Christopher Ole Sendeka, Msemaji wa CCM na Mjumbe wa Halmashauri kuu ya Taifa akizungumza kwenye mkutano wake na waandishi wa habari ...
TAARIFA KWA VYOMBO
VYA HABARI
Ndugu wanahabari,
Kwa muda sasa kumekuwepo na usambazaji
wa taarifa za upotoshaji zinazotolewa na baadhi ya wanasiasa wakishirikiana na
baadhi ya vyombo vya habari zinazolenga kukejeli, kudhihaki, kukatisha tamaa, kubeza
na kudhoofisha jitihada zinazofanywa na Chama Cha Mapinduzi na Serikali zake
katika kuleta maendeleo kwa Watanzania.
Kumekuwepo na makala zinazoandikwa na
magazeti mawili ya nje ambazo hutolewa kila baada ya miezi miwili na ambazo
zinapotosha na kuandika habari zisizo za kweli kuhusu Tanzania.
Pia, yapo magazeti mawili ya ndani
ambayo yamekuwa yakitoa makala mfululizo kwa kila wiki zinazolenga kumchafua
Mheshimiwa Rais na kuichafua taswira ya nchi yetu.
Tumesikitishwa na waandishi wa makala hizo
walioamua kujivua uzalendo na kushiriki mpango wa kuiharibu heshima na taswira
ya nchi yetu kwa maslahi ya maadui zetu wa nje na baadhi ya wanasiasa.
Tunafuatilia kujua nini kinawasukuma kufanya hivyo na kwa maslahi ya nani
ilhali sote ni Watanzania. Je ni tamaa ya madaraka tu au mengine? Hakuna
anayepinga ukosoaji bali unapaswa uwe ukosoaji wenye nia njema kwa nchi.
Ndugu wanahabari,
Mtakumbuka hivi karibuni aliyewahi kuwa
Waziri Mkuu aliyejiuzulu kwa tuhuma za ufisadi ambaye ni mjumbe wa Kamati Kuu
ya CHADEMA, Edward Lowassa, alisambaza taarifa kwa vyombo vya habari aliyoiita
ya tathmini ya mwaka mmoja baada ya uchaguzi mkuu wa Oktoba 25, 2015.
Katika taarifa yake hiyo, alidai kuwa
alileta msisimko mpya katika siasa za Tanzania, kwamba ameshirikiana na wenzake
kuionyesha nchi yetu maana ya demokrasia na kukosoa juhudi za serikali na
wateule wa Rais.
Demokrasia kimsingi ni dhana
inayohusisha ushiriki na kuheshimu mawazo ya wengi katika kufikia uamuzi. Ikiwa
maana halisi ni hii, tunajiuliza ni ipi demokrasia aliyoionyesha Lowassa ambayo
leo anajisifu kuwa nayo?
-
Tulishuhudia akiwa mgombea urais wa chama ambacho hakijui, hakushiriki
kukijenga wala kutoa mchango wowote unaompa hadhi ya kupeperusha bendera huku
katiba na kanuni ya chama hicho ikivunjwa. Kidemokrasia, anayepewa
fursa ya kupeperusha bendera ya chama chochote makini duniani ni kiongozi au
mwanachama aliyethibitika kwa imani na matendo, kuzielewa, kuzitekeleza,
kuzitetea falsafa, itikadi na malengo ya msingi ya chama hicho. Mgombea ni
taswira halisi na alama muhimu inayoakisi dhamira ya chama husika machoni kwa
wananchi.
-
Demokrasia ya kweli lazima ianzie ndani ya chama, ni demokrasia ipi iliyotoa
mamlaka kwa vyama vinavyounda UKAWA kuwanyima wanachama wao haki ya kuomba
ridhaa ya kupeperusha bendera za vyama walivyoviasisi, kuvitetea, kuvigharamia
na walivyovitumikia kwa kuamua kumteua mgombea “MTUNGUO” (ambaye
hajapimwa wala hajawahi kuvipigania). Kitendo hicho cha kutowashirikisha
wanachama na kuwanyima haki yao ya kikatiba ya kuchagua na kuchaguliwa
kilidhihirisha usaliti wa hali ya juu wa misingi ya demokrasia.
-
CHADEMA watuambie njia iliyotumika kuwapata wabunge wa viti maalumu. Ni
demokrasia gani inayotoa fursa kwa baadhi tu ya viongozi kuteua wabunge
ambao wanakiwakilisha chama chote. Ambapo kila kiongozi aliteua maswahiba zake
na wengine kwa ugeni wao ndani ya CHADEMA walikosa watu wanaowafahamu na kuamua
kuwateua wanawake maswahiba wao ndani ya CCM. Msingi wa kawaida wa kupata
wabunge wa viti maalum ukiacha kura za maoni, kigezo kingine muhimu ni mchango
wa mgombea/mwanachama huyo katika kukijenga na kukitumikia chama chake.
Yaliyotokea kwa CHADEMA kwenye wabunge wake wa viti maalum ni mapya kwenye
ulimwengu wa demokrasia. Inahitaji wataalamu wa sayansi ya siasa kufanya
utafiti wa aina hii mpya ya demokrasia.
Tulidhani baada ya mwaka mmoja kupita,
wenzetu hawa wangelikuwa wamejifanyia tathmini, kujikosoa, kujisahihisha na
hata kufanya uungwana wa kuwaomba radhi wanachama wao kwa uvunjifu mkubwa wa misingi
ya demokrasia, katiba na kanuni za vyama vyao.
Tunatoa wito kwa vyama vya siasa nchini
kutochukulia kwa wepesi masuala ya demokrasia na mabadiliko, yasiwe ni nyimbo
za kuburudisha au kutoa matumaini hewa kwa wanachama na wananchi. Kanuni mojawapo
ya demokrasia ndani ya vyama ni lazima ionekane katika muundo wake na katika
utekelezaji wa muundo huo.
Umefika wakati vyama vya siasa
vinapaswa kujifunza kuuza sera ili kujijenga na sio kusubiri matukio kwa ajili
ya kupata huruma ya wananchi. Tunasubiri kushuhudia na kusikia demokrasia
itakavyoendeshwa katika uchaguzi wa ndani wa vyama hivyo ambapo kuna taarifa
mmoja wa vigogo amefanikiwa kupata kiasi cha dola milioni 15 zitakazomsaidia
kupanga safu yake ya uongozi.
Katika kutimiza mpango huo, tayari yapo
mawasiliano ya mara kwa mara ya baadhi ya viongozi wakitoka Zanzibar na sehemu
zingine za nchi kuja Dar es Salaam, na imeonekana dhahiri mazungumzo yao
kutowashirikisha viongozi wenzao waandamizi kwani yanalenga kufanikisha mpango
huo.
Mheshimiwa Rais Dk. John Pombe
Magufuli, ameendela kufanya juhudi kubwa katika kuijenga nchi kwa kuimarisha
utendaji na nidhamu ya utumishi serikalini, kukusanya mapato na kusimamia
matumizi sahihi ya fedha, kupambana na kuzuia mianya ya rushwa pamoja na kusimamia
haki, usawa na wajibu kwa raia. Mwenzetu anayaona haya kuwa ni kuufanya
utumishi wa umma kaa la moto.
Juhudi hizi na nyinginezo ikiwemo
ununuzi wa ndege mpya, ujenzi wa miundombinu ya barabara, reli, afya kwa
kununua vitanda vya wazazi, kutoa elimu bure kuanzia shule ya msingi hadi
sekondari na nyinginezo hazipaswi kukatishwa tamaa kwa maslahi ya
wachache, ni vyema kuziunga mkono kwa maslahi ya taifa letu.
Katika kipindi hiki cha mwaka mmoja wa
Rais Dk. Magufuli madarakani, CCM inawaomba wananchi kuendelea kumuunga mkono
katika dhamira yake safi ya kuwaondolea kero, kuboresha huduma za jamii na
kuwaletea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.
KIDUMU CHAMA CHA
MAPINDUZI
Imetolewa na;-
CHRISTOPHER OLE SENDEKA
MJUMBE
WA NEC NA MSEMAJI WA CCM
28/10/2016.
COMMENTS