MKUU wa Jeshi la Polisi, Inspekta Jenerali, Ernest Mangu amefunguka kuhusu mambo juu ya utendaji wa jeshi hilo na kueleza kuwa wakati wo...
MKUU
wa Jeshi la Polisi, Inspekta Jenerali, Ernest Mangu amefunguka kuhusu mambo juu
ya utendaji wa jeshi hilo na kueleza kuwa wakati wowote litamburuza mahakamani
Katibu Mkuu wa Taifa wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Shariff Hamad kwa
kuhamasisha uchochezi visiwani Zanzibar.
Amebainisha
kuwa jeshi hilo, kamwe halikandamizi wala kuonea chama chochote cha siasa,
kwani limekuwa likitekeleza wajibu wake kwa kufuata sheria na taratibu
zilizopo.
Akizungumza
katika mahojiano yaliyofanyika kwenye kipindi cha Funguka, kinachorushwa na
Kituo cha Televisheni ya Azam jana, IGP Mangu alisema hali ya siasa Zanzibar
ilikuwa shwari katika chaguzi zote mbili na kwamba machafuko na vurugu vilianza
kutokea baada ya uchaguzi wa pili.
Alisema
vurugu hizo zilianza baada ya kubainika kuwa Maalim Seif, alikuwa akifanya
mikutano ya ndani na mingine ya chini kwa chini na wafuasi wake katika maeneo
ya Kaskazini na Kusini.
“Kwa
sababu ilikuwa ni mikutano ya ndani, Polisi hatukuona tatizo na wala
hatukumzuia, tuliona ni mwananchi anataka kuzungumza na wafuasi wake, tukasema
mwache aongee nao tu,” alisema IGP Mangu.
Alisema
baadaye jeshi hilo liligundua kuwa kiongozi huyo wa CUF, alikuwa anawachochea
wananchi waichukie serikali iliyopo madarakani na wapinzani wao ambao ni Chama
Cha Mapinduzi (CCM) kwa kuwafanyia uhalifu.
Alisema
baada ya vikao hivyo vya Maalim Seif, visiwani humo kukaanza kuibuka matukio ya
vurugu kama vile mashamba kuchomwa moto na mazao kung’olewa.
“Haya
mambo hayakutokea kabla ya vikao vya Seif, yalitokea baada ya vikao vyake,”
alifafanua mkuu wa polisi.
Alisema
wafuasi hao walichochewa, kiasi cha kususa hadi shughuli za kijamii, kama vile
misiba na wakati mwingine ilifikia hatua ya kususa kuwauzia bidhaa wafuasi wa
CCM.
“Tukasema
kama wameona kugeuza biashara zao siasa, basi waendelee tu. Biashara inadumu
kwa sababu unatengeneza faida, sasa kama umeamua kuchagua wa kumuuzia ni shauri
yako. Hawa tuliwaacha kwa sababu tuliona hawana makosa,” alisema.
Hata
hivyo, alisema jeshi hilo kamwe halikuwanyamazia wahalifu waliochoma na kung’oa
mazao kwenye mashamba ya wenzao, eti tu kwa kigezo cha ufuasi wa chama au
siasa.
“Hawa
tuliwakamata na wapo wengine tunaendelea kuwatafuta, watakapoacha ndio
hatutawatafuta. Wale wahalifu ndio tunaowatafuta. Pengine kwa sababu ya siasa
wanadhani Polisi tunawaonea wananchi tunawakamata bila sababu. Sasa hawa watu
tunawaoneaje wakati tunawapeleka mahakamani?” Alihoji.
Maalim
Seif kuhojiwa Alisema kutokana na matukio hayo, tayari Maalim Seif amehojiwa na
jalada lake halijaamuliwa, lipo kwa Mwendesha Mashtaka wa Serikali (DPP)
Zanzibar. “Lakini pia tunataka tumpeleke mahakamani kumshitaki kwa makosa
aliyofanya ya kuchochea fujo,” alieleza.
Alisema
kazi kubwa ya Polisi kwa sasa si kujiingiza kwenye siasa au kupatanisha pande
mbili zinapokwaruzana, bali kazi yake ni kuhakikisha inadhibiti na kuwakamata
wahalifu.
Alisema
endapo vyama viwili vinavyolumbana visiwani Zanzibar, vitaamua kuchukua hatua
za kisheria kumaliza tofauti zao, polisi haina tatizo, lakini endapo vyama
hivyo vitachukua hatua za kijinai au kukomoana, jeshi hilo halitokaa kimya.
“Kazi
ya polisi iko wazi, tunakamata tunapeleleza na kupeleka mahakamani umma
unatuona tunachofanya hatuna cha kuficha,” alisisitiza.
Maandamano
na mikutano
Akizungumzia
madai ya jeshi hilo kukandamiza demokrasia na wapinzani kwa kudhibiti shughuli
za siasa nchini, IGP Mangu alisema hakuna mwanasiasa au chama chochote,
kilichozuiwa kufanya shughuli zake, ikiwemo mikutano.
Alisema
kinachotakiwa ni kwa mwanasiasa au chama hicho, kupeleka maombi yake Polisi kwa
mujibu wa sheria na baada ya jeshi hilo kufanyia tathmini maombi hayo, endapo
yataonekana hayana tatizo yataruhusiwa kuendelea.
Alisema
endapo jeshi hilo linazuia shughuli za kisiasa, hutokana na uchunguzi au
tathmini lililofanya na kujiridhisha kuwa shughuli husika si salama na
inatishia usalama wa raia.
“Unajua
unapozungumzia masuala hayo tuwe makini kidogo, kwa sababu hapa kuna watu wa
aina mbili kuna wanaofanya siasa na sisi watendaji tunaotekeleza sheria. Ila
sisi pia hatuko juu ya sheria, kama kuna mahali tunakiuka upo utaratibu wa
kutushughulikia,” alisisitiza.
Alisema
hata katika suala la kuzuia shughuli za kisiasa, kama vile mikutano na
maandamano endapo, kuna chama au mwanasiasa anahisi kuwa jeshi hilo,
halikutenda haki au limeenda nje ya mstari, taratibu zinamruhusu kukata rufaa
kwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Rais na
Mahakama.
Hata
hivyo, alisema jeshi hilo halifanyi jambo lolote nje utaratibu wa kisheria,
akifafanua, “lakini sisi hatuwezi kujiingiza kwenye siasa kwa sababu sisi sio
wanasiasa, pia hatuwezi kuzuia wanasiasa kulumbana kwa sababu ni uwanja wao wa
kulumbana. Sasa kama tulitoa maelekezo fulani basi ujue tulikuwa tunatekeleza
sheria na utaratibu uliopo.”
“Sidhani
kama sisi tunakandamiza upinzani, tunachofanya sisi ni kufuata sheria na
taratibu zilizowekwa na watu wako huru kama wanafikiri tumeenda nje ya mipaka
yetu wakatuchukulie hatua,” alisisitiza.
Alitoa
mfano wa matukio yaliyozuiwa na Polisi kwa sababu za kiusalama kuwa ni pamoja
na mkutano wa mahafali wa Dodoma, ambao ulifanyika siku moja na mkutano wa
mahafali uliofanyika Ukumbi wa Karimjee, Dar es Salaam ambao wenyewe
haukuzuiwa. Yote ilikuwa mikutano ya wanafunzi wafuasi wa Chadema.
“Kama
sisi tuna sera ya kuzuia, mbona wa Karimjee hatukuuzuia? Dodoma kulikuwa na
sababu na imeelezwa na viongozi wa Dodoma. Hii si sera yetu, usichukulie
mkutano mmoja kuzuiwa basi ndio yote nchi nzima imezuiliwa. Haiwezekani,”
alifafanua.
Alisema
sheria inazungumzia wanaohitaji kufanya mkutano au kufanya maandamano, wanatoa
taarifa kwa mkuu wa polisi wa hilo eneo, na mkuu huyo ataangalia kama mazingira
yanaonesha hakuna tatizo, mkutano utaendelea, kama kuna tatizo atauzuia.
“Sasa
ni wapi sisi tumefanya kitu ambacho ni kinyume na tunaonekana tunakandamiza
upinzani? Na ikumbukwe kuwa kuna mikutano baadhi iliombwa tukaizuia kwa sababu
kipindi hicho kulikuwa na kelele za mauaji Mwanza, Sengerema, Tanga mpaka
tunahojiwa Polisi mko wapi,” alisema.
Alisema
wakati Polisi ikihojiwa kuhusu dawa ya mauaji, baadhi ya vyama viliwasilisha
maombi ya maandamano.
“Hivi
kweli? Kwanza mauaji yenyewe mtindo wake ni mpya unajuaje kama wanaoomba
wangeenda nao kuvamiwa? Lazima tuchukue tahadhari,” alisema na kuongeza kuwa
Polisi imepewa jukumu la kisheria kuhakikisha panakuwepo na amani. “Sasa
tunapochukua hatua kuhakikisha kuna amani, naomba tuvumiliane. Msione kuna
amani, basi mkajua ipo tu na ni ya kudumu, mjue kuna wengine wameumia
kuhakikisha hiyo amani inakuwepo. Lazima iwe hivyo ndio utaratibu wa kuongoza
nchi, sisi hatubagui wala kukandamiza chama chochote,” alieleza IGP Mangu.
Matumizi
ya nguvu
IGP
Mangu alisema si kweli jeshi hilo limekuwa likitumia zaidi nguvu katika
kudhibiti vurugu na kubainisha kuwa nguvu hutumika, pale tu inapobainika kuwa
upande wa pili unaodhibitiwa nao unatumia nguvu.
Hata
hivyo, alisisitiza kuwa Polisi nchini imekuwa ikitekeleza wajibu wake vyema
bila kukandamiza wala kutumia nguvu, kwani hata taasisi ya kimataifa iliyofanya
tathmini juu ya utendaji wa jeshi hilo katika uchaguzi mkuu nchini ilibainisha
kuwa jeshi hilo lilifanya vyema.
Polisi
na rushwa Akizungumzia tuhuma zinazorushiwa Jeshi la Polisi kwamba kuna baadhi
ya askari wake, wanatuhumiwa kwa rushwa, alisema askari hawana mamlaka ya kula
rushwa na kujilimbikizia mali halafu wasiguswe na mtu.
“Hili
haliwezekani. Kwa hiyo nasema bado wananchi wanaweza wakasaidia kama kweli
wanazo taarifa za Polisi na zitafanyiwa kazi. Kama hawaamini kama sisi wenyewe
hatuwezi kudhibitiana, vipo vyombo vingine vinaweza kufanya hivyo,” alisema.
Hata
hivyo, alisema wapo askari Polisi wenye maisha mzuri kwa maana ya nyumba na
magari, ambao wamepata mali hizo kupitia taasisi mbalimbali za mikopo ikiwemo
Saccos ya Polisi, ambayo ndio kubwa nchini.
“Askari
polisi kumiliki gari nzuri si kosa, la msingi amepataje hilo gari, kama kuna
polisi ana mali au gari isiyo na maelezo tuleeteni, polisi hazuiliwi kuwa na
gari nzuri. Siku hizi kuna taasisi nyingi zinakopesha anaweza kukopa,”
alisisitiza.
Kashfa
ya Lugumi
Akizungumzia
suala la kashfa ya mkataba tata wa Kampuni ya Lugumi Enterprises Ltd
inayomilikiwa na mfanyabiashara Said Lugumi, IGP Mangu alisema suala hilo
lilichukuliwa na Bunge na kufanyiwa uchunguzi hivyo, matokeo ya uchunguzi
hawezi kuyazungumzia.
Alisema
anachoweza kukizungumzia ni maelekezo ambayo jeshi hilo limepatiwa na Bunge,
ambayo ni kukamilisha yale ambayo hayajakamilishwa.
“Tunaendelea
kuchukua hatua za kukamilisha.Kuhusu uchunguzi kazi ilifanywa na Bunge kwa
anayetaka anaweza kuwasiliana na Bunge na kupatiwa matokeo kwa kuwa naamini
Bunge linawakilisha wananchi, taarifa zao ziko wazi,” alisema.
Source:Halima Mlacha, Habarileo
COMMENTS