Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa na Waziri wa Biashara na maendeleo wa Finland, Kai Mykkanen wakatizama moja ya mitambo ya umeme katika ...
WAZIRI MKUU Kassim
Majaliwa amewataka wakazi wa Jiji la Dar es Salaam watumie fursa ya uwepo wa
umeme wa uhakika kwa kuanzisha viwanda vidogo na vikubwa ili waweze kujiongzea
kipato.
Ametoa wito huo leo
(Jumatano, Novemba 16, 2016) wakati akizungumza na wananchi na viongozi
mbalimbali waliohudhuria uzinduzi wa mradi wa uboreshaji miundombinu ya umeme
jijini Dar es Salaam uliofanyika kwenye Ofisi za TANESCO zilizoko Mikocheni
jijini humo.
Akizungumza kabla ya
kubonyeza kitufe kuashiria uzinduzi wa mradi huo, Waziri Mkuu amesema: “Umeme
ni mhimili mkubwa sana kwa maendeleo ya nchi yoyote ile. Tumepata umeme wa
uhakika, tumieni fursa hii ya uwepo wa umeme wa uhakika kujiongezea kipato.”
“Hivi sasa
tumepata umeme wa uhakika, fanyeni kazi kwa bidii ili mfaidi matunda ya kuwepo
kwa umeme huo. Serikali inategemea kwamba sasa wananchi mtaanzisha
na kukuza viwanda vidogo vidogo na vikubwa, biashara zitapanuka na kilimo bora
huko vijijini kitaongezeka,” amesema.
Amesema Serikali
ya Awamu ya Tano imedhamiria kujenga uchumi wa viwanda na moja ya nyenzo kuu ya
kuendesha uchumi wa viwanda kwa tija na ufanisi ni upatikanaji wa nishati ya
umeme ya uhakika, na ndiyo maana kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo
Serikali imefanya jitihada kubwa kuhakikisha miundombinu ya umeme
inaboreshwa ili kuondoa tatizo la kukatika kwa umeme.
“Wataalam
wamenieleza kuwa mradi huu ulihusisha ujenzi wa kituo kikubwa cha kupozea umeme
cha MVA 100, ujenzi wa njia za usafirishaji umeme wa msongo wa kilovoti 132
katika maeneo mbalimbali ya Jiji kupitia chini ya ardhi, ujenzi wa njia za
usambazaji umeme wa msongo wa kilovoti 33, pamoja na ujenzi wa ujenzi
kituo cha udhibiti mifumo ya usambazaji umeme (Distribution SCADA System) katika
msongo wa kilovoti 33 na 11.”
“Kukamilika
kwa mradi huu kunaondoa adha zilizokuwepo awali kutokana na kukatika umeme mara
kwa mara. Jiji la Dar es Salaam ni kitovu cha shughuli za biashara katika
kuleta maendeleo ya Taifa ambapo upatikanaji wa umeme wa uhakika ni wa lazima,”
ameongeza.
Mapema,
akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na hadhira iliyokuwepo, Waziri wa Nishati
na Madini, Prof. Sospeter Muhongo amesema Wakala wa Jiolojia Tanzania kwa
kushirikiana na Wakala wa Jiolojia wa Finland wanaunda mpango wa pamoja wa
kuibua madini ya kisasa ambayo yanatafutwa zaidi duniani kukidhi mahitaji ya
kiteknolojia.
“Hivi sasa madini kama
graphite na lithium yanahitajika zaidi kwenye teknolojia za kisasa kama za
utengenezaji wa simu, tuachane na madini yaliyozoeleka kama vile dhahabu na
Tanzanite,” alisisitiza.
Alitumia fursa kuuagiza
uongozi wa TANESCO uhakikishe kuwa hakuna mgao wa umeme nchi nzima kwani
Watanzania wamechoshwa na tabia ya kukatiwa umeme mara kwa mara. “Ili tujenge
nchi ya viwanda, tunahitaji umeme wa uhakika, umeme unaotabirika na zaidi ya
yote umeme wa bei nafuu,” alisema huku akishangiliwa.
Naye Waziri
wa Biashara za Nje na Maendeleo wa Finland, Bw. Kai Mykkanen alisema Serikali
yake imedhamini ujenzi wa mradi huo kwa vile inaamini kuwa umeme wa uhakika ni
suluhisho la kuondoa umaskini kwa hiyo kukamilika kwa mradi huo kutaondoa adha
ya kukatika umeme kila mara.
Aliahidi kuwa nchi yake
itaendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika eneo la nishati ya umeme
na nishati mbadala.
Katika hatua nyingine,
Mkurugenzi Mtendaji
wa TANESCO, Eng. Felchesmi Mramba alisema ujenzi wa mradi huo umegahirimu sh.
bilioni 74.6 ambapo kati ya hizo, sh. bilioni 63.56 zimetolewa na Serikali ya
Finland na sh. bilioni 11.03 zimetolewa na Serikali ya Tanzania.
Alisema kukamilika kwa mradi huo kumewezesha
sehemu kubwa ya Jiji la Dar es Salaam kuwa na njia za mzunguko (ring circuit)
zinaoingizaa umeme. “Teknolojia hii iliyotumika itawezesha vituo vya kupozea
umeme kuwa na njia mbadala ya kupata umeme endapo njia mojawapo inayopeleka
umeme itapata hitilafu,” alisema.
Naye Meneja wa Kituo cha Kudhibiti Mifumo ya
Usambazaji, Eng. Alex Kalanje alimweleza Waziri Mkuu kwamba kwa kutumia mifumo
ya kisasa ya kompyta, (distribution SCADA SYSTEM) kituo hicho cha udhibiti wa
mifumo ya usambazaji umeme katika jiji la Dar es Salaam kitawasaidia watoa
huduma wao waweze kufuatilia kwa haraka zaidi pale matatizo yanapotokea.
“Baada ya kukamilika kwa kituo hiki, lengo letu ni
kujenga kituo kama hiki kwenye mjai ya Arusha, Mbeya, Dodoma na Mwanza,”
alisema.
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
2 MTAA WA MAGOGONI,
S. L. P. 3021,
11410 DAR ES SALAAM.
JUMATANO, NOVEMBA 16, 2016.
COMMENTS