TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI *Aongoza kikao cha wadau kujadili utekelezaji wa Serikali kuhamia dodoma *Awapa siku 14 wakamilis...
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
*Awapa siku 14 wakamilishe na kumkabidhi mpango kazi wao
WAZIRI
MKUU Kassim Majaliwa amesema uamuzi wa Serikali kuhamia siyo siasa kama watu
wanavyodhani bali ni utekelezaji wa maamuzi kamili na kwamba Serikali
inakamilisha eneo la kisheria juu ya uamuzi huo.
“Hapa
tulipofika ni hatua ya utekelezaji wa pamoja na hakuna namna nyingine kwa
sababu uamuzi umeshatolewa. Nataka niwahakikishie kwamba hii siyo siasa,
tunachokamilisha ni eneo dogo tu la kisheria juu ya uhamishaji wa makao makuu
kuja Dodoma na katika Bunge la Septemba sheria hii itapitishwa,” amesema.
Ametoa
kauli hiyo leo jioni (Jumanne, Julai 26, 2016) wakati akizungumza na viongozi
wa mkoa, Serikali za mitaa, viongozi wa dini, wajasiriamali, wazee wa mji huo,
wasafirishaji, wafanyabiashara, wakuu wa taasisi za elimu, za kifedha na watoa
huduma mbalimbali katika mkutano uliofanyika kwenye ukumbi wa Hazina ndogo
mjini Dodoma.
Waziri
mkuu ambaye aliitisha kikao cha kazi na wadau hao mjini Dodoma, ameutaka
uongozi wa mkoa huo pamoja na wadau wake wakae na kuandaa mpango kazi wa jinsi
ya kupokea na kutekeleza uamuzi wa Serikali kuhamia Dodoma.
Pia
ametoa siku 14 kwa uongozi wa mkoa wa Dodoma kukamilisha mpango kazi wao na
kumkabidhi mapendekezo yao ili yaweze kuingizwa kwenye mpango mkubwa wa
Serikali kuu.
“Uongozi
wa Mkoa, ukishirikiana na Ofisi yangu kupitia Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri
Mkuu na Ofisi ya Rais TAMISEMI usimamie na kuyaratibu majukumu haya. Ndani ya
siku 14 nipate proposal ya kwanza namna mtakavyoyatekeleza. Naagiza
kiundwe kikosi kazi chini yenu kitakachowajumuisha makundi yote niliyoyataja,”
amesema Waziri Mkuu.
Waziri Mkuu amesema chimbuko la uamuzi wa kuhamia
Dodoma kuifanya makao makuu ya Serikali lilikuwa ni ndoto ya Baba wa Taifa,
Mwl. Julius Kambarage Nyerere ambayo imeendelea kudumu katika Ilani ya Uchaguzi
ya Chama cha Mapinduzi ikiwemo Ilani ya Uchaguzi ya Mwaka 2015 chini ya Ibara
ya 151.
“Napenda kumshukuru Mheshimiwa Dkt. John Pombe
Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Makamu wa Rais Mheshimiwa
Samia Suluhu Hassan, na viongozi wengine wote wa Chama kwa
kusimamia ndoto ya Baba wa Taifa ya kuhamishia Makao Makuu hapa
Dodoma. Ni imani yangu kuwa wananchi wote mtaunga mkono uamuzi huu muhimu kwa
Serikali yetu na wananchi kwa ujumla, amesema.
Akiweka msisitizo juu ya kazi kubwa inayowakabili
viongozi hao, Waziri Mkuu amesema masuala yanayotakiwa kufanyika kuanzia sasa
ni pamoja na Mamlaka ya Ustawishaji
Makao Makuu (CDA) kuhakikisha eneo la makazi ya Serikali Kuu
litakalotumika kwa ofisi za wizara na taasisi zake, makazi ya watumishi na
huduma za biashara elimu na taratibu zote za kisheria za kulitwaa zinakamilika
kwa haraka na linakuwa tayari kwa matumizi.
“Natambua kazi iliyopo
mbele yetu ni kubwa na inahitaji jitihada za pamoja. Hivyo kila taasisi na mtu
mmoja mmoja ana jukumu la kuhakikisha kuwa tunajipanga vizuri na kuweka
mazingira ya ujio wa Serikali katika maeneo yote muhimu,” amesema.
Amezitaka Mamlaka za Mipango Miji na hasa CDA
wahakikishe wanaweka mfumo mmoja wa upatikanaji wa viwanja ambao utajulikana na
kila mmoja, utakuwa wazi usio na urasimu. “Mfumo huu wa viwanja uwekwe kwenye
mfumo wa kompyuta na uuzaji wa viwanja hivyo uwe wa kieletroniki kuepusha
udanganyifu kutoka kwa madalali,” amesisitiza.
Waziri Mkuu ameonya CDA na Manispaa zisibadili
ramani ya mipango miji iliyokwishawekwa awali kama vile maeneo ya wazi kutumika
tofauti na makusudio yaliyokusudiwa na akaagiza maeneo hayo yote yarejeshwe na
kufufuliwa.
“Natambua katika makazi hapa Dodoma kulitengwa
maeneo ya vituo maalum vijulikanavyo kama D Centers kwa ajili ya kutoa
huduma mbalimbali. Cha ajabu sasa kuna magenge, groceries na sasa
naagiza kwa hadhi ya Makao Makuu haya maeneo sasa yatumike kuwekeza maduka
makubwa (shopping malls) ambamo huduma zote mbalimbali hupatikana,” amesema.
Ameitaka Manispaa
iboresha usafi wa mazingira na bustani zake kwa kushirikiana na taasisi
mbalimbali kuzitunza. Pia ameitaka manispaa ya mji huo ishirikiane na TANROADS
kuboresha barabara zote za mitaa na taa za barabarani mji ukae kisasa, na
usalama uwe bora zaidi.
“Eneo jingine muhimu ni Manispaa na CDA kuhamisha
makundi mbalimbali ya wafanyabiasahra na huduma za masoko yasiyo rasmi na
kuyapa maeneo yaliyo rasmi na bora zaidi. Hii ni pamoja na maeneo ya
maegesho ya bajaji, bodaboda, taxi na daladala. Pia mazingira ya Stendi Kuu yaboreshwe,
vyoo vya kulipia pia vijengwe katikati ya mji,” amesisitiza.
Waziri Mkuu ameuagiza uongozi wa Wakala wa majengo
(TBA) waorodheshe majengo yote ya Serikali na taasisi zake yanayotumika kwa
sasa na yasiyotumika, “Nataka muyawekee utaratibu maalum wa matumizi yake ili
tupate kujua yanayoweza kutumika kwa muda kwa baadhi ya wizara na taasisi zake.
Hii ni pamoja na jengo jipya la Mkuu wa Mkoa, linaloendelea kujengwa.”
Amewataka
wakazi wa Dodoma watumie fursa hiyo kujenga nyumba za kuishi za kutosha, nyumba
za kulala wageni na mahoteli ili watu watumishi na wageni wanapokuja wasipate
taabu mahali pa kuishi.
(mwisho)
IMETOLEWA
NA:
OFISI
YA WAZIRI MKUU,
S.
L. P. 980,
DODOMA.
JUMANNE,
JULAI 26, 2016.
COMMENTS