Na Martin Mhando Nasikitika kuwa sitoweza kuwa na ndugu zangu wasanii na wadau katika sanaa na utamaduni katika majadiliano haya muhi...
Na Martin Mhando
Nasikitika kuwa sitoweza kuwa na ndugu zangu wasanii na wadau katika sanaa na utamaduni katika majadiliano haya muhimu kuhusu impact ya bajeti ya serikali kwa sanaa nchini. Haya ni majadiliano ambayo yalikuwa yafanyike miezi sita kabla ya bajeti, ambapo hayakufanyika, na pia wiki moja baada ya bajeti- kama hivi itakavyofanyika Jumanne hii tarehe 23 Juni.
Lakini kukosekana kwangu kusitupe shida maana dunia imebadilika na tusipotumia fursa zilizopo hatutakuwa na haki ya kulalamika. Hivyo hata kwa kutoweza kuwepo kwangu kushiriki kizoom au kigoogle-meeting ni alama ya uzembe wangu na labda uzembe wako wewe mdau wa sanaa mwenzangu pia.
Tuliache hilo ingawa kimsingi tatizo letu linaanzia hapo.
Maana kukosa ubunifu ni tatizo kubwa katika nchi zinazoendelea, na hilo halitokei kwa sababu wananchi hawana huo ubunifu, la hasha. Kama kuna kitu ambacho wanadamu tumepewa kwa magunia na sio kwa kijiko, ni ubunifu. Lakini tunapotaka kuweka miongozo mikalimikali (hiyo ninayoiita miundombinu) ili kuwezesha ubunifu ndipo tunapokosea na kujikuta tunaua ubunifu.
Ubunifu ni uwezo muhimu ambao huwezesha watu au hata taasisi kushughulikia na kusimamia mabadiliko, ambayo kimsingi ndio nia ya mipango. Mara nyingi, ubunifu hujumuisha pia kuona vitu kutoka kwa mtazamo mpya na kuacha fikra za jadi ambazo zinaweza kuwa zimepitwa na wakati.
Ubunifu hauna mpango na wala hausubiri mpango, na saa nyingine huchukia hasa mipangilio. Ubunifu hutaka wenyewe kujitengenezea mpango na kuuendeleza hadi hapo unapoweza kubuni mpango mwingine. Hilo mara kwa mara linakuwa gumu kueleweka ingawa, japo siye sote sio wanafilosofia, mtakubaliana nami kuwa ili kubuni kitu mtu unaanzia pale unapopaweza. Aghalabu unaweza kubuni kitu kizuri zaidi mara unapoweza kujenga uwezo mkubwa zaidi kuliko ule ulionao wakati ule. Haijalishi ni kwa njia gani utapata ule uwezo mkubwa zaidi, lakini huo uwezo unahitajika ili uweze kuvuka pale. Shurti uwezo huo upatikane, na kwa njia yeyote ile. (By all means necessary)
Sasa sisi tunapoangalia wenzetu katika tasnia za sanaa duniani, na tukaona jinsi walivyojijengea taasisi zinazofanyakazi vizuri tunadhani kuwa hizo taasisi ndio misingi ya maendeleo yao. La hasha, misingi ni zile fujo walizokuwa wanafanya na walizotaka kufanya hata ikabidi au wakaweza kujijengea miundombinu ya kujiongoza ili kuwezesha mfumo fulani wa ufanyaji kazi kibunifu, uwepo na ukuwe.
Kwa mfano hiyo Hollywood tunayoisifia ilitokana na majaribio mengi yanayofanana na jinsi Nollywood na Bongo movies walivyojitengenezea miundombinu iliyoweza kujenga taasisi kama kimasiharamasihara vile.
Hapa kwetu Bongo movies ililalia katika vitu vitatu:
Lugha ya Kiswahili- ili kupata soko kubwa (social access)
Kutengeneza kitu kwa bei nafuu ili kupata faida- (production formula)
Kupambana kiharamia katika soko - ili kujenga soko (piracy)
Ukiangalia vyote vitatu vilikuwa vinakwenda pamoja na japo vilikuwa na mapungufu mengi hayo mapungufu hayakuzuia kukua kwa biashara na papo hapo kujenga miundombinu inayokidhi haja za wakati ule.
Sasa sisi kwa kutaka kutengeneza miundombinu kamili tukaanza kwa kuona makosa tu. Hatukuangalia nini kinafanya kazi na kuweza kuisaidia tasnia kutokea ndani. Sisi tulikuja na mipango kamambe ya kusahihisha makosa. Kumbe kusahihisha kukawa ndio kisa na mkasa wa kuua tasnia.
Ni wazi kabisa kuwa kina Steps, GMC na Pilipili walikuja na mifumo yao ya kiajabu na hata ya kutisha. Na wote wakaanza kujenga miundombinu yao ili kujikuza katika soko. Haikuwa rahisi, na walipambana hata baina yao, lakini taratibu waliweza kukua. Shida ikawa mtazamo wetu wa kijamii ulioona kuwa huo ni wizi tu, na haukuona kuwa humo pia mlikuwa na fursa nyingi zaidi. Kwa kweli kuachia mapambano ya ndani kwa ndani katika tasnia kati ya majogoo wale kuliwezesha pia tasnia kukua. Kilichokuwa kinatokea ni kuuweka huru ubunifu.
Je huo ulikuwa mfumo usio waa (perfect)? Hapana, ulikuwa unahitaji kubadilika lakini si kwa kuungalia kutoka kwenye ubaya wake tu, bali pia katoka uzuri wake. Nadhani sisi tulikosea na mpaka sasa tunakosea kwa kuangalia makosa yanayotokea katika taratibu za kibiashara badala ya kuona fursa zilizopo na zinazoendelea kuwepo kwa sababu ya uhuru uliokuwepo. Taasisi zile zilikuwa zinamenyana lakini pia ziliachia wengine kujiunga na kumenyama katika tasnia.
Ninachosema hapa ni kuwa katika tasnia nyingi za utamaduni kitu kinachohitajika kwanza ni kukubali kuwa uhuru wa kufikiri na kufanya makosa ndicho kinachohitajika zaidi kuliko kitu kingine chochote. Unapozuia uhuru huo basi ujuwe chochote kile utachofanya kitapunguza kasi ya kukua kwa tasnia yeyote ya sanaa. Saa nyingine inabidi tufumbe macho kwa kusema mabadiliko fulani ni ya lazima. Kwa mfano Mwalimu Nyerere alipoona mini sketi zimeingia nchini na Waziri wake Rashid Kawawa akasimama na kukamata wasichana mitaani, yeye alisema, “jamani hii ni fasheni tu na kama ni fasheni basi itapita, tusijiudhi”. Ingezewezekana kabisa kuwa tungevuka msimu ule wa minisketi kwa kuwalazimisha wasichana wavae nguo ndefu lakini nina uhakika tusingejua ni kitu gani ambacho tumekikosa kwa kuzuia vile.
Serikali lazima iwe na mtazamo tofauti kwa tasnia za sanaa. Mtuvumilie kwa sababu msingi wa tasnia yetu ni utafouti wa mtazamo na kile kinachoendelea- kwa wakati wowote ule, ili tuweze kuendelea. Ikibidi basi tujenge mifumo ambayo itaruhusu huo uhuru kwa kiwango kikubwa cha kufumbia macho ili tusizuie matokeo makubwa zaidi toka tasnia hii muhimu.
Umuhimu wake unatoka wapi? Unatoka katika kuipa jamii nzima nguvu ya kujikuza haraka zaidi. Kujikuza kwa kuongeza ubunifu katika kila nyanja.
Unajua tunapenda kusahau kuwa, katika miaka ya 1980 wakati serikali ya China ilipoona kuwa haina fedha ya kuzipa taasisi zao za maendeleo ilisema “sisi hatuwapi fedha bali tunawapa nafasi ya kutengeneza fedha kwa njia yeyote ile ili nyie mkuze uchumi ambao utatuletea fedha katika serikali kuu. Miaka mingi baadaye, baada ya serikali ya China kupata fedha, ndipo ilipoaanza kujenga miundombinu ya serikali kuu kusaidia na kuongoza taasisi za sanaa mitaani.
Mimi nasema nini sasa? Naiomba serikali ianze kwa kuingalia sanaa kama chombo wanachokihitaji sana ili kuweza kujikwamua hapa tulipo. Serikali inaweza kutumia fedha nyingi sana kujenga miundombinu ya kuisadia tasnia lakini fedha hiyo ikaishia mikononi mwa maofisa na tusione mabadiliko katika tasnia kwa sababu mtazamo huo haujengi ubunifu. Tutoe nafasi za wasani kujitathmini wenyewe, kwa kufanya makosa na kuigana na kujikosoa zaidi bila kuingiliwa na utaona jinsi tasnia hii itakavyopanuka. Mfano upo. Bongo movies.
Miaka michache huko nyuma tasnia ilikuwa inakua kwa mapana lakini baada ya serikali kuanza kuiingilia, ili kuondoa uharamia, tasnia imezidi kudidimia.
Wako wasanii watakaosema mawazo haya yataturudisha nyuma maana tunataka mirabaha, lakini ukweli utabakia kuwa mirabaha haikuzi ubunifu. Kuwa na fursa nyingi zaidi za kubuni ndiko kutakakotuinua na kuleta na kukuza mirabaha.
Najua kuna wale watakaoona mtazamo huu hauna mpango na hautatupa njia ya kujipima. Hapana. Kwanza kama nilivyoanza kusema, mpango umo ndani ya kutokuwepo mpango. Maana, kukua kwa mtoto wa Binaadamu kungechekwa sana na mtoto wa Twiga maana mtoto wa binaadamu anachukuwa muda mrefu mno kukua na watoto wote wangeliwa na Simba kama wangelizaliwa porini.
Sisi aghalabu tungeweza kuwabeza Twiga kwamba japo watoto wao wanainuka haraka na kuwakimbia Simba lakini risasi wanazopigwa nazo na mitego wanayowekewa na majangili vinazidi kuwanasa kwa uzuri zaidi kuliko hata Simba anavyoweza kuwala.
Tuwe na ujasiri wa kukubali kuwa tasnia ya ubunifu inahitaji uhuru wa kubuni zaidi kuliko mipango.
Siku zote nawaambia wanafunzi wangu kuwa kama tungekuwa na uwezo wa kujua filamu gani itakuwa bora sokoni basi tusingekuwa na filamu nyingi kama hizi zinazotengenezwa na wala tusingekuwa na biashara ya filamu, hata hii yenye tija hafifu. Lakini kule kutokuwa na tija tegemezi ndiko kunakoikuza tasnia hii, na hilo ni jambo jema. Kwa watazamaji au walaji wa filamu duniani kutuamini watengeneza filamu kuwa tutawapa kitu kizuri waendapo kuangalia filamu ndio msingi bora wa mahusiano kati ya tasnia na jamii. Imani.
Mtoto wa Binaadamu hapimwi kwa viwango vya mtoto wa Twiga.
Asalaam Aleykum!
Martin Mhando
Zanzibar
COMMENTS