*Ahimiza nyumba za ibada zisaidie vita ya dawa za kulevya WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amepiga marufuku usafirish...
*Ahimiza nyumba za ibada zisaidie
vita ya dawa za kulevya
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amepiga marufuku usafirishaji wa
chakula kwenda nje ya nchi kuanzia leo.
“Kuanzia leo, ni marufuku kwa mtu yoyote kusafirisha mazao
ya chakula kwenda nje ya nchi bila ya vibali. Serikali inahamasisha
uwekezaji kwenye ujenzi wa viwanda nchini. Kama tutatoa vibali, ni lazima mtu
alazimike kusaga nafaka ili kutoa ajira nchini,” amesema.
Waziri Mkuu ametoa agizo hilo leo (Jumatatu, Juni 26, 2017)
wakati akitoa nasaha kwenye Baraza la Eid lililofanyika kitaifa kwenye msikiti
wa Masjid Riadha, mjini Moshi, mkoani Kilimanjaro mara baada ya kuswali sala ya
Eid.
“Jana nimeona kwenye televisheni taarifa kuhusu malori 10
yaliyokamatwa Tarakea yakiwa na mahindi tayari kuvushwa mpaka. Mheshimiwa RC
akasema chakula hicho ni lazima yarudishwe kwa ajili ya usagaji.”
“Mimi nasema kuanzia leo, yeyote atakayekamatwa akitorosha
chakula kwenda nje ya nchi, chakula hicho kitataifishwa na
kupelekwa ghala la Taifa na gari lake tutalitaifisha na litaishia Jeshi la
Polisi. Tunafanya hayo kwa lengo la kuwalinda Watanzania tusikumbwe na baa la
njaa.”
Akitoa tahadhari kuhusu uuzwaji wa chakula nje ya nchi, Waziri
Mkuu amesema kumekuwa na wimbi kubwa la usafirishaji wa chakula kwenda nje ya
nchi bila kibali. “Hilo ni kosa kubwa kwa sababu litasababisha nchi yetu kupata
baa la njaa huko mbele,” amesema.
Amesema mipaka ya Tarakea, Holili, Mwanga, Horohoro, Siha,
Namanga na Sirari imekuwa inapitisha kiasi kikubwa cha mazao ya chakula kwenda
nje ya nchi jambo ambalo ni hatari sana. “Hii ni kwa sababu chakula cha
ndani hakitoshelezi mahitaji. Kwa sababu nchi zote za jirani hazina chakula cha
kutosha. Tusipokuwa makini, tutabaki tunalia njaa."
Waziri Mkuu ametumia fursa hiyo kuwasihi wafanyabiashara wa ndani,
wachukue mahindi kutoka maeneo yenye mavuno mengi na kuyapeleka kwenye sehemu
zenye mavuno kidogo. “Watanzania tushirikiane, kama ni biashara tutoe huku
kwenye mavuno mengi na tuyapeleke Shinyanga na Geita ambako wanayahitaji au
tukanunue Sumbawanga na kuyapeleka kwenye mikoa mingine yenye upungufu,”
alisisitiza.
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amewataka viongozi
wa dini waisadie Serikali katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya kwa kupitia
kwenye nyumba za ibada. “Naomba tuendelee kushirikiana kupambana na janga hili
la dawa za kulevya kwa ustawi wa nchi yetu. Naamini viongozi wa dini mnayo
nafasi kubwa katika mapambano haya, kwa kuwafunda vijana wetu kuishi katika
maadili ya kidini na kutojiingiza kwenye janga hilo.”
Alisema Serikali kwa upande wake itaendeleza mapambano hayo
bila ajizi wala mzaha. “Tunaomba wananchi wote watuunge mkono kwa kutoa taarifa
sahihi za wanaojihusisha na uzalishaji, utengenezaji, usambazaji na utumiaji wa
dawa za kulevya pindi tu wanapowabaini.”
Wakati huo huo, akitoa tafsiri ya Qur’aan tukufu
kwenye Baraza la Eid, Sheikh wa Mkoa wa Arusha, Sheikh Shaaban Juma alisema
kila nguzo katika Uislamu inapaswa kufuatwa na kwamba mtu akiharibu nguzo moja
tu anakuwa ameharibu nguzo zote tano.
Alisema siku ya kiyama, watatokea watu wenye thawabu kama milima
ya Usambara ama Upareni na akawataka Waislamu wote nchini wadumu katika kutenda
mema ili wapate thawabu.
Mapema, akitoa khutba katika swala ya Eid el Fitr iliyoswaliwa
kwenye msikiti huohuo wa Masjid Riadha, Sheikh Mlewa Shaban alisema sikukuu ya
Eid ni siku ya kujiepusha na madhambi kama ulevi, kamari na lugha chafu, bali
aliwataka waumini wote waitumie siku hiyo kuwapa furaha maskini, yatima na
wajane.
“Mtu asiseme mwezi wa Ramadhan umepita, sasa narudia mambo yangu
ya zamani. Adhabu za Mwenyezi Mungu hazina mipaka na wale waliotulizana
watapata thawabu yao, kumbukeni neema na Mwenyezi Mungu na mcheni Mwenyezi
Mungu.”
“Kitu tunachopaswa kufanya kila wakati ni kumcha Mwenyezi Mungu.
Lazima tupendane, tuondoe tofauti zetu na tuujenge Uislam. Hatuwezi kuujenga
uislam kama hatupendani. Lazima tuilinde ibada yetu kwa sababu hatuna garantii,
ni lini tutaondoka,” alisema.
Sherehe hizo zilihudhuriwa na Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania,
Sheikh Abubakar Zubeir bin Ally; Wajumbe wa Baraza la Ulamaa, Waziri wa
Maliasili na Utalii, Prof. Jumanne Maghembe; Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Mama
Anna Mghwira; IGP Mstaafu, Bw. Said Mwema; Mbunge wa Moshi Mjini, Bw. Jaffary Michael;
Wakuu wa Wilaya za Mkoa huo na viongozi mbalimbali wa dini na Serikali.
(mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI
MKUU,
JUMATATU, JUNI 26, 2017.
COMMENTS