Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiteta na Mwenyekiti wa Bunge na Mbunge wa Ilala, Mussa Azan Zungu, bungeni mjini Dodoma Februari 10, 2017....
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiteta na Mwenyekiti wa Bunge na Mbunge wa Ilala, Mussa Azan Zungu, bungeni mjini Dodoma Februari 10, 2017. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu) |
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
* Waziri Mkuu asema Serikali haitamuonea mtu yeyote
*Aomba Watanzania wote waunge mkono juhudi za Serikali
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali itapambana na janga la dawa za kulevya na kwa dhati bila kumuonea
mtu yeyote na kwa kuzingatia misingi ya sheria na haki.
Ametoa kauli hiyo leo jioni (Ijumaa, Februari 10, 2017) bungeni mjini
Dodoma wakati akitoa hoja ya kuahirisha mkutano wa sita wa Bunge la 11.
“Lengo la Serikali ni kuwasaidia walioathirika na dawa za kulevya na
kuwachukulia hatua kali wale waliowaathiri kwa maana ya wauzaji na wasambazaji.
Dhamira ya Serikali ni kupambana na janga hili kwa dhahiri na kwa dhati bila
kumuonea mtu yeyote na kwa kuzingatia misingi ya sheria na haki,” amesema.
Akizungumzia
idadi ya watu ambao hadi sasa wamekwishakamatwa katika nchi mbalimbali, Waziri
Mkuu amesema takwimu za jumla zinaonyesha kuwa Watanzania 515 wamekamatwa na
kufungwa gerezani kwa makosa ya kujihusisha na biashara ya madawa ya kulevya.
“Nchini China Watanzania walioko magerezani ni zaidi ya 200; Brazili kuna Watanzania
12; Iran wako Watanzania 63; Ethiopia Watanzania saba na Afrika Kusini wako
Watanzania 296,” amesema.
Waziri Mkuu amesema moja ya hoja za Kamati za Kudumu za Bunge
iliyojadiliwa na kuibua hisia kali katika mkutano huu wa Bunge ni kuhusu vita inayoendelea
nchini dhidi ya dawa za kulevya na akawaomba Watanzania wote waiunge mkono
Serikali juu ya vita hiyo.
“Watanzania wote ni mashahidi kwamba vijana wetu wengi wameendelea
kudhoofika kiafya kutokana na matumizi ya dawa za kulevya. Dawa za kulevya ni
hatari sana kwa usalama na ustawi wa Taifa letu. Vita hii inayopiganwa sasa
dhidi ya uagizaji, uzalishaji, usambazaji na matumizi ya dawa za kulevya ni
kubwa. Sote tunapaswa kuunga mkono jitihada hizo,” amesisitiza.
Amesema dawa
hizo za kulevya, huingia zaidi kutumia njia za bandari bubu kupitia Bahari ya
Hindi na mipakani kwa njia ya magari binafsi au mabasi kupitia nchi za Kenya,
Uganda na Mpaka wa Tunduma.
Ameyataja madhara ya kiafya yanayosababishwa na matumizi ya dawa za
kulevya ni pamoja na kuathirika kwa mfumo wa fahamu kwa mtumiaji ikiwamo
kuchanganyikiwa, kuwa na ulevi usioponyeka kirahisi na kusababisha kifo kama
mtumiaji atazidisha matumizi ya dawa za kulevya. “Madhara ya kiuchumi ni pamoja
na gharama kubwa za kuwatibu waathirika wa dawa za kulevya, gharama kubwa za
uchunguzi wa kimaabara kwenye Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali na watumiaji
wa dawa za kulevya kushindwa kujisimamia na kuendesha maisha yao,” ameongeza.
Katika hatua nyingine, Waziri
Mkuu ameziagiza Halmashauri zote nchini zifanye maoteo na kuyawasilisha Bohari
Kuu ya Dawa kabla au ifikapo tarehe 05 Machi 2017 ili kutekeleza azma ya
Serikali ya kusambaza dawa kwa wakati.
“Dhamira ya Serikali ya kusambaza
dawa kwa wakati kwenye Halmashauri zetu haitafanikiwa endapo Halmashauri
zitachelewa kuwasilisha maoteo ya dawa, vifaa tiba na vitendanishi. naomba
kutoa rai kwa Waheshimiwa Wabunge, mpate wasaa wa kufuatilia mchanganuo wa
usambazaji dawa katika Halmashauri zenu ambao hutolewa na Mheshimiwa Waziri wa
Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto,” amesema.
Amesema hali ya upatikanaji wa dawa
nchini inaendelea kuimarika huku akitolea mfano kiasi cha sh. bilioni 91
ambacho kimeshatolewa, kati ya sh. bilioni 251 zilizotengwa sawa na wastani wa
sh. bilioni 20 kwa mwezi.
Ili kuboresha upatikanaji wa dawa na
vifaatiba nchini, Waziri Mkuu amesema Serikali imeamua kununua madawa na vifaa
tiba moja kwa moja kutoka kwa wazalishaji badala ya mawakala.
“Napenda kuliarifu Bunge lako tukufu kwamba, utaratibu huo umeanza na
tayari Serikali imekamilisha taratibu za kimkataba na wazalishaji watano
wakubwa wa ndani ambao watanunua baadhi ya dawa kutoka ndani ya nchi, wakati
mikataba mingine 76 ya wazalishaji wa nje iko katika hatua za mwisho. Matarajio
yetu ni kwamba, utekelezaji wa mikataba ya nje utaanza katika mwaka wa fedha
2017/18,” amesema.
Amesema kutokana na
uamuzi huo wa Serikali pamoja na jitihada za Serikali za kuongeza bajeti ya
ununuzi wa dawa, Bohari ya Dawa imeweza kununua aina 105 za dawa muhimu sawa na
asilimia 78 ya aina 135 ya dawa muhimu zinazohitajika nchini.
“Shabaha yetu ni kwamba,
ifikapo Juni, 2017 usambazaji wa dawa muhimu nchini kote uwe umefikia asilimia
85. Taarifa hiyo imetolewa kwa kila Mheshimiwa Mbunge ili aweze kufuatilia kwa
karibu dawa na vifaatiba vinavyoletwa na Serikali kwenye Halmashauri zenu,”
amesema.
Bunge limeahirishwa hadi
Jumanne, Aprili 4, 2017.
(mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA
WAZIRI MKUU,
S. L. P.
980,
DODOMA.
IJUMAA,
FEBRUARI 10, 2017
COMMENTS