Kudumu la Wapiga Kura
- Katiba Mpya
Pamoja na
Mwenyekiti wetu kumkamata wakidhani kwamba watakuwa wamefanikiwa kutuzuia
tusiandamane, halikadhalika watu wawili waliuliwa siku moja kabla, yaani tarehe
26 Januari pale Zanzibar, kwa agizo la aliekuwa Makamo wa Rais Marehemu Dk.
Omari Alli Juma wakiamini watakuwa wametutisha kiasi cha kutosha, lakini wapi,
tuliandamana na wenzetu wengine wakawa muhanga. MWENYEZI MUNGU ZILAZE ROHO ZA MAREHEMU WOTE WALIOJITOA MUHANGA MAHALI
PEMA PEPONI – AMINY!!
Narudia tena kwa msisitizo; ni hali
ya kusikitisha kila inapofika siku kama ya leo, inatukumbusha madhila
tuliofanyiwa ndani ya nchi yetu kwa kudai haki, inatukumbusha damu ya ndugu
zetu iliyomwagika kwa sababu ya kudai haki, inatukumbusha ulemavu walioupata
ndugu zetu kwa sababu ya kudai haki, inatukumbusha dada zetu na mama zetu
walioachwa vizuka kwa waume zao waliuwawa kwa sababu ya kudai haki,
inatukumbusha binti, dada zetu na mama zetu walibakwa kwa sababu ya kudai haki,
inatukumbusha watoto walioachwa yatima kwa sababu yakudai haki, inatukumbusha
watu walisamehe Ubunge wao na Uwakilishi wao katika baraza la wawakilishi kwa
sababu ya kudai haki.
Muhanga
huu waliojiotoa ndugu zetu, ndio matokeo na mafanikio yaliyojitokeza sasa hivi
hadi kufikia wengine kujidai na kujifaragua na kufikia hata kutoa kejeli na
maneno ya kifedhuli na kebehi, wakati ndugu zetu wanapoteza maisha yao kwa
kuandamana wao waliona tunaigiza.
Mafanikio
katika madai yetu yale manne;
1.
Kuhusu kutomtambua aliekuwa Rais wa Zanzibar Amani
Karume na kudai uchaguzi kurudiwa; kulipelekea kufikiwa kwa muafaka kati yake
na Katibu Mkuu wetu Maalim Seif Sharif Hamad, ndio uliopelekea kupatikana kwa
Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar, ambapo chama chetu kipo varandani Ikulu
kwa Maalim Seif kuwa Makamu wa kwanza wa Rais Zanzibar, na tunatarajia mwishoni
mwaka huu Oktoba 2015 tunaichukua wenyewe Ikulu ya Zanzibar.
2.
Kuhusu madai ya Tume Huru ya Uchaguzi, kwa upande
wa Zanzibar Tume hiyo iliundwa pamoja na
kugubikwa na wingi wa makada wa Chama cha Mapinduzi kutokana na mfumo
mbovu wa uteuzi, lakini tunaamini huu ni mwanzo tu, kilichobakia ni kupigania
maboresho ya Tume hiyo kuwa Huru Kwelikweli na si kama ilivyo sasa. Tunaiasa
CCM na Serikali yake Bila Uchaguzi huru na wa Haki Oktoba 2015 Taifa linaweza likarudia
historia ya mwaka 2001.
3.
Kuhusu Daftari la Kudumu la Wapiga kura
tulifanikiwa kulipata, nalo huwa linachafuliwa na wajanja wa Chama cha
Mapinduzi kwa kulitia mikono, lakini nalo tutalipigania kuhakikisha linatumika
ipasavyo na kama tulivyokusudia wakati wakulidai, na kwa vile kuna maboresho ya
mfumo mpya wa daftari, tunawaomba wanachama wetu tuhamasishane tujitokeze wote
kwenda kujiandikisha kwa Dar es Salaam uandikishaji unaanza Februari 15 mwezi
ujao.
4. Kuhusu
kupatikana kwa Katiba Mpya, ambapo ndani yake kungekuwa na Tume Huru ya
Uchaguzi na mengineyo yaliyomuhimu kwetu
sisi katika kuleta haki na usawa kwa wote, CCM na Serikali yake wameuteka
mchakato huo hatua za Mwisho za Bunge la Katiba na kuyatupilia mabali mambo
yote muhimu yatokanayo na michango ya wananchi wenyewe yaliyokusanywa na Tume
ya Kukusanya Maoni ya Katiba Mpya iliyokuwa ikiongozwa na Jaji Joseph Warioba
na kuingiza mambo yao yenye maslahi ya kifisadi kwa Taifa. CUF –
Chama Wananchi tunatoa AGIZO ni marufuku kwa wanachama na wapenzi wetu wote
nchi nzima kujitokeza kwenda kupiga kura ya maoni, kwani kushiriki kwa aina
yoyote hata kupiga kura ya hapana ni kubariki mchakato haramu uliofanywa na
Mafisadi wa Chama cha Mapinduzi.
Waheshimiwa
Wanachama katika kuyaenzi Maadhimisho haya tunatakiwa kuongeza nguvu,
mshikamano, umoja na kupeana nafasi kwa mujibu wa taratibu tulizojiwekea kwa
kuzingatia katiba yetu na kanuni zetu, kwa kuhakikisha kwamba chaguzi zijazo za
kura za maoni ndani ya chama zinatupatia Wagombea wanaokubalika katika jamii
katika nafasi za Udiwani, Ubunge na Urais.
Tuepuke majungu na makundi yanayoleta faraka ya wenyewe kwa wenyewe,
kama waliowengi wanakuona huwezi kuwafikisha wanakotaka, wewe kubali yaishe,
ikifika wakati wa kuaminika kwako watakupa nafasi, tuache kususa na hata
kuingia msituni baada ya matokeo ya kura
za maoni ndani ya chama.
Waheshimiwa
wanachama wenzetu, tunawaomba na tunawasihi sana tuyatumie maadhimisho
haya katika kushauriana namna bora ya
kuboresha chama chetu, na hasa katika kuongeza wanachama watakao kipatia chama
chetu ushindi, na tunaendelea kusisitiza kimbilio letu kubwa liwe ni kwa vijana
wetu tulionao, ni aibu kubwa sana kama utakuwa na kijana mwenye umri wa kupiga
kura na asikuunge mkono wewe kama mzazi wake au mlezi wake, tukumbuke wosia wa
Muasisi wetu Marehemu Shaaban Khamis
Mloo, kuwa tuhamasishane kunzia katika sahani ya chakula, kitandani, ndani
ya shuka, uwani, barazani, chumba kwa chumba, mlango kwa mlango, nyumba kwa
nyumba, katika vijiwe vya kahawa, mabaraza ya bao, kinamama wanaposukana,
vilabu vya mipira, maofisini na kila penye mkusanyiko wa watu na tujiwekee
ahadi kila mwanachama mmoja imalizikapo miezi mitatu angalau awe ameingiza
ndani ya chama sio chini ya wanachama wapya
watatu.
MWISHO;
Tunawaomba
radhi na tunawapa pole Wanachama wenzetu wote wa CUF – Chama cha Wananchi, kwa
kuwakumbusha siku hii nzito kwetu na ya majonzi makubwa TUNAJUA MMEGUSWA,
lakini tujifute machozi yetu kwa kuenzi moyo wa kujitoa kwa ajili ya chama ili
kuhakikisha haki inapatikana na chama chetu kinapata ushindi katika uchaguzi
huu ujao, hii ndio namna bora ya kuwaenzi WAHANGA wetu, tukumbuke “WOGA NI ADUI
WA HAKI”
HAKI
SAWA KWA WOTE
Prof.Ibrahim Lipumba
Mwenyekiti CUF Taifa
COMMENTS