MSIMU wa tamasha la filamu la kimataifa la Zanzibar (ZIFF) umefika na waandaazi wake wamewakumbusha wasanii na watengeneza filamu p...
MSIMU
wa tamasha la filamu la kimataifa la
Zanzibar (ZIFF) umefika na waandaazi
wake wamewakumbusha wasanii na watengeneza filamu pamoja na wawezeshaji, kwamba
sasa ni muda wa kuwasilisha kazi zao kwa ajili ya kuangaliwa na zikipasi
ziwekwe katika kabati la kuoneshwa.
Wiki
iliyopita meneja wa tamasha hilo, Dan Nyalusi
alisema kwamba kuna siku chache zilizobaki ambazo watu wanaweza
kuwasilisha kazi zao na si lazima wafike Zanzibar bali wanaweza kusafirisha
kazi hizo kwa njia ya kisasa ya mtandao.
Wakati
sampuli ndio zinatakiwa, wageni wao ndio wamekuwa kila mara makini zaidi
kuchangamkia fursa hiyo inayotokana na tamasha hilo linalofanyika katika ardhi
ya Tanzania, likileta kila aina ya watu kushiriki katika utamaduni wa mwambao,
kuliko wenyeji.
Kazi
zinazotakiwa kuwasilishwa ni za filamu, muziki, sanaa za uchoraji na uchongaji
na kadhalika.
ZIFF moja ya
matamasha makubwa kabisa ya filamu Afrika Mashariki linalofanyika nchini
Zanzibar katika visiwa vya Unguja kwa siku takribani kumi linawawezesha wasanii kukutana na kuonesha
kazi zao kwa jamii na kwao wenyewe na kuwezesha mawasiliano ya kikaribu kama
soko la filamu na kadhalika.
Kutoka pande
zote za Afrika na dunia kuna muziki, kuna sanaa, kuna filamu na kuna fasihi
inayojadiliwa, kudadavuliwa na kupewa majibu yanayopelekea wanazuoni kuona siku
za mbele za binadamu kwa kuangalia historia yake.
Kuna faida
kubwa ya kushiriki tamasha hili uwe msanii wa muziki au filamu na faida kubwa ni kuangalia soko, ladha ya
kazi yako na wengine na kuona namna ya kutumia changamoto mbalimbali kama fursa
katika kukuza usanii ulionao.
Dan Nyalusi
anasema kwamba kazi za watu zinaweza kupelekwa kwa njia ya YouTube, Vimeo,
Sound Cloud, picha na kuandika wasifu wa msanii kwa mpa@ziff.or.tz
na mwisho wa maingizo ni Machi 31 mwaka
huu.
Kwa
filamu kuna ushindani mkubwa
unaotarajiwa hasa kutokana na kukua kwa masimulizi ya filamu duniani na hasa
masimulizi ya karibu na ukweli yenye ladha ya changamoto za binadamu katika
maisha yake ya kila siku kutengeneza maisha katika serikali na maisha ya ndani
kama mapenzi na matunzo.
Katika
tamasha hili tuzo kubwa kabisa ni ya jahazi ya dhahabu na fedha. Na hii
hutolewa kwa watengeneza filamu wanaotoka nchi za majahazi pekee. Nchi hizo ni
pamoja na zile zinazopakana na bahari ya Hindi na visiwa ndani ya bahari hiyo
ikiwamo Iran, Irak na Afghanistan na nchi zote za Afrika.
Tuzo
nyingine ni ya Sembene Ousmane ambayo imewekwa kwa ajili ya ushindani kwa
watengeneza sinema wa Kiafrika na wale wanaoishi Ughaibuni na maprojuza wao
ambao huenda wakati mwingine ni mapatna.
Kuna kila
sababu ya watanzania kutafuta tuzo hizi
ambazo mara ya mwisho ilinyakuliwa na waliotengeneza sinema ya maangamizi na
baada ya hapo zimeishia mikononi mwa wageni
na wakati mwingine kutoka nje ya bara la Afrika.
Ushindani wa
kupata tuzo upo katika filamu za makala na zile fupi, za kubuni, dokumentari na
za vikaragosi zikiwa zimepigwa picha na waafrika na madarekta kutoka nchi za
majahazi.
Kwa mujibu
wa Nyalusi katika upande wa Dokumentari, seksheni hii iko wazi katika fomati za aina zote.
Seksheni za maendeleo hii iko wazi kwa watengeneza sinema wa kiafrika na
pia kwa watengenezaji waliopo ughaibuni
na mapatna zao.
Pia kuna
eneo la muziki ambalo limetengwa kwa ajili ya kazi njema ya ubunifu wa muziki
kwa watu wa Afrika Mashariki na pia kutakaribisha filamu lukuki kwa ajili ya starehe, yaani kuburudika lakini
hazipo katika ushindani.
Tamasha hili
pia lina tuzo nyingine kama ya vipaji Afrika Mashariki inayotolewa na Signis, tuzo
ya filamu bora ya Kiafrika kwa mtazamo wa Mtandao wa matamasha ya Ulaya na
Afrika na pia kuna tuzo ya Zuku kwa ajili ya filamu zilizotengenezwa kwa
Kiswahili za Bongo.
Tamasha la
Zanzibar ukiangalia ukuaji wake na
ukubwa wake na mtandao wa kuheshimika unaoendelea kutokea duniani, ni sahihi
kusema kwamba ipo haja kwa Watanzania si kuingiza sinema za kuonwa bali za
kushindana katika madaraja mbalimbali.
“Ni
matarajio yangu kwamba ndugu zangu wa Tanzania na hata Afrika Mashariki
watazingatia ushiriki wa ushindani na si tu ushiriki,” anasema Dan Nyalusi
ambaye kwa sasa amekomaa na tamasha hilo.
Anasema katika mahojiano
kwamba kila mwaka tamasha hilo linaonesha sinema zilizokwenda shule kutoka
pande mbalimbali za Afrika hata duniani na katika hilo heshima yake kubwa pia
inapatikana kutokana na baadhi ya filamu kuamua kufanya primia.
Filamu za ZIFF ni babu kubwa
kwa kuwa zinaangalia sinema zilizozalishwa katika kipindi cha mwaka mmoja na
hivyo utimamu wa kufuatilia utamaduni wa sinema na simulizi zake unakuwa wa
kisasa zaidi.
Moja ya vitu ambacho kinavutia katika tasnia ya sinema ni kule
kuwa na mambo mengi ya kujifunza pamoja na kwamba unapeleka kazi yako. Tamasha
hili limesukwa kwa namna ambavyo linaibua vipaji mbalimbali kutokana na mfumo wake hasa wa maonesho, matamasha
mbalimbali ya sanaa, makongamano na hata maonesho ya jukwaa katika kazi
mbalimbali.
Tamasha hili lenye vitu
mbalimbali bado ni tamasha linaloweza
kutumika kuinua wasanii Tanzania hasa
wale ambao wanataka kwenda kimataifa.
Tamasha hili linafanyika
Julai lakini maandalizi ndiyo hayo yako mbioni huku waandaazi wakikumbusha
watanzania ujio huo.
Wakiwa wanapatikana katika
jengo la zamani ambalo ni ngome al maarufu kama Ngome Kongwe tamasha hili lina
kitu cha ziada kwamba sinema huangaliwa katika
uwanja wa wazi na kufanya ladha yake kuwa ya aina yake . Ni wakati
wasanii tuchangamkie fursa.
COMMENTS