HOTUBA YA WAZIRI WA HABARI, VIJANA, UTAMADUNI NA MICHEZO, MHE. DKT. FENELLA E. MUKANGARA (MB), AKIWASILISHA BUNGENI MAKADIRIO ...
HOTUBA YA WAZIRI WA HABARI, VIJANA, UTAMADUNI NA MICHEZO, MHE.
DKT. FENELLA E. MUKANGARA (MB),
AKIWASILISHA BUNGENI MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA BAJETI
KWA MWAKA WA FEDHA 2012/2013
A. UTANGULIZI
1.
Mheshimiwa Spika, kufuatia taarifa iliyowasilishwa leo kwenye Bunge lako Tukufu na
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maendeleo ya Jamii, sasa naomba
kutoa hoja ya kwamba Bunge lako Tukufu likubali kupitisha makadirio ya mapato
na matumizi ya Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo na Asasi zake
katika mwaka wa fedha wa 2012/2013.
2.
Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa napenda kutumia fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa
kutuwezesha kukutana tena kwenye Bunge lako tukufu tukiwa wenye afya na uzima.
Namshukuru pia kwa kuijalia nchi yetu kubaki katika hali ya amani na utulivu. Aidha,
sina budi kukushukuru wewe binafsi na waheshimiwa Wabunge wote kwa ushirikiano
mzuri mnaonipa unaoniwezesha kutekeleza kikamilifu majukumu niliyokabidhiwa.
3.
Mheshimiwa Spika, napenda kumshukuru kwa dhati Rais wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete kwa
heshima aliyonipa ya kuniteua kuwa Waziri anayesimamia Sekta za Habari, Vijana,
Utamaduni na Michezo na pia kumteua Mheshimiwa Amos Gabriel Makalla (Mb), Mbunge wa Jimbo la
Mvomero kuwa Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo. Aidha, namshukuru
Mhe. Dkt. Emmanuel John Nchimbi (Mb), Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi kwa
ushirikiano na maelekezo yake ya kazi wakati akiwa Waziri wa Habari, Vijana,
Utamaduni na Michezo. Nashukuru pia familia yangu, hasa mume wangu
mpendwa, Prof. Daudi Mukangara na watoto wangu Cleopatra, Natasha na Jackson,
kwa ushirikiano na uvumilivu wao muda mwingi ninapokuwa nikitekeleza majukumu
ya Kitaifa.
4.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2011/12, Bunge lako Tukufu liliwapoteza
Mheshimiwa Jeremia Sumari, aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Arumeru Mashariki (CCM),
Mheshimiwa Regia Mtema, aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalum (CHADEMA) pamoja na
Mheshimiwa Mussa Khamis Silima aliyekuwa Mwakilishi wa Jimbo
la Uzini (CCM). Mungu
azilaze roho zao mahali pema peponi.
5.
Mheshimiwa Spika, napenda kwa namna ya pekee niwapongeze Mawaziri na Naibu Mawaziri pamoja
na Wakuu wa Mikoa na Wilaya walioteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania. Pongezi za pekee ziwaendee Wabunge wote wapya waliochaguliwa na
wananchi na walioteuliwa na Mhe. Rais na ambao wamejiunga katika Bunge
lako tukufu kutoka katika Chama cha
Mapinduzi, CHADEMA na NCCR - Mageuzi.
6.
Mheshimiwa Spika, kipekee nitumie fursa hii kumpongeza Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania kwa kuteua wajumbe wa Tume ya Katiba wenye dhamana ya kuratibu maoni
ya wananchi kuhusu Katiba Mpya. Vilevile, nawapongeza Mawaziri
waliotangulia kuwasilisha hoja zao, hususan Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania, Mhe. Mizengo Kayanza Peter Pinda (Mb), kwa hotuba yake fasaha
yenye maelekezo ya utekelezaji wa kazi za Serikali kwa kipindi cha mwaka wa
fedha 2012/2013. Waziri Mkuu ameainisha malengo ya Utekelezaji wa Mpango wa
Maendeleo wa Miaka Mitano kutokana na Dira ya Taifa ya Maendeleo, Malengo ya
Milenia na Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini (MKUKUTA II).
Aidha, nampongeza Mhe. Stephen
Wassira (Mb), Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mahusiano na Uratibu kwa hotuba
yake iliyoonyesha Hali ya Uchumi wa Taifa kwa mwaka 2011 na Mpango wa Maendeleo
wa mwaka wa fedha 2012/2013. Pia, nampongeza Mhe. Dkt. William Mgimwa (Mb),
Waziri wa Fedha, kwa hotuba yake nzuri iliyoainisha Makadirio ya Mapato na
Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2012/2013. Kwa namna ya pekee
niwashukuru Waheshimiwa Wabunge waliochangia hotuba za Mawaziri
walionitangulia. Maoni waliyotoa yamesaidia kuboresha mipango ya Serikali
katika sekta mbalimbali, zikiwemo Sekta ambazo ziko chini ya Wizara ninayoiongoza.
7.
Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo ya awali, naomba sasa kutumia fursa hii kuipongeza
na kuishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maendeleo ya Jamii ambayo inaongozwa
na Mbunge wa Jimbo la Peramiho, Mhe. Jenista Joakim Mhagama na Makamu
Mwenyekiti wake Mbunge wa Jimbo la Kondoa Kusini, Mhe. Juma Nkamia, kwa
kuiongoza vizuri Kamati hii. Aidha, naishukuru Kamati ya Bunge lako Tukufu kwa kutoa ushauri na
maelekezo wakati wa kujadili bajeti ya Wizara kwa mwaka
wa fedha 2012/2013.
8.
Mheshimiwa Spika, hotuba yangu imegawanyika katika maeneo makuu manne kama ifuatavyo: Eneo
la kwanza ni majukumu ya Wizara,
eneo la pili ni Mapitio ya utekelezaji
wa bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2011/2012, eneo la tatu linahusu Mpango na Bajeti kwa Mwaka wa fedha
2012/2013 na eneo la nne ni hitimisho
lenye kujumuisha shukrani, makadirio ya bajeti kwa mwaka wa Fedha
2012/2013 na maombi rasmi ya fedha kwa ajili ya kutekeleza Mpango wa mwaka wa
fedha 2012/2013.
B.
MAJUKUMU YA WIZARA
9.
Mheshimiwa Spika, majukumu ya Wizara hii ni haya yafuatayo:-
·
Kuandaa na Kusimamia utekelezaji wa Sera za Sekta za Habari, Vijana,
Utamaduni na Michezo pamoja na kuwa Msemaji Mkuu wa Serikali;
·
Kuratibu na kusimamia masuala ya maendeleo ya Vijana ili kuwawezesha
kujiajiri na kujitegemea;
·
Kusimamia Vyombo vya Habari nchini;
·
Kuratibu tasnia ya utengenezaji wa sinema, maigizo, maonyesho na utoaji wa
leseni;
·
Kusimamia utendaji wa Taasisi, Mashirika ya Umma, Wakala, Miradi na
programu zilizo chini ya Wizara;
·
Kuendeleza, kuwezesha na kuratibu masuala ya kuwajengea uwezo watumishi wa
Wizara.
C. MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA
BAJETI KWA MWAKA WA FEDHA WA 2011/2012
Mapato na Matumizi
10.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha wa 2011/2012 Wizara ilipanga kukusanya Mapato ya jumla ya Shilingi 766,907,385 kutoka vyanzo
mbalimbali. Hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Juni, 2012 jumla ya Shilingi 682,374,217 zilikuwa zimekusanywa
ambazo ni sawa na asilimia 89 ya
lengo la makusanyo ya mwaka. Mchanganuo wa makusanyo upo katika Kiambatisho
Na. I. Kadhalika Wizara
ilitengewa jumla ya Shilingi 14,671,877,000
kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida. Fedha hizo zilijumuisha mishahara ya
Wizara Shilingi 2,076,869,000
na ya Taasisi Shilingi
5,991,270,000; Matumizi Mengineyo (OC) ya Wizara Shilingi
3,806,163,200 na ya Asasi zake Shilingi 2,797,574,800. Hadi mwezi
Juni, 2012 jumla ya Shilingi 14,671,877,000
zilipokelewa na kutumika.
Miradi ya Maendeleo
11.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha wa 2011/2012
Wizara ilitengewa jumla ya Shilingi 3,880,851,000
fedha za ndani kwa ajili ya kutekeleza
Miradi ya Maendeleo. Hadi kufikia mwezi Juni, 2012, Shilingi 3,600,000,000 zilikuwa
zimetolewa na kutumika, sawa na asilimia
92.8. Miradi iliyotekelezwa ni Ujenzi wa Eneo Changamani la Michezo na Mradi wa Upanuzi wa Usikivu wa TBC, eneo la
kuimarisha mitambo ya Radio na Televisheni.
SEKTA YA HABARI
12.
Mheshimiwa Spika, Waraka wa mapendekezo ya Kutungwa kwa Sheria ya Kusimamia Vyombo vya
Habari umekamilishwa na kuwasilishwa kwenye ngazi ya juu kwa maamuzi ya
Serikali na hatimaye Bunge lako tukufu katika kipindi cha mwaka huu wa fedha
2012/13. Aidha, kutungwa
kwa sheria hii kutaimarisha weledi na
uwajibikaji wa vyombo vya habari hapa nchini.
13.
Mheshimiwa Spika, Wizara kupitia Idara ya Habari imeendelea kukusanya taarifa mbalimbali za Serikali,
kuandika habari na kuzitoa katika vyombo vya habari, kupiga picha za matukio
mbalimbali ya kitaifa, kuzitoa katika magazeti na kuzihifadhi katika maktaba ya
kumbukumbu ya picha kwa njia ya elektroniki.
14.
Mheshimiwa Spika, kupitia Tovuti ya Wananchi, wananchi wanaendelea kupata haki yao ya
kikatiba ya kutoa maoni kwa uhuru katika masuala yanayowahusu. Tovuti
imewawezesha wananchi kuwa na mawasiliano ya moja kwa moja na Serikali. Aidha,
katika kipindi cha mwaka ulioanza Julai, 2011 hadi Juni, 2012,
jumla ya hoja 38,247 zimepokelewa. Hoja 36,466 zimeshughulikiwa kwa
kupelekwa katika Wizara na Taasisi husika ili kupatiwa majibu na ufumbuzi. Hoja
nyingi zilihusu ucheleweshwaji wa malipo ya pensheni, mgao wa umeme, ukosefu wa
maji, ajali kazini hasa kwenye migodi na mabadiliko ya Katiba. Hoja 1,781 hazikushughulikiwa kwa
sababu hazikuihusu Serikali.
15.
Mheshimiwa Spika, katika kuendeleza uhuru wa upatikanaji wa habari na vyombo vya habari,
Wizara imeendelea na usajili wa magazeti na majarida. Hadi mwezi Juni, 2012
jumla ya magazeti na majarida 763 yalisajiliwa, hii ikiwa ni ongezeko la magazeti
52 kutoka mwaka jana. Magazeti yaliyosajiliwa kuchapishwa kila siku na yaliyo
hai ni 14 na yale yanayochapishwa
kila wiki ni 62. Aidha, magazeti matano (5) yaliyokiuka maadili ya
uandishi wa habari yalipewa onyo.
16.
Mheshimiwa Spika, Sekta ya Utangazaji imeendelea kukua kwa kasi na watu wengi wanazidi
kuomba leseni za kuanzisha vituo vya utangazaji. Mpaka sasa kuna vituo 85 vya redio na vituo 26 vya televisheni. Mchanganuo upo kiambatisho Na. VI. Kwa kipindi cha mwaka 2011/12 vituo vipya 12 vya redio na kituo kimoja (1) cha
televisheni chenye kutoa huduma ya matangazo ya malipo (Subscription Sattelite
TV) vimesajiliwa.
17.
Mheshimiwa Spika, Shirika
la Utangazaji Tanzania (TBC) limeendelea kuwa chombo mahiri cha utangazaji
nchini likiwa na Idhaa tatu (3) za redio na mbili (2) za televisheni. Aidha,
limeendelea kuongoza kati ya vyombo vya utangazaji vilivyopo nchini kwa kueneza
usikivu wa matangazo yake kupitia vyombo vyake vya redio na televisheni katika
eneo kubwa zaidi la nchi yetu. Jumla ya mitambo 22 ya redio za mfumo wa FM
imejengwa Zanzibar na katika mikoa ya Kagera, Mwanza, Mara, Arusha, Dodoma,
Manyara, Kigoma, Shinyanga, Singida, Tanga, Tabora, Rukwa, Katavi, Morogoro,
Dar es Salaam, Lindi, Mtwara, Ruvuma, Mbeya, Iringa na Kilimanjaro. Mitambo
hiyo inarusha matangazo ya Idhaa mbili za TBCTaifa na TBCFM.
Aidha, kwa
upande wa redio kuna mitambo 9 ya Masafa ya Kati inayorusha matangazo ya TBCTaifa
katika mikoa ya Dar es Salaam, Lindi, Dodoma ,
Arusha, Kigoma, Mbeya, Mwanza na Ruvuma . Na kwa
upande wa Televisheni, mitambo ipo katika mikoa ya Dar es Salaam, Arusha,
Tanga, Dodoma, Tabora, Kigoma, Mwanza, Kagera, Mara, Lindi na Mbeya kwa mfumo
wa analojia, na mikoa ya Dar es Salaam, Arusha, Tanga, Dodoma, Mwanza, Mbeya na
Kilimanjaro kwa mfumo wa dijitali. Matangazo yake yanapatikana kwa satelaiti na
kwenye mtandao wa DSTV ndani na nje ya nchi.
18.
Mheshimiwa Spika, katika maadhimisho
ya miaka 50 ya Uhuru wa Tanzania Bara, TBC ilishiriki kwa ufanisi mkubwa kufanikisha
maadhimisho hayo. Aidha, vipindi vingi viliandaliwa na kurushwa. Matangazo ya kilele cha sherehe yalirushwa
moja kwa moja kwenye redio na televisheni. Vilevile vipindi vya elimu kwa umma,
burudani na biashara vimeendelea kurushwa kama kawaida.
19.
Mheshimiwa Spika, katika kupanua vyanzo vya mapato, Kampuni ya
Magazeti ya Serikali (TSN) imezindua Gazeti la Kiswahili la michezo la kila
wiki, Spoti Leo, ambalo limepokelewa
vyema na wasomaji. Aidha, Kampuni imekamilisha ukarabati na kuhamia Jengo lake
la ofisi lililopo Barabara ya Mandela jijini Dar es Salaam. Kukamilika kwa
jengo hili, kunatoa fursa ya uendelezaji wa jengo la Mtaa wa Samora kama kitega
uchumi. TSN imeendelea kuimarisha magazeti yake ya Daily News, Sunday News
na Habari Leo. Kampuni hii inajiendesha
kwa faida, ambapo katika kipindi cha mwaka wa fedha 2011/12 imechangia gawio la
Shilingi 16,000,000 kwenye mfuko mkuu wa Serikali.
Kamati ya Maudhui
20.
Mheshimiwa Spika, Kamati ya Maudhui ilianzishwa kwa Sheria ya Mamlaka
ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) Na. 10 ya mwaka 2003. Kamati hii inatekeleza
majukumu yake kwa kuzingatia Sera ya Utangazaji ya mwaka 2003, Sheria ya Bunge
Na. 3 ya mwaka 2010 pamoja na Kanuni za Utangazaji za mwaka 2005. Kamati hiyo
inateuliwa na Waziri mwenye dhamana ya utangazaji. Kwa mujibu wa Kifungu cha 27
cha sheria hiyo, Kamati ina jukumu la kumshauri Waziri kuhusu masuala ya Sera
ya Utangazaji nchini, kufuatilia na kudhibiti maudhui potofu ya utangazaji.
Kamati pia inasimamia na kuhakikisha kuwa maadili na kanuni za utangazaji
zinafuatwa. Aidha, Kamati inashughulikia malalamiko yatokanayo na maudhui ya
utangazaji kutoka kwa watumiaji wa huduma za utangazaji nchini.
21.
Mheshimiwa Spika, Kamati ya Maudhui imeendelea kupokea na kushughulikia malalamiko
yatokanayo na vipindi vinavyorushwa ambavyo vinakiuka maadili ya utangazaji na
utamaduni wa Mtanzania. Kamati imekuwa ikiyafanyia kazi malalamiko yote na
kuyatolea maamuzi. Ilipobidi Kamati ilitoa makaripio kwa vituo vilivyokuwa
vikienda kinyume cha sheria na kanuni za utangazaji za mwaka 2005 na maadili
katika utangazaji. Katika kipindi hicho, Kamati ya Maudhui ilisikiliza mashauri
manne (4) ya ukiukwaji wa Kanuni za
Utangazaji. Katika kipindi cha mwezi Julai, 2011 hadi mwezi Juni, 2012 TCRA
ilipokea jumla ya malalamiko kumi na
nane (18) ambapo kati ya hayo kumi
na tatu (13) yaliwasilishwa na wananchi na matano (5) yalitokana na ufuatiliaji wa wajumbe wa Kamati ya
Maudhui. Vituo saba (7) vilipewa
onyo na vituo viwili (2) vilipewa
mwongozo. Aidha, Wizara yangu imeelekeza kuanzia sasa kila kituo cha utangazaji
kiwe na Miongozo ya Sera za Uhariri (Editorial Policy Guidelines). Miongozo hii itasaidia kuweka misingi ya
vituo vya utangazaji ili kuviwezesha kufanya kazi kwa kuzingatia kanuni
zilizowekwa. Vituo vitakavyokwenda kinyume na miongozo hii vitachukuliwa hatua na
ikibidi kuvifungia.
22.
Mheshimiwa Spika, TCRA kwa kushirikiana na Wizara yangu pamoja na wadau wa Sekta ya
Utangazaji, imefanya marekebisho ya Kanuni za Utangazaji kufuatia kukua kwa
Sekta ya Utangazaji na kubadilika kwa mfumo wa utangazaji hasa kuelekea kwenye
mfumo mpya wa utangazaji wa dijitali. Aidha, naomba kuchukua fursa hii ya pekee
kuwashukuru wadau wote wa Sekta ya Utangazaji kwa michango, mapendekezo na
maoni yao
katika kufanikisha zoezi lote la kuziandaa upya kanuni hizi. Kadhalika,
shukrani zangu za dhati ziende kwa uongozi wa TCRA kwa mchango wake mkubwa
katika kufanikisha zoezi hili.
23.
Mheshimiwa Spika, kama mnavyofahamu mwaka 2011/2012, TCRA
imefanya mikutano na wadau wa Sekta ya Utangazaji katika kutoa elimu kwa umma
kuhusu mchakato wa kuhama kutoka teknolojia ya utangazaji ya analojia kwenda
dijitali. Uhamaji huo unatakiwa uwe umekamilika ifikapo tarehe 17 Juni 2015,
kwa mujibu wa makubaliano ya nchi wanachama wa Shirika la Mawasiliano Duniani
(ITU).
24.
Mheshimiwa Spika, nchi za Jumuiya ya Afrika ya Mashariki zimeazimia kusitisha matangazo
ya analojia ifikapo tarehe 31 Desemba, 2012. Kiufundi, kusitisha katika kipindi
hicho cha miaka mitatu kabla ya muda uliokubaliwa ulimwenguni, kutaziwezesha
nchi wanachama kupata fursa ya kutathmini iwapo kutatokea matatizo ya kiufundi
washirikiane kuyatatua mapema ili kuondoa usumbufu usio wa lazima. Pili, katika
kipindi cha mpito makampuni yanayotoa huduma za utangazaji yatahitajika
kuendelea kutoa huduma kwa mfumo wa analojia kwa maeneo ambayo mfumo mpya
haujafika na pia kwa dijitali kwa mujibu wa Kanuni za TCRA. Hata hivyo,
mchakato wa mabadiliko haya kutoka teknolojia ya analojia kwenda dijitali
utagusa utangazaji kwa njia ya televisheni pekee na siyo utangazaji wa redio.
Mchango wa Vyombo vya Habari
25.
Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuthamini mchango wa Vyombo
vya Habari, ili kuimarisha Tasnia ya Habari nchini. Wizara yangu inaendelea
kuhimiza Vyombo vya Habari kuhakikisha vinaajiri wahitimu bora wa taaluma ya
uandishi wa habari na utangazaji. Umefika wakati kwa Vituo vya Televisheni kuwatumia
wahitimu hao ili viweze kutoa matangazo bora kwa wasikilizaji na watazamaji.
Kwa hili, nitaendelea kuhimiza ili kuhakikisha weledi wa uandishi wa habari
unashamiri hapa nchini. Nahimiza pia matumizi ya lugha ya Kiswahili sanifu
katika vituo vya televisheni na redio. Ni matumaini yangu vituo vyote vitawajibika
katika matumizi bora ya Kiswahili sanifu, na vitajiwekea utaratibu wa
kutathmini mwelekeo mzima wa lugha hii ya taifa ambayo ndiyo inayotumika kwa Watanzania
wote.
26.
Mheshimiwa Spika, naomba kulipongeza Baraza la Habari Tanzania (MCT) kwa mchango wake katika kuboresha mitaala ya Mafunzo kwa
ajili ya Uandishi wa Habari. Mitaala hiyo ambayo iliandaliwa na kupewa ithibati na Baraza la
Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE) ni kwa ngazi ya 4 ya
Cheti cha Awali cha uandishi wa habari (Basic Certificate in Journalism), ngazi
ya 5 ya Cheti cha Uandishi wa Habari (Certificate in Journalism) na
ngazi ya 6 ya Stashahada ya Uandishi wa Habari (Diploma in Journalism).
Kukamilishwa kwa mitaala hiyo na kupewa ithibati ya NACTE ni hatua muhimu
katika kuimarisha mafunzo yanayotolewa kwa waandishi wa habari kwenye vyuo
mbalimbali vya hapa nchini.
27.
Mheshimiwa Spika,
napenda pia kutambua juhudi zinazofanywa na Vyama na Taasisi
mbalimbali za habari katika kuimarisha weledi, uwajibikaji na maadili ya
uandishi wa habari kwa kuwatambua na kuwatuza waandishi wa habari ambao
wamefanya vizuri zaidi. Chini ya uongozi wa Baraza la Habari Tanzania , vyama mbalimbali vya
uandishi wa habari vimekubaliana kutoa tuzo za pamoja ambazo zinaheshimika
kwenye maeneo mbalimbali ikiwa ni pamoja na habari za afya, mazingira,
biashara, michezo, sayansi na teknolojia, watoto na jinsia. Katika kufanikisha
hili, mwezi Machi, 2012, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania , Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho
Kikwete, alikuwa Mgeni rasmi katika Tuzo za Umahiri wa Uandishi wa Habari za
mwaka 2011.
28.
Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kuvipongeza kwa dhati Vyombo vya
Habari kwa kushiriki kikamilifu katika
Maadhimisho ya Miaka 50 ya Uhuru wa Tanzania Bara. Vyombo hivi vimehabarisha
wananchi kuhusu maendeleo na mafanikio yaliyopatikana nchini mwetu katika
kipindi hicho. Aidha, navipongeza vyombo hivyo kwa namna vilivyotoa taarifa kuhusu
maafa makubwa yaliyotokana na mafuriko ya mwaka jana na kusababisha
kupotea kwa maisha ya watu, mali zao pamoja na uharibifu wa miundombinu. Vyombo
vya Habari vilikuwa bega kwa bega katika kutoa taarifa muhimu kwa wananchi,
kuhamasisha uokoaji na utoaji wa misaada mbalimbali kwa wananchi walioathirika.
29.
Mheshimiwa Spika,
ni matumaini ya Wizara yangu kuwa juhudi hizi za pamoja
kati ya Serikali na wadau wote wa habari zitaendelea katika kuimarisha Sekta ya
Habari ili iendelee kutoa mchango mkubwa zaidi katika kuharakisha maendeleo na ustawi
wa nchi yetu.
SEKTA YA MAENDELEO YA VIJANA
30.
Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea kufanikisha utekelezaji wa
Mwongozo wa Stadi za Maisha kwa vijana
walio nje ya shule. Kupitia Mwongozo huu ambao utasaidia kukabiliana na changamoto za maisha, Wizara
imewapa mafunzo ya kuwajengea uwezo Maafisa Vijana wote nchini ili waweze
kuufahamu na hivyo kusimamia utekelezaji wake katika maeneo yao. Aidha, mtaala
wa kufundishia stadi za maisha kwa waelimisha rika umeshaandaliwa.
31.
Mheshimiwa Spika, Wizara imewezesha kuridhiwa kwa Mkataba wa Vijana wa Afrika wa mwaka 2006.
Mkataba huu umeridhiwa na Bunge lako Tukufu mnamo tarehe 1 Februari, 2012. Wizara yangu kwa kushirikiana na Wizara ya
Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa imepeleka taarifa za kuridhiwa mkataba
huo Makao Makuu ya Umoja wa Afrika (AU) ili nchi yetu iweze kuwekwa kwenye
orodha ya nchi zilizokwisha ridhia mkataba huo.
Aidha, Wizara kwa kushirikiana na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali
imeanza kuchukua hatua za kuandaa muswada wa sheria ya utekelezaji wa mkataba
huu.
32.
Mheshimiwa Spika, Mbio za Mwenge wa Uhuru kwa mwaka 2011
zilizinduliwa tarehe 14 Oktoba, 2011 katika Kijiji cha Butiama Mkoani Mara.
Mgeni Rasmi wakati wa uzinduzi alikuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania ,
Mheshimiwa Dkt. Mohamed Gharib Bilal. Siku hii pia ni ya kuadhimisha kumbukumbu
ya kifo cha Baba wa Taifa na Muasisi wa Mwenge wa Uhuru, Mwalimu Julius
Kambarage Nyerere. Aidha, Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2011 zilikuwa maalum kama sehemu ya maadhimisho ya Miaka 50 ya Uhuru wa
Tanzania Bara chini ya kauli mbiu “Tumethubutu, Tumeweza na
Tunazidi Kusonga Mbele”. Mbio hizo pia zilitumika kuwahamasisha
wananchi na hasa vijana kushiriki katika shughuli za maendeleo ya kiuchumi na
kijamii, kupambana na maambukizi ya virusi vya UKIMWI, kuepuka matumizi ya dawa
za kulevya na vitendo vya rushwa. Sambamba na maadhimisho hayo Mwenge wa
Uhuru pia ulipandishwa katika Kilele cha Mlima Kilimanjaro usiku wa kuamkia Desemba
9, 2011 kukumbuka siku ya uhuru wa nchi yetu.
33.
Mheshimiwa Spika, Sherehe za
Kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru zilifanyika Mkoani Dar es salaam tarehe 01 Desemba, 2011. Mgeni
Rasmi katika sherehe hiyo alikuwa Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania .
Aidha, kwa mujibu wa taarifa zilizokusanywa kupitia Mbio za Mwenge, jumla ya
miradi 273 yenye thamani ya Shilingi
232,357,556,185 ilizinduliwa
na kuwekewa mawe ya msingi.
34.
Mheshimiwa Spika, Mbio za Mwenge
wa Uhuru kwa mwaka 2012 zilizinduliwa tarehe 11 Mei, 2012 katika Uwanja wa Kumbukumbu
ya Sokoine, Mkoani Mbeya. Mgeni Rasmi katika sherehe hizo za uzinduzi alikuwa
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania , Mheshimiwa Mizengo
Kayanza Peter Pinda. Kauli mbiu ya Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka huu ni, “Sensa ni Msingi wa Mipango ya Maendeleo
Yetu Shiriki Kuhesabiwa 26 Agosti, 2012”. Aidha, ujumbe huu unaambatana na kauli mbiu nyingine za uhamasishaji
wananchi kuhusu mambo yafuatayo; Mabadiliko
ya Katiba, Mapambano Dhidi ya UKIMWI, Rushwa na Matumizi ya Dawa za Kulevya. Sherehe za kilele cha Mbio za Mwenge
wa Uhuru 2012 zitafanyika tarehe 14 Oktoba, 2012 katika Mkoa wa Shinyanga.
35.
Mheshimiwa Spika, Maadhimisho ya Wiki ya Vijana yalifanyika sambamba na Maadhimisho ya Miaka 50 ya
Uhuru wa Tanzania Bara yaliyoadhimishwa mkoani Dar es Salaam. Vijana kutoka
sehemu mbalimbali za Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania walishiriki. Aidha, katika banda la maonyesho la kila mkoa kulikuwa
na uwakilishi wa shughuli za maendeleo ya vijana.
36.
Mheshimiwa Spika, Wizara kwa kushirikiana na wadau wengine imeadhimisha Siku ya Kujitolea
Duniani mkoani Dar es Salaam. Sherehe za mwaka 2011 ziliadhimishwa sambamba na
maadhimisho ya Miaka 50 ya Uhuru. Aidha, vijana kutoka sehemu mbalimbali
nchini wameshiriki katika makongamano ya kimataifa nchini Marekani, Australia, Guinea
ya Ikweta, Kenya na Rwanda.
SEKTA YA MAENDELEO YA UTAMADUNI
37.
Mheshimiwa Spika, Wizara yangu imeratibu mchakato wa kuridhia
Mikataba miwili ya UNESCO ambayo ni Mkataba unaohusu Kulindwa kwa Urithi wa
Utamaduni Usioshikika wa mwaka 2003 na Mkataba unaohusu Kulindwa na Kukuzwa kwa
Uanuwai wa Kujieleza Kiutamaduni wa mwaka 2005. Aidha, hati ya kuridhiwa Mikataba hii ilipelekwa UNESCO
Makao Makuu na kusainiwa na Mkurugenzi Mkuu wa UNESCO tarehe 8 Agosti, 2011.
Katika kutekeleza Mikataba hiyo Wizara iliandaa mafunzo kwa wadau wa Sekta ya Utamaduni
ili kujenga uelewa wa pamoja wa utekelezaji. Baadhi ya masuala yaliyomo katika
Mikataba hiyo ni pamoja na utafiti, kuorodhesha amali na urithi wa utamaduni
usioshikika, kuhifadhi, kusambaza na kukuza utamaduni kwa maendeleo ya jamii.
38.
Mheshimiwa Spika, katika
kipindi cha mwaka wa fedha 2011/12 Wizara
imeendelea kutoa elimu juu ya Utamaduni wa Mtanzania kwa jamii katika
kutambua, kupokea na kuheshimu maadili yetu ya Kitanzania. Elimu hii imekuwa ikitolewa kwa kuandaa na
kurusha vipindi vya redio kuhusu ‘Maadili ya Mtanzania’ kupitia kituo cha TBCTaifa. Katika kipindi hicho jumla ya vipindi 42
vilirushwa.
39.
Mheshimiwa Spika, Wizara yangu
iliunda Kamati ya kukusanya maoni ya Wananchi kuhusu dhana ya kuwa na Vazi la
Taifa. Maoni yalikusanywa kikanda na Wizara imepokea mapendekezo ya Vitambaa kutoka katika mikoa yote ya Tanzania Bara.
Mapendekezo yaliyowasilishwa na wengi ni kuwa na kitambaa mahususi kitakachoshonwa
Vazi la Taifa. Kutokana na hatua hiyo, napenda kuliarifu Bunge lako tukufu kuwa
utaratibu wa kupata Vazi hilo upo katika ngazi za ushauri Serikalini na
matarajio yetu ni kukamilisha zoezi hili katika kipindi cha mwaka wa fedha
2012/13.
40.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2011/12 Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) lilitekeleza kazi muhimu zifuatazo:-
·
Miswada 46 ya vitabu vya taaluma ilisomwa na kupewa ithibati ya lugha.
·
Baraza lilitoa huduma ya tafsiri ya miswada, brosha, hati mbalimbali kama
vile vyeti vya shule, vyeti vya kuzaliwa, hati za ndoa na talaka. Pia lilithibitisha tafsiri mbalimbali
zilizofanywa na wafasiri wa nje.
·
Baraza liliratibu na kutoa huduma ya ukalimani wa Kiswahili kwenye mikutano
ya Umoja wa Afrika iliyofanyika mwezi Julai, 2011 huko Guinea ya Ikweta na
Januari, 2012 huko Ethiopia. Aidha,
Baraza lilitoa huduma ya tafsiri na ukalimani wa Kiswahili kwenye mikutano ya Bunge la Afrika iliyofanyika mwezi Oktoba,
2011 huko Afrika Kusini.
·
Baraza lilichunguza makosa yanayofanywa na Vyombo vya Habari na watumiaji wengine wa
Kiswahili. Jumla ya makosa 120 yalibainishwa na kuorodheshwa pamoja na
usahihi wake. Makosa hayo yamekuwa yakisahihishwa katika vipindi vya redio na
televisheni vinavyoshirikisha wataalamu wa BAKITA.
41.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2011/12 Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) lilitekeleza
kazi zifuatazo:-
·
Kuendesha midahalo 47 ya Jukwaa la Sanaa ambapo jumla ya mada 47 ziliwasilishwa kwa wadau 4,055. Midahalo hii inalenga kuwapa wadau uelewa
mpana wa tasnia ya sanaa.
·
Kuendesha mafunzo kwa walimu 54
kutoka shule za Msingi 20 katika mkoa wa Morogoro. Mafunzo hayo
yamewajengea uwezo walimu wa kuwapa stadi za uchoraji na utambaji wa sanaa
watoto shuleni.
·
Kusimamia uchaguzi wa viongozi wa Mashirikisho manne (4) ya
Sanaa za Maonesho, Ufundi, Muziki na Filamu kwa kupata viongozi wapya kwa
mujibu wa katiba zao.
·
Kushiriki katika Mkutano Mkuu wa Tano
wa Shirikisho la Mabaraza ya Sanaa Ulimwenguni Australia na kujenga mahusiano
na Mabaraza ya Sanaa ya mataifa mbalimbali.
42.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2011/12 Bodi ya
Ukaguzi wa Filamu na Michezo ya Kuigiza imekagua jumla ya filamu 98 ambapo
filamu za ndani 48 zilikaguliwa na kupewa madaraja. Kati ya hizo, 1 ilipewa daraja R ikimaanisha filamu hiyo
hairuhusiwi kuoneshwa mahali pa hadhara. Filamu zilizokaguliwa kutoka nje ya nchi ni 50, kati ya hizo, 3 zilipewa daraja R ambapo moja ni kutoka Liberia na mbili kutoka Norway.
Aidha, Bodi imeweka alama maalum kwenye filamu zilizokaguliwa ikiwa ni moja ya
njia ya kuhakikisha filamu zote zisizokaguliwa zinajulikana na wahusika
kuchukuliwa hatua. Katika kipindi cha mwezi
Julai, 2011 hadi Juni, 2012 Bodi ilitoa
vibali 21 vya kutengeneza filamu kwa Watanzania, na 84 kwa wageni.
43.
Mheshimiwa Spika, Bodi ya Ukaguzi wa filamu na Michezo ya Kuigiza iliandaa na kufanya mafunzo
elekezi kwa Maafisa Utamaduni wa Wilaya nchini kwa lengo la kuboresha Bodi za Filamu za Wilaya. Bodi ilisambaza Sheria
na Kanuni za Filamu na Michezo ya
Kuigiza kwa Makatibu Tawala wa Mikoa na Wakurugenzi wa Wilaya nchini. Bodi imeendesha mijadala mitatu kwa
wadau wakiwemo watengenezaji filamu na wasanii wa filamu. Vilevile, imefanya mkutano kuhusu Mustakabali
wa Tasnia ya Filamu katika kuadhimisha miaka 50 ya Uhuru na mkakati kwa kipindi
cha miaka 50 ijayo. Mkutano huu umesaidia wadau walioshiriki
kubuni mikakati mbalimbali ya kuboresha tasnia hii. Mikakati hiyo ni pamoja na
kuhakikisha kuwa filamu na michezo ya kuigiza vinalenga zaidi katika kutangaza
utaifa, uzalendo, maadili na utamaduni wa Tanzania. Nia ni kuondokana na filamu
ambazo zimemezwa na tamaduni za nje. Vile vile, kuhakikisha kuwa tasnia ya
filamu inakuwa rasmi ili ichangie pato la taifa na la msanii binafsi.
44.
Mheshimiwa Spika, Bodi ya Filamu ilizindua Kanuni za
Sheria ya Filamu na Michezo ya Kuigiza ambapo nakala 4,200 za Kanuni na nakala 4,200
za Sheria zilisambazwa. Aidha, utafiti uliofanywa na Bodi kwa
kushirikiana na wadau wa filamu umebaini kuwepo kwa Makampuni 127 yanayojihusisha na uongozaji,
utengenezaji, uzalishaji na usambazaji wa filamu kwa Mkoa wa Dar es Salaam
pekee. Makampuni hayo yameajiri watu
kati ya watatu (3) na kuendelea na kwa
pamoja yanatoa wastani wa ajira 508.
SEKTA YA MAENDELEO YA MICHEZO
45.
Mheshimiwa Spika, Wizara kwa kushirikiana na wadau wengine wa Michezo,
iliendesha kongamano maalum kuhusu Michezo kwa Amani na Maendeleo. Kongamano
hilo lililenga kuonyesha fursa za
kutumia michezo katika kufanikisha malengo ya maendeleo ya Kitaifa na
Kimataifa.
46.
Mheshimiwa Spika, katika kushiriki mashindano ya kimataifa, Timu
za Taifa ziliandaliwa na kuwezeshwa kushiriki katika Michezo ya Afrika. Tanzania iliwakilishwa na zaidi ya
wanamichezo 60 katika mashindano hayo yaliyofanyika nchini Msumbiji, mwezi
Septemba, 2011. Katika mashindano hayo,
timu ya Taifa ya Mchezo wa Netiboli ilishika nafasi ya pili na kujinyakulia
medali ya fedha. Aidha, timu hiyo ya Netiboli
ilishiriki katika mashindano ya Netiboli ya Kimataifa yaliyofanyika Dar es
Salaam ambayo yalishirikisha timu 8 kutoka mataifa mbalimbali. Tanzania ilijinyakulia ushindi wa pili katika
mashindano hayo.
47.
Mheshimiwa Spika, Wizara iliendesha mafunzo kwa wanachuo 38 katika fani za Stashahada
ya Elimu ya Ufundishaji wa Michezo na Stashahada ya Uongozi na Utawala wa
Michezo katika Chuo cha Maendeleo ya Michezo Malya. Mafunzo ya muda mfupi
yalitolewa kwa wadau wa michezo zaidi ya 300 katika Vituo vya Michezo Kanda ya
Kaskazini, Arusha na Kanda ya Kusini, Songea. Aidha, katika kupima
ubora wa walimu wa michezo, mfumo maalum wa kitaifa wa kutathmini sifa na kutoa
madaraja ya Walimu wa Michezo mbalimbali ulianzishwa. Mfumo huu umeanza kwa majaribio kwa michezo
mitatu ya Riadha, Soka la Wanawake na Mpira wa Wavu kwa kushirikisha walimu 86
katika hatua ya awali. Utekelezaji wa mfumo huu upo chini ya mradi wa kuboresha
maisha ya watoto milioni mbili walioko shuleni kupitia michezo (International
Inspiration) ifikapo mwaka 2014. Katika hatua ya awali, Mpango unaendeshwa kwa
kujumuisha shule 15 zilizoko Zanzibar na mikoa ya
Arusha, Mwanza, Dar es Salaam na Ruvuma .
48.
Mheshimiwa Spika, ushauri wa kitaalamu ulitolewa kuhusu miundombinu
na vifaa bora vya michezo katika Mikoa
ya Mara, Dar es Salaam na Dodoma.
Ushauri huu ulitolewa kwa wadau mbalimbali wa michezo wakiwemo wamiliki
na viongozi wa viwanja vya michezo zaidi ya 50. Sambamba na ushauri huu huduma
ya kinga na Tiba kwa Timu za Taifa zilitolewa kwa Timu zilizoshiriki mashindano
ya Nchi za Afrika huko Msumbiji, Timu ya Taifa ya Wanawake (Twiga Stars) na
SHIMIWI iliyofanyika huko Tanga.
49.
Mheshimiwa spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2011/12 Wizara
imeboresha Uwanja wa Uhuru kwa kuufanyia ukarabati mkubwa na kuujenga
katika umbo la “U”. Ukarabati huu utakapokamilika Uwanja utakuwa na uwezo wa
kukaa watazamaji elfu ishirini (20,000).
50.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2011/2012 Baraza la
Michezo la Taifa (BMT) lilitekeleza kazi
zifuatazo:-
·
Kujenga
uwezo wa wafanyakazi wa Baraza la Michezo la Taifa na Vyama vya Michezo vya
Taifa kwa kuwaandalia mafunzo kulingana na mahitaji yaliyopo. Watumishi 12 wa Baraza walishiriki mafunzo ya
sheria ya ununuzi yaliyoendeshwa na PPRA.
·
Kushirikiana
na Halmashauri za Manispaa, Miji na Wilaya kuhamasisha na kuendesha matamasha
ya michezo kwa jamii. Matamasha haya yalilenga kujenga mahusiano na kuboresha
afya ya jamii. Halmashauri zilizoshiriki ni Musoma, Magu, Mpwapwa na Ngara.
·
Kuanzisha
na kuendesha mafunzo ya ufundishaji michezo kwa viongozi vijana kwa ushirikiano
na Vyama vya Michezo vya Taifa na Baraza la Michezo la Uingereza (UK Sport
International). Vijana walioshiriki mafunzo hayo walitoka Dar
es Salaam (800), Arusha (750), Mwanza (350) na Ruvuma
(450).
·
Kuendesha
mafunzo ya muda mfupi ya ufundishaji kwa Walimu wa Michezo mbalimbali wapatao
500 katika Wilaya 10 za Tanzania Bara.
·
Kuandaa,
kusimamia na kuendesha mafunzo ya Uongozi kwa Vijana kupitia michezo kwa
washiriki wapatao 1,200 na pia kuwashirikisha katika mabonanza wanafunzi
wapatao 2,000 wa shule za Msingi na Sekondari.
·
Kuanzisha
mpango maalum wa mafunzo ya Uongozi wa Michezo kwa Wanawake.
UTAWALA
NA RASILIMALI WATU
51.
Mheshimiwa Spika, hivi karibuni Serikali imeidhinisha miundo mipya ya kada za watumishi wa Wizara ya Habari, Vijana,
Utamaduni na Michezo. Miundo hii imeainisha vizuri wajibu na sifa za Maafisa Habari,
Vijana, Utamaduni na Michezo katika ngazi ya Mikoa, Wilaya na Halmashauri. Kupitia miundo hii, Wizara sasa itaweza
kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi zaidi kwani itakuwa na kiungo kizuri kati
yake na ngazi za chini walipo wananchi. Nitumie fursa hii kuwaomba Wakuu wa
Mikoa, Wilaya na Halmashauri kuhakikisha kuwa wanawawezesha maafisa hao ili
waweze kutumika ipasavyo katika kuleta matokeo tarajiwa.
52.
Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha Utawala Bora na
ushirikishwaji wa Wafanyakazi Sehemu za kazi, Wizara imekuwa ikifanya vikao vya
Baraza la Wafanyakazi ili kutatua kero mbalimbali zinazowakabili watumishi wa
Wizara. Aidha, Wizara imehakikisha kwamba Watumishi wapya waliojiunga na
Utumishi wa Umma kwa mara ya kwanza wanapewa mafunzo elekezi ambayo lengo lake
ni kuwapa mwelekeo wa utendaji katika Serikali ikiwemo kuwafahamisha matarajio
ya mwajiri, taratibu za utumishi na maadili katika Utumishi wa Umma.
53.
Mheshimiwa Spika, Wizara
imeendelea na zoezi la kuwapandisha vyeo watumishi wanaostahili kulingana na
miundo ya utumishi ya kada zao na kwa kuzingatia Sera ya Menejimenti na Ajira
katika Utumishi wa Umma ya mwaka 1999 na 2008. Katika kipindi cha mwaka wa fedha 2011/2012 watumishi 46 walipandishwa vyeo. Aidha, Wizara imewezesha kutoa mafunzo kwa
Watumishi 17, kati ya hao 2 wamemaliza mafunzo na 15 wanaendelea.
C: MPANGO NA BAJETI KWA MWAKA WA FEDHA
2012/2013
IDARA YA HABARI
54.
Mheshimiwa
Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2012/2013, Wizara itatekeleza
yafuatayo:-
·
Kuratibu
shughuli za Vitengo vya Habari vilivyomo katika Wizara, Idara zinazojitegemea
na Wakala za Serikali na kutoa mafunzo ya utoaji habari za Serikali kwa Maofisa
Habari wa Vitengo hivyo.
·
Kuendelea
na mchakato wa kuanzisha mtandao wa kulinda na kuuza picha za viongozi na
matukio mbalimbali ya kitaifa popote duniani kupitia mradi wa “e-commerce”.
Mtandao huo utawawezesha wadau kupata picha hizi popote kutoka katika maktaba
ya picha.
·
Kuchapisha
machapisho mbalimbali ya Serikali likiwemo gazeti la Nchi Yetu.
·
Kupokea
maoni ya wananchi kupitia Tovuti ya Wananchi na kufuatilia majibu ya hoja hizo.
·
Kukusanya na kuandika habari
za matukio mbalimbali ya Kiserikali.
55.
Mheshimiwa
Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha wa 2012/2013, Shirika la Utangazaji
Tanzania (TBC) linatarajia kuimarisha vituo vya televisheni ili kuongeza
usikivu.
56.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2012/2013, Kampuni ya Magazeti ya Serikali (TSN) inalenga kutafuta fedha
za mradi wa upanuzi wa kiwanda cha uchapaji na kukamilisha mkakati wa ubia
wa kuendeleza viwanja vyake vilivyopo Dodoma na Dar es Salaam . Aidha,
kampuni itaendelea na juhudi za kuinua ubora wa magazeti yake na
kuimarisha usambazaji, hasa mikoani.
SEKTA YA MAENDELEO YA
VIJANA
57.
Mheshimiwa spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha
2012/2013 Wizara imepanga kutekeleza
malengo yafuatayo:-
·
Kumpata mshauri mwelekezi ili kufanya upembuzi wa mradi
wa kuanzisha Benki ya Vijana. Mchakato huu utahusisha ukusanyaji wa maoni toka
kwa wadau mbalimbali. Tayari mawasiliano
ya awali yamefanyika kati ya Wizara yangu na uongozi wa Benki Kuu ya Tanzania
na Benki ya Wanawake, kwa lengo la kupata maoni ya kiufundi, uzoefu na mstakabali
wa uanzishaji wa Benki hiyo. Lengo la kuanzisha Benki hii ni kuwa na chombo
maalum cha fedha kitakachotoa mikopo nafuu na inayokidhi mahitaji halisi na
uwezo wa Vijana.
·
Kuendelea na maandalizi ya awali yanayohusiana na
mapendekezo ya kutungwa kwa sheria ya uundwaji wa Baraza la Vijana Tanzania .
Rasimu ya Waraka wa Baraza la Mawaziri inayohusu suala hili tayari imeandaliwa na
ipo katika ngazi za ushauri na maamuzi serikalini.
·
Kuboresha utendaji wa Mfuko wa Maendeleo ya Vijana
kwa kuzijengea uwezo SACCOS 242 ambazo tayari ni wateja wa mfuko huu. Inatarajiwa pia kwamba mara Benki ya Vijana
itakapoanzishwa, SACCOS zilizopo na nyingine zitakazoanzishwa ndizo
zitakazokuwa wateja wakubwa wa Benki hiyo.
·
Kuwapatia mafunzo maalum ya muda mfupi ya
kujiajiri, ujasiri na ujasiriamali wahitimu wa shule na vyuo mbalimbali. Moja ya mikakati ya kutekeleza lengo hili ni
kwa kutumia vituo vyetu vya vijana vilivyoko Ilonga – Kilosa, Sasanda – Mbozi
na Marangu – Moshi.
SEKTA YA MAENDELEO YA
UTAMADUNI
58.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2012/2013, Wizara kupitia Sekta hii
itatekeleza yafuatayo:-
·
Kukamilisha utaratibu wa urasimishaji tasnia ya
filamu na muziki ili wasanii wanufaike na kazi zao pamoja na kuchangia Pato la
Taifa. Maelezo ya kina kuhusu utaratibu
huu yalitolewa ndani ya Bunge lako tukufu na Waziri wa Fedha wakati
akiwasilisha Hotuba ya bajeti ya Serikali
kwa mwaka wa fedha 2012/13.
·
Kuendelea kukusanya taarifa muhimu
zinazohusu Urithi wa Ukombozi wa Bara la Afrika kwa kushirikiana na Wizara,
Idara na Taasisi mbalimbali.
·
Kusimamia utekelezaji wa mapendekezo
ya vitambaa vya kushonwa Vazi la Taifa yaliyokusanywa Kikanda kwa kuhusisha
mikoa yote na makundi maalumu, wakiwemo vijana na wanawake.
·
Kufanya utafiti wa lugha za jamii 12
za Mikoa ya Arusha, Kilimanjaro, Rukwa na Kagera kwa lengo la kukuza na
kuhifadhi lugha za jamii zinazotafitiwa.
·
Kusimamia na kuendesha Mkutano Mkuu wa
Sekta ya Utamaduni unaofanyika kila mwaka kwa kuwashirikisha wadau na watendaji
wa sekta hii. Lengo la mkutano huo ni kupokea, kujadili na kupitisha maazimio
na mustakabali wa Utamaduni nchini.
·
Kuandaa na kurusha vipindi 52 vya
redio kuhusu Maadili ya Mtanzania. Vipindi hivyo vina lengo la kuelimisha jamii
kutambua nini ni maadili na nini sio maadili ya Mtanzania, ili kuelekeza vijana
na Watanzania wote kwa ujumla kuthamini maadili ya taifa letu.
·
Kuratibu na kusimamia maadhimisho ya
Siku ya Utamaduni Duniani pamoja na vikundi vya ngoma za asili kushiriki katika
maadhimisho ya Sherehe za Kitaifa.
59.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2012/2013 Baraza la Kiswahili la Taifa
(BAKITA) limepanga kutekeleza kazi zifuatazo:-
·
Kuandaa na
kurusha vipindi 52 vya “Lugha ya Taifa”, vipindi 52 vya “Kumepambazuka” katika
redio na vipindi 52 vya “Ulimwengu wa Kiswahili” katika televisheni ili
kupunguza matumizi ya Kiswahili ambayo siyo sanifu.
·
Kuendelea kusoma
miswada ya vitabu vya taaluma na kuipatia ithibati ya lugha.
·
Kuratibu na
kutoa huduma za tafsiri na ukalimani katika mikutano ya kitaifa na kimataifa,
shughuli za mashirika, makampuni na watu binafsi.
·
Kuendelea
kuchunguza makosa ya Kiswahili
yanayofanywa na Vyombo vya Habari na watumiaji wengine na kusambaza masahihisho
yake.
·
Kuhamasisha
matumizi sahihi ya Kiswahili Sanifu katika mabango, matangazo na lebo.
·
Kuchunguza
maneno ya lugha za makabila na lahaja za Kiswahili yanayoweza kusanifiwa katika
mikoa ya Kanda ya Mashariki, Magharibi, Kusini na Kati.
·
Kukarabati na
kuboresha majengo yaliyonunuliwa kutoka
Shirika la Bima la Taifa ili yaweze kukidhi mahitaji ya kiofisi kwa ajili ya
matumizi ya BAKITA.
60.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2012/2013 Baraza la
Sanaa la Taifa (BASATA) limepanga kutekeleza kazi zifuatazo:-
·
Kuratibu midahalo 52 kupitia Jukwaa la Sanaa kwa Wasanii, Waandishi wa
Habari 4,500 ili kuwapa ufahamu, elimu na ujuzi katika masuala ya sanaa.
·
Kuhuisha kanzidata ya wasanii, vyama vya sanaa, mashirikisho na wadau. Lengo kwa mwaka huu ni kupata taarifa
mbalimbali za wasanii 2,000, vyama vya sanaa 50, mashirikisho manne (4) na
wadau 100 wanaojishughulisha na kazi za sanaa.
·
Kuendesha Mafunzo kwa ajili ya utengenezaji wa batiki na uchapaji kwa Wakufunzi
wa wasanii 20 kutoka mkoa wa Dar es
Salaam na Singida.
61.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2012/2013 Bodi ya Ukaguzi wa Filamu imepanga
kutekeleza kazi zifuatazo:-
·
Kupitia miswada 105 ya filamu na
kutoa ushauri wa kitaalamu kuhusu maboresho ya miswada hiyo.
·
Kukagua filamu 105 na kutoa ushauri
wa kitaalamu wa maboresho na kuziwekea madaraja na alama maalum filamu zote
zitakazokaguliwa.
·
Kushirikiana na Kamati ya Taifa ya
utoaji vibali vya filamu, kutoa vibali 25 vya kutengeneza filamu kwa raia wa
Tanzania na vibali 100 kwa waombaji kutoka nje ya Tanzania.
·
Kutoa mafunzo ya kuongeza weledi kwa kushirikiana na wadau wa tasnia ya filamu.
·
Kushirikiana na taasisi nyingine, kufanya msako maalum kukamata filamu ambazo
hazijakaguliwa na kuwachukulia hatua za kisheria wahusika.
·
Kuimarisha Bodi na Sekretarieti yake kwa kuwapa mafunzo na kuweka vifaa vya
kisasa vya ukaguzi vinavyoendana na teknolojia ya kisasa.
62.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2012/2013 Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa)
imepanga kutekeleza kazi zifuatazo:-
·
Kuendesha mafunzo ya Stashahada kwa washiriki 150 na mafunzo ya muda mfupi
kwa wasanii 200 walio kazini.
·
Kuendesha mafunzo ya cheti cha “National Technical Award” (NTA) katika fani
ya uzalishaji na usanifu wa muziki.
·
Kukamilisha mitaala ya shahada ya kwanza ya sanaa za maonyesho na sanaa za
ufundi na kuwasilisha NACTE kwa madhumuni ya kupewa ithibati.
·
Kusimamia
na kuendesha Tamasha la 31 la sanaa na Utamaduni wa Mtanzania.
SEKTA YA MAENDELEO YA
MICHEZO
63.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2012/2013 Wizara itatekeleza kazi
zifuatazo:-
·
Kuendelea kutoa mafunzo ya muda mfupi ya fani mbalimbali
za Michezo kwa walimu na viongozi wa michezo 400 katika Vituo vya Michezo Kanda
ya Kaskazini (Arusha) na Kanda ya Kusini (Songea).
·
Kuendelea kusimamia utekelezaji wa tafiti kuhusu
fani mbalimbali za Maendeleo ya Michezo.
·
Kusimamia uanzishwaji na utekelezaji wa mikataba
ya ushirikiano kati ya Tanzania
na nchi marafiki kuhusu ushirikiano katika Sekta ya Michezo.
·
Kuendesha mafunzo ya Stashahada ya Elimu ya
Ufundishaji Michezo na Stashahada ya Uongozi na Utawala wa Michezo kwa wanachuo
40 wa Chuo cha Maendeleo ya Michezo Malya.
·
Kuwezesha Timu za Taifa kushiriki katika michezo
ya Olimpiki na Paralimpiki Uingereza.
·
Kuendelea na jitihada za kutafuta fedha kwa ajili
ya uendelezaji wa awamu ya pili ya ujenzi wa eneo Changamani la Michezo la Taifa
lililoko Jijini Dar es Salaam.
64.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2012/2013 Baraza la Michezo la Taifa (BMT)
litatekeleza kazi zifuatazo:-
·
Kuendesha
mafunzo ya muda mfupi kwa Walimu wa Michezo wapatao 3,000 nchini kwa
kushirikiana na Halmashauri za miji na Manispaa.
·
Kutoa
mafunzo ya elimu ya michezo na kupanga wataalamu wa michezo katika viwango
stahiki (madaraja) kwa kushirikiana na Vyama vya Michezo vya Taifa.
·
Kuendelea
kutoa mafunzo ya Utawala Bora kwa Viongozi wa Vyama vya Michezo vya Taifa kwa
lengo la kuongeza ufanisi na tija katika Sekta ya Michezo.
·
Kuwajengea
uwezo wafanyakazi wa Baraza la Michezo la Taifa na Vyama vya Michezo vya Taifa
kwa kuwaandalia mafunzo kulingana na mahitaji yaliyopo.
·
Kuendelea
kusimamia mafunzo ya uongozi kwa Vijana kupitia michezo kwa walimu na vijana wa
Shule za Msingi na Sekondari kwa kushirikiana na Serikali za Mitaa.
·
Kuimarisha
ushiriki wa wanawake katika michezo na uongozi wa michezo kwa kushirikiana na
Baraza la Michezo la Uingereza (UK Sport International) kwa kuandaa mfumo wa
utambuzi na uendelezaji wa vipaji katika michezo mbalimbali kupitia Mradi wa kuboresha
maisha ya watoto (International Inspiration).
UTAWALA
NA RASILIMALI WATU
65.
Mheshimiwa Spika, Katika kipindi cha mwaka wa fedha 2012/13, Wizara
imepanga kuwaendeleza watumishi katika mafunzo. Wizara itaendelea kuwasomesha
watumishi 21, kati ya hao kumi na tano
(15) ni wa mwaka wa fedha 2011/12, wawili (2) wapya, na wengine wanne (4)
wanaotarajiwa kustaafu. Wizara itatoa mafunzo elekezi kwa watumishi ishirini
(20), wanaotarajiwa kuajiriwa.
D: HITIMISHO
66.
Mheshimiwa Spika, Wizara
yangu itaendeleza mafanikio yaliyopatikana
katika Sekta inazozisimamia ili ziweze
kuchangia zaidi katika maendeleo ya nchi yetu. Hii ni pamoja na kuongeza ajira,
kipato, kulinda mazingira, kuleta amani na furaha katika jamii. Pamoja na
kutumia fursa hizo bado kuna changamoto ambazo zinahitaji zipatiwe ufumbuzi ili
kuzitumia ipasavyo katika kuleta maendeleo ya nchi. Matarajio yangu ni kwamba
changamoto zilizopo zitaendelea kupatiwa ufumbuzi hatua kwa hatua hasa kwa
kushirikiana na Sekta Binafsi na wadau wengine wa maendeleo.
SHUKRANI
67.
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Serikali na kwa niaba yangu binafsi naomba kuwashukuru kwa
dhati wale wote walioshirikiana nasi katika kipindi cha mwaka wa fedha
2011/2012 katika kutimiza malengo yetu. Mafanikio ya utekelezaji wa majukumu na
malengo ya Wizara yamewezekana kutokana na ushirikiano uliopo miongoni mwa
viongozi na wafanyakazi wa Wizara na wadau wengine walio nje ya Wizara.
Shukrani zangu za pekee ziende kwa Mheshimiwa Amos Gabriel Makalla, (Mb),
Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo ambaye amekuwa msaada
mkubwa kwangu, Bw. Sethi Kamuhanda,
Katibu Mkuu na Bibi Sihaba Nkinga, Naibu Katibu Mkuu.
Aidha, nawashukuru Wakurugenzi, Wataalamu, na Watumishi wote wa Wizara ya
Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo pamoja na Asasi zilizo chini ya Wizara kwa
juhudi walizofanya kuhakikisha kwamba wanatimiza ipasavyo majukumu
tuliyokabidhiwa na Taifa.
68.
Mheshimiwa Spika, kwa dhati kabisa nitumie fursa hii tena kuwashukuru washirika wetu wa
maendeleo ambao wametuunga mkono wakati wote wa kutekeleza majukumu ya Wizara
yangu. Shukrani hizi ziwaendee wahisani
waliotusaidia nikitarajia kuwa wataendelea na moyo huo. Siyo
rahisi kuwataja wote lakini nitaje wachache ambao ni Serikali ya Jamhuri ya
Watu wa China, Finland, Uingereza, Denmark, Japan, Sweden, Norway, Iran, Cuba,
Korea ya Kusini, Marekani na Ujerumani pamoja na Mashirika ya kimataifa ya
UNESCO, CYP, UNV, ILO, UNICEF, UNFPA, IYF na UNDP.
69.
Mheshimiwa Spika, napenda kuvishukuru vyombo vyote vya habari
nchini ambavyo vimefanya kazi nzuri ya kuitangaza nchi yetu. Ninaamini kuwa
vyombo hivyo vitaendelea na kazi ya kuhabarisha, kuburudisha na kuelimisha umma
kwa kuzingatia maadili. Aidha, ninamshukuru sana Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali
kwa kuchapisha hotuba hii kwa wakati, bila kuvisahau vituo vya Televisheni na
Radio ambavyo kwa namna ya pekee vinarusha hotuba hii hewani.
MAKADIRIO YA BAJETI KWA MWAKA WA
FEDHA 2012/2013
Mapato
70.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa
fedha 2012/2013 Wizara imepanga kukusanya
jumla ya shilingi 714,209,000 kutoka
katika vyanzo vyake mbalimbali vya mapato. Mchanganuo wa makusanyo kifungu kwa kifungu upo katika Kiambatisho Na. I.
Matumizi ya Kawaida
71.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2012/2013 Wizara imetengewa bajeti ya Shilingi 16,210,999,000 kwa ajili ya
Matumizi ya Kawaida (Matumizi Mengineyo na Mishahara), fedha hizo
zinajumuisha:-
·
Mishahara ya Wizara
- Shilingi 2,410,357,920.
·
Mishahara ya Asasi
- Shilingi 7,761,301,000.
·
Matumizi Mengineyo ya Wizara - Shilingi 4,635,340,080
·
Matumizi Mengineyo ya Asasi - Shilingi 1,404,000,000
Mchanganuo wa makadirio ya Matumizi ya Kawaida ya Wizara
upo katika Kiambatisho Na. II. Aidha, Matumizi ya Kawaida kwa Wizara
peke yake yapo Kiambatisho Na. III na
kwa Asasi yapo Kiambatisho Na. IV.
Miradi ya Maendeleo
72.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2012/2013
Wizara imetengewa jumla ya shilingi 3,096,600,000 kwa ajili ya kutekeleza Miradi ya Maendeleo, Fedha za ndani ni shilingi
2,740,000,000 na fedha za nje ni shilingi
356,600,000. Mchanganuo kamili upo katika Kiambatisho
Na. V.
MAOMBI YA FEDHA KWA AJILI YA KUTEKELEZA MPANGO WA
MWAKA 2012/2013
73.
Mheshimiwa Spika, ili Wizara yangu iweze kutekeleza majukumu na malengo yake ya mwaka wa
fedha 2012/2013, naomba sasa Bunge
lako Tukufu liidhinishe
bajeti ya jumla ya shilingi 19,307,599,000 ambapo kati ya hizo, fedha za Matumizi ya Kawaida ni shilingi 16,210,999,000 na fedha za
Miradi ya Maendeleo ni shilingi 3,096,600,000. Mchanganuo wa fedha hizi upo katika
viambatisho nilivyovitaja hapo awali ambavyo ni sehemu ya Hotuba hii.
74.
Mheshimiwa Spika, napenda nitoe tena shukrani zangu za dhati kwako binafsi na kwa
Waheshimiwa Wabunge kwa kunisikiliza. Hotuba hii inapatikana pia katika tovuti
ya Wizara kwa anuani ya: www.hum.go.tz.
75.
Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.
Kiambatisho I
MAKISIO YA MAPATO MWAKA 2011/12 NA MAKADIRIO YA
MWAKA 2012/13 (Tsh.)
KIFUNGU/
KIJIFUNGU
|
MAELEZO
|
MAKISIO YA MAPATO
2011/12
|
UKUSANYAJI HADI
JUNI, 2012
|
MAKADIRIO YA 2012/13
|
(1)
|
(2)
|
(3)
|
(4)
|
(5)
|
1001-Utawala
na Rasilimali Watu
|
140368
- Makusanyo mengineyo.
|
1,000
|
371,000
|
1,000
|
140370
- Madeni.
|
1,000
|
-
|
1,000
|
|
140283-
Mauzo ya Tenda.
|
2,289,538
|
|
200,000
|
|
Jumla
ya Kifungu 1001
|
2,291,538
|
371,000
|
202,000
|
|
|
|
|
|
|
6001-Maendeleo
ya Utamaduni.
|
140312
-
|
191,152,354
|
4,205,500
|
2,000,000
|
140368
- Makusanyo Mengineyo.
|
1,000
|
-
|
1,000
|
|
140370-
Madeni.
|
1,000
|
-
|
1,000
|
|
140386
– Vibali vya Filamu
|
114,462,711
|
210,478,745
|
198,000,000
|
|
Jumla
ya Kifungu 6001
|
305,617,245
|
214,684,245
|
200,002,000
|
|
|
|
|
|
|
6004-Maendeleo
ya Michezo.
|
140259
- Uwanja wa Taifa.
|
343,389,556
|
380,492,072
|
400,000,000
|
140315
-
|
43,493,720
|
31,080,000
|
51,000,000
|
|
140368
- Makusanyo Mengineyo.
|
1,000
|
-
|
1,000
|
|
140370
- Madeni.
|
1,000
|
-
|
1,000
|
Jumla
ya Kifungu 6004
|
386,885,276
|
411,572,072
|
451,002,000
|
|
|
|
|
|
|
7003
– Habari.
|
140202
- Machapisho
|
45,784,969
|
15,980,000
|
20,000,000
|
140264
- Usajili wa Magazeti.
|
4,578,497
|
26,950,000
|
30,000,000
|
|
140265
- Ukumbi.
|
11,446,242
|
10,050,000
|
7,000,000
|
|
140310
-
|
4,578,497
|
-
|
1,000
|
|
140368
- Mengineyo.
|
1,000
|
-
|
1,000
|
|
140370
- Madeni.
|
1,000
|
-
|
1,000
|
|
1051017-Vitambulisho
vya wanahabari.
|
5,723,121
|
2,766,900
|
6,000,000
|
|
Jumla
ya Kifungu 7003
|
72,113,326
|
55,746,900
|
63,003,000
|
|
Jumla
ya Fungu 96
|
766,907,385
|
682,374,217
|
714,209,000
|
Kiambatisho II
MUHTASARI WA BAJETI YA MATUMIZI YA KAWAIDA
2012/2013
WIZARA
NA ASASI
IDARA/KITENGO
|
MAKISIO 2012/2013
|
||
MISHAHARA (PE)
|
MATUMIZI MENGINEYO (OC)
|
JUMLA MATUMIZI YA KAWAIDA (3+4)
|
|
(1)
|
(3)
|
(4)
|
(5)
|
1001-UTAWALA NA
RASILIMALI WATU
|
620,297,320
|
2,124,258,180
|
2,744,555,500
|
1002 – FEDHA NA
UHASIBU
|
121,855,200
|
129,254,400
|
251,109,600
|
1003 – SERA NA
MIPANGO
|
160,334,000
|
274,200,000
|
434,534,000
|
1004-HABARI, ELIMU
NA MAWASILIANO
|
55,086,700
|
75,920,000
|
131,006,700
|
1005-UNUNUZI NA
UGAVI
|
75,044,800
|
213,300,000
|
288,344,800
|
1006-UKAGUZI WA
NDANI
|
57,397,200
|
131,294,400
|
188,691,600
|
1007- TEHAMA
|
44,175,100
|
32,600,000
|
76,775,100
|
1008 – SHERIA
|
29,012,000
|
20,400,000
|
49,412,000
|
6001 –UTAMADUNI
|
2,438,510,400
|
616,888,600
|
3,055,399,000
|
6002 – VIJANA
|
370,156,800
|
814,222,400
|
1,184,379,200
|
6004 – MICHEZO
|
631,925,200
|
1,089,912,900
|
1,721,838,100
|
7003 – HABARI
|
5,567,941,400
|
517,012,000
|
6,084,953,400
|
JUMLA
KUU
|
10,171,736,120
|
6,039,262,880
|
16,210,999,000
|
Kiambatisho III
MUHTASARI
WA BAJETI YA MATUMIZI YA KAWAIDA KWA WIZARA MWAKA WA FEDHA 2012/13
IDARA/KITENGO
|
MAKISIO 2012/2013
|
||
MISHAHARA (PE)
|
MATUMIZI MENGINEYO (OC)
|
JUMLA MATUMIZI YA KAWAIDA (3+4)
|
|
(1)
|
(3)
|
(4)
|
(5)
|
1001-UTAWALA NA
UTUMISHI
|
620,297,320
|
2,124,258,180
|
2,744,555,500
|
1002 – FEDHA NA
UHASIBU
|
121,855,200
|
129,254,400
|
251,109,600
|
1003 – SERA NA
MIPANGO
|
160,334,000
|
274,200,000
|
434,534,000
|
1004-HABARI, ELIMU
NA MAWASILIANO
|
55,086,700
|
75,920,000
|
131,006,700
|
1005-UNUNUZI NA
UGAVI
|
75,044,800
|
213,300,000
|
288,344,800
|
1006-UKAGUZI WA
NDANI
|
57,397,200
|
131,294,400
|
188,691,600
|
1007- TEHAMA
|
44,175,100
|
32,600,000
|
76,775,100
|
1008 – SHERIA
|
29,012,000
|
20,400,000
|
49,412,000
|
6001 –UTAMADUNI
|
321,690,400
|
247,888,600
|
569,579,000
|
6002 – VIJANA
|
370,156,800
|
814,222,400
|
1,184,379,200
|
6004 – MICHEZO
|
298,302,000
|
354,990,100
|
653,292,100
|
7003 – HABARI
|
257,006,400
|
217,012,000
|
474,018,400
|
JUMLA YA
IDARA/VITENGO
|
2,410,357,920
|
4,635,340,080
|
7,045,698,000
|
Kiambatisho IV
MUHTASARI WA MATUMIZI YA KAWAIDA KWA ASASI MWAKA
WA FEDHA 2012/13
TAASISI/MASHIRIKA
|
MAKISIO YA
2012/13
|
||
MISHAHARA (PE)
|
MATUMIZI MENGINEYO (OC)
|
JUMLA MATUMIZI YA KAWAIDA (3+4)
|
|
(1)
|
(3)
|
(4)
|
(5)
|
6001–280402 EACTRONAL
|
-
|
9,000,000
|
9,000,000
|
6001-280514 BODI YA
FILAMU.
|
-
|
90,000,000
|
90,000,000
|
6001- 280515
BARAZA LA SANAA LA TAIFA (BASATA)
|
570,566,000
|
90,000,000
|
660,566,000
|
6001-280516
BARAZA
LA KISWAHILI LA TAIFA (BAKITA)
|
494,638,000
|
90,000,000
|
584,638,000
|
280328 – TaSUBa
|
837,771,000
|
90,000,000
|
927,771,000
|
Mfuko
wa Utamaduni
|
213,845,000
|
-
|
213,845,000
|
6004 – 280518
BARAZA
LA MICHEZO LA TAIFA (BMT)
|
333,546,000
|
90,000,000
|
423,546,000
|
6004 – 280518
BARAZA
LA MICHEZO LA TAIFA (MAKOCHA)
|
-
|
400,000,000
|
400,000,000
|
6004 -280594
SHIMIWI
|
-
|
5,000,000
|
5,000,000
|
6004 – 270380
CHUO
CHA MAENDELEO YA MICHEZO-MALYA
|
-
|
200,000,000
|
200,000,000
|
6004 – 270839
KITUO
CHA MICHEZO –ARUSHA
|
-
|
20,000,000
|
20,000,000
|
6004 – 270840
KITUO
CHA MICHEZO- SONGEA
|
-
|
20,000,000
|
20,000,000
|
7003 – 280577
SHIRIKA
LA UTANGAZAJI
|
5,310,935,000
|
300,000,000
|
5,610,935,000
|
JUMLA TAASISI
/MASHIRIKA
|
7,761,301,000
|
1,404,000,000
|
9,165,301,000
|
Kiambatisho V
BAJETI YA MAENDELEO 2012/13
MRADI
|
MAKADIRIO YA 2012/13
|
||
FEDHA ZA NDANI
|
FEDHA ZA NJE
|
JUMLA
|
|
1001 – IDARA YA UTAWALA NA RASILIMALI WATU
|
|||
5495-Kinga ya
Maambukizi ya UKIMWI.
|
-
|
-
|
-
|
Jumla
|
-
|
-
|
-
|
1003 – IDARA YA SERA NA MIPANGO
|
|||
6260-Maendeleo ya
Taasisi.
|
-
|
-
|
-
|
5414- Ushiriki na ushirikishwaji
wa vijana
|
-
|
-
|
-
|
5417- Mpango wa Kuibua Fursa za
Ajira kwa Vijana
|
-
|
-
|
-
|
Jumla
|
-
|
-
|
-
|
6001 – IDARA YA MAENDELEO YA UTAMADUNI
|
|||
4353-Ukarabati wa
TaSUBa.
|
-
|
-
|
-
|
6343-Ujenzi wa
Ofisi (BAKITA).
|
300,000,000
|
-
|
300,000,000
|
6293-Programu ya
Ukombozi wa Bara la Afrika.
|
120,000,000
|
|
120,000,000
|
6355-Ujenzi wa
Ukumbi wa Wazi wa Maonyesho ya Sanaa.
|
50,000,000
|
-
|
50,000,000
|
6356-Ujenzi wa
Jumba la Utamaduni.
|
90,000,000
|
356,600,000
(Kutoka
UNESCO)
|
476,600,000
|
6364-Mfuko wa
Utamaduni.
|
-
|
-
|
-
|
Jumla
|
560,000,000
|
356,600,000
|
916,600,000
|
6002 – IDARA YA MAENDELEO YA VIJANA
|
|||
6380- Ukarabati wa Vituo vya
Vijana
|
300,000,000
|
-
|
300,000,000
|
Jumla
|
300,000,000
|
-
|
300,000,000
|
6004 – IDARA YA MAENDELEO YA MICHEZO
|
|||
6385-Ujenzi wa
Chuo cha Michezo Malya.
|
330,000,000
|
-
|
330,000,000
|
6523-Ujenzi wa
Eneo Changamani la Michezo.
|
1,000,000,000
|
-
|
1,000,000,000
|
Jumla
|
1,330,000,000
|
|
1,330,000,000
|
7003 – IDARA YA HABARI
|
|||
6567-Habari kwa
Umma.
|
50,000,000
|
-
|
50,000,000
|
4279-Upanuzi na
Usikivu wa TBC
|
500,000,000
|
-
|
500,000,000
|
Jumla
|
550,000,000
|
|
550,000,000
|
JUMLA KUU
|
2,740,000,000
|
356,600,000
|
3,096,600,000
|
Kiambatisho VI
IDADI YA VYOMBO
VYA HABARI VILIVYOANDIKISHWA KWA MWAKA WA FEDHA 2011/12
NA
|
MKOA
|
VITUO VYA RADIO
|
VITUO VYA
TELEVISHENI
|
|||
2011
|
2012
|
2011
|
2012
|
|||
1
|
Arusha
|
4
|
4
|
-
|
-
|
|
2
|
D’Salaam
|
20
|
20
|
11
|
11
|
|
3
|
Dodoma
|
3
|
5
|
-
|
-
|
|
4
|
Iringa
|
8
|
8
|
2
|
2
|
|
5
|
Kagera
|
4
|
4
|
-
|
-
|
|
6
|
Kigoma
|
-
|
-
|
-
|
-
|
|
7
|
Kilimanjaro
|
4
|
4
|
-
|
-
|
|
8
|
Lindi
|
-
|
-
|
-
|
-
|
|
9
|
Manyara
|
2
|
2
|
-
|
-
|
|
10
|
Mara
|
1
|
1
|
-
|
-
|
|
11
|
Mbeya
|
5
|
5
|
3
|
3
|
|
12
|
Morogoro
|
4
|
8
|
2
|
2
|
|
13
|
Mtwara
|
2
|
3
|
2
|
2
|
|
14
|
Mwanza
|
7
|
11
|
1
|
1
|
|
15
|
Pwani
|
-
|
-
|
-
|
-
|
|
16
|
Rukwa
|
1
|
1
|
1
|
1
|
|
17
|
Ruvuma
|
2
|
3
|
1
|
1
|
|
18
|
Shinyanga
|
3
|
3
|
-
|
-
|
|
19
|
Singida
|
-
|
-
|
1
|
1
|
|
20
|
Tabora
|
2
|
2
|
1
|
1
|
|
21
|
Tanga
|
1
|
1
|
1
|
1
|
|
JUMLA
|
73
|
85
|
26
|
26
|
Chanzo: Idara ya Habari na Mamlaka ya
Mawasiliano Tanzania
(TCRA)
COMMENTS