Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Mikopo Bw. Abdul-Razaq Badru akifafanua jambo katika mkutano na wanahabari jijini Dar es Salaam leo (Ju...
HESLB yafafanua vigezo utoaji mikopo
· Uhakiki wa
wanafunzi wanaoendelea na masomo waja
· Waliokosa
sababu zatajwa, wapewa nafasi ya kukata rufaa
Na Mwandishi Wetu
Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi
wa Elimu ya Juu (HESLB) imetoa ufafanuzi kuhusu vigezo inavyotumia katika
kuchambua, kupanga na kutoa mikopo kwa wanafunzi 20,183 (asilimia 74) wa mwaka
wa kwanza hadi sasa kati ya 25,717 iliyopanga kuwapa mikopo katika mwaka huu wa
masomo, 2016/2017.
Idadi iliyobaki (asilimia 26)
ya wanafunzi wa mwaka wa kwanza itajazwa na waombaji ambao baadhi ya nyaraka
walizowasilisha zinaendelea kuchambuliwa ili kuthibitisha uhalisi wake na
baadhi zitajazwa na waombaji ambao wanakata rufaa na kuwasilisha nyaraka
zinazothibitisha uhitaji wao kwa mujibu wa vigezo vya mwaka huu.
Aidha, katika mwaka huu wa
masomo, Serikali imepanga kutumia jumla ya Tshs 483 kutoa mikopo kwa wanafunzi
93,295 wanaoendelea na 25,717 wa mwaka wa kwanza.
Katika mkutano na waandishi
wa habari leo (Jumapili, Oktoba 30, 2016), Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB Bw.
Abdul-Razaq Badru amesema vigezo vikuu vinavyotumika mwongozo uliotangazwa na
Bodi hiyo wakati ilipotangaza kuanza kupokea maombi mwezi Juni mwaka huu ambao unataja
makundi makuu matatu ya watakaopata mikopo.
Vigezo
vilivyotumika kutoa mikopo
Kwa mujibu wa Bw. Badru,
kundi la kwanza linajumuisha wanafunzi waombaji wa mikopo wenye uhitaji maalum
kama wenye ulemavu uliothibitishwa na Waganga Wakuu wa Wilaya na yatima ambao
katika maombi yao waliwasilisha nakala za vyeti vya vifo zilizothibitishwa na
makamishna wa viapo.
“Kundi la pili linajumuisha
waombaji wa mikopo ambao baada ya uchambuzi wa taarifa zao walizowasilisha na
baada ya kulinganisha na gharama za jumla za masomo yao ya sekondari,
wamebainika kuwa wana uwezo mdogo wa kugharamia masomo yao ya elimu ya juu na
hivyo kuwa na uhitaji zaidi wa mikopo,” amesema Bw. Badru.
Katika mkutano huo
uliofanyika katika Ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO), Bw. Badru ametaja kundi
la tatu na la mwisho kuwa linajumuisha waombaji wa mikopo ambao wenye ufaulu wa
juu katika matokeo yao ya kidato cha sita na wamechaguliwa kujiunga na fani za
kipaumbele kwa taifa.
Fani hizo ni Sayansi za Tiba,
Ualimu wa Sayansi na Hisabati, uhandisi wa Kilimo, Mafuta na Gesi na Sayansi za
Ardhi, Usanifu Majengo na Miundombinu.
Makundi ya
wanafunzi waliopata mikopo
“Hivyo basi, hadi sasa
tumetoa mikopo kwa wanafunzi 20,183 wakiwemo wanafunzi yatima 4,321, wenye
ulemavu 118, wanafunzi wenye uhitaji waliosomeshwa na taasisi mbalimbali katika
masomo ya sekondari (87), wanafunzi wanaosoma kozi za kipaumbele 6,159 na
wanafunzi wanaosoma kozi zisizo za kipaumbele lakini wanaotoka kwenye familia
duni 9,498,” amefafanua Bw. Badru.
Sababu za
kukosa mikopo
Katika mkutano huo, kiongozi
huyo wa HESLB pia ameeleza kwa kina sababu nyingine za waombaji 27,053 ambao
hawajapangiwa mikopo.
Ametaja sababu hizo kuwa ni
pamoja na baadhi ya waombaji (90) kuwa na umri wa zaidi ya miaka 30, waombaji
mikopo waliopata udahili kwa sifa linganishi (equivalent qualifications) na
waombaji waliomaliza masomo ya kidato cha sita zaidi ya miaka mitatu iliyopita.
Kundi jingine la waombaji
waliokosa mikopo katika awamu ya kwanza ni waombaji waliopata nafasi katika
vyuo kwa ufaulu wa mitihani waliyofanya kama watahiniwa binafsi (Private
Candidates) na waombaji ambao hawakurekebisha fomu zao za maombi ingawa
waliitwa kufanya hivyo.
Nafasi ya
rufaa na uhakiki wa wanafunzi wanaoendelea na masomo
Katika mkutano huo,
Mkurugenzi Mtendaji huyo pia amewataka waombaji ambao hawajaridhika na upangaji
wa mikopo unaotangazwa, kuwasilisha rufaa zao kwa njia ya mtandao
utakaofunguliwa kuanzia katikati ya wiki ijayo.
“Tunafahamu kuwa kuna baadhi
ya wanafunzi wamekosa mkopo kwa kutowasilisha baadhi ya nyaraka ingawa
tuliwaomba kufanya hivyo, hawa na wengine wenye sababu za msingi, watapata
fursa ya kuwasilisha rufaa zao kwa njia ya mtandao na nakala kuzituma kwa
utaratibu tutakaoutangaza wiki inayoanza kesho,” amesema Bw. Badru.
Aidha, katika mkutano huo,
Bw. Badru amesema bodi ya Mikopo inatarajia kuanza kazi kuhakiki taarifa za
wanafunzi wanaoendelea na masomo ambao wanapata mikopo ya elimu ya juu kwa
lengo la kubaini kama ni wana uhitaji wa mikopo hiyo kwa mujibu wa vigezo au
hapana.
Katika zoezi hili
linalotarajiwa kufanyika kwa siku 30 kuanzia mwezi ujao (Novemba, 2016),
wanafunzi wote ambao ni wanufaika watalazimika kujaza dodoso maalum
litakalokusanya tarifa za kiuchumi za wazazi na walezi wao ili kuweza kupata
uhalisia wa sasa.
“Wanafunzi watakutana na
dodoso katika akaunti zao katika mtandao wetu wa maombi ya mikopo (OLAMS) na
watapaswa kujaza. Wale ambao hawatajaza dodoso hili kwa njia ya mtandao
tutasitisha mikopo yao na wale ambao baada ya uchambuzi tutabaini hawana
uhitaji, nao tutasitisha mikopo yao na watapaswa kuanza kurejesha fedha
walizokopokea,’ amefafanua.
HESLB ilianzishwa mwaka 2004
na kuanza kazi rasmi mwezi Julai mwaka 2005 kwa lengo la kutoa mikopo kwa
watanzania wahitaji waliopata nafasi za masomo katika vyuo vya elimu ya juu na
kukusanya mikopo iliyoiva kutoka kwa wadaiwa walionufaika na mikopo tangu mwaka
1994.
COMMENTS