Imeelezwa kuwa ushirikiano unaoonyeshwa na viongozi wa Afrika katika kuukabili ugonjwa wa malaria , kupitia mtandao wao ujulikanao kama A...
Imeelezwa kuwa ushirikiano unaoonyeshwa na viongozi wa Afrika katika kuukabili ugonjwa wa malaria , kupitia mtandao wao ujulikanao kama Afrian Leaders Malaria Alliance (ALMA) unaweza kutumiwa na viongozi hao katika kuzikabili changamoto nyingine.
Hayo yameelezwa na Bw. Raymond Chambers, mwakilishi maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, kuhusu malaria, wakati wa hafla ya utiaji saini mkataba wa makubaliano(MOU) kati ya ALMA na Taasisi isiyo ya kiserikali inayojihusisha na masuala ya elimu , teknolojia na huduma za utafiti (AED-ARTS) ya kimarekani.
Kupitia makubaliano hayo AED-ARTS pamoja na mambo mengine itafanya utafiti na kutoa ushauri kuhusu athari za kodi na ushuru hasa zile zinazotozwa katika bidhaa na huduma zinazohusu ugonjwa wa malaria. Utafiti na ushauri huo utafanyika katika nchi 76 zilizoathiriwa zaidi na ugonjwa wa malaria duniani kote.
Moja ya vikwazo vinavyokwamisha vita dhidi ya malaria, ni kodi na ushuru mkubwa unaotozwa kwa madawa, hali inayosababisha wagonjwa wengi wa malaria kutopata matibabu au matibabu kuwa ghari au kutopatikana kwa urahisi na kwa wakati.
Kupitia mtandao huo wa viongozi wa Afrika baadhi ya nchi ikiwamo Tanzania zimefuta baadhi ya ushuru na kodi zinazotozwa katika dawa za malaria zinazoingizwa nchini na bidhaa nyinginezo zinazohusiana na ugonjwa huo.
Vilevile AED-ARTS pia kwa kushirikiana na ALMA na wadau wengine, itajihusisha na utoaji wa ushauri wa kiufundi katika eneo la utoaji wa elimu ya uhamasishaji katika ngazi za kijamii.
Akizungumza wakati wa utiaji sahihi wa makubaliano hayo,Bw. Raymond Chambers amesema katika muda mfupi wa uhai wake tayari mtandao huo wa viongozi wa Afrika kuhusu malaria, umeonyesha mafanikio makubwa katika kuukabili ugonjwa wa malaria barani Afrika.
Akasema ni kwa kupitia ALMA kumekuwapo na mwitikio mkubwa kutoka kwa wahisani mbalimbali wakiwamo matajari wakubwa, mashirika yasiyo ya kiserikali, makampuni yanayotengezeza dawa za malaria, wa kuchangia kwa hali na mali katika miradi na program za kukabiliana ugonjwa huo Afrika.
Amesema mwamko huo unatokana kwa kiasi kikubwa na imani yao kuhusu mtandao huo ambao Mwenyekiti wake wa Kwanza ni Rais wa Tanzania, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete.
“Tunapozungumizia mafanikio ya ALMA sina budi kutambua mchango mkuubwa wa Rais Jakaya Mrisho Kikwete yeye amekuwa mstari wa mbele sana katika kulikabili jukumu hili, ni kiongozi ambaye amekuwa na mtazamo wa aina yake na kwa kweli kama si kuona kwake mbali, leo hii tusingekuwa tunazungumzia mafanikio haya. Balozi Omben Sefue naomba unikishie salama na shukrani zangu kwa Mhe.” akasisitza Raymond Chambers.
Akaongeza kuwa kupitia mtandao huo, imekuwa rahisi hata kwa nchi ndogo na maskini za Afrika si tu urahisi wa kupata misaada lakini pia ya kukaa na washirika wa kimataifa na kujadiliana nao. Hali ambayo anasema isingekuwa rahisi kama kila nchi ingekuwa inahangaika kivyake vyake.Akabainisha kuwa imekuwa rahisi kwa nchi za afrika hata zile ndogo kunufaika na misaada hiyo kupitia ALMA hali aliyosema isingekuwa rahisi kufikiwa kama nchi moja moja.
“Mimi naamini kwamba ALMA inatoa mfano nzuri kwamba viongozi wa afrika wakiungana na kushirikiana wanaweza kabisa kuzikabili changamoto nyingine ambazo bado zinaikabili Afrika” akasema Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa.
ALMA ambayo ilianzishwa rasmi mwaka jana ikiwa na nchi wanachama 35, hadi sasa imeweza kuzisaidia nchi 14 kuandika michanganuo ya kuomba misaada katika mashirika ya kimataifa likiwamo Global Fund. Imesaidia kuanzishwa kwa njia rahisi za utangazaji wa tenda kwa nchi 6 ambazo zimeweza kununua vyandarua milioni 24 katika kipindi kifupi.
Aidha ALMA imetoa misaada ya kiufundi kwa nchi wanachama 11, imeongeza idadi ya nchi ambazo ama zimekwisha kuondoa au ziko mbioni kuodoa kodi katika bidhaa na dawa za kutibu malaria. Vilevile imefanikisha ushirikiano kati ya nchi wanachama na wadau mbalimbali kukusanya raslimali kwaajili ya kudhibiti ugonjwa wa malaria katika nchi saba.
Lengo la Viongizi wa Afrika kwa Kushirikiana na Umoja wa Mataifa na wadau mbalimbali ni kupunguza kwa zaidi ya nusu vifo vitokanavyo na ugonjwa wa malaria ifikapo mwaka 2015, kusambaza vyandarua vyenye viatilifu na kuuthibiti na hatimaye kuutokomeza kabisa ugonjwa huo barani Afrika.
pichani:RAIS WA MUDA WA TAASISI YA AED-ARTS YENYE MAKAO YAKE WASHINGTON. BW. GEORGE INGRAM AKISAINI MKATABA WA MAKUBALIANO NA MKURUGENZI MTENDAJI WA ALMA BIBI JOHANNAH PHUMAPHI, HAFLA HIYO ILIYOFANYIKA NEW YORK ILIANDALIWA NA UBALOZI WA TANZANIA KATIKA UMOJA WA MATAIFA NA SEKRETARIETI YA ALMA NA KUHUDHURIWA NA MABALOZI MBALIMBALI NA WAFADHILI WA JUHUDI ZA VIONGOZI WA AFRIKA KATIKA KUUKABILI UGONJWA WA MALARIA. WALIOSIMAMA NYUMA NI BALOZI OMBENI SEFUE NA BW. RAYMOND CHAMBERS, MWAKILISHI MAALUM WA KATIBU MKUU WA UMOJA WA MATAIFA KUHUSU MALARIA
Source:Maura Mwingira
COMMENTS