Mwanahabari Simon Mkina wa Pambazuko Online ameibuka mshindi bora wa jumla katika Tuzo za 16 za Umahiri wa Uandishi wa Habari Tanzania (EJAT...
Mwanahabari Simon Mkina wa Pambazuko Online ameibuka mshindi bora wa jumla katika Tuzo za 16 za Umahiri wa Uandishi wa Habari Tanzania (EJAT) mwaka 2025 zilizofanyika jijini Dar es Salaam na kukabidhiwa hundi ya shilingi milioni tatu na mgeni rasmi, Rais wa Mahakama ya Afrika Mashariki, Jaji Nestor Kayobera.
Mkina aling’ara vilivyo katika usiku huo wa tuzo zinazoandaliwa na Baraza la Habari Tanzania (MCT) kwa kunyakua pia Tuzo ya Habari Bora ya Afya pamoja na Tuzo ya Uandishi Bora wa Habari za Uchunguzi.
Gazeti la Jamhuri nalo lilionyesha ubabe wake kwa kutwaa Tuzo ya Mahojiano Bora ya Mwaka kupitia mahojiano mahiri yaliyofanywa na Mhariri wake, Manyerere Jacton, na Waziri Mkuu mstaafu Jaji Joseph Warioba, huku gazeti hilo likiongeza tuzo nyingine mikononi mwao ambayo ni Tuzo ya Uhifadhi ya Mwalimu Julius Nyerere.
Orodha ya washindi wa umahiri wa uandishi iliendelea kutawaliwa na weledi mkubwa ambapo Julius Maricha wa Gazeti la Mwananchi alishinda Tuzo ya Afya ya Uzazi, huku Philip Mwihava wa Clouds FM akitwaa Tuzo ya Habari Bora ya Elimu na kumwacha Leonard Mubale wa Trigen Media katika nafasi ya pili. Tuzo ya Habari Bora ya Siasa ilienda kwa Antony Rwekaza wa Watetezi TV, nayo Tuzo ya Michezo ikanyakuliwa na Mackriner Siyovelwa wa Crown Media.
Ushindani uliendelea kuwa mkali katika vipengele vingine ambapo Devotha Kihwelo wa gazeti la Mwananchi alitunukiwa Tuzo ya Utawala Bora, huku Joseph Kirati wa The Chanzo akiondoka na Tuzo ya Picha Bora ya Habari. Mwanahabari Abel Kilumbu wa EATV alifanya kweli kwa kutwaa Tuzo ya Habari Bora ya Video, Sauti, Maandishi na Picha, huku Daniel Samson wa Nukta Afrika akijitwalia Tuzo ya Maudhui Bora ya Mtandao.
Katika tuzo maalum za umahiri wa kipekee, Manyerere Jacton alitangazwa kuwa Mhariri Bora wa Mwaka, Sanula Athanas wa gazeti la Nipashe akatwaa Tuzo ya Mwanahabari Mbobevu na Mchambuzi Mahiri, Esau Ng’umbi wa Nukta Afrika akatawazwa kuwa Mwanahabari Mchanga Bora wa Mwaka, na Neema Abel wa The Guardian akaibuka kidedea kama Mwanahabari Bora Mwanamke wa Mwaka.
Katika upande wa taasisi, Kampuni ya Magazeti ya Serikali (TSN) iliibuka kidedea kwa kushinda Tuzo ya Chombo Bora cha Habari cha Serikali Kinachotii Sheria zaidi, ushindi ambao Mkurugenzi Mtendaji wa TSN, Asha Dachi, amebainisha kuwa ni uthibitisho thabiti wa namna taasisi hiyo inavyosimamia viwango vya taaluma, maadili, na weledi tangu kuanzishwa kwake.
Dachi alipongeza juhudi za wahariri na timu nzima ya wanahabari akieleza kuwa msingi wa mafanikio ya TSN unaanzia kwenye mchakato thabiti wa ajira na mafunzo ya kitaaluma yanayowajenga watumishi kufanya kazi kwa kuzingatia sera na utumishi wa umma.
Ushindi wa TSN ulienda sambamba na mafanikio ya Mhariri Msaidizi wa gazeti la HabariLEO, Halima Mlacha, aliyetwaa Tuzo ya Uandishi Bora wa Habari za Afya ya Uzazi iliyodhaminiwa na MSI Tanzania, hatua ambayo Dachi aliiitaja kama chachu kwa waandishi wa Daily News, HabariLEO, na majukwaa ya kidijiti ya TSN kuendelea kuzalisha kazi za uchunguzi zenye ubora na athari chanya kwa jamii.
Kwenye kundi la vyombo binafsi, kampuni ya Azam Media ilijizolea sifa kwa kushinda Tuzo ya Chombo Bora cha Habari Binafsi Kinachotii Sheria huku Nukta Afrika ikishika nafasi ya pili, ingawa Nukta Afrika haikuondoka patupu kwani ilinyakua Tuzo ya Uandishi Bora wa Habari za Ugonjwa wa Sikoseli.
Kilele cha hafla hiyo kilipambwa na uzinduzi wa kumbukumbu ya miaka 30 tangu kuanzishwa kwa MCT, ambapo baraza hilo lilitambua mchango wa viongozi 10 walioacha alama katika maendeleo yake akiwemo Jaji Joseph Warioba, Profesa Issa Shivji, Geoffrey Mmari, Anthony Ngaiza, na Kajubi Mukajanga. Aidha, Dk Samwilu Mwaffisi alitunukiwa Tuzo ya Heshima ya Mafanikio ya Maisha katika Uandishi wa Habari kama ishara ya kuthamini mchango wake wa kudumu na wa kihistoria katika kuijenga na kuisitawisha tasnia ya habari nchini Tanzania.
MAJINA KAMILI WASHINDI WA EJAT HAYA HAPA
1. Dkt. Maurice Samwilu Mwaffisi - Tuzo ya Mafanikio ya Maisha katika Uandishi wa Habari (LAJA) 2025.
2. Simon Martha Mkina - Pambazuko Online, Mwanahabari Bora wa Mwaka 2025.
3. Simon Martha Mkina - Pambazuko Online, Tuzo ya Habari Bora ya Afya 2025 (Best Health Reporting 2025)
1. Sanula Athanas – Nipashe, Tuzo ya Habari Bora ya Elimu 2025 (Best Education Reporting 2025)
2. Anthony Rwekaza – Watetezi Online TV, Tuzo ya Habari Bora ya Siasa 2025 (Best Political Reporting 2025)
3. Mackriner Siyovelwa – Crown Media,Tuzo ya Habari Bora ya Michezo 2025 (Best Sports Reporting 2025)
4. Devotha Kihwelo - Mwananchi ,Tuzo ya Habari Bora ya Utawala Bora 2025 (Best Good Governance Reporting 2025)
5. Joseph Kirati – The Chanzo, Tuzo ya Picha Bora ya Habari 2025 (Best Photojournalist 2025)
6. Abel Kilumbu – EATV, Tuzo ya Habari Bora ya video, sauti, maandishi na picha (Best Multimedia Reporting 2025)
7. Isack Lukumay - Orkonerei FM, Tuzo ya Maudhui Bora ya Habari za Vijijini 2025 (Best Rural Reporting 2025)
8. Abdallah Kurwa – ITV, Tuzo ya Maudhui Bora ya Televisheni 2025 (Best Television Content 2025)
9. Daniel Samson – Nukta Africa, Tuzo ya Maudhui Bora ya Mtandaoni 2025 (Best Online Content 2025)
10. Esau Ng’umbi – Nukta Africa, Tuzo ya Ufanisi 2025: Mwanahabari Mchanga Bora wa Mwaka (Recognition Award 2025: The Best Youngest Journalist of the Year)
11. Neema Abel – The Guardin, Tuzo ya Ufanisi 2025: Mwanahabari Bora Mwanamke wa Mwaka (Recognition Award 2025: Best Woman Journalist of the Year)
12. Manyerere Jackton – Jamhuri Media, Tuzo ya Ufanisi 2025: Mhariri Bora wa Mwaka (Recognition Award 2025: Outstanding Editor of the Year 2025)
13. Sanula Athanas – Nipashe, Tuzo ya Mwanahabari Mbobevu na Mchambuzi Mahiri 2025 (Most Specialized Journalist of the Year 2025)
14. Simon Martha Mkina - Pambazuko Online, Tuzo ya Uandishi Bora wa Uchunguzi wa Mwaka 2025 (Best Investigative Reporting 2025)
TUZO VYOMBO VYA HABARI
1. Azam Media Ltd - Tuzo ya Chombo cha Habari Binafsi Kinachotii Sheria Zaidi 2025 (Recognition Award 2025: The Most Compliant Private Media House of the Year)
2. Tanzania Standard Newspaper (TSN) - Tuzo ya Chombo cha Habari cha Serikali Kinachotii Sheria Zaidi 2025 (Recognition Award 2025: The Most Compliant Private Media House of the Year)
3. Jamhuri Newspaper - Tuzo ya Mahojiano Bora ya Gazeti 2025 (The Best Print Interview of the Year)
4. Nukta Africa - Tuzo ya Ubobevu na Umahiri wa Uandishi wa Habari za Ugonjwa wa Sikoseli 2025 (The Best Specialized Media House of the Year on Sickle cell reporting)
TUZO ZA WASHIRIKA (NCAA, MSI Tanzania na UWEZO Tanzania)
1. Jamhuri Newspaper - Tuzo ya Uhifadhi ya Julius Nyerere 2025 (Recognition Award 2025: Mwalimu Julius Nyerere Conservation Award).
2. Julius Maricha – The Citizen, Tuzo ya Afya ya Uzazi ya MSI Tanzania (The MSI Tanzania Reproductive Health Reporting Award 2025).
3. Hamad Rashid -The royal Media, Tuzo ya Elimu ya Uwezo Tanzania (The Uwezo Tanzania Education Reporting Award 2025)
TUZO ZA MAADHIMISHO YA MIAKA 30, YA BARAZA LA HABARI TANZANIA (MCT).
Waliopata tuzo hii ni -;
1. Mhe.Jaji Joseph Sinde Warioba
2. Prof. Geoffrey Mmari
3. Prof. Issa G. Shivji
4. Hayati Mhe. Jaji Mstaafu Robert Kisanga
5. Mhe. Jaji Thomas Mihayo
6. Hayati Mhe. Jaji Mstaafu Juxon Isaac Mlay
7. Mhe. Jaji Mstaafu Agusta Bubeshi
8. Ndg. Anthony Ngaiza
9. Ndg. Kajubi Mukajanga


COMMENTS