TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora imepokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya vitendo vya u...
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Tume ya Haki za
Binadamu na Utawala Bora imepokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya vitendo vya
uhalifu na uvunjaji wa haki za binadamu vinavyoendelea kufanyika Zanzibar,
hususan kisiwani Pemba.
Kwa muda mrefu sasa
hivi tokea kufutwa kwa Uchaguzi Mkuu wa tarehe 25 Oktoba, 2015 na hasa baada ya
kufanyika Uchaguzi Mkuu wa Marejeo Zanzibar tarehe 20 Machi, 2016 kumekuwapo
vitendo vya uhalifu na uharibifu wa mali, ikiwemo kukata vipando mbalimbali
yakiwemo mazao ya muda mrefu na mfupi. Vilevile kumefanyika vitendo vya hujuma
ikiwemo kuchoma moto nyumba katika baadhi ya makazi ya watu Kisiwani Pemba.
Aidha kumekuwepo na taarifa
za matukio kama vile migomo takriban maeneo mengi ya Mikoa ya Pemba na baadhi
ya maeneo katika kisiwa cha Unguja, yenye kuashiria vitendo vya kubaguana, kwa
maana ya kutoshirikiana katika shughuli za kijamii na huduma za kijamii. Kwa
mfano baadhi ya watu wananyimwa usafiri katika magari, kususiwa harusi, maziko
na nyumba za ibada.
Vitendo vya kukata na
kuharibu mali, ikiwemo kuchoma nyumba moto ni kinyume na haki za binadamu kwani
kila mtu ana haki ya kumiliki mali kama ilivyoelezwa katika Ibara ya 24(1) ya
Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, na Kifungu cha 17 cha
Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984.
Kuwanyima watu huduma
ya aina yoyote katika jamii ni kinyume na misingi ya haki za binadamu, hasa
haki ya kutobaguliwa kama ilivyoelezwa katika ibara ya 12 ya Katiba ya Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, na Kifungu cha 11 cha Katiba ya Zanzibar
ya mwaka 1984. Vitendo vyote hivyo vinaathiri shughuli za kijamii na kiuchumi
pia ni kinyume na haki za binadamu kwa mujibu wa Katiba na Sheria.
Tume pia imepata
taarifa kuwa tofauti za itikadi za kisiasa zinasababisha ndoa kuvunjika
kutokana na wanawake kuadhibiwa kwa kupewa talaka kutokana na kutotii amri za
waume zao za kuwazuia kushiriki uchaguzi wa marejeo.
Kifungu cha 21(1) cha
Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, kama ilivyorekebishwa mwaka 2010 kinaeleza
kuwa, “kila Mzanzibari anayo haki ya kushiriki katika shughuli za utawala wa nchi,
ama moja kwa moja au kupitia wawakilishi waliochaguliwa kwa hiari”. Haki hii haitakiwi
kuingiliwa na mtu yeyote, kwani ni haki inayotambua uhuru na utu wa kila
mwanadamu kuamua yeye mwenyewe kushiriki au kutoshiriki katika shughuli za
kisiasa, awe mwanamume au mwanamke.
Aidha Kifungu cha
21(2) cha Katiba ya Zanzibar kinatamka kuwa ”kila Mzanzibari anayo haki na
uhuru wa kushiriki kwa ukamilifu katika kufikia uamuzi juu wa mambo
yanayomuhusu yeye maisha yake au yanayolihusu Taifa”.
Wakati Tume ikiyasema
haya, inapenda kutamka kwamba imeshangazwa na kusikitishwa na tamko la Naibu Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa
ya Jinai Zanzibar kuhusu kuwakataza Mawakili kuwawakilisha watuhumiwa katika
kesi zinazotakana na uvunjifu wa amani Zanzibar, au makosa yanayoashiria
kufanyika kwa msukumo wa kisiasa. Zuio hilo la mawakili ni batili, kwani ni kinyume na misingi ya haki za
binadamu, na misingi ya haki sawa, yaani (fair trial principles,) ambayo inatamka
kwamba kila mtu hatotiwa hatiani mpaka ikithibitika hivyo,(presumption of innocence until proven guilty), au kila mtu
ana haki ya kuwakilishwa mahakamani (right of legal representation).
Tume inatamka kwamba
matamko hayo hayaendani na dhana ya utawala wa sheria na utawala bora, ambapo
kila taasisi, na kila mtu anatakiwa kutenda kazi zake kwa kuzingatia Katiba, yaani
Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, Katiba ya Zanzibar ya
mwaka 1984 na Sheria ya mwenendo wa Makosa ya Jinai ya Zanzibar, Namba 7 ya
mwaka 2004, pamoja na Mikataba ya Kimataifa hasa Mkataba wa haki za kisiasa na
kiraia wa mwaka 1966 ambao Tanzania imeridhia.
Ibara ya 13(6) Katiba
ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania 1977 na kifungu cha 12(6), ya Katiba ya
Zanzibar 1984 zinaweka miongozo ya usimamizi wa haki, ambayo ni pamoja na mtu
kupewa haki ya kusikilizwa kwa ukamilifu, wakati wa upelelezi na uendeshaji wa
kesi za jinai, na wakati mtu anapokuwa chini ya ulinzi, utu wake utaheshimiwa,
zinapiga marufuku mateso au adhabu za kinyama au zinazomtweza au kumdhalilisha
mtu.
Kifungu cha 41 cha
Sheria ya Mwenendo wa Jinai 2004, kinampa haki Wakili aliyesajiliwa na Mahakama
Kuu chini ya Sheria ya Legal Practitioners Decree Cap. 28 kumuwakilisha au
kumshauri mtu yeyote anayetuhumiwa au kushtakiwa kwa kosa lolote.
Tume inasisitiza kuwa mamlaka zote zenye
kusimamia upelelezi na kuendesha mashtaka zitekeleze kazi zake kwa weledi na kuheshimu
matakwa hayo ya Katiba na sheria.
Tume inapendekeza
kwamba ili hali ya maelewano irudi kama ilivyokuwa hapo awali kisiwani Pemba na
Zanzibar kwa ujumla, panahitajika hatua za makusudi zitakazo leta
maelewano katika jamii. Tume inashauri
yafuatayo:-
(i)
Hatua za makusudi na haraka zifanyike kwa Viongozi
wa Kitaifa na wa vyama vyote vya siasa vikiwemo CUF na CCM wakae pamoja kwa ajili ya kutafuta
ufumbuzi wa suluhisho la kudumu litakalozuia matatizo ya uvunjifu wa amani kujirejea.
(ii)
Taasisi zinazosimamia ulinzi na usalama, hususan Jeshi
la Polisi na vyombo vingine vya dola, ziwe makini katika kufanya kazi zake kwa
kufuata misingi ya utawala bora, haki za binadamu na utawala wa sheria ili
kuepukana na madhara yasiyotarajiwa katika jamii.
(iii)
Wananchi wote wanatakiwa kutii sheria za nchi, na
kutojiingiza katika vitendo vya uvunjifu wa amani na usalama.
SIGNED
Bahame
Tom Nyanduga
Mwenyekiti
TUME
YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA.
COMMENTS