SERIKALI imeziagiza kila halmashauri nchini kubaini wazee walio katika maeneo yao na kuhakikisha wanapata huduma zote za msingi ikiwa...
SERIKALI imeziagiza kila halmashauri nchini kubaini wazee walio katika
maeneo yao na kuhakikisha wanapata huduma zote za msingi ikiwa ni pamoja na
huduma za afya kutoka kwenye mapato yao wenyewe.
Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa
Afya,Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu, jana wakati akizindua
kampeni ya kitaifa ya “Mzee Kwanza – Toa
Kipaumbele Apate Huduma”, mkoani Morogoro leo.
Alisema
katika uzinduzi huo kuwa anajua tangu
serikali ipitishe maamuzi kwamba wazee watatibiwa bure katika maeneo yao,
utekelezaji wake umekuwa wa kusuasua katika baadhi ya maeneo hivyo kuchukua
fursa hiyo kuagiza viongozi wote wa halmashauri mbalimbali kuhakikisha kuwa
hilo linasimamiwa na kutekelezwa kwa ufanisi wote.
Uzinduzi huo uliofanywa kwa kushirikiana na
Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya umelenga kuikumbusha jamii ya watanzania wajibu
wake wa kuwapa wazee hadhi wanayostahili katika maeneo mbalimbali ya huduma za
kijamii.
“Wazee katika jamii yoyote wana nafasi muhimu sana katika ujenzi wa taifa. Wazee
ndiyo hazina ya busara, hekima, amani na utulivu wa jamii yoyote. Familia
isiyoheshimu wazee aghalabu itakuwa na vurugu na ugomvi kila kukicha. lakini
jamii au familia inayoenzi wazee na kuwapa nafasi zao katika kushauri, kukosoa na
kuelekeza utendaji wa siku hadi siku, jamii hiyo itakuwa na baraka siku zote,”
alisema waziri Ummy
Alisema serikali ina matamanio mengi ya kuhakikisha wazee wote hapa nchini
wanaishi maisha bora katika uzee kwa jamii
kuthamini mzee na kumpa kipaumbele katika huduma.
Aidha, alisema lengo la kampeni ni kuhakikisha kuwa wazee wanapewa
kipaumbele na wanahudumiwa kwanza wakati wote wanapokwenda kupata huduma mahali
popote.
Aidha alisema kutokana na changamoto zilizopo sasa serikali imeanza
kuchukua hatua ikiwamo ya kuandaa sera ya wazee ambayo wanaipeleka bungeni ili
ipitishwe kuwa sheria kutoa haki kwa wazee na mahitaji yao ikiwemo pesheni,
afya na huduma mbalimbali za jamii.
Aidha aliagiza kila mfuko wa hifadhi ya jamii kuhakikisha hakuna mzee
anaenyanyasika katika kupata stahili yake tena kwa wakati.
Akifafanua zaidi kuhusu kampeni hiyo alisema kwamba imelenga kurejesha
utamaduni wa zamani wa kuthamini wazee.
“Kwa kupitia kampeni hii ya mzee kwanza ni wajibu wa kila mtanzania kuona
kuwa anafanya kila aweza kurejesha hadhi ya wazee na kuwapa umuhimu wa kwanza
katika kupata huduma za kijamii.”
Kwa kutambua umuhimu wa wazee katika taifa, alisema Waziri Ummy, serikali ya awamo ya tano imeunda kitengo
maalumu cha kuhudumia wazee na kukiweka chini ya wizara Afya.
Alisema kuundwa kwa kitengo hicho kumetokana na serikali kutambua
changamoto wanazokabili wazee wapatao 2,507,568 wenye miaka kati ya 60 na
kuendelea sawa na asilimia 5.6 ya watanzania wote kwa mujibu wa sensa ya mwaka
2012.
Aidha Tanzania ina wazee takriban 474,053
wenye miaka 80 na kuendelea.
Katika tathmini inaonesha kwamba kundi la Wazee wenye
umri kati ya miaka 60 – 64 wapo asilimia 31, miaka 60-69 wapo asilimia 20,
kundi la miaka 70-74 wapo asilimia 19, wakati wazee wenye umri kati ya miaka
75-79 wapo asilimia 12 huku kundi la wazee wenye umri wa zaidi ya miaka 80 ni
asilimia 19 ya wazee wote nchini.
Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii,Jinsia Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu akizinduzi kampeni ya Wazee kwanza toa kipaumbele apate huduma leo Mkoani Morogoro |
Tathmini ya ki mkoa inaonesha kuwa Mikoa inayoongoza kuwa
na wazee wengi ni Kilimanjaro (6.4%), Mbeya (6.1%), Dar es Salaam (6.1%),
Morogoro (5.6%), Tanga (5.6%), Dododoma (5.6%), Kagera (5%) na Mwanza (4.9%).
Alisema wazee hao wanakabiliwa na changamoto ya kipato cha matumizi ya
msingi huku akiwa na ongezeko la uhitaji wa huduma za afya kutokana na kutokana
na mwili kuchoka.
Ingawa mzee alikuwa mwajiriwa wa sekta rasmi, anayo nafasi ya kupata malipo
ya pensheni ili kujikimu na kwa wale ambao walikuwa wanachama wa nhif wana nafasi ya kuendele
kupata huduma za bima ya afya maisha yako yote, Waziri aliuliza ni wangapi wana
fursa hizi za pensheni na bima ya afya
ni asilimia ngapi ya wazee wote nchini.
“Mathalan, NHIF wametujuza hapa kwamba wanahudumia wastaafu 52,000 tu
lakini pia takwimu zao zinaonesha wanahudumia wazee wapatao 244,000 kupitia
huduma zao mbalimbali za bima ya afya. takwimu za mifuko mingine ya pension
hazitakuwa mbali na ukweli huu kwamba hii ni asilimia ndogo ukilinganisha na
idadi ya wazee nchini.
Alitaka kila Mtanzania kushiriki katika kampeni ya mzee kwanza kwa viongozi wa halmashauri kuweka mikakati na
ubunifu anuai kuhakikisha mzee popote alipo anaheshimiwa na kupewa kipaumbele.
mwisho
COMMENTS