*Waziri Mkuu amtaka Sheikh Kishki akaonane na Waziri wa Ardhi atoe maamuzi ya kiwanja KIJANA wa Kitanzania, Shujaa Suleim...
*Waziri Mkuu amtaka Sheikh Kishki
akaonane na Waziri wa Ardhi atoe maamuzi ya kiwanja
KIJANA wa Kitanzania, Shujaa
Suleiman Shujaa ameibuka kidedea na kitita cha sh. milioni 15 katika mashindano
ya 19 ya Afrika ya kuhifadhi Quran kwenye kundi la washiriki wa juzuu 30.
Shujaa mwenye miaka 23 ambaye ni
mkazi wa Morogoro, amejishindia pia laptop, kiwanja chenye hati eneo la
Kigamboni kilichotolewa na kampuni ya Property International ya jijini Dar es
Salaam pamoja na dola za Marekani 500 kutoka kwa Bw. Ahmed Seif “Magari”
aliyetoa dola 500 kwa washindi wote watano.
Akizungumza na maelfu ya waumini na
Watanzania waliofurika kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam leo mchana
(Jumapili, Mei 27, 2018), Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amewataka Watanzania
waendelee kuilinda amani iliyopo nchini kwani ikipotea hakuna atakayeweza
kufanya ibada.
“Mtakubaliana nami kuwa amani ya
nchi yetu, ndiyo inatufanya tutembee vifua mbele dhidi ya wenzetu, ni neema
kubwa ambayo kila muumini anapaswa kuilinda kwani ikipotea hata mkusanyiko wetu
huu wa leo si rahisi kufanyika mahali kama hapa,” amesema.
“Leo hii tuko hapa uwanjani kwa
sababu tuna amani, kama Serikali isingekuwa inashirikisha Watanzania wote
kulinda amani, basi tusingeweza kukutanika hapa. Kuna nchi 18 ziko hapa, na
watu wake wamekuja hapa uwanjani kwa kuwa wana uhakika na amani tuliyonayo sisi
Watanzania,” alisema.
Alisema katika nchi ambazo amani
imetoweka, watu wanalazimika kufanya shughuli za ibada majumbani au kwa
kujificha. “Wenzetu hao, hawapati fursa adhimu kama hii ya kujumuika pamoja na
majirani, ndugu, jamaa na marafiki kusikiliza na kufurahia kisomo cha Quran au
kufanya shughuli nyingine za kiuchumi na kijamii,” aliongeza.
Aliwataka Watanzania waendelee
kubeza na kupuuza kauli za walio wachache ambao kwao kuzungumzia amani ni
kujipendekeza kwa Serikali. “Watu hao wamesahau kwamba tofauti katika Uislamu
hazikuanza leo, lakini tofauti hizo hazikuwa sababu ya wema waliotangulia
kuacha kuheshimiana na kushirikiana,” alisisitiza.
Mshindi wa pili kwenye kundi hilo la
juzuu 30 ni Ahmed Noor wa Sudan ambaye ameshinda sh. 12,564,750 pamoja na
laptop akifuatiwa na Muzamil Awadh Mohamed wa Sudan alijishindia sh. milion 7.5
pamoja na laptop zilizotolewa na kampuni ya Camara Education.
Mshindi wa nne ni Abdulally A.
Mohammed wa Kenya aliyepata zawadi ya sh. 5,711,000 na wa tano ni Ibrahim
Maazur kutoka Niger, aliyepata sh. 3,426,000. Washindi hao wote watano walipewa
zawadi ya kwenda hijja na Waziri wa Mambo ya Dini wa Saudi Arabia, Dk. Saleh
Ally Sheikh.
Washiriki wengine kwenye kundi la
juzuu 30 walitoka nchi za Rwanda, Burundi, Msumbiji Djibouti, Kenya, Ethiopia,
Congo DRC, Nigeria, Ghana na Afrika Kusini.
Washiriki wengine waliopewa zawadi
ni wale walioweza kuhifadhi Juzuu tatu (washindi watatu), Juzuu tano (washindi
watatu); Juzuu 10 (washindi watatu) na Juzuu 20 (washindi watatu).
Viongozi wengine waliohudhuria
mashindano hayo ni Makamu wa Rais Mstaafu wa awamu ya nne, Dk. Mohammed Gharib
Billal, Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana na mabalozi wanaoziwakilisha
nchi zao hapa Tanzania kutoka Saudi Arabia, Comoro, Oman, Uturuki, Kenya,
Msumbiji na Nigeria, Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Sheikh Abubakar Zubeir
bin Ally na Rais wa taasisi ya Al-Hikma, Sheikh Sharif Abdilkadir Al-Ahdal.
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu
amemtaka Sheikh Nurdin Mohammed Ahmad (maarufu kama Sheikh Kishki) akaonane na
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Bw. William Lukuvi ili atoe
maamuzi ya kiwanja chao kilichopo eneo la Matumbi ambacho mwaka jana aliagiza
kifuatiliwe taratibu zake na kisha wapatiwe.
“Kuhusiana na suala la kiwanja
mlichosema, mamlaka ya awali ni Manispaa ya Temeke na ilishakamilisha taratibu
zote za kisheria, ikapeleka kwa Afisa Ardhi wa Mkoa kuona kama limepita kwenye
vikao vyote ndipo wanaenda wizarani kupata kibali. Hakuna sababu ya wizara
kuikatalia manispaa huku eneo lenyewe likiwa kwenye ramani kuu ya manispaa
yenyewe, nenda mumuone Waziri mwenye dhamana, awape ardhi,” alisema.
Waziri Mkuu amefikia hatua hiyo baada
ya kupewa taarifa akiwa jukwaani kwamba taasisi ya Al-Hikma iliwasiliana na
Manispaa ya Temeke, hadi mkoani wakapewa barua zinaonyesha eneo liko sawa
lakini walipofika wizarani wamekwamishwa na Afisa mmoja aliyemtaja kwa jina
moja la Mama Mpetula.
Juni 11, mwaka jana katika
mashindanio ya 18, taasisi ya Al-Hikma waliomba wapatiwe kiwanja na.118 kwenye
kitalu E kilichoshikamana na kiwanja na. 117 chenye shule yao ya Al-Hikma Girls
iliyoko Temeke ili waweze kujenga zahanati.
(mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMAPILI, MEI 27, 2018.
COMMENTS