SEKTA ya Elimu ni miongoni mwa vipaumbele muhimu vya maendeleo vilivyopewa mkazo na Serikali ya Awamu ya Tano katika kufanikisha utoaji wa ...
SEKTA ya Elimu ni miongoni mwa vipaumbele muhimu vya maendeleo
vilivyopewa mkazo na Serikali ya Awamu ya Tano katika kufanikisha utoaji wa
huduma muhimu kwa wananchi ili kuchochea adhma ya kufikia uchumi wa kati
ifikapo mwaka 2025.
Kupitia Sera Mpya ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014, Serikali
imeazimia kutekeleza mipango mbalimbali ikiwemo utoaji elimu ya msingi bila
ada, kuongeza ubora wa elimu kwa kuimarisha ukaguzi shuleni, na kuboresha
miundombinu.
Aidha Serikali ilikusudia pia kuhakikisha upatikanaji wa vifaa
stahili vya kufundishia na kujifunzia, kuongeza ubora wa walimu kwa kutoa
mafunzo, motisha pamoja na
udhibiti wa taaluma ya ualimu.
Ili kufanikisha malengo hayo, Serikali imekuwa ikitekeleza miradi,
mipango na programu mbalimbali za elimu ili kuleta
maendeleo ya haraka ya rasilimali watu kwa kutayarisha idadi ya kutosha ya
Watanzania walioelimika na kupenda kujielimisha.
Miongoni mwa Programu hizo ni Programu ya Lipa Kulingana na
Matokeo inayotekelezwa na Serikali katika kipindi cha miaka mitano 2014-18
iliyokusudia kuimarisha usimamizi wa raslimali fedha na manunuzi ya umma katika
mipango ya elimu kwa Serikali Kuu na Serikali za Mitaa.
Programu hiyo inatekelezwa katika sekta za elimu ya msingi na
Sekondari na kufadhiliwa na Benki ya Dunia, Shirika la Kimataifa la Maendeleo
la Sweden (SIDA) na Ubalozi wa Uingereza
Aidha programu hiyo pia imelenga kuanzisha njia ya moja kwa moja
ya ugharimiaji elimu inayolenga kuipa motisha Serikali katika utekelezaji wa
mipango inayolenga matokeo ya haraka.
Maeneo muhimu yaliyochaguliwa kupitia programu hiyo ni pamoja na
utoaji wa zawadi na motisha ya fedha na zisizo za fedha kwa walimu na shule
zilizofanya vizuri, kutoa mafunzo kazini kwa walimu na kuimarisha mfumo wa
Serikali na kufanya ufuatiliaji ya utolewaji na utumiaji wa fedha za ruzuku.
Aidha kupitia programu hiyo Serikali imekusudia kuimarisha uwazi
wa matokeo ya mitihani kwa shule za Msingi na Sekondari na kufanya tathimni ya
kujua kusoma, kuhesabu na kuandika kwa shule za halmashauri zilizoteuliwa
katika zoezi hilo.
Katika kuhakikisha kuwa Programu hiyo inaleta tija iliyokusudiwa,
Serikali imeanisha vipaumbele vikuu vitatu vinavyotumika katika kila
Halmashauri ili kupima matokeo na kutoa motisha (fedha) kulingana na mahitaji
na matumizi iliyojiwekea.
Vipaumbele hivyo ni pamoja na upangaji wa walimu katika shule
zenye mahitaji, upelekaji wa ruzuku ya fedha za shule kutoka hazina pamoja na
uwezo wa halmashauri kukusanya takwimu kwa usahihi na kuziweka mtandaoni kwa
wakati.
Taarifa ya Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
inasema kuwa hadi sasa kiasi cha Tsh. Bilioni 90 zimeweza kupatikana kutokana na Serikali kutekeleza
vipaumbele vyake kwa ufanisi kulingana na fedha za motisha zinazotolewa katika
kila Halmashauri iliyopo katika mradi huo.
Aidha Serikali imetoa kiasi cha Tsh. Bilioni 22 za motisha kwa Halmashauri 179
zilizohakikiwa kwa mwaka 2015/16 ambapo zilitolewa kufuatana na viwango vya
utekelezaji wa viashiria vya utendaji katika sekta ya elimu.
Akiwasilisha Hotuba ya makadirio ya Bajeti ya mwaka 2017/18,
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI George Simbachawene anasema Programu ya
Lipa kulingana na matokeo imekusudia kuongeza ufanisi na uwajibikaji wa kutoa
elimu nchini na kujenga uwezo wa
Serikali wa kutekeleza vipaumbele vyake ilivyojiwekea.
Anasema Programu hiyo imeweza kuongeza kiwango cha ufaulu wa
Mtihani wa Taifa wa Darasa la Nne na Darasa la Saba, kutokana na jitihada
zilizofanywa na Serikali katika kuboresha mazingira ya kufundishia na
kujifunzia.
“Ufaulu katika Mtihani wa Taifa wa Kumaliza Shule ya Msingi
umeongezeka kutoka asilimia 68.4 mwaka 2015 hadi asilimia 70.36 mwaka 2016. Wanafunzi
wote waliofaulu Mtihani huo wamechaguliwa kujiunga na Kidato cha Kwanza mwaka
2017” anasema Simbachawene.
Aidha Simbachawene anasema kupitia Programu hiyo, Serikali katika
mwaka 2016/17 imeweza kutoa mafunzo kwa Maafisa Elimu Vifaa na Takwimu 370
kutoka Halmashauri 184 na Maafisa Elimu Taaluma
Mikoa 26 kuhusu matumizi ya mfumo wa uingizaji na utoaji wa takwimu kwa njia ya
kielektroniki ili kuboresha upatikanaji wa takwimu za Elimu kwa usahihi na kwa
wakati.
Kwa mujibu wa Simbachawene anasema Ofisi yake pia imeweza
kusambaza nakala za vitabu 1,412,832 vya masomo ya Historia, Jiografia na
Kiingereza kwa Kidato cha Kwanza hadi cha Nne na vitabu 159,737 vikiwemo 83,189
vya masomo ya sayansi na vitabu 76,548 vya masomo ya sanaa kwa Kidato cha Tano
na Sita zilizopo katika Halmashauri 184 nchini.
Kuhusu ujenzi wa Maabara, Simbachawene anasema Serikali kupitia
Mpango wa Uimarishaji wa Stadi za Kusoma Kuandika na Kuhesabu imefanikiwa
kununua vifaa vya maabara vyenye thamani ya Tsh. bilioni 16 na kuvisambaza
katika shule 1,696 zilizokamilisha ujenzi sawa na asilimia 47 ya shule za
sekondari 3,602.
“Shule za Sekondari nchini zinahitaji maabara 10,840 na zilizopo
kwa sasa ni 5,562 sawa na asilimia 51.3 na upungufu ni maabara 5,278 ambazo
zinaendelea kujengwa” anasema Simbachawene.
Simbachawene anasema kupitia kupitia Mpango wa Elimu wa Lipa kwa
Matokeo, Serikali kwa kushirikiana na SIDA, Ubalozi wa Uingereza na Benki ya
Dunia imeweza kutumia kiasi cha Tsh. Bilioni 21 kwa ajili ya upanuzi wa
miundombinu katika Shule 85
za Sekondari za Kidato cha Tano na Sita nchini.
Akifafanua zaidi Simbachawene anasema katika mwaka wa fedha
2016/17, Serikali imetuma kiasi cha Tsh. Bilioni 36.8 katika akaunti za Shule
za Sekondari Kongwe 23 kwa ajili ya ukarabati na Tsh. Bilioni 3.5 zimepelekwa
katika Shule saba (7) za Sekondari za Ufundi kwa ajili ya ukarabati wa
karakana.
Dhana ya Programu ya Lipa kulingana na Matokeo ikieleweka kwa
wadau wote na kufanyiwa kazi kulingana na viashiria vilivyowekwa itasaidia
kuijengea Serikali utamaduni wa kufanya kazi kwa matokeo na kutekeleza malengo
iliyojiwekea kwa wakati.
Aidha Programu hiyo itaisaidia Serikali kufikia azima na kusudio
la kuboresha kiwango cha elimu itakayoleta ushindani na mchango mkubwa katika
maendeleo ya viwanda nchini.
Source:Ismail Ngayonga
MAELEZO
DAR ES SALAAM
27.6.2017
COMMENTS