THE UNITED REPUBLIC OF TANZANIA DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS Telephone: 255-22-2114512, 2116898 E-mail:...
THE
UNITED REPUBLIC OF TANZANIA
DIRECTORATE
OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS
Telephone: 255-22-2114512,
2116898
E-mail: ikulumawasiliano@yahoo.com
Fax: 255-22-2113425 |
|
|
TAARIFA
KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ametoa
maagizo thabiti saba ya kuhifadhi mazingira nchini akisema “tusipokuwa makini na kuchukua
hatua thabiti za kuhifadhi mazingira, uhai na ustawi wetu utakuwa mashakani.
Tusipofanya hivyo, huko mbele ya safari kuna giza nene la maangamizi.”
Aidha, Rais
Kikwete ametoa mifano saba ya kuthibitisha uharibifu wa mazingira duniani na
kueleza njia nne ambazo kwa kiasi kikubwa zinachangia katika uharibifu wa
mazingira nchini.
Amesisitiza
kuwa jukumu la kutunza na la kuhifadhi mazingira ni la Watanzania wote, linalohitaji
juhudi za pamoja na ushirikiano wa karibu wa wadau wote katika ngazi zote
nchini.
Rais
Kikwete ameeleza athari hizo za mazingira na hatua za kuchukuliwa kupambana na
hali hiyo wakati alipohutubia mamia ya wananchi kwenye Uwanja wa Mashujaa mjini
Moshi kwenye Kilele cha Maadhiminisho ya Siku ya Mazingira Duniani ambako pia
amezindua Kampeni ya Kitaifa ya Usafi na Ujenzi wa Vyoo Bora.
Baada ya
kueleza kwa ufasaha kuhusu athari za uharibifu wa mazingira nchini, Rais
Kikwete ametoa maagizo thabiti saba ya jinsi ya kupambana na hali hiyo nchini
ikiwa ni pamoja na kuzingatia umuhimu wa kuhifadhi ardhi na misitu kwa kupanda
miti; kuhifadhi vyanzo vya maji, milima na misitu ya asili; na kudhibiti
kilimo, ufugaji na uchimbaji wa madini usiokuwa endelevu.
Maagizo
mengine ya Rais Kikwete ni kudhibiti matumizi mabaya ya dawa za mifugo na
kilimo; kudhibiti uchafuzi wa mazingira katika maeneo ya makazi na viwandani;
kusimamia uzalishaji bora usiochafua mazingira kwenye viwanda nchini; na
kulinda mazingira ya pwani, mito, maziwa na bahari.
Rais
Kikwete pia amewaeleza wananchi mifano saba ya kuthibitisha jinsi hali ya
mazingira ilivyoharibika duniani ikiwa ni pamoja na ukweli kuwa majira ya mvua
yamebadilika, mvua siyo ya uhakika na vipindi vya ukame vimeongezeka; theluji
inapungua kwa kasi kwenye ncha za Kaskazini na Kusini mwa dunia na kwenye
vilele ya milima ukiwamo Mlima Kilimanjaro; na kuongezeka kwa maji baharini na
hivyo kuzidi kula nchi kavu na kuyaweka maeneo mengine katika hatari ya kumezwa
na maji.
Mifano
mingine ni magonjwa kama malaria kuzidi kusambaa katika maeneo ambayo zamani
yalikuwa hayana mbu kwa sababu yalikuwa baridi na sasa yamekuwa joto; kuzidi
kupungua kwa maji safi kwenye mito, chemichemi, vijito, maziwa na mabwawa;
kuzidi kuendelea kupungua kwa eneo la misitu na kusambaa zaidi kwa jangwa; na kupungua
kwa ubora wa ardhi na hivyo kupungua kwa mazao na malisho ya mifugo.
Kuhusu
uharibifu wa mazigira nchini, Rais Kikwete amesema kuwa umekuwa unachangiwa
pamoja na mambo mengine ukataji miti kwa wingi kwa ajili ya shughuli za kilimo;
uvunaji miti kwa kasi zaidi kuliko ile inayopangwa; kuwepo kwa mifugo mingi
kupita uwezo wa ardhi; na shughuli za viwanda na hasa mahitaji ya nishati na
malighafi kusababisha uharibifu wa mazingira.
Kuhusu
umuhimu wa kushirikiana kupambana na janga la uharibifu wa mazingira, Rais
Kikwete amewaambia wananchi: “ Jukumu la kutunza na kuhifadhi mazingira
ni letu sote, linahitaji juhudi za pamoja na ushirikiano wa karibu wa wadau
husika katika ngazi zote. Sisi peke yetu Serikalini hatuwezi kwani wahenga
wamesema: ‘kidole kimoja hakivunji chawa.’ Tunataka wote tuhusike – Serikali
Kuu, Serikali za Mitaa, wananchi, NGO’s na kadhalika.”
Ameongeza
Rais Kikwete: “Napenda kutumia nafasi hii kuzipongeza baadhi ya Serikali za Mitaa ambazo
zimeunda Kamati za Mazingira ili kuratibu shughuli za kuhifadhi mazingira
katika maeneo yao. Napenda kutoa mwito kwa Serikali za Mitaa ambazo bado
hazijaunda Kamati hizo, wafanye hivyo mapema iwezekanavyo. Tayari nimewaagiza
Wakuu wa Mikoa na Wilaya zote nchini kusimamia kwa makini Sheria na Kanuni za
Hifadhi ya Mazingira katika maeneo yao. Natumaini hili litafanyika.”
Wakati wa
sherehe hizo, Rais Kikwete pia amewakabidhi washindi wa mwaka huu wa mashindano
ya usafi nchini na washindi wa mashindano ya kuhifadhi mazingira nchini ambako
Shule ya Sekondari ya Kameyu ya Mkoa wa Manyara imechukua ushindi wa jumla wa
ubora wa kuhifadhi na kutunza mazingira nchini.
Aidha,
wakati wa sherehe hizo, Rais Kikwete amezindua Kampeni ya Taifa ya Usafi na
Ujenzi wa Vyoo Bora ambao unaendeshwa kwa ushirikiano baina ya Serikali,
Wananchi na Washirika wa Maendeleo wa Tanzania ikiwemo Benki ya Dunia na
Shirika la Umoja wa Mataifa la Mfuko wa Watoto (UNICEF).
Mapema
leo asubuhi, Rais Kikwete amezindua Mpango wa Upandaji Miti wa Kanisa la
Kiinjili la Kilutheri (KKKT), Dayosisi ya Kaskazini ambako maelfu kwa maelfu ya
miti itapandwa katika mikoa ya Kilimanjaro, Arusha na Manyara. Rais amezindua
Mpango huo kwa kupand mti aina ya Mzeituni kwenye eneo la Hosteli ya Uhuru
mjini Moshi.
……..Mwisho…..
Imetolewa na:
Kurugenzi
ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu.
Dar
es Salaam.
5 Juni, 2012
COMMENTS