Bw. Michael Dunford Mwakilishhi wa WFP nchini Tanzania (kulia) na Mhe. Bw. Roeland Van De Geer, Balozi wa Umoja wa ...
Shirika la
Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Dunini
(WFP) limepokea mchango wa Euro (€) milioni 9.5 kutoka Umoja wa Ulaya (EU) kwa
lengo la kuunga mkono Mradi wenye thamani ya Euro milioni 24.5 (takribani
Shilingi za Tanzania bilioni 50) wa kusaidia kukuza Usalama wa Chakula na Lishe
katika mikoa ya kati nchini Tanzania.
Mradi
umeandaliwa ili kuimarisha usalama wa chakula na lishe kwa watu wapatao 40,000 na wakati huohuo ukichangia katika kupunguza
utapiamlo katika wilaya zinazolengwa za Bahi na Chamwino mkoani Dodoma na
Ikungi na Singida Vijijini katika mkoa wa Singida.
Mchango wa EU ulitangazwa
leo wakati wa hafla ya kutiliana saini makubaliano katika Jengo la Umoja jijini
Dar es Salaam uliofanywa na Dr. Mpoki Ulisubisya, Katibu Mkuu Wizara ya Afya,
Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Michael Dunford, Mwakilishi wa WFP
nchini Tanzania na Roeland Van De Geer, Mkuu wa Ubalozi wa Umoja wa Ulaya
nchini Tanzania.
“Licha ya
kuimarika kwa viashiria vingi vya afya katika muongo uliopita, bado hakuna
hatua kubwa katika kuimarisha hali ya lishe ya watoto na wanawake nchini
Tanzania,” Roeland Van De Geer, Mkuu wa Ubalozi wa Umoja wa Ulaya nchini
Tanzania, alisema wakati wa hafla hiyo. “Viwango vya juu vya kudumaa, kukosa
uzito wa kuridhisha na upungufu wa viinilishe nchini kunaashiria dharura ya
kimyakimya. Utayari wa kisiasa katika safu ya viongozi wa juu katika kukabili
lishe duni nchini Tanzania kwa mtazamo wa sekta nyingi kwa hakika ni mageuzi
makubwa. Kupitia mradi huu, EU pamoja na WFP ziko katika nafasi nzuri ya kubaini
na kuunga mkono uhusiano kati ya kilimo, afya, usalama wa chakula na lishe,
ambao hapo kabla haukuwa umeelezwa kwa kina au kufuatiliwa kikamilifu.”
Mradi huu
unatumia uwepo wa muda mrefu wa WFP katika mikoa ya kati nchini Tanzania na
uzoefu wake katika kutoa chakula chenye lishe na mawasiliano yenye lengo la
kubadilisha tabia ya kijamii kupitia vituo vya afya. Shughuli hizi
zitakamilishwa na jitihada katika sekta nyingine ili kutoa mtazamo ulio kamili
zaidi wa kupunguza kudumaa nchini. Viwango vya Taifa vya kudumaa viko katika
asilimia 34 ambapo kwa Dodoma ni asilimia 36.5 na Singida ni asilimia 29.2
“Tunashukuru
kwa mchango huu kutoka Umoja wa Ulaya kwani umeiwezesha WFP kuendelea na
programu hii bunifu inayolenga kukidhi mahitaji ya watu walio hatarini zaidi,
hasa watoto katika kile kipindi muhimu sana cha ukuaji wao, yaani siku 1,000 za
mwanzo tangu kubebwa mimba hadi kutimiza miaka miwili,” Mwakilishi wa WFP Michael
Dunford alisema katika hafla hiyo. “Programu hii itatoa ushahidi ambao utatoa
mwongozo kwa jitihada za baadaye, na kwa hiyo ina uwezekano wa kuleta mabadiliko
ya kudumu nchini Tanzania.”
Nchini Tanzania,
viwango vya utapiamlo sugu miongoni mwa watoto unatokana na umaskini, ukosefu
wa usalama wa chakula na ukosefu wa chakula cha kutosha kwa watoto wachanga na
unyonyeshaji watoto. Mradi utalenga kukuza maarifa kuhusu lishe, mtawanyiko wa
lishe na taratibu za kutumia maji, usafi wa mazingira na usafi wa mwili (WASH).
Shughuli hizi zitapewa nguvu kwa kuhamasisha ufugaji wa idadi inayofaa ya
mifugo, kupanda mazao tofautitofauti na kuhamasisha vijiji kuanzisha vikundi
vya kuweka akiba na kukopa, yote yakilenga kukuza uwezekano wa kupata mtaji.
Shirika la Save
the Children ni mshirika wa WFP katika kuimarisha ushirikiano na uwezo wa asasi
zilizojikita katika jamii ili kuhamasisha uwezeshaji wa jinsia na uhusiano wa
sekta mbalimbali katika suala la lishe, pamoja na kuratibu utekelezaji wa
kipengele cha kilimo katika mradi.
Kwa kuratibu
shughuli hizi chini ya mwamvuli wa WFP, Umoja wa Ulaya na Shirika la Save the
Children zitakuwa zikishughulikia changamoto nyingi zinazolenga kuimarisha
usalama wa chakula na lishe nchini Tanzania.
Mradi huu ni
sehemu ya majukumu ya WFP katika kufanikisha Lengo la 2 katika Malengo ya
Maendeleo Endelevu: Kufuta Njaa. Ili Kuondoa Njaa kabisa ifikapo mwaka 2030,
WFP inashirikiana na washirika mbalimbali kama vile serikali, sekta binafsi na
vyama vya kiraia.
# # #
WFP ni shirika kubwa zaidi duniani la misaada
ya kiutu linalopiga vita njaa duniani kote, kutoa msaada wa chakula katika
maeneo ya dharura na linaloshirikiana na jamii ili kuimarisha lishe na kujenga
uwezo wa kujinusuru. Kila mwaka, WFP linawasaidia takribani watu milioni 80
kote duniani katika nchi zipatazo 80.
Tufuate katika Twitter:
Shirika la Mpango wa Chakula: @WFP_Tanzania
and @WFP_Media
Umoja wa Ulaya: @EUinTZ and @EuropeAid
Kwa taarifa zaidi,
tafadhali wasiliana na:
Fizza Moloo, WFP/Dar es
Salaam, Simu. +255 (0) 692 274 729 or +255 (0) 784 720 022,
fizza.moloo@wfp.org
Susanne Mbise, Umoja wa
Ulaya, Ofisa Habari & Mawasiliano,
+255 (0) 754 323 245,
susanne.mbise@eeas.europa.eu
COMMENTS