Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 21 Juni, 2017 amezindua viwanda vikubwa vitatu na mrad...
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe
Magufuli leo tarehe 21 Juni, 2017 amezindua viwanda vikubwa vitatu na mradi wa
upanuzi wa mtambo wa maji wa Ruvu Juu na ulazaji wa mabomba makuu kutoka
Mlandizi hadi Dar es Salaam ikiwa ni siku yake ya pili ya ziara ya kikazi ya
siku 3 mkoani Pwani.
Kwanza, Mhe.
Rais Magufuli amezindua kiwanda cha kutengeneza vifungashio cha Global Packaging
Tanzania Ltd kilichopo katika eneo la viwanda Kibaha ambacho kina uwezo wa
kutengeneza mifuko ya sandarusi 53,000 kwa siku kwa ajili ya kuhifadhia mazao.
Kiwanda hicho kinachomilikiwa na Mtanzania Bw. Joseph Otieno
Wasonga kimeajiri watu 110 na kimejengwa kwa gharama ya takribani Shilingi
Bilioni 8.
Pili, Mhe.
Rais Magufuli amezindua mradi wa kutengeneza matrekta 2,400 aina ya Ursus ambao utagharimu Shilingi
Bilioni 55, na matrekta hayo yatasambazwa nchi nzima kwa ajili ya kuboresha
sekta ya kilimo.
Mradi huu unamilikiwa na Serikali ya Tanzania kwa asilimia 100
na utazalisha matrekta ya aina 6 zenye nguvu ya kuanzia HP50 hadi HP 85.
Tatu, Mhe.
Rais Magufuli amezindua kiwanda cha chuma cha Kiluwa Steel Group kilichopo
Mlandizi ambacho katika awamu hii ya kwanza kina uwezo wa kuzalisha tani
500,000 za nondo kwa mwaka na awamu ya pili kitaongeza uzalishaji hadi kufikia
tani 1,200,000 kwa mwaka.
Balozi wa China hapa nchini Mhe. Dkt. Lu Youqing amesema
kiwanda hicho kiwanda hicho kinachomilikiwa na Mtanzania Bw. Mohamed Said
Kiluwa kwa asilimia 51 na asilimia 49 zinamilikiwa na mwekezaji kutoka China ni
muendelezo wa uhusiano na ushirikiano mzuri uliopo kati ya China na Tanzania.
Aidha, Shirika la Reli Tanzania (TRL) limejenga njia ya reli
ya kilometa 3.5 inayounganisha kiwanda hicho na reli ya kati ikiwa ni juhudi za
kurahisisha usafirishaji wa malighafi na vyuma vinavyozalishwa kiwandani hapo
kwenda ndani na nje ya nchi.
Akizungumza katika miradi hiyo, Mhe. Rais Magufuli amepongeza
uwekezaji huo na ameagiza vyombo vinavyohusika kutoa vibali kwa ajili ya ujenzi
wa viwanda hapa nchini viondoe urasimu ambao umekuwa ukiwakatisha tamaa
wawekezaji kujenga viwanda.
Mhe. Dkt. Magufuli ametoa wito kwa wamiliki wa viwanda hivyo
kujali maslahi na usalama wa wafanyakazi waliowaajiri, amezitaka benki hapa
nchini kujielekeza kufanya biashara na wananchi kwa kuwakopesha mitaji
wafanyabiashara na wajasiriamali badala ya kutaka kufanya biashara na Serikali
na ameiagiza Wizara ya Nishati na madini na Wizara ya Viwanda, Biashara na
Uwekezaji kuhakikisha viwanda vya chuma vinatumia malighafi za hapa nchini
kutoka Mchuchuma na Liganga.
Wakati
huo huo, Mhe. Rais Magufuli amezindua mradi wa upanuzi wa
mtambo wa maji wa Ruvu Juu na ulazaji wa mabomba makuu ya maji ya kutoka
Mlandizi hadi Dar es Salaam uliojengwa na Serikali ya Tanzania kwa gharama ya
Shilingi Bilioni 200 ikiwa ni mkopo kutoka Serikali ya India.
Kabla ya Mhe. Rais Magufuli kuzungumza na wananchi
waliohudhuria sherehe za uzinduzi wa mradi huo, Waziri Mkuu wa India Mhe.
Nalendra Modi ametoa salamu kwa njia ya luninga ambapo amempongeza Mhe. Rais
Magufuli na Serikali yake kwa kufanikisha mradi huo ambao utasaidia kuondoa
kero ya uhaba wa maji iliyowakabili wananchi wa Jiji la Dar es Salaam kwa miaka
mingi na utaboresha maisha ya watu.
Katika salamu hizo zilizowasilishwa na Balozi wa India hapa
nchini Mhe. Sandeep Arya Mhe. Waziri Mkuu Modi ametangaza kuwa Serikali yake
imepitisha kiasi cha Dola za Kimarekani Milioni 500 sawa na zaidi ya Shilingi
Trilioni 1 ambazo Tanzania itakopeshwa kwa ajili ya kusaidia miradi ya maji
katika maeneo mbalimbali hapa nchini.
Kwa upande wake Mhe. Rais Magufuli amemshukuru Waziri Mkuu wa
India Mhe. Nalendra Modi kwa kutoa mkopo huo na amesema upanuzi wa mradi wa
maji wa Ruvu Juu pamoja na mkopo huo vinaendeleza na kuimarisha zaidi uhusiano
na ushirikiano mzuri na wa kihistoria kati ya Tanzania na India.
Mhe. Rais Magufuli pia ameitaka Wizara ya Maji na Umwagiliaji
kujipanga vizuri kusimamia utekelezaji wa miradi ya maji inayosuasua, kudhibiti
upotevu na wizi wa maji na kuwakatia maji wadaiwa sugu wote.
Kesho tarehe 22 Juni, 2017 Mhe. Rais Magufuli atakamilisha
ziara yake ya kikazi ya siku 3 Mkoani Pwani kwa kuzindua kiwanda cha vinywaji
baridi cha Sayona Drink Ltd, kuzindua kiwanda cha kukausha matunda cha Elven
Agric Company na kuzindua mradi wa barabara ya Bagamoyo – Msata.
Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Kibaha, Pwani
21 Juni, 2017
COMMENTS