KWA mara ya kwanza katika historia ya kuanzishwa kwake miaka 25 iliyopita, Tamasha la Kimataifa la Filamu la Zanzibar (ZIFF) limepata mawasi...
KWA mara ya kwanza katika historia ya kuanzishwa kwake miaka 25 iliyopita, Tamasha la Kimataifa la Filamu la Zanzibar (ZIFF) limepata mawasilisho 3,498 ya filamu kwa ajili ya tamasha litakalofanyika Juni mwaka huu.
ZIFF ambayo ilibuniwa kwa malengo kadhaa lakini likiwa na mtazamo wa muda mrefu ulikuwa ni kuanzisha tamasha la filamu litakalodumu, la kuaminika na muhimu katika ulimwengu wa sinema, sanaa na utamaduni , mawakilisho ya mwaka huu yametia fora.
Hiyo inatokana na ukweli kuwa katika miaka 25, urithi wa ZIFF umekuwa kielelezo chema kwa watu binafsi, mashirika, taifa na ulimwengu wa filamu na sanaa.
Aidha kama shirika lisilo la kiserikali ZIFF linalenga kuongeza uwezo wa ubunifu na mapato ya wanajumuia wa tasnia ya ubunifu kupitia kuboresha mifumo ya soko na ubora wa huduma za kiufundi na miundombinu.
Kuanzia mwaka wa 1998 lengo lake ni kuchangia ukuaji wa kijamii na kitamaduni na wa kikanda na tamaduni za kimataifa za uvumilivu. Hii inafanywa kwa kutoa nafasi kwaa matukio ambayo filamu, muziki, maonyesho na aina nyingine za sanaa hushirikishwa katika kukuza, kuendeleza, kufanya maonyesho, kuchunguza, na kuutambulisha utamaduni wa kikanda.
Ikiwa inakwenda na mabadiliko ya kiteknolojia na sayansi kwa kuwa na matumizi makubwa ya tehama, njia mpya ya mawasilisho ya filamu katika ushiriki wa tamasha kwa kutumia majukwaa ya mtandaoni ya Filmfreeway na Festhome yanayomilikiwa na tamasha hilo, yameleta maingizo hayo.
Mkurugenzi wa Tamasha, Profesa Martin Mhando anasema kutokana na uwingi wa filamu walilazimika kualika idadi kubwa ya wateuzi wa awali wapatao 40 klusaidia kazi za uchambuzi kupata zinazoweza kushiriki katika mashindano zipatazo 85.
Kwa kutumia Jukwaa la Filmfreeway wamepokea filamu fupi 2124, filamu za makala 415 na filamu za dokumentari 766 na filamu za wanafunzi 424.
Aidha alisema taifa lililoongoza kwa kupeleka mawasilisho mengi ni Iran iliyoingiza filamu 668 ikifuatiwa na India filamu 268 na Ufaransa 160.
Nchi zingine zilizowasilisha filamu ni Brazil (160), Marekani (155),Italia (115), Hispania (112),Tanzania (77),Ujerumani (76),Uganda (71),Kenya (54),Uingereza (53), Mexico (53),China (46), Nigeria (46), Rwanda (38), Afrika Kusini (35),Korea (34), Ukraine (23), Ghana (17),Ubelgiji (16),Tunisia (16), Iraq (15),Congo(15), Uswis (13),Lebanon (13),Senegal (10),Zambia (7),Pakistan( 5)Nepal (5) Sudan (4) Ethiopia (4) na Japan (4).
Kwa maingizo ya mwaka huu inadhirisha kuwa kulikuwa na maana kubwa kuanzishwa kwa shirika hili miaka 25 iliyopita, wakati tasnia ya sinema ilipotetereka.
“ ZIFF ilizaliwa kwa ahadi ya kuzaliwa upya kwa tasnia hio, ambayo tunajivunia. Kusema kweli Afrika Mashariki ina tasnia ya filamu iliyochangamka, inayochochewa na lugha ya Kiswahili” anasema Profesa Mhando.
ZIFF likiwa ni tamasha la kitamaduni linaloipa Tanzania na Afrika Mashariki muda wa kuisanifu tasnia ya filamu kwa kupitia mitazamo kadhaa, mwaka huu imeingiza sinema 14 za Kitanzania katika mashindano pamoja na usaili wa sinema 77.
Profesa Mhando katika mazungumzo amezitaja filamu hizo za kitanzania kuwa ni Janga ya Ben Royal, Mvamizi ya Phillipo Ngonyani, Mpiganaji ya Daniel Manege,Mgeni ya Juma Saada,Obambo ya Fred Feruzi, Vuta N'Kuvute ya Amil Shivji, Uncle ya Hatibu Madudu na Nuru ya Maisha iliyotengenezwa na Juma Saada.
Pia kuna filamu fupi za Binti Jasiri ya Juma Saada, Binti Maringo ya Mohamed Hamis, Kazija ya Mohamed Suleiman (Muddy Sule, Black live Matter, Chumba 61 ya Edwin Kazoka na Urithi wa Mila ya Mohamed Suleiman (Muddy Sule).
Anasema kutokana na mabadiliko makubwa yaliyofanyika katika sinema za Kitanzania anatarajia zitatoa ushindani wa kimataifa hasa ukizingatia moja ya filamu ilishafanyiwa uzinduzi wa kimataifa mjini Toronto Canada
Filamu hiyo Vutan ikuvute ndiyo itafungua pazia la ZIFF miaka 25 pale Ngome Kongwe mjini Unguja.
Pamoja na kuonesha filamu tamasha la Mwaka huu pia litajumuisha warsha kuu 6 zitakazotolewa na wakufunzi wanaotambulika zikiangazia jukumu la tamasha kwa taaluma ya filamu barani Afrika.
Profesa Mhando anazitaja warsha hizo kuwa ni pamoja na: On Documentary (Docubox- Kenya); uandishi wa vipindi vya TV (Pilipili Entertainment, Tanzania); Wanawake na Filamu (EU); Maabara ya filamu fupi (Kenya/Wales); Utengenezaji filamu wa majaribio (Hispania na Ajabu-Ajabu); Uhariri wa filamu (Off-courts-Ufaransa).
Warsha nyingine ni ya Wanawake na Filamu ambayo itawasilisha maoni ya waongozaji wa filamu wanawake jinsi wanavyoendeleza wahusika wao wanawake, na vile vile wanavyotamani watazamaji wawatambue.
Pia kutakuwa na mipango kadhaa ya kikanda ya filamu itayozinduliwa wakati wa ZIFF ikiwa ni pamoja na kikao cha kwanza cha The East Africa Screen Collective (EASC), ambao ni muungano wa makampuni na mashirika yanayotetea uhuru wa simulizi katika sekta ya sanaa katika Afrika Mashariki.
Kama kawaida, tamasha litawasilisha programu zake ikiwa ni pamoja na Panorama za Wanawake, Watoto na Vijiji ambapo kunaangaziwa filamu na shughuli zinazozunguka vikundi vitatu vya jamii.
Kazi hiyo inafanywa kwa kuungwa mkono na Umoja wa Ulaya (EU) na mwaka huu kutafanya shughuli za filamu na utamaduni Pemba baada ya kushindwa kufanya hivyo mwaka jana. Kutakuwa na maonyesho ya filamu juu ya mada ya wanawake na ujasiriamali, na vikundi vya uzalishaji vya wanawake vitafadhiliwa kuzalisha sanaa za mwonekano wa ZIFF na bidhaa nyinginezo.
Jambo kuu la tamasha hili mwaka huu ni utayarishaji wa Kitabu cha ZIFF@25. Kwa msaada wa EU na GIZ (Deutsche Gesellschaft für Internationale Zusammenarbeit).
“Tutachapisha kitabu cha ukumbusho katika safari ya kusherehekea historia ya miaka 25 ya ZIFF na kuweka kumbukumbu ya uungaji mkono wa wafadhili wetu kwa hafla hii muhimu ya kitamaduni nchini Tanzania.
Pamoja na kuwapo kwa mambo mengi yanayogusa filamu na uandazi wake mwaka huu kunaanzisha jukwaa la kudumu la ZIFF kwenye YouTube kwa filamu zilizopata kuoneshwa katika tamasha hilo. Mrejeo huo utajumuisha filamu ambazo zimeshinda au kuvutia katika ZIFF.
“Tunakusudia jukwaa letu la Youtube liwe kituo cha kuangalizia na cha majadiliano ya ambapo watengenezaji filamu wanaweza kufikia hadhira muhimu na kufanya mazungumzo nao,” anasema Profesa Mhando.
Kwa miaka 25 ZIFF imejitambulisha kama miongoni mwa matamasha matatu bora ya filamu barani na kwa kujiamini Profesa Martin anasema: “ZIFF sio tu imedumu pale ambapo wengine wameshindwa bali pia imejitengenezea misingi imara wa kuendelea. Udhaifu wowote ambao ZIFF inaweza kuonyesha, tutabaki kujivunia hivyo, ndio maana tunasema Lake Mtu Halimtapishi! Kama ilivyo katika bango litalaotumika mwaka huu kuwasilisha msimu wa 25 wa maonesho ya ZIFF.
mwisho
COMMENTS