KUGOMBEA UENYEKITI WA CHAMA CHA WANANCHI CUF. TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI. Kutoka kwa Mwanachama mwandamizi wa Chama Cha Wananc...
KUGOMBEA UENYEKITI WA CHAMA CHA WANANCHI CUF.
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI.
Kutoka kwa Mwanachama
mwandamizi wa Chama Cha Wananchi CUF,
Julius Sunday Mtatiro.
09 Julai 2016
Ndugu
zangu,
Napenda
kutumia fursa hii kuwatakia mapumziko mema baada ya sherehe za Iddi. Hata hivyo
ninalo jambo muhimu ambalo ningependa kuliweka wazi. Kwa kipindi kirefu sana
kumekuwa na msukumo mkubwa kutoka kwa viongozi wa chama ngazi za wilaya,
wajumbe wa mkutano mkuu, wabunge, madiwani, wanachama wa kawaida, wafuasi na
wapenzi wa kada mbalimbali kunitaka nishiriki katika kinyang'anyiro na hatimaye
kuchukua nafasi ya Mwenyekiti wa chama. Misukumo hiyo ni mikubwa kiasi cha
kutoelezeka.
Misukumo
hiyo pia imetoka kwa wananchi na wanaharakati mbalimbali ambao wanaunga mkono
mabadiliko. Ni jambo la kujivunia sana unapoungwa na kiaminiwa na watu wengi,
ndani na nje ya chama chako, katika jambo lolote lile hasa kuwania nyadhifa za
uongozi. Naahidi kuwa ntaendelea kulinda tunu zote ambazo zinawafanya wanachama
na watanzania wenzangu waone kuwa ninazo sifa na vigezo vya kushikilia wadhifa
mkubwa kiasi hicho.
Katika
kipindi chote cha misukumo hiyo nimekuwa nikiwajibu wahusika wote kuwa
"sina nia ya kuchukua uongozi wa juu wa chama" kwa sababu bado
nahitaji muda wa kujiimarisha katika maeneo mbalimbali ya maisha huku nikizidi
kujenga "uandamizi" katika siasa za nchi na chama changu.
Leo
nitoapo taarifa hii, mbio za kuchukua fomu zimenoga na najulishwa kuwa wapo
wanachama wamekwishajitokeza kwa ajili hiyo na wengine wengi wanaendelea, hilo
ni jambo kubwa na la kujivunia sana.
Kwa
sababu mibinyo na misukumo imekuwa mikubwa sana, kupita kiasi, siyo vema
nikaendelea tu kuwajulisha wale tu wanaonifikia, kwamba sina nia ya kugombea
nafasi hiyo, bali ni vema nikajulisha jamii nzima ya CUF na watanzania wote,
kwamba hadi leo SIJAWA NA NIA YA KUCHUKUA MAJUKUMU YA UENYEKITI WA CHAMA CHA
WANANCHI CUF na wala SOTACHUKUA FOMU KWA AJILI HIYO. Naomba tamko hili lifute
misukumo, tetesi na kila aina ya taarifa kwamba ninayo nia au nitakuwa na nia
hiyo.
Niliposimama
hadharani kushauri kuwa Mwenyekiti Mstaafu wa CUF (namheshimu sana), Prof.
Lipumba, anapaswa kupumzika uongozi na kusitisha nia yake ya kurudi kwenye
nafasi aliyoondoka mwaka mmoja uliopita, wapo watu walitumia uhuru wao kueleza
kuwa simtaki Prof. Lipumba kwa sababu nautaka uenyekiti wa CUF, watu hao
watakumbuka niliwajulisha kwamba sina nia wala sijawahi kufikiria kugombea
nafasi hiyo kubwa katika siasa za CUF na Tanzania kwa ujumla.
Huo ndiyo
umeendelea kuwa msimamo wangu hadi leo, kwa mambo yote mawili, kwamba
sitogombea nafasi ya UENYEKITI na siungi mkono Mwenyekiti mstaafu kurudi kwa
sababu siasa za Tanzania zinakokwenda zinahitaji viongozi wapya, damu tofauti
na wanaoweza kutizama mambo kisasa zaidi na kwa mahitaji ya kizazi cha sasa
zaidi. Na kwa sababu Prof. Lipumba anayo heshima kubwa kwa CUF na watanzania,
ni muhimu zaidi ailinde heshima na abaki kuwa mshauri mkuu wa chama.
CUF ya
sasa inahitaji kuwa na mwenyekiti imara, anayeweza kukisimamia chama na
kikajijenga lakini pia mwenye uwezo na ushawishi wa kufanya siasa za
ushirikiano wa haki "A Fair Coalition" wakati wa uchaguzi wa Serikali
za Mitaa 2019 na Uchaguzi Mkuu 2020. Hapa nina maana kuwa anahitajika mtu
mwenye upeo mzuri wa kuweza kuilinda CUF lakini akiwa muwazi, mkweli na anayeamini
katika ushirikiano wa vyama vya upinzani kama silaha mojawapo ya mapambano
dhidi ya CCM.
Baada ya
kueleza masuala haya, napenda kutumia fursa hii kuwatakia kila la heri
wanachama wote ambao wanaendelea na uchukuaji fomu, bila shaka miongoni mwao
tutapata mwenyekiti mzuri kwa ajili ya kukiendeleza chama miaka ijayo. Jukumu
langu kama mwanachama mwandamizi ni kuendelea kukisaidia chama changu kiushauri
na katika masuala yote muhimu yatakayokuwa yanahitaji
"professionalism" kama ambavyo nimekuwa nikifanya.
Nitabaki
kuwa mwana CUF imara, ninayejitambua na ambaye nilijiunga katika chama hiki
baada ya kuvutiwa na kuamini sera na itikadi. Kamwe, sitakuwa mwanachama ambaye
alijiunga na chama ili kumfuata kiongozi au mtu fulani. Katika hili naomba
misimamo yangu iheshimiwe kama ambavyo mimi pia nimekuwa nikiheshimu mitizamo
ya watu wengine.
"Naitakia
CUF mkutano Mkuu Mwema na kila la heri kwa viongozi wote wapya".
"MUNGU
IBARIKI TANZANIA, KIBARIKI CHAMA CHA WANANCHI CUF na MFUNULIE RAIS JOHN POMBE
MAGUFULI KUWA KUZUIA SHUGHULI ZA VYAMA VYA SIASA NI KUJARIBU KUIINGIZA NCHI
YETU KWENYE MIGAWANYIKO, MIVUTANO NA HATA MACHAFUKO"
Julius Sunday Mtatiro, Dar
Es Salaam.
Jumamosi, 09 Julai 2016,
+255787536759 (Ujumbe
mfupi na Whatsup tu),
juliusmtatiro@yahoo.com
(Barua Pepe).
COMMENTS