MSAFARA WA WAZIRI MKUU WAZUIWA KWA MABANGO NEWALA
· Wananchi wakaa njiani, akubali kushuka na kuwasikiliza
· Wamzomea mbunge wao, wakataa kumsikiliza
MSAFARA wa Waziri Mkuu Mizengo Pinda jana ulilazimika kusimama njiani baada ya wakazi wa kijiji cha Mkunya wilayani Newala, Mtwara kuziba njia wakiwa na mabango huku bango kubwa likimwomba asimame na kuwasikiliza japo kwa dakika 10.
Baadhi ya mabango hayo yalisomeka: “Waziri Mkuu tunakuomba usimame japo dk.10 usikilize kilio chetu”; “Maji ni mradi wa wakubwa”; “walinda chanzo cha maji hawana maji”; “Mfumo wa Stakabadhi Ghalani haufai”; “Korosho kwa mkopo ni ufisadi pia”; na “Malipo ya pili 2005 wakulima wa korosho bado hatujalipwa.”
Tukio hilo lilitokea jana mchana (Jumamosi, Novemba 21, 2009) wakati akielekea kwenye bonde la mto Ruvuma kukagua kituo cha maji cha Mkunya na kupokea taarifa ya kilimo cha umwagiliaji kwenye bonde la mto Ruvuma ambako pia alikabidhi powertillers mbili kwa vikundi vya Mpilipili na KIWOPA kutoka kata ya Kitangari wilayani humo.
Mara baada ya kukuta njia imefungwa, Waziri Mkuu aliteremka garini na wakazi hao walipoomba wamkabidhi risala yao, ili awasikilize kwa dadika chache, yeye aliwaruhusu waisome.
Katika risala yao, wakazi hao walisema wana kero za maji za kutopata maji safi na salama, kutolipwa malipo ya korosho na kutopatiwa pembejeo za ruzuku lakini uongozi wa wilaya umekuwa ukiwapuuza na kuficha taarifa badala ya kuwasaidia.
“Sisi tunaishi kwenye vijiji vya mwanzo kutoka katika chanzo cha maji lakini yanatupita na kwenda kuwafaidisha wengine... zamani tulikuwa tukipata lakini sasa umegeuzwa kuwa mradi mkubwa kwa mhandisi na vigogo wengine...” ilisema sehemu ya risala yao.
Walisema kwamba tatizo la uhaba wa maji katika eneo lao limedumu kwa zaidi ya miaka 15 jambo ambalo linawafanya watumie muda mwingi kusaka maji badala ya kuutumia muda huo kwenye kilimo.
Walisema kuna watu wachache wanaopelekewa maji na kujaziwa katika visima vyao ili wayauze kwa wananchi wengine kwa sh. 500/- kwa kila ndoo na baadhi ya watu wanajaziwa maboza na kupita mitaani wakiyauza maji hayo kwa sh. 500/- hadi 700/- kwa ndoo moja.
Wakizungumzia kuhusu mfumo wa stakabadhi za mazao ghalani, wakazi hao walisema hawautaki mfumo huo kwa sababu hawalipwi hela yote ya sh. 700/- kwa kila kilo kama walivyoahidiwa. “Tuliambiwa bei ya dira ni sh. 700/- kwa kilo kwa mikupuo ya sh. 490/- na sh. 210/- lakini hailipwi yote... tuliambiwa tutahusishwa wakati wa mauzo ya mnada, tunaomba bei ya dira itangazwe upya na wananchi washirikishwe kwenye minada ili wajue kinachoendelea.”
Pia waliiomba Serikali iwasaidie kuwapatia pembejeo na mbolea za ruzuku kwani bei ni kubwa na wengi wanashindwa kuzimudu.
Akijibu hoja zao, Waziri Mkuu alisema kupitia risala yao amebaini kuwa tatizo kubwa linalowakabili ni ukosefu wa maji katika vijiji 12 wakati bomba la maji kutoka chanzo cha maji hadi Newala mjini linapita hapo. Chanzo cha maji cha Mkunya kipo urefu wa mita 800 kwenda chini kutoka safu za milima ya (plateau) Makonde ambako wakazi hao wanaishi.
Aliwaahidi wakazi hao kwamba kabla hajaondoka tarehe 24 atakuwa amepata ufumbuzi wa tatizo hilo. “Hata kama maji hayatoshi itabidi kuwe na mgao walau mara mbili au tatu kwa wiki ili wa huku chini mpate na wa mjini nao wapate, ” alisema huku akishangiliwa na wakazi hao.
Alisema ili kukabiliana na tatizo la watu kuuza maji kwenye maboza au visima vyao binafsi, mhadisi mkazi atapaswa aweke ratiba ya kugawa maji na kuyasambaza kwenye viula vya maji (public water points) ili watu wote wapate.
Akizungumzia kuhusu mfumo wa stakabadhi za mazao ghalani, Waziri Mkuu alisema mfumo huo hauna tatizo ila una mapungufu ambayo itabidi yaangaliwe upya na kumtaka Mkuu wa Mkoa huo. Kanali (mst) Anatoli Tarimo kujipanga upya na kusambaza elimu ya mfumo huo kwa wakulima wa mkoa huo.
Kuhusu pembejeo za ruzuku, Waziri Mkuu ambaye jana alikuwa katika siku ya tatu ya ziara yake mkoani Mtwara, alisema atahakikisha anafuatilia suala hilo ili katika mwaka wa fedha ujao mikoa ya Lindi na Mtwara iingizwe katika programu hiyo. “Mikoa hii miwili haikuwemo kwenye orodha kwa sababu tulijua ninyi ni wakulima wa korosho tu... nimegundua mnalima mazao mengi tu yanayohitaji mbegu bora na mbolea kama vile ufuta, karanga, mpunga na mahindi.”
Katika hali isiyo ya kawaida, Waziri Mkuu alipomwita Mbunge wa jimbo hilo ambaye pia ni Waziri wa Habari na Utamaduni, Bw. George Mkuchika ili awasalimie, wakazi hao walimzomea na kusambaa huku wakisema hatumtaki! Mkutano huo ulilazimika kuisha na Waziri Mkuu kuendelea na safari hadi kwenye chanzo cha maji.
Leo Waziri Mkuu anaendelea na ziara yake ya siku sita katika mkoa wa Mtwara kwa kutembelea wilaya ya Tandahimba ambako ataweka jiwe la msingi kwenye ghala la mazao katika kijiji cha Mahuta na bwawa la malamba katika kijiji cha Malamba kabla ya kufungua jengo la OPD katika hospitali ya wilaya hiyo. Mchana atafungua tawi la benki ya NMB wilayani hapo na kuweka jiwe la msingi kwenye kiwanda cha kubangua korosho kabla ya kufanya mkutano wa hadhara kwenye kijiji cha Kitama.
SOURCE:OFISI YA WAZIRI MKUU


