Balozi wa Anwani za Makazi Duniani Prof. Anna Tibaijuka akiongea akimkabidhi Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe....
Waziri
Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa ameziagiza halmashauri
zote nchini kutekeleza mpango kazi wa anwani za Makazi na Postikodi kwa
kushirikisha wadau mbalimbali wakiwemo wananchi.
Waziri Mkuu Majaliwa
ametoa agizo hilo leo kabla ya kuzindua Mwongozo wa Mfumo wa Anwani za Makazi
na Mwongozo wa Postikodi uliofanyika katika ukumbi wa Pius Msekwa uliopo ndani
ya viwanja vya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dodoma.
“Nikizingatia hatua
ambazo zimechukuliwa na Serikali katika kuweka mazingira ya utekelezaji wa
anwani za makazi, naagiza halmashauri zote nchini kuzifanyia kazi changamoto
ambazo hazihitaji fedha ama ambazo hazihitaji gharama kubwa” amesema Waziri
Mkuu Majaliwa.
Waziri Mkuu
amebainisha baadhi ya changamoto ambazo hazihitaji gharama kuwa ni pamoja na
kuhakikisha barabara na mitaa yote inakuwa na majina yaliyorasimishwa na
wananchi wenyewe, kudhibiti mipango miji dhaifu na ujenzi holela, kuwa na
takwimu za idadi ya barabara na mitaa na nyumba katika kila kata na kuwa na
taarifa za wakazi katika kila kata.
Changamoto nyingine
zisizohitaji gharama kubwa ni kujengea uelewa wadau na wananchi kuujua na kuwa
mfumo huo, kuimarisha matumizi ya daftari la wakazi ambapo taarifa za
utekelezaji wa kazi hizo Waziri Mkuu ameagiza ziwasilishwe Ofisi ya Rais
TAMISEMI kabla ama ifikapo mwezi Desemba, 2016.
Aidha, Waziri Mkuu
Majaliwa amesema kuwa kufuatia nia ya Serikali kuhamia Dodoma, manispaa ya
Dodoma na halmashauri ya Chamwino zipewe kipaumbele cha utekelezaji ili kuweka
mazingira mazuri ya kuishi na kufanya kazi.
“Utekelezaji wa
Mpango katika Manispaa ya Dodoma na Halmashauri ya Chamwino ukamilike kabla ama
ifikapo mwezi Desemba, 2016 na kuhakikisha utekelezaji huo kukamilika kwa
wakati” amesema Waziri Mkuu Majaliwa.
Kwa upande mwingine
Waziri Mkuu amezitaka wizara za Ofisi ya Rais TAMISEMI, Wizara ya Ujenzi,
Uchukuzi na Mawasiliano, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi,
Manispaa ya Dodoma, Halmashauri ya Chamwino, CDA; TCRA na TPC zishirikiane
ipasavyo katika kukamilisha mpango wa anwani katika mkoa huo.
Mbali na hayo, Waziri
Mkuu amezitaka taasisi za TANROADS, TBA, NHC, Mipango Mji na Mradi wa Kuboresha
Miji (TSC) zinapoandaa mipango hususan mipango ya miundombinu na makazi,
ziainishe pia anwani za makazi kwa kushirikiana na Halmashauri katika maeneo
husika.
Katika kufanikisha
hilo, Waziri Mkuu amezitaka Ofisi ya Rais (TAMISEMI), Wizara ya Unjenzi,
Uchukuzi na Mawasiliano na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, TCRA
na TPC kushiriki ipasavyo katika utekelezaji wa mpango hususan katika kujenga
uelewa na uwezo kwa viongozi na watendaji wa halmashauri ili waweze
kutekeleza mpango huo ipasavyo.
Kwa upande wake
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa George
Simbachawene amesema kuwa Mpango huo umefanyiwa majaribio katika majiji mawili
ya Dar es salaam na Arusha pamoja na manispaa za Dodoma na Zanzibar.
Waziri Simbachawene
aliongeza kuwa ili kuwa na Tanzania ya kisasa, anwani za makazi ni kigezo
muhimu cha kuzingatiwa katika kundeleza majiji, manispaa, halmashauri, kata na
hata mitaa ambayo ndio inajenga taswira ya nchi.
Wakati
huo huo Waziri Mkuu amesema kuwa Mfumo wa Anwani za Makazi na Postikodi una
manufaa mengi ambao utarahisisha ukusanyaji wa mapato kutoka vyanzo mbalimbali
nchini.
Waziri
Mkuu Majaliwa amesema hayo leo mjini Dodoma wakati alipokuwa akizindua Mwongozo
wa Mfumo wa Anwani za Makazi na Mwongozo wa Postikodi ambao utatumika nchi
nzima.
“Kama
kila mlipa kodi tutamfahamu kwa uhakika anaishi wapi, tutamutoza
kodi stahiki na hili ni jambo muhimu la utawala bora” amefafanua Waziri Mkuu.
Waziri
Mkuu Majaliwa amesema kuwa uwepo wa anwani ya makazi nchini utasaidia
kurahisisha ukusanyaji wa mapato mbalimbali ikiwa ni jukumu muhimu la utawala
bora.
Aidha,
amesema kuwa mfumo huo wa anwani za makazi utaiwezesha Serikali
kuwahudumia wananchi wake kirahisi ikiwa ni pamoja na kutoa ulinzi, kurahisisha
mawasiliano miongoni mwa wananchi na Serikali.
Vile
vile mfumo huo utasaidia kurahisisha na kuongeza ufanisi katika utoaji huduma
za kijamii, huduma za kibiashara, huduma za dharura na uokoaji, kurahisisha
sensa, kuboresha daftari la wapiga kura, kuboresha huduma za posta na kuwezesha
utoaji wa biashara mtandao.
Waziri
Mkuu ameongeza kuwa katika nchi nyingi za viwanda na nchi zilizoendelea suala
la miundombinu ikiwemo Mfumo wa Anwani za Makazi na Postikodi ni muhimu na
linaeleweka kwa kila mtu katika kuanzisha, kukuza na kuendeleza uchumi wa
viwanda.
“Kwa
kutumia mfumo huu, viwanda viwe vikubwa au vidogo vinatambulika viko wapi kwa
anwani zao za makazi na hivyo kuweza kupima kirahisi ukuaji wa viwanda”
alifafanua Waziri Mkuu.
Waziri Mkuu amesisitiza taasisi zote za
umma na zile za binafsi zianze kutumia anwani za makazi na postikodi ili
kuchochea kasi ya maendeleo ya nchi ikiwa ni pamoja na kutumia katika makusanyo
ya mapato.
Waziri Mkuu Majaliwa
amewasisistiza wadau wote nchini kuzingatia kuwa na anwani ni haki ya kila mtu
na pia kupata huduma za msingi kupitia mfumo huo ni haki ya kila mtu.
Aidha, dhana ya kuwa
“dunia ni kijiji” inapaswa kuwa chachu ya kupata huduma zote mahali ulipo,
inahitaji juhudi za makusudi za kuhakikisha Tanzania imekuwa sehemu ya kijiji
hicho na inakuwa ni moja ya mataifa kinara wa kutoa huduma mbalimbali kwa
ufanisi kwa kutumia Mfumo wa Anwani za Makazi na Postikodi.
Kwa upande wake
Balozi wa Anwani za Makazi Duniani Prof. Anna Tibaijuka amesema kuwa anajivunia
mradi huo kutekelezwa nchini ambao utasaidia kuonesha watu mahali wanapoishi
ambapo Tanzania imefanikiwa kuwa na anwani za makazi nchi nzima licha ya
changamoto ya kuwa na miji mingi ambayo haijapangwa.
Zao la anwani za
makazi linatokana na Umoja wa Posta Dunia (UPU) iliyopitishwa katika mkutano
mkuu wa 25 uliofanyika mjini Doha, Qatar mwaka 2012 ambao ulipitisha azimio la
kuzitaka nchi zote duniani kuhakikisha kuwa kila mtu anakuwa na anwani.
Source:Beatrice Lyimo na Eleuteri Mangi, MAELEZO, Dodoma
COMMENTS