TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI Jumbe Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amemtumia salamu za rambiram...
TAARIFA
KWA VYOMBO VYA HABARI
Jumbe |
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amemtumia salamu za rambirambi Rais wa
Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein kufuatia
kifo cha Rais Mstaafu wa Awamu ya Pili wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi na pia Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Aboud
Jumbe Mwinyi kilichotokea leo tarehe 14 Agosti, 2016 Jijini Dar es Salaam.
Mhe. Aboud Jumbe Mwinyi alikuwa
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na pia alikuwa Makamu wa Kwanza
wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuanzia Mwaka 1972 hadi 1984.
Kufuatia kifo hicho Rais Magufuli
amesema Taifa limempoteza mtu muhimu ambaye alijitoa kupigania Uhuru, Umoja, Haki
na Maendeleo ya Wananchi wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla katika kipindi
kigumu ambacho Taifa lilikipitia.
"Nimeshitushwa sana na kifo
cha Mzee wetu Mhe. Aboud Jumbe, kwa hakika Tanzania imepoteza mtu muhimu ambaye
katika kipindi cha uongozi wake alitoa mchango mkubwa wa kuipigania na kuijenga
Tanzania tunayoiona leo" Amesema Rais Magufuli.
Dkt. Magufuli ameendelea "Kupitia
kwako Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed
Shein napenda kuwapa pole familia ya Marehemu, Ndugu, Jamaa na Marafiki wote, Wananchi
wa Zanzibar na Watanzania wote kwa ujumla kwa kufikwa na msiba huu mkubwa"
Rais Magufuli amemuombea marehemu
Aboud Jumbe Mwinyi apumzike mahali pema peponi.
Nayo
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeeleza kusikitishwa kwake na kifo cha
aliyekuwa rais wa Zanzibar na mwenyekiti wa baraza la mapinduzi Alhaji Aboud
Jumbe Mwinyi kilichotokea nyumbani kwake Mji mwema Dar-es-Salaama.
Kwa
mujibu wa taarifa iliyotolewa na waziri wa nchi Ofisi ya Makamo wa pili wa rais
Mohamed Aboud , SMZ inaukumbuka mchango mkubwa wa hayati Jumbe katika kipindi
cha uongozi wake wa miaka 13.
'Serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar imesikitishwa na kifo cha hayati Alhaji Aboud Jumbe
ambaye alikuwa rais wa Zanzibar kwa muda wa miaka 13 huku mchango wake mkubwa
katika kukuza na kuimarisha demokrasia ukibakia kielelezo kwa wananchi wa
Zanzibar na Tanzania kwa ujumla'alisema.
Kwa
mujibu wa taarifa za kutoka kwa familia ya hayati Jumbe mazishi yake
yanatazamiwa kufanyika kesho mchana hapo nyumbani kwake Migombani nje kidogo ya
mji wa Zanzibar eneo ambalo watoto wake watatu wamezikwa hapo.
Jumbe
alishika madaraka ya kuongoza Zanzibar katika mwaka 1972 mara baada ya kuuwawa
kwa aliyekuwa rais wa kwanza wa Zanzibar hayati Abeid Amani Karume ambapo
baraza la mapinduzi kwa kauli moja lilimchaguwa kushika wadhifa huo wa rais wa
Zanzibar.
Kufuatia
kuchafuka kwa hali ya kisiasa Zanzibar katika mwaka 1984 Jumbe alilazimika
kujiuzulu pamoja na viongozi wengine akiwemo waziri kiongozi Ramadhan Haji Faki
na hivyo kupoteza nyadhfa zote ikiwemo makamo wa rais wa muungano na makamo
mwenyekiti wa chama cha mapinduzi.
Alhaji
Aoud Jumbe Mwinyi atakumbukwa kwa mambo mengi akiwa ni mmoja ya viongozi
walioshirikiana na baba wa taifa mwalimu Nyerere kuzaliwa kwa chama cha mapinduzi CCM hapo mwaka 1977 katika
uwanja wa Amaan Zanzibar.
Kabla
ya kuzaliwa kwa CCM Jumbe alikuwa rais wa chama cha ASP ambapo ushawishi mkubwa
wa hayati Jumbe ndiyo uliosababisha kuunganishwa kwa vyama hivyo na kuzaliwa
kwa CCM ikiwa ni moja ya juhudi za kuimarisha muungano wa Tanganyika na
Zanzibar.
Nacho
Chama cha Mapinduzi Zanzibar kimearifu kusikitishwa na kifo cha mmoja ya
viongozi wake ambaye alikuwa Makamo Mwenyekiti wa kwanza wa chama hicho Aboud
Jumbe Mwinyi.
Kwa
mujibu wa taarifa iliyotolewa na naibu katibu mkuu wa chama cha Mapinduzi
Zanzibar Vuai Ali Vuai alisema mchango wa hayati Jumbe katika chama cha
Mapinduzi hautosahaulika ambapo yeye kwa kushirikiana na baba wa taifa mwalimu
Nyerere walihakikisha kinazaliwa chama chenye nguvu katika Jamhuri ya Muungano
hapo mwaka 1977.
'Chama
cha mapinduzi kinatoa masikitiko yake makubwa kufuatia msiba mkubwa wa
aliyekuwa makamo mwenyekiti wake wa kwanza hayati Aboud Jumbe
Mwinyi........mchango wa Jumbe hautosahaulika katika chama cha
Mapinduzi'alisema.
Alisema
Jumbe alihakikisha kinazaliwa chama kipya kitakachokuwa na nguvu pamoja na sura
ya Muungano kwa ajili ya faida ya wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania'alisema.
Alisema
tangu kuzaliwa kwa chama hicho,kimeendelea kupata mafanikio makubwa ikiwemo
kushinda katika chaguzi zote kuanzia za mfumo wa chama kimoja hadi vyama vingi.
Aidha
chama hicho kimeendelea kuwa imara bila ya kuyumba na kuendelea kushika hatamu
ya kuongoza dola katika kipindi chote kuanzia mwaka 1977 hadi leo.
'Mafanikio
yote ya chama cha mapinduzi hatuna budi kukumbuka juhudi zilizofanywa na hayati
Jumbe kwa sababu ndie aliyekiunganisha chama hicho kutoka ASP na TANU na
kuzaliwa CCM'alisem Vuai.
Aidha
Vuai alisema katika kuimarisha demokrasia na sauti za wananchi kusikika,Jumbe
alianzisha chombo cha kutunga sheria ambacho alikiita baraza la wawakilishi.
Baraza
la wawakilishi liliasisiwa katika mwaka 1979 kwa kuanzia viongozi kutoka katika
wilaya za Unguja na Pemba kwa kuzishirikisha jumuiya za chama ikiwemo umoja wa
vijana,wazazi ushirika na Umoja wa wanawake UWT.
'Huo
ndiyo mchango mkubwa wa hayati Jumbe katika kuanzisha chombo cha Baraza la
Wawakilishi ambalo aliliita ngome ya wananchi katika kusikiliza maoni yao
kusikika'alisema.
COMMENTS