WAZIRI MKUU AWAAGIZA WAKUU WA MIKOA 12 WASIMAMIE LISHE BORA *Azindua mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa WAZIRI MKUU Kassim Majali...
WAZIRI MKUU AWAAGIZA WAKUU WA MIKOA 12 WASIMAMIE
LISHE BORA
*Azindua mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka Wakuu wa Mikoa 12 wachukue hatua stahiki kutatua tatizo
la udumavu uliozidi wastani wa kitaifa kwenye mikoa yao na kuhimiza lishe bora.
“Mikoa yenye kiwango kikubwa cha udumavu zaidi
ya wastani wa kitaifa ni pamoja na Iringa inayoongoza kwa asilimia 56.9, Njombe
(asilimia 50.4), Rukwa (asilimia 49.8), Geita (asilimia 38.6) Ruvuma (asilimia
35.6), Kagera (asilimia 34.3), Simiyu (asilimia 33.2), Tabora (asilimia 33.1),
Katavi (asilimia 32.2), Manyara (asilimia 32), Songwe (asilimia 31.9) na Mbeya
(asilimia 31.5). Viongozi wa Mikoa hii waitafakari hali hii na kuchukua hatua
stahiki,” amesema.
Ametoa wito huo leo mchana (Jumamosi, Aprili Mosi, 2023) wakati
akizungumza na maelfu ya wakazi wa Mtwara na mikoa ya jirani waliofika
kushuhudia uzinduzi wa mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa uliofanyika kwenye
uwanja wa CCM Nangwanda Sijaona, katika Manispaa ya Mtwara.
“Taarifa zilizopo
zinaonesha hali ya lishe miongoni mwa Watanzania hairidhishi kutokana na
kuathiriwa na tatizo la udumavu kwa watoto wenye umri chini ya miaka mitano,
uzito pungufu, ukondefu na uzito uliozidi pamoja na uliokithiri (kiribatumbo)," amesema.
Kwa upande mwingine, Waziri Mkuu Majaliwa
amesema hali ya uzito uliozidi na uzito uliokithiri (kiribatumbo) ndicho
kiashiria pekee ambacho hakijawahi kupungua na kimeendelea kuongezeka kutoka
asilimia 11.3 mwaka 1991 hadi kufikia asilimia 31.7 mwaka 2018 kwa Tanzania
Bara na kwa Zanzibar uzito uliozidi umefikia asilimia 41.8 katika kipindi
hichohicho.
Amesema tatizo la uzito uliozidi na kiribatumbo
ni kubwa katika mikoa ya Kilimanjaro ambako wana asilimia 49, Dar es Salaam
(asilimia 48.6), Mjini Magharibi (asilimia 47.4) na Kusini Unguja (asilimia
39.4). “Hali hii inaelekea kuwa janga la kitaifa na kisababishi kikubwa cha
kuongezeka baadhi ya magonjwa yasiyo ya kuambukiza kama kisukari, saratani na
magonjwa ya moyo.”
“Wananchi wenzangu, sasa ni wakati muafaka wa
kubadili mitindo ya maisha yetu kwa kufanya mazoezi angalau nusu saa kila siku
na kula mlo kamili sambamba na kuepuka vyakula vyenye mafuta mengi, sukari
nyingi, pombe na sigara,” amesisitiza.
Mwenge wa Uhuru utakimbizwa kwenye mikoa yote 31 na Halmashauri 195 kwa
siku 196. Waziri Mkuu aliuwasha mwenge huo saa 6.06 mchana na saa 6.07
akamkabidhi Kiongozi wa mbio hizo kitaifa, Bw. Abdallah Shaib Kaim (anayetoka
Kaskazini Pemba). Saa 6.08, Bw. Shaib alikiri kuupokea mwenge huo na kuahidi
kuwa ataukabidhi kwa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ifikapo Oktoba 14,
mwaka huu ukiwa salama.
Wakimbiza mwenge wengine na mikoa wanayotoka ni Bw. Martin Michael Mkanga
(Mtwara), Bi. Atupokile Elia Mhalile (Dodoma), Bi. Zainab Hemed Mbetu (Kusini
Unguja), Bw. Emmanuel Jackson Hondi (Manyara) na Bw. Juma Silima Sheha
(Kaskazini Unguja).
Kaulimbiu ya mwaka huu imelenga maeneo makuu sita yakiwemo ya
kukabiliana na uharibifu wa mazingira,
mapambano dhidi ya rushwa, UKIMWI, dawa za kulevya, malaria na lishe bora.
Ujumbe maalum wa mbio hizo ni: “Umuhimu wa kuhifadhi mazingira na utunzaji wa
vyanzo vya maji kwa ustawi wa
viumbe hai na uchumi wa Taifa.”
Wakati huohuo, Waziri Mkuu amesema dhamira ya
Serikali ya awamu ya sita ni kuboresha huduma za kijamii na maisha ya
Watanzania katika sekta za elimu, afya, maji na barabara. Hatua hizo,
zinakwenda sambamba na uwekezaji mkubwa katika usafiri na usafirishaji nishati
ya umeme, kilimo cha uhakika na viwanda.
“Hata hivyo, nyote mtakubaliana nami kwamba ufanisi wa huduma hizi kwa
kiasi kikubwa unaathiriwa sana na mabadiliko ya tabianchi na uharibifu wa
mazingira ambao kwa takribani asilimia 95 ni matokeo ya shughuli za
kibinadamu.”
Amesema Tanzania ni moja ya nchi zinazoathiriwa na changamoto za
uharibifu wa mazingira unaosababisha mabadiliko ya tabianchi kupitia shughuli
zisizo endelevu za kibinadamu zikiwemo uvamizi wa maeneo tengefu, vyanzo vya
maji na matumizi holela ya mbolea zenye kemikali na viuatilifu; ufugaji wa
kuhamahama unaojumuisha makundi makubwa ya mifugo na ukataji holela wa miti kwa
ajili ya kuni.
Shughuli nyingine ni uchomaji wa mkaa na upanuzi wa mashamba na makazi;
uchomaji moto ovyo wa misitu na mbuga, uchimbaji wa madini usio endelevu na uvuvi
haramu, uvunaji haramu wa mikoko na kuenea kwa viumbe vamizi.
Mbio za mwenge wa uhuru ziliasisiwa mwaka 1961 na Baba wa Taifa, Hayati
Julius K. Nyerere ikiwa ni ishara ya kuwepo kwa Taifa huru la Tanganyika. Na umekuwa ukikimbizwa katika mikoa yote ili kuhamasisha amani,
uzalendo, umoja na mshikamano.
(mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMAPILI, APRILI MOSI, 2023.
COMMENTS