Nimejulishwa na vyanzo vyetu kuwa msemaji wa CCM amefanya mkutano na wanahabari na kutoa madai mbalimbali ya uzushi kwa CHADEMA ...
Nimejulishwa na vyanzo
vyetu kuwa msemaji wa CCM amefanya mkutano na wanahabari na
kutoa madai mbalimbali ya
uzushi kwa CHADEMA baada ya CHADEMA kuendelea kutekeleza
mikakati na mipango yake
ya kuwaunganisha watanzania kupitia falsafa ya ‘nguvu ya
umma’ katika kuchangia
vuguvugu la mabadiliko (M4C) katika maeneo mbalimbali nchini.
Nitatoa tamko kamili na
kueleza hatua za ziada baada ya kupata taarifa iliyotolewa
kwa ukamilifu, hata hivyo
kwa kuwa tayari baadhi ya vyombo vya habari vimetaka kauli
ya awali naomba kueleza
machache:
Kuibuka huku kwa CCM na
kufanya propaganda chafu ni ishara ya kwamba CCM inaumizwa
na namna ambavyo
watanzania wanajitokeza kuunga mkono CHADEMA kwa hali na mali hivyo
CCM sasa
inatapatapa kujaribu kudhibiti wimbi la mabadiliko kwa kutumia siasa
chafu. Mwenyekiti wa CCM
Rais Jakaya Kikwete anapaswa kueleza watanzania iwapo
mikakati hiyo michafu ina
baraka zake na za serikali anayoiongoza kwa kurejea pia
madai yaliyotolewa na
Waziri wa Ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu) Steven Wassira
kuwa CHADEMA
itasambaratishwa katika kipindi cha mwaka mmoja kwa mbinu mbalimbali.
CCM kwa kuwa
imekuwa na kawaida ya kufanya usanii kuhalalisha fedha haramu kama
ilivyofanya kwenye
chaguzi zilizopita baada ya viongozi waandamizi wa CCM na makada
wake kuchota fedha za
chafu kifisadi kama zile za kutoka kwenye Akaunti ya Madeni ya
Nje (EPA) na vyanzo
vingine vichafu na kuzisafisha kupitia harambee za hadaa
zilizofanywa na CCM kwa
nyakati mbalimbali; inataka kuichafua CHADEMA inayopata
fedha kutoka vyanzo
halali kwa njia za wazi ili kukatisha tamaa umma wa watanzania
unaochangia vuguvugu la
mabadiliko.
Viongozi wa CCM wameamua
kujidanganya, kuidanganya Serikali yao na kujaribu
kuwapotosha watanzania
lakini CHADEMA inatambua kwamba watu wachache wanaweza
kudanganyika kwa muda
mchache lakini si watu wote wakati wote; na kwamba watanzania
wa leo kwa uwingi wao
hawawezi kudanganyika na uzushi wa kijinga wa CCM.
Ni ukweli ulio wazi
kwamba CHADEMA imekuwa ikifanya harambee kwa uwazi kwa nyakati
mbalimbali katika kumbi
na katika mikutano ya hadhara ikiwemo ya vijijini ambapo
michango hutolewa kwa
uwazi, aidha michango kwa njia ya simu inaweza kufuatiliwa na
kuthibitisha bila shaka
yoyote kwamba watanzania wameamua kuchangia mabadiliko ya
kweli.
Madai ya CCM kuwa CHADEMA
imepokea au itapokea mabilioni ya shilingi kutoka mataifa
ya nje ni ya uzushi na
narudia kwa mara nyingine tena kuitaka CCM itaje majina ya
serikali, taasisi ama
makampuni ya nje ambayo CCM inadai kwamba CHADEMA imepokea
mabilioni ya shilingi
katika siku za karibuni au inatarajia kupokea.
Badala ya CCM kuisingizia
CHADEMA ilipaswa CCM ieleze watanzania orodha ya vigogo wa
Serikali inayoongozwa na
wanachama waandamizi wa CCM ambao wanaelezwa kuwa na
akaunti nchini Uswisi na
nchi zingine wakituhumiwa kupewa fedha za kifisadi kutoka
kwa makampuni ya
utafutaji wa mafuta, gesi asili pamoja na uchimbaji wa madini.
CCM ilipaswa ieleze
watanzania sababu za kuendelea kusuasua kujivua magamba ya
ufisadi kinyume na
maazimio ya CCM yaliyofikiwa baada ya msukumo wa CHADEMA kutaja
orodha ya mafisadi kwa
kuwa kati ya mafisadi hao ni pamoja na viongozi wa CCM
walioiingiza nchi katika
mikataba mibovu.
Ikumbukwe kwamba madai
haya si mapya kutolewa na CCM, yaliwahi kutolewa na
Mwenyekiti wa Umoja wa
Wanawake wa CCM (UWT) Sophia Simba mara baada ya uchaguzi
mkuu wa 2010 akidai kuwa
CHADEMA imepokea fedha kutoka mataifa ya ulaya kwa ajili ya
kufanya maandamano ya kuiondoa
CCM madarakani.
Itakumbukwa kwamba wakati
huo nilimtaka ataje nchi hizo na kueleza kusudio la
kumchukulia hatua zaidi
na kwa upande mwingine niliyataka mataifa hayo ya Ulaya
yatoe kauli kuhusu madai
hayo. Izingatiwe kwamba mataifa hayo yalikanusha madai hayo
ya CCM na Sophia Simba
hakuna madai hayo dhidi ya CHADEMA.
Nimeelezwa kuwa CCM
imetoa madai mengine ya uzushi kuwa CHADEMA inapewa mabilioni
toka nje kwa kuwa nchi
imegundua rasilimali za mafuta na gesi na kudai kuwa fedha
hizo ni kwa ajili ya kuiweka
nchi rehani.
Madai haya yaliwahi
kutolewa pia kwa Katibu wa CCM wa Fedha na Uchumi Mwigulu
Nchemba na nikamtaka
Waziri wa Mambo ya Nje Benard Membe kutaja nchi hizo na
mikataba hiyo hata hivyo
mpaka sasa hakuna kiongozi yoyote wa CCM na Serikali
aliyejitokeza kutaja
CHADEMA imepokea au itapokea mabilioni kutoka nchi gani na kwa
mikataba gani.
CCM inatoa madai hayo
kuhamisha mjadala baada ya CHADEMA wa uongozi bora, sera
makini, mikakati sahihi
na oganizesheni thabiti kuwa mstari wa mbele katika kutetea
rasilimali za taifa na
watanzania kutambua kwamba taifa letu litaepushwa kutumbukia
kwenye laana ya
rasilimali kwa kuiondoa CCM madarakani katika chaguzi za mwaka 2014
na 2015 na kuichagua
CHADEMA.
CCM na Serikali yake
ndiyo imekuwa kinara wa kupokea fedha kutoka nje kwa kisingizio
cha misaada na kuingia
mikataba mibovu na mataifa ya nje pamoja na makampuni ya
kigeni na kuachia mianya
ya uporoji wa rasilimali za nchi na CHADEMA imeanika hali
hii kwenye orodha ya
mafisadi kwa kutaja majina ya viongozi waliohusika kwenye
mikataba ya madini na
tutaendelea kufanya hivyo hata katika masuala ya mafuta na
gesi ambayo tayari vigogo
wa Serikali inayoongozwa na CCM wameshaanza kuingia
mikataba mibovu na
kuingiziwa fedha katika akaunti zao za nje ya nchi.
Hivyo, badala ya CCM
kutoa madai ya uzushi kuhusu CHADEMA kuingia mikataba na
serikali au makampuni ya
nje, CCM ieleze watanzania imechukua hatua gani mpaka sasa
juu ya viongozi na wanachama
wake waliongia mikataba mibovu kwenye rasilimali muhimu
nchini ikiwemo madini,
mafuta, gesi na maliasili zingine za taifa letu na kutoa
mikataba hiyo hadharani
ili watanzania waweze kuchukua hatua za kufanya mabadiliko
ya kweli.
Hivi karibuni Rais Kikwete
ambaye pia ni mwenyekiti wa CCM alisema kwamba serikali
inayoongozwa na CCM
haitarudia makosa ya kuachia mianya ya ufisadi kwenye gesi;
hivyo CCM ilipaswa wakati
huu kuwaomba radhi watanzania kwa ufisadi uliofanyika
kwenye madini na
rasilimali nyingine na kuishukuru CHADEMA kwa kuendelea
kuwaunganisha watanzania
wakati wote kusimamia mabadiliko ya kweli.
CCM badala ya kutishia
kuwa ina mikataba inayoihusu CHADEMA ingetoa mikataba hiyo na
hali hii ya CCM
inayoongoza Serikali kudai CHADEMA kufanya mikakati, mipango na
shughuli iliyo kinyume
cha sheria bila vyombo vya dola kuchukua hatua ni ishara ya
CCM kukiri wazi kuwa
chama legelege chenye serikali legelege kimeshindwa kuongoza
nchi na badala yake
kimejikita katika propaganda chafu.
CHADEMA tangu kuanzishwa
kwake imekuwa na mikataba ya makubaliano ya ushirikiano
(MOU) na vyama rafiki vya
ndani ya Afrika na duniani na makubaliano hayo yamekuwa
yakifikiwa kwa uwazi
ikiwa ni sehemu ya CHADEMA kuwa na mtandao wa kitaifa na
kimataifa na hayajawahi
kuhusisha wala hayatawahi kuhusisha CHADEMA kusaidiwa
mabilioni ya shilingi kwa
ajili ya kufanya kazi zake kama inavyodaiwa na CCM.
CHADEMA kimekuwa chama
kiongozi kwa nyakati mbalimbali kueleza viwango cha matumizi
yake ya fedha na vyanzo
vya fedha husika huku kikitegemea kwa kiwango kikubwa
michango ya wanachama na
wapenzi wa chama hapa nchini pamoja na kutumia kwa ufanisi
ruzuku inayotolewa kwa
vyama vya siasa.
CCM imekuwa na kawaida ya
kutoa madai ya uzushi wakati mwingine yakiambatana na
kutoa nyaraka za kughushi
inazodai kuwa ni za CHADEMA. Ikumbukwe kwamba wakati wa
uchaguzi wa mdogo wa
Igunga, CCM ilitoa madai ya uzushi kuwa CHADEMA inafadhiliwa na
nchi za nje ikiwemo
kupewa mafunzo ya ugaidi na kudai kuwa tayari magaidi
wameingizwa na CHADEMA
toka nje katika uchaguzi huo; hata hivyo katika mwenendo wa
kesi ya uchaguzi ya
Igunga Katibu Mkuu wa CCM Wilson Mukama aliyetoa madai hayo
alitoa ushahidi
mahakamani kwamba CHADEMA haijawahi kuleta magaidi bali kauli hizo
za CCM zilikuwa ni za
siasa za uchaguzi.
Hivi karibuni, CCM
imeghushi waraka mwingine na kuusambaza kile ilichodai kuwa ni
maazimio ya kamati
kuu ya CHADEMA ya kupanga migomo ya walimu, madaktari na mipango
mingine ya kuhujumu
serikali; hata hivyo waraka huo ulidhihirika wazi kuwa ni wa
kughushi.
Mikakati yote hiyo
michafu hupangwa na CCM mara kwa mara wakati ambapo CHADEMA
inaanza operesheni
Sangara na mikakati mingine ya kuleta mabadiliko nchini na
kujipanga kuiondoa CCM
madarakani kama ilivyo sasa ambapo CHADEMA inaendelea na
operesheni katika mkoa wa
Morogoro hivyo watanzania wanapaswa kuipuuza CCM na
kuendelea kujiunga
CHADEMA na kuchangia mabadiliko kwa hali na mali mpaka kieleweke.
John Mnyika (Mb)
Mkurugenzi wa Habari na
Uenezi
12/08/2012
COMMENTS