CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimeibuka kidedea katika uchaguzi mdogo wa ubunge na udiwani wa Tarime uliofanyika juzi. Mgombea...
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimeibuka kidedea katika uchaguzi mdogo wa ubunge na udiwani wa Tarime uliofanyika juzi.
Mgombea ubunge wa chama hicho, Charles Mwera, alitangazwa kumrithi Chacha Wangwe aliyekufa ajalini Julai mwaka huu, baada ya kushinda kwa kupata kura 34,545 huku mgombea wa CCM Christopher Kangoye akipata kura 28,996.
Mgombea wa NCCR-Mageuzi, Haruni Marwa alipata kura 949 wakati mgombea wa DP Benson Makanya alipata kura 305.
Kwa ushindi huo wa ubunge na udiwani Chadema inaendelea kuongoza halmashauri ya wilaya ya Tarime huku CCM ikiendelea kubaki chama cha upinzani katika halmashauri hiyo.
Kwa upande wa udiwani mgombea wa udiwani wa Chadema, John Heche, alishinda kwa kupata kura 4,820 akifuatiwa na mgombea wa CCM, Peter Wambura, aliyepata kura 3,239.
Mdogo wake marehemu Wangwe, Gideon Wangwe wa NCCR- Mageuzi aliambulia kura 169, John Rotente wa CUF kura 79 na Johanes Sando wa DP alipata kupata kura 24.
Baada ya matokeo hayo kutangazwa jana na msimamizi wa uchaguzi huo Trasias Kagenzi, mgombea huyo wa CCM Kangoye alisema hakuridhika na matokeo hayo kwa kile alichodai kuwa kulikuwa na hitililafu wakati wa kuhesabu kura na wakati wa kampeni.
Kangoye ambaye alifika katika ofisi ya halmashauri muda mfupi baada ya kutangazwa matokeo hayo huku akiwa amefuatana na Katibu wa CCM wa wilaya ya Tarime, Iddi Stambuli, alisema atapinga matokeo hayo kwa msimamizi wa uchaguzi na ikishindikana ataenda mahakamani.
Mgombea huyo pia alikataa kusaini matokeo hayo na kukinzana na Msimamizi wa Uchaguzi ambaye awali alisema wagombea wote wamekubali na kusaini matokeo.
Licha ya msimamo huo wa Kangoye, msimamizi wa uchaguzi alimkabidhi Mwera hati ya kumtambua kuwa ni mbunge wa halali wa jimbo la Tarime.
Kangoye alisema msimamizi alitangaza matokeo huku akiwa bado anajumlisha kura za vituo alizopewa na mawakala wa CCM. Alianisha kasoro nyingine kuwa ni vitisho vya nguvu vilivyowafanya wapiga kura wasijitokeze kupiga kura.
Akizungumza kwa huzuni, Kangoye alisema vitisho vya mambo yatakuwa kama Kenya na makundi ya vijana ya kujaa katika vituo vya kupigia Kura, ndivyo vilivyofanya wapiga kura 78,186 ambao hawakujitokeza kutumia demokrasia yao kati ya 146, 919 ambao walijiandikisha katika Daftari la Kura.
Kangoye alipingana na kauli ya Katibu Mwenezi wa Chama hicho, John Chiligati, ambaye alisema mwishoni mwa wiki kuwa kama wagombea wao watashindwa watakubali matokeo kwa maelezo kuwa hiyo ndio demokrasia ya kweli.
Kwa upande wake, Mwera licha ya kutangazwa mshindi, alikiri kuwa uchaguzi huo ulikuwa na kasoro nyingi za vitisho vya polisi, watu kukatwa mapanga lakini wananchi wamekubali sera zao na wamemchagua awe mwakilishi wao bungeni na kuahidi kuwa ataanza kazi mara moja ya kuwatetea bila kubagua Itikadi za vyama,
Mwera alifafanua kuwa atavaa viatu cha marehemu Wangwe kwa kutetea haki za wanyonge.
Naye Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, Zitto Kabwe alisema amepata mpiganaji mwenzake ambaye ataongeza nguvu ya upinzani ya kuwashughulikia mafisadi.
Zitto alikumbusha kuwa ni mara ya kwanza katika kuanzishwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1992 kwa Chadema kushinda uchaguzi mdogo.
Kabla ya kutangazwa matokeo wafuasi wa Chadema walianza kushangilia kutokana na matokeo ya awali kuonyesha ilikuwa inaongoza kwa kwenda ofisi za Halmashauri ya Wilaya zilizotumiwa na Tume ya Uchaguzi.
Wakiwa bado mita 400 kufika eneo ambako matokeo yalikuwa yatangazwe walikumbana na kigingi cha polisi na kushindwa kujizuia huku wakiimba nyimbo kuwa Chama cha wahuni chashinda, mende kaangusha kabati na kuanza kujibizana na polisi waliokuwa na silaha mbalimbali.
Baada ya majibizano hayo, polisi walianza kupiga mabomu ya kutoa machozi huku nao wakiwapiga na kuwajeruhi polisi kadhaa kwa mawe na kuanza kutimua huku wakipiga yowe. Tukio hilo lilichukua saa nne na kufanya kazi za biashara mjini hapa kufungwa na shughuli za mahakama ya mwanzo kusitishwa.
Katika sakata hilo polisi ambao walikuwa wanaongozwa na Kamanda wa operesheni maalum nchini Venance Tossi iliwakamata zaidi ya watu 50.
Wananchi hao walikuwa wakipiga kelele kuwa kucheleweshwa kwa matokeo ni jaribio la kuwapokonya ushindi.
Polisi waliokuwa wamejipanga kila kona ya kuzunguka hizo za halmashauri walifikia hatua za kuwazuia hata watumishi mbalimbali wa Serikali akiwemo Hakimu wa Mahakama ya mwanzo ya Tarime Mjini, Samweli Gimeno ashindwe kwenda katika eneo lake la kazi.
Mchakato wa kuwania kiti cha ubunge Tarime kilianza Septemba 14 kwa vyama vyote kunadi sera zake kwa wananchi na kufikia tamati juzi huku kampeni hizo zikigubikwa na mbwembwe na vurugu, fujo za kila namna na kufikia hatua za watu kumwaga damu kwa kukatwa mapanga.
Miongoni mwa watu ambao walionja chungu ya kampeni ni kiongozi wa DP taifa Mchungaji Christopher Mtikila ambaye alishambuliwa kwa mawe mawe hadi kumjeruhi kichwani. Pia baadhi ya watu wengine walijeruhiwa kwa mapango na wengine kuuana kwa ushabiki wa vyama.
Miongoni mwa mwembwe katika kampeni hiyo ni kurushwa kwa helkopita tatu. Chadema ndicho kilichoanza mbwembwe hizo kwa kupaua anga kwa kutumia Helkopta na CCM kujibu mapigo kwa kupeleka mbili kwa mpigo ambazo licha ya kuyafikia maeneo mengi vijijini lakini Helkopta ya mbowe imezitungua na kuibuka Mshindi wa Udiwani na Ubunge.
Nashon Kennedy anaripoti kutoka Mwanza kuwa Katibu Mkuu wa CCM Yusuf Makamba amesema CCM inakubaliana na ushindi huo na kukiri kuwa ingawa walijiandaa kwenda kumg'oa mtu lakini haikuwa bahati yao.
Aliipongeza Chadema kwa ushindi ilioupata lakini akawatahadharisha kuwa wakae mkao wa kuondoka ifikapo mwaka 2010 kwa maelezo kuwa CCM ni kama wamejikwaa tu.
"Unapoanguka usiulize umeangukia wapi, angalia ulipojikwaa, tunawapongeza Chadema kwa ushindi huu walioupata,” alisema.
Pichani Mbunge mpya wa Tarime
COMMENTS