JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA WIZARA YA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO TAMKO LA MHE. UMMY A. MWALIMU (MB) ...
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA WIZARA YA AFYA, MAENDELEO YA
JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO
TAMKO LA MHE. UMMY A. MWALIMU
(MB) - WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO KATIKA KILELE
CHA MAADHIMISHO YA SIKU YA MALARIA DUNIANI -
TAREHE 25 APRILI, 2017
Ndugu Wananchi,
Siku ya Malaria Duniani, huadhimishwa kila mwaka
ifikapo tarehe 25 mwezi Aprili. Maadhimisho haya yaliridhiwa katika Mkutano wa
60 wa Afya Duniani (World Health Assembly) huko Geneva nchini Uswisi.
Lengo kuu la maadhimisho haya ni kuielimisha na
kuikumbusha jamii ili kutambua athari za ugonjwa wa malaria, jinsi unavyoambukizwa,
na namna ya kujikinga. Aidha maadhimisho haya pia hutumika kuihamasisha jamii kuhusu
umuhimu wa kutambua dalili za malaria mapema; kuwahi kituo cha kutolea huduma
za afya ili kupima na kuthibitisha uwepo wa vimelea vya malaria kabla ya kuanza
kutumia dawa, kutumia dawa sahihi ya kutibu malaria pale itakapothibitika kuwa
na vimelea vya malaria na kukamilisha matibabu ya malaria kulingana na maelekezo
ya mtoa huduma. Kauli Mbiu ya mwaka huu inasema “Shiriki Kutokomeza Malaria
Kabisa, kwa Manufaa ya Jamii”.
Ndugu
Wananchi,
Takwimu kutoka katika vituo vya kutolea huduma za
Afya zinaonesha kuwa, takribani wastani wa
watu million 12 huripotiwa kuwa
na ugonjwa wa malaria katika vituo vya kutolea huduma za Afya kwa mwaka.
Aidha Takwimu za viashiria vya malaria kutoka tafiti
zilizofanyika katika kaya zimeonesha kuwa maambukizi ya malaria yalikuwa
asilimia 18 mwaka 2008, aslimia 10 mwaka 2012 na asilimia 14.8 kwa mwaka 2015.
Utafiti wa mwaka 2015-2016 unaonesha mikoa mitatu ya;
Kagera, Geita na Kigoma ina kiwango kikubwa cha maambukizi ya malaria, (Kagera
41%, Geita 38% na Kigoma 38%). Makundi yanayoathirika zaidi na malaria ni wajawazito
na watoto umri chini ya miaka mitano.
Mikakati inayopendekezwa kimataifa ambayo inatekelezwa
na Wizara yangu kwa kushirikiana na wadau
wetu ni pamoja na:
- Udhibiti wa mbu waenezao malaria; Udhibiti hufanyika kwa kutumia mbinu mbalimbali, ikiwa ni pamoja na matumizi ya vyandarua vyenye viuatilifu vya muda mrefu (LLINs); unyunyiziaji wa viuatilifu ukoko katika kuta ndani ya nyumba (IRS); kusafisha mazingira na kuua viluwiluwi vya mbu kwa kutumia viuadudu vya kibailojia (LSM) hasa katika maeneo ya mjini.
- Uchunguzi na matibabu ya ugonjwa wa malaria; Kwa kuongeza kasi ya upimaji wa ugonjwa wa malaria kwa kutumia kipimo mRDT au hadubini, na kutumia dawa mseto pale mgonjwa anapogundulika kuwa ana vimelea vya malaria; kuwapatia wajawazito vyandarua vyenye viuatilifu na dawa ya Sulphadoxine Pyrimethamine (SP) kwa vipindi maalumu wakati wa ujauzito ili kuwakinga na madhara yanayotokana na malaria.
Ndugu
Wananchi,
Nchi yetu imepata mafanikio makubwa ambayo yametokana
na utekelezaji wa mikakati na afua za kupambana na ugonjwa wa malaria na
ushiriki wa wadau mbalimbali. Miongoni mwa mafanikio hayo ni pamoja na:
- Kukamilika kwa kampeni: Kampeni ya ugawaji wa Vyandarua vyenye viuatilifu vya muda mrefu (LLINs) katika kaya bila malipo katika mikoa 23 nchini, ambapo jumla ya vyandarua zaidi ya millioni 27 vimegawiwa kwa jamii bila malipo. Lengo likiwa ni kuhakikisha kuwa kila mwananchi anatumia chandarua kujikinga na ugonjwa huu. Mikoa mitatu ya; Mtwara, Lindi na Ruvuma inapata vyandarua kupitia Mpango wa wanafunzi shuleni unaojulikana kama School Net Program (SNP) toka mwaka 2013.
Chandarua Kliniki: Ili kuhakikisha
upatikanaji wa vyandarua unakuwa endelevu hususan kwa makundi yanayopata athari
zaidi kwa ugonjwa wa malaria (Wajawazito na Watoto), utaratibu endelevu unaojulikana
kama CHANDARUA KLINIKI umeanzishwa ambapo wajawazito na watoto chini ya mwaka
mmoja hupewa chandarua wanapohudhuria kliniki kwa huduma mbalimbali. Hadi sasa
utaratibu huo unatekelezwa katika Mikoa saba (9) ya Lindi, Mtwara, Ruvuma,
Mwanza, Geita, Kagera, Mara, Simiyu na Kigoma.
Ugawaji vyandarua kupitia Shuleni:
Mpango mwingine ni wa ugawaji
wa vyandarua kupitia wanafunzi shuleni, ambapo wanafunzi wanapata chandarua kila mwaka,
kama njia ya kufikisha chandarua hicho kwa matumizi ya familia. Mpango huu wa
vyandarua shuleni unatekelezwa katika mikoa saba (7) ya; Mtwara, Lindi, Ruvuma,
Mwanza, Geita, Kagera na Mara kupitia ufadhili wa PMI.
Upuliziaji viatilifu Ukoko (IRS):
Utekelezaji wa mkakati wa
upuliziaji viuatilifu-ukoko katika kuta ndani ya nyumba, unatekelezwa katika
Halmashauri za mikoa ya Kanda ya Ziwa yenye maambukizi makubwa ya malaria. Ambapo
kwa mwaka huu, zoezi la upuliziaji limefanyika katika mikoa 4 na Halmashauri 10
za Sengerema, Buchosa na Kwimba (Mwanza);
Chato na Nyang’wale (Geita) Ngara,
Misenyi na Bukoba (V) (Kagera); Musoma
(V) na Butiama (Mara). Jumla ya nyumba
487,553 zimepuliziwa viuatilifu-ukoko na takriban wakazi 2,437,760 wamekingwa dhidi
ya malaria katika maeneo hayo.
Tiba Sahihi ya Malaria:
Tiba sahihi kwa wagonjwa
wa malaria imeendelea kutolewa katika vituo vya kutolea huduma za Afya, ikiwa
ni pamoja na kuhakikisha kuwa vipimo vya kutambua uwepo wa vimelea vya malaria kwa
kutumia hadubini au mRDTs vinapatikana
katika vituo vya kutolea huduma za afya wakati wote. Aidha, inasisitizwa kuwa dawa
zinatolewa kwa wale tu ambao watathibitika kuwa na vimelea vya malaria
(confirmed cases).
Serikali imeendelea
kuhakikisha kuwa wataalamu wanajengewa uwezo kwa kuwapatia mafunzo mbalimbali
ili kufanya kazi kwa ufanisi na weledi. Kwa kupitia juhudi hizi, kumekuwepo na
ongezeko la upimaji kufikia asilimia 90 katika vituo hivyo; zaidi ya lengo
ambalo Wizara ilijiwekea la asilimia 80.
Kwa upande wa dawa za
malaria zimeendelea kupatikana katika vituo vyote vya umma vya kutolea huduma
za afya.
Dawa katika Sekta Binafsi:
Upatikanaji wa Dawa Mseto za
malaria kwa bei punguzo kupitia sekta binafsi kupitia mpango wa Dawa Mseto kwa bei Punguzo (Co- payment mechanism
for subsidized ACTs in the private sector) ambao
unajumuisha vituo vya kutolea huduma za afya vya binafsi na maduka ya dawa. Mpango
huu, unalenga kuhakikisha kuwa hakuna mwananchi atakayekosa dawa za malaria
pale anapougua na kuamua kwenda kutibiwa katika vituo vya serikali au binafsi.
Viuadudu vya Kibailojia (Larvicides):
Serikali
kwa kushirikiana na kampuni ya (LABIOFAM) kutoka nchini Cuba, imekamilisha
ujenzi wa kiwanda cha kuzalisha viuadudu (biolarvicides)
ambavyo vitatumika kuua viluwiluwi vya mbu katika mazalia (madimbwi, mabwawa na
sehemu nyingine zinazozalisha mbu). Tayari kiwanda kimeanza uzalishaji wa
viuadudu, hivyo natoa wito kwa Halmashauri kutenga bajeti ya kununua
viuadudu hivyo kwa ajili ya utekelezaji
wa afua ya kuangamiza viluwiluwi vya mbu kwenye mazalia.
Changamoto:
Pamoja na mafanikio kadhaa yaliyopatikana, bado
tuna changamoto katika maeneo yafuatayo:
- Wanajamii kutotumia vyandarua ipasavyo wakati wote katika kujikinga na ugonjwa wa malaria pamoja na mitazamo potofu juu vyandarua;
- Hamasa ndogo ya Jamii kupima kabla ya kutumia dawa na kukubali matokeo ya vipimo. Hii huchangia katika matumizi yasiyo sahihi ya dawa za malaria na hivyo kuchangia katika usugu wa vimelea dhidi ya dawa.
- Jamii kutoshiriki kikamilifu katika kutunza mazingira na kuharibu mazalia ya mbu kwa kufukia madimbwi, kusafisha mifereji, kuweka mazingira safi na kuharibu mazalia ya mbu kwa kuondoa maji yaliyotuama.
- Changamoto kubwa ni upatikanaji wa rasilimali kwa ajili ya kuendeleza mafanikio tuliyoyapata. Kwa mfano misaada iliyokuwa ikitolewa katika nchi za Afrika imepungua kwa kiasi cha dola za kimarekani bilioni 3.6 kwa mwaka, Tanzania ikiwa miongoni mwa nchi hizo.
Ili kupunguza au kuondoa kabisa changamoto
zilizopo, Wizara yangu inahakikisha inaendelea kutekeleza ipasavyo mikakati
iliyopo ya kupamabana na ugonjwa wa malaria kwa kushirikiana na wadau.
Ujumbe
Muhimu kwa jamii
Niwakumbushe kuwa Ugonjwa wa malaria bado ni
hatari kwa uhai wetu, maendeleo na ustawi wa Taifa letu. Wakati tunaadhimisha
siku ya malaria Duniani, napenda kusisitiza yafuatayo:
- Wanajamii kushiriki kikamilifu katika kutekeleza na kutumia afua zote za kupambana na malaria.
- Kila mwanafamilia alale kwenye chandarua chenye viuatilifu kila siku ili kujikinga na malaria. Ni kosa kutumia vyandarua kwa matumizi yasiyo sahihi mf. Kuvulia samaki, kufugia kuku na kuzungushia bustani.
- Wanajamii kushiriki katika kuharibu mazalia ya mbu kwa kufukia madimbwi, kusafisha mifereji, kuweka mazingira safi na na kuondoa maji yaliyotuama.
- Kila mwanafamilia mwenye dalili za malaria ahakikishe anawahi kwenye kituo cha kutolea huduma na kupimwa kabla ya kutumia dawa, na endapo atagundulika kuwa na vimelea ahakikishe anatumia dawa kulingana na maelekezo ya mtoa huduma.
- Wajawazito kuhakikisha wanahudhuria Kliniki mapema ili kupata huduma zote muhumu ikiwemo kupata tiba ya tahadhari kwa vipindi kwa kutumia SP.
·
Wakurugenzi
wa Halmashauri kutenga bajeti ya kununua viuadudu hivyo kwa ajili ya utekelezaji wa afua ya
kuangamiza viluwiluwi vya mbu kwenye mazalia katika Halmashauri zao.
Msisitizo wa Wizara ya Afya, ni kwa wananchi na
wadau wote kuendelea kuona umuhimu na kutoa kipaumbele katika mapambano dhidi
ya ugonjwa wa malaria hususan kwa kutumia fursa zilizopo, kuwekeza katika
mapambano dhidi ya malaria na kutekeleza ipasavyo mikakati niliyoitaja hapo
juu.
Shukrani:
Napenda nichukue fursa hii kwa niaba ya Serikali,
kutoa shukrani zangu za dhati kwa wadau wetu wote waliochangia katika mafanikio
tuliyofikia wakiwemo; Mfuko wa Dunia wa kushughulikia ugonjwa wa UKIMWI, Kifua
Kikuu na Malaria (The Global Fund), Mfuko wa Rais wa Marekani unaoshughulikia Malaria
(PMI), Shirika la Misaada la Uingereza (DFID), Shirika la Maendeleo la Uswisi
(SDC), Shirika la Afya Duniani (WHO), Shirika la UNITAID, Taasisi zisizo za
Kiserikali, Sekta binafsi kupitia Mpango wa Malaria Safe Initiative, Taasisi za
Utafiti (NIMR na Ifakara Health Institute) nikitaja kwa uchache; na bila
kuwasahau ninyi wanahabari, wananchi na jamii kwa ujumla kwa kuwa tayari
kutumia mikakati hiyo kwa kushirikiana na Serikali.
Nimalizie kwa kusisitiza kwamba iwapo tutaitekeleza
ipasavyo mikakati niliyoitaja hapo juu, nina imani kabisa, tunaweza kujikinga
na ugonjwa wa malaria na hatimae
kuufanya ugonjwa wa malaria kuwa si tatizo kubwa tena katika jamii yetu.
Mwisho
kabisa niwakumbushe kuwa zama zimebadilika “Sio kila homa ni Malaria nenda
ukapime”, na “lala kwenye chandarua chenye viuatilifu kila siku” ili kujikinga
na malaria.
ASANTENI SANA KWA KUNISIKILIZA.
COMMENTS