Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetenga maeneo ya uwekezaji mjini Dodoma kwa ajili ya kujenga viwanda, mahoteli makubwa,...
Serikali ya Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania imetenga maeneo ya uwekezaji mjini Dodoma kwa ajili ya kujenga
viwanda, mahoteli makubwa, nyumba za makazi na huduma muhimu za kijamii.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mkuu wa
Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu Dodoma (CDA) Mhandisi Paskas Muragili
amesema kuwa maeneo hayo ni Njedengwa, hekta 580 ambapo miundombinu muhimu
imewekwa ikiwemo maji, umeme na barabara
ya lami ili kurahisisha uwekezaji, eneo la
Iyumbu hekta 78 na Western Industrial Area hekta 334.6 (WIA).
Mhandisi Muragili
ameongeza CDA imetenga hekta
14,700 eneo la Kikombo, Chigongwe hekta
6, 278, Nyankali hekta 2,495 na Mtumba hekta 8,000, kwa ajili ya kujenga mji
wa Serikali ambapo kutajengwa
Wizara mbalimbali, Idara za Serikali,
Taasisi, na mashirika yatakayowekeza Dodoma.
Vilevile, eneo hilo litajengwa
makazi ya watumishi wa Umma na huduma mbalimbali za kijamii kama masoko,
zahanati, hoteli, maduka na nyumba za kuabudia kulingana na imani zao.
Akikaribisha wawekezaji kuwekeza
Dodoma, Muragili amewahasisha Watanzania
na wasio watanzania kuchangamkia fursa hiyo kwa kujenga hoteli za kitalii za nyota tano na zile za
kawaida, kwa kuwa mji unategemea kupata wageni wengi siku za usoni.
“Nawakaribisha wawekezaji wa
ujenzi wa viwanda vikubwa, vya kati na vidogo, bila wasiwasi niwahakikishie ardhi iliyopo Dodoma inatosha
kwa uzalishaji mkubwa wa malighafi mbalimbali zitakazohitajika
viwandani”.
“Aidha, Mkoa huu upo katikati ya
Tanzania hivyo malighafi yoyote
itakayohitajika ni rahisi kufika Dodoma ambayo imeunganishwa kila kona na
barabara za lami,” alisema Muragili.
Pia mikoa inayoizunguka Dodoma
ikiwemo Manyara, Singida, Iringa na Morogoro inaweza kunufaika kwa wepesi zaidi
na fursa hizo.
Akiwatoa hofu wakazi wa Dodoma
Muragili amesema; “Ardhi itauzwa kwa bei ya kawaida ili wananchi waweze kumiliki viwanja”.
Ameyasema hayo akijibu hoja za
waandishi wa habari kuhusu kauli za wananchi kudai bei ya viwanja itapanda, kutokana
na ujio wa Makao Makuu ya Serikali, ambapo wananchi wa kipato cha chini hawataweza
kumiliki viwanja hivyo.
Muragili alisisitiza kuwa viwanja
havitapandishwa bei kwani kwa sasa CDA inauza mita moja ya mraba ya
kiwanja cha makazi Shilingi 5,500 hadi
10,000 za fedha ya Tanzania, katika maeneo ambayo kitaalamu tunayaita “medium
density”.
Aidha, alisema kuwa viwanja kwa
ajili ya uwekezaji mkubwa mita moja ya mraba ni Shilingi 13,300 fedha ya Tanzania, maeneo hayo kitaalamu
yanaitwa “low density”.
Mhandisi Paskasi Muragili ametoa
angalizo kwa wanaohitaji kununua viwanja mjini Dodoma ya kwamba anayetaka
kiwanja lazima afike na kufuata taratibu za
ofisi za CDA kwa kuwa ndiko viwanja vinakopatikana. “
“Tusinunue viwanja kienyeji,
mwisho wa yote utakuwa umedanganywa na madalali ambao kisheria ardhi ya mji wa
Dodoma iko chini ya CDA na haihitaji dalali ila ufuate taratibu zilizowekwa”,
alisema Muragiri.
Alimalizia kwa kusema “Kwa wale
wanaohitaji ardhi nje ya Dodoma kama Mpwapwa, Kongwa, Bahi, Kondoa, Chemba na Chamwino wahakikishe wanawasiliana na Mkuu
wa Mkoa wa Dodoma ili wapate taratibu rasmi za ununuzi wa ardhi.
Mapaka sasa eneo la WIA lina
viwanda kama Machinjio ya kisasa Dodoma na viwanda vya magodoro QFL na Dodoma
Halisi.
Mamlaka ya Ustawishaji Makao
Makuu (CDA) ni miongoni mwa Mamlaka zilizopata ufadhili wa kutekeleza mradi wa
Uboreshaji Miji Kimkakati unaofadhiliwa na Mkopo wa Benki ya Dunia na msaada
kutoka Serikali ya Denmark.
Aidha, tamko la serikali la mwaka
1973 lenye tangazo namba 230 la tarehe 12 Oktoba 1973 ndio liilianzisha Mamlaka
ya Ustawishaji Makao Makuu Dodoma kama
mji mkuu wa Serikali ulipewa majukumu
makuu 8.
Kutokana na wimbi la mataifa ya
Afrika kubadili miji mikuu, liliingia pia hapa nchini, na Hayati Mwalimu Julius
Kambarage Nyerere Rais wa kwanza wa Tanzania, ambaye ni miongoni mwa wana
watiifu wa Afrika alionyesha dhamira hiyo “kuhamia’ Dodoma kama njia ya kuunga
mkono.
Historia ya kuhamisha miji mikuu
ilitokea miaka ya 1970 nchi nyingi za kiafrika zilibadili miji mikuu ya
serikali. Mathalani Malawi ambayo ilibadilisha mji mkuu kutoka Blantyre kwenda jiji la Lilongwe,na Nigeria ilihama
kutoka Lagos kwenda Abuja.
Hoja kubwa iliyopelekea Mwalimu
Nyerere kuchagua mkoa huo ni kwamba
Dodoma ni katikati mwa Tanzania, hivyo itarahisisha kuleta maendeleo katika
mikoa yote kwa urahisi hususan utoaji wa huduma za msingi kwa wananchi.
Hiyo ndio hoja ya msingi iliyomsukuma
Mwalimu Nyerere kutoa maamuzi hayo ambapo alikuwa na uhakika iko siku dhana
yake itatimia, Hongera Rais Dkt. John Pombe Mangufuli kwa jitihada zako za
kutimiza ndoto za Muasisi wa taifa hili, sote tunaziona juhudi zako na
Watanzania wanakuunga mkono, Hapa Kazi Tu”.
Source: Judith Mhina - MAELEZO
COMMENTS