W aziri Mkuu, Kassim Majaliwa akisaidiwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mohamed Chande Othaman kukata utepe wakati alipozindua Mpango Mkak...
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amezitaka taasisi za
umma kuhakikisha zinasogeza huduma za kijamii karibu na wananchi ili wazipate
kwa urahisi na kwa gharama nafuu.
Ametoa wito huo leo (Jumatano, Septemba 21, 2016)
wakati akizindua Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania (2015-2020) na Mradi wa
Maboresho ya Huduma za Mahakama ya Tanzania kwenye eneo inapojengwa Mahakama ya
Hakimu Mkazi Pwani na Mahakama ya Wilaya ya Kibaha, mkoani Pwani.
Waziri Mkuu amesema wananchi wengi
wanapata shida ya kufikia huduma mbalimbali za kijamii zikiwemo za mahakama
katika ngazi ya kata na wilaya jambo ambalo halikubaliki.
“Nichukue fursa hii kuwakumbusha wenzetu wa
mahakama kuwa, sisi sote tupo kwa ajili ya kuwahudumia Watanzania, hivyo
mipango na mikakati yetu iangalie utaratibu utakaotoa
haki kwao ili kuwaongezea imani kwa Mahakama na Serikali kwa ujumla,” amesema.
Amesema mpango mkakati
aliouzindua leo ni dalili nzuri ya uongozi na utendaji wa Mahakama ambayo
inajitambua, inajua inataka kwenda wapi na kwa muda upi na kuweka utaratibu
wa kujipima na kujitathmini kwa kila hatua.
“Naamini mtajielekeza
vizuri katika utekelezaji wa Mpango Mkakati huu na kimsingi Serikali ya awamu
ya Tano chini ya Rais Dkt. John Magufuli ipo bega kwa bega nanyi na inaunga
mkono jitihada zote za kuimarisha Mahakama.”
Waziri Mkuu pia alizindua
Mpango Mkakati wa mwaka 2015/16 – 2019/20 na Mradi wa Maboresho ya Huduma za
Mahakama ya Tanzania unaohusisha wilaya ya Kibaha, Mkuranga na Bagamoyo. Mradi
huo utakaogharimu sh. bilioni 139.5 (sawa na dola za Marekani milioni 65)
utagharimiwa kwa fedha kutoka katika bajeti ya Serikali na mkopo wa masharti
nafuu kutoka Benki ya Dunia.
Amesema Serikali itahakikisha fedha zilizotolewa
na Benki ya Dunia katika mradi huo zinatumika kwa uaminifu mkubwa ili kufikia
malengo yaliyokusudiwa na kuahidi kuwa Serikali itaendelea kutoa fedha
ili kuwezesha utekelezaji wa mradi huo.
Mapema,
akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na hadhira iliyohudhuria uzinduzi huo,
Jaji Mkuu wa Tanzania, Othman Chande alisema mahakama imeanzisha kada mpya ya
watumishi wa kusimamia masuala ya fedha ili kada ya sheria iendelee na shughuli
za mahakama tu.
Alisema kuzinduliwa kwa
mpango mkakati wa mwaka 2015/16 hadi 2019/20 pamoja na na Mradi wa Maboresho ya
Huduma za Mahakama ya Tanzania kutaiwezesha mahakama kujenga mahakama Kuu kati
ya tano hadi saba katika kipindi cha miaka mitano ijayo.
Alisema kati ya mikoa 26
nchini, ni mikoa 14 tu ambayo ina Mahakama Kuu na kwamba mahakama hizo zinaweza
kujengwa kwenye mikoa ya Njombe, Geita, Simiyu, Katavi, Singida, Manyara,
Songwe, Lindi, Pwani na Morogoro.
Katika hatua nyingine, Waziri
Mkuu amesema amefarijika na hatua na Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Bw. Hussein
Katanga kwa kuamua kushirikiana na Chuo Kikuu cha
Ardhi (ARU) na Baraza la Taifa la Ujenzi (NCC) katika kuhakikisha kuwa
Mtanzania wa kawaida anasogezewa huduma za kisasa za mahakama kwenye majengo
yenye ubora wa hali ya juu yatakayowezesha utoaji wa huduma kwa haraka na
gharama nafuu.
Amesema uamuzi wa kukitumia Chuo cha Ardhi ni wa busara
sana kwani umepunguza gharama za ujenzi kwa zaidi ya sh. milioni 800 kwa
kutumia teknolojia ya ujenzi wa nyumba na Ofisi kwa gharama nafuu ijulikanayo
kama Moladi.
“Mheshimiwa Katanga aliamua kutagaza zabuni
na katika waliojitokeza, wa kwanza alitaka kujenga kwa sh. bilioni 1.73, wa
pili alitaka sh. bilioni 1.55 na wa tatu alitaka sh. bilioni 1.3.”
“Lakini Chuo cha Ardhi kwa kimetumia gharama ya
sh. milioni 550 tu, sasa kwa nini tusijifie watu wa aina hii? Na ndiyo maana
Profesa Mshoro (Makamu Mkuu wa Chuo) ni miongoni mwa watu walioko kwenye Kamati
ya kuishauri Serikali juu ya ujenzi mpya wa Mji Mkuu wa Dodoma,” alisema.
Amemtaka Prof. Mshoro aimarishe kitengo chake cha
ujenzi ili kiweze kuendana na kasi ya mahitaji hasa katika suala la ujenzi wa
makzi na Ofisi Dodoma. Pia amemshauri awasiliane na Benki ya
Rasilmali (TIB Corporate na TIB Development) ili kupata ushauri wa mitaji ya
kufanya kazi kubwa kubwa.
“Imarisha kitengo chako cha ujenzi ili upate Vijana
wengi wa kusimamia miradi hasa ya ujenzi wa nyumba za walimu, mabweni ya
wanafunzi, hospitali na vituo vya afya ambavyo mahitaji yake ni makubwa hapa
nchini,” alisisitiza.
(mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
2 MTAA WA MAGOGONI,
S. L. P. 3021,
11410 - DAR ES SALAAM.
JUMATANO, SEPTEMBA 21,
2016
COMMENTS