
TAASISI ya World Economic Forum (WEF) imemtangaza mjasiriamali kijana nchini, Mohammed Dewji (pichani) kuwa mshindi wa Tuzo ya Kiongozi Kijana wa Duniani (YGL) wa mwaka huu.
Dewji, ambaye anajulikana zaidi kwa jina la MO, ni Ofisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Mohammed Enterprises Tanzania Limited (MeTL) na Mbunge wa Singida Mjini, na kwamba ni mjasiriamali pekee Afrika Mashariki aliyepewa heshima hiyo mwaka huu.
Heshima hiyo hutolewa kila mwaka na WEF ambayo hutambua zaidi ya vijana viongozi 200 duniani kote kutokana na mafanikio yao, ushiriki wao katika jamii na mchango wao katika kutengeneza dunia ya baadaye.
Kamati ya uteuzi huo iliyoongozwa na mwenyekiti wake, Malkia Rania Al Abdullah wa Ufalme wa Jordan, ilimchagua Dewji baada ya kupitia taarifa za vijana wengi kutoka maeneo mbalimbali duniani.
Vigezo vya kuteuliwa kwake kushika heshima hiyo ni rekodi yake ya kitaaluma katika mafanikio yake, uwajibikaji wake katika jamii na kutumia nafasi ya uongozi na kuwa mfano duniani.
Washindi wa Tuzo ya YGL 2012 wataungana na jumuiya kubwa ya Mkutano wa Viongozi Vijana wa Dunia ambao unawajumuisha watu 668. Mkutano huo wa YGL unafanyika kila mwaka, ambao mwaka huu utafanyika Mexico kuanzia Aprili 14 hadi 18.
Viongozi Vijana wa Dunia hujikita katika shughuli za kijamii, kujumuika katika matukio yanayoandaliwa na WEF na kuandaa matukio yao wenyewe na kufanya ubunifu wao pamoja na vikosikazi.
“Ninaishukuru sana WEF kwa kunipatia heshima hii kama kiongozi kijana, ninaweza kuwasaidia vijana wa Tanzania kutimiza ndoto za maisha yao ili kuweza kupata maisha mazuri,” alisema Dewji leo.
MO anakuwa Mtanzania wa tatu kushinda katika tuzo hiyo akitanguliwa na mmiliki wa kampuni inayoshughulikia ndege binafsi, Executive Jets, Suzan Mashibe na aliyekuwa Mshauri wa Uchumi wa Rais Jakaya Kikwete, Elsie Kanza.
Mfanyabiashara huyo alizaliwa mwaka 1975 mkoani Singida, na alipata elimu yake ya awali katika Shule ya Kimataifa ya Tanganyika (IST) na mwaka 1992 alienda Marekani na kupata elimu ya juu ya sekondari.
Katika Shule ya Sekondari ya Florida ndipo alipoanza kuonesha dalili za uongozi baada ya shuleni hapo kuchaguliwa kuwa Rais wa wanafunzi na ndipo jina la MO liliposhika.
MO baadaye alihamia katika Chuo Kikuu cha Georgetown jijini Washington DC, ambako alisomea masuala ya biashara ya kimataifa na fedha, na masomo machache ya Theolojia. Chuo hicho huwajenga wanafunzi wake kufanya kazi zao kwa mafanikio. Kutokana na hilo, kuanzia mwaka 1998, alianza kujikita katika biashara za familia yake ambako alipanda hadi kufikia katika uongozi wa juu katika muda wa miaka miwili.
Chini ya uongozi wake, MeTL Group ilijibadilisha na kuwa kundi la makampuni lililokuwa na kampuni tanzu 12 katika muda usiozidi muongo mmoja. Hilo limeiwezesha kampuni hiyo kuchangia asilimia tatu katika Pato ya Taifa na kuajiri watu 24,000. Dewji ni mpenzi na mfadhili wa soka ya Tanzania na amekuwa akichangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya timu ya Taifa (Taifa Stars).
Katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005, MO aliwania na kushinda kiti cha ubunge cha Singida Mjini kwa tiketi ya CCM kwa zaidi ya asilimia 90 ya kura zote. Mwaka 2007, alichaguliwa kuwa Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa na alishinda tena ubunge 2010.